Monday, June 16, 2008

JENGA TABIA YA KUJIAMINI NA KUTOKUKATA TAMAA

MTU anayejiamini mara nyingine anaweza kuangushwa na kukata tamaa. Wengi husema kuwa hakuna njia, lakini mtu anayejiamini mara zote hutafuta njia muafaka. Wengi hawafanikiwi kwa sababu wanakata tamaa.
Anayejiamini hufanikiwa kwa kiwango kikubwa kwa sababu hakati tamaa. Hapa duniani hakuna kitu cha maana kama kuwa na mtazamo wa kujiamini.
Mtazamo wako unaweza ukakujenga au kukuvunja moyo, kukuponya au kukuumiza, kukufanya rafiki au kukufanya adui, kukushikilia au kukuachilia, kukufanya mnyonge au mwenye furaha, kukufanya ushindwe au ufanikiwe. Kumbuka unatakiwa kuishi katika dunia inayofaa kuwa mtu makini wa kufikiria.
Mwenye mamlaka ya kuchagua mwenendo bora ni wewe. Kwa kuwa mwanadamu anaweza kuwa na sababu, hisia za msisimko, uwezo wa kufikia mawazo yanayomzunguka, mlango wa fahamu, kumbukumbu na hali ya kufichika akilini hivyo anakuwa na uamuzi wa kuchagua kufanya lile analolitaka.
Usipende kumsemea mtu mwingine bali isemee nafsi yako. Kwa kufanya hivyo moyo wako uliovunjika unaweza ukabaki katika hali hiyo au ukaiondoa. Haijalishi ni jambo gani ulilokutana nalo, utakapolikabili jambo hilo ndipo ushindi wako utakapopatikana. Msimamo wako ni muhimu kuliko kuwa na sababu.
Tuangalie njia zinazoweza kuondoa fikra potofu na kukupatia nzuri. Kujiamini siyo kitu kinachotokea chenyewe lakini kinakuja katika maisha ya kujilinda. Hivyo ndivyo unavyoweza kuishi katika hali ya kujiamini.
Unatakiwa kuwa balozi wa maneno mema kwa kila mtu unayekutana naye kila siku.
Bila kujali yanayotokea, tarajia kufanya mema na utayaona. Mtu yeyote anayejiamini anatakiwa kutambua mambo yaliyo kinyume na kuyarekebisha kwa ajili ya matokeo bora.
Wakati wote inawezekana kuangalia mambo yaliyo mazuri, kutegemea matokea bora kwako wewe hata kama mambo yanakwenda kombo.
Kwa utashi wako, jaza moyo wako kwa mambo yaliyo mazuri. Weka mawazo yako katika jambo la kweli, zuri na lililo sawa. Fikiria mambo ambayo ni safi na yenye upendo kwa wengine.
Kamwe usijisalimishe kwa mawazo mabaya. Wakati unapokuwa kwenye kipindi kigumu unatakiwa kufanya jambo gani? Likubali jambo hilo, likabili lakini usijiachie. Kumbuka njia ya kupambana na magugu katika shamba lako ni kupanda majani manene na yenye afya.
Njia ya kuondoa hisia mbaya ni kwa kuongea maneno yenye uhakika. Unaweza kushinda hisia mbaya kwa kuweka mambo bayana.
Mfano, mtu ambaye ni mvutaji wa sigara anajisikia vibaya kwa kushindwa kuacha tabia hiyo.
Na kutokana na hali hiyo anasema kuwa anatamani kama angeweza kuacha kuvuta sigara.
Kwa kusema hivyo, ameamua kuondokana na hali hiyo na amepata nguvu ya kutamka hivyo.
Hivyo anakuwa na ujasiri wa kuacha kuvuta kwa kuwa anachukia tabia hiyo. Pia anapenda mdomo wake uwe na ladha nyingine tofauti na ile aliyoizoea ya harufu ya sigara.
Fuata misingi ya kubadili yaliyo mabaya kuwa mazuri. Jizoeze kubadili misimamo uliyonayo.
Katika kila hisia hasi kuna hisia chanya. Wewe unaweza kuchagua kuondokana na hisia hasi.
Hivyo waweza kuondoa kinyongo kwa kuwa na upendo kwa mtu unayemchukia au anayekuumiza maisha yako.
Kuondoa hali ya wasiwasi kwa kuwa mkweli, hali ya kukata tamaa kwa kuwa na tumaini, hali ya tamaa kwa kuwa mkarimu, kuondoa huzuni kwa kuwa na furaha, kuondoa ulalamishi kwa kuwa mtu wa shukrani, kuondoa wasiwasi kwa kuwa katika hali ya kuamini pamoja na kuondoa hali ya hatia inayokukabili kwa kusamehe.
Angalia yaliyo mazuri kwa wenzako. Wote tunajua watu wanaojenga uhasama wanakoelekea. Kwa nini? Kwa sababu wanapenda kuongea kuhusu kila kitu na kila mmoja katika hali inayopotosha. Tazama hili kama haliko sahihi. Kila wakati unapozungumza jambo baya kuhusu mtu mwingine, unaathiri mtazamo wako kuwa na hisia mbaya kwa jamii.
Endeleza mwenendo wa kufanya mema na mazuri kwa wengine. Hakuna kitu kibaya kama kuwa na mwonekana mbaya.
Badili mtazamo wako juu ya wengine nao watabadili mwonekano wao juu yako. Mtazamo wako juu ya wengine wanaokuzunguka wakati wote unakwamisha mawasiliano.
Inasemekana kuwa mbwa anajua kama unampenda au la. Vizuri, kama anajua kuwa humpendi, haitakuwa kwa mwanadamu, ambaye anaufahamu mkubwa zaidi ya mnyama? Huisi una hisia za kweli? Jifunze kupenda watu nawe utapendwa.
Kuwa mwepesi kutoa shukrani na salamu mwanana kwa wengine. Asilimia 99 ya muda, mawazo mabaya yanakuwa yameshikilia mawazo yetu mazuri katika fikra zetu, kwa sababu ni mawazo ya ubinafsi.
Uhitaji wetu wa kila mara ni kutokuwa na mawazo ya ubinafsi katika maisha yetu. Hivyo ukiamua unaweza kuondoka katika hali hiyo na ukawa na maisha yenye mwonekano mzuri kwa jamii inayokuzunguka.
Njia ya kuondokana na hali hiyo ni kuachilia fikra za ubinafsi. Unaweza ukafanya hilo kwa kuonyesha moyo wako wa shukrani kwa wengine.
Dawa ya uponyaji katika maisha yako ni kujenga urafiki na kutoa huduma kwa wengine.
Jizoeze kumwomba Mungu. Maombi ni ushindi wa mafanikio yetu unapotarajia matukio bora maishani mwako. Lakini kama unatarajia mambo mabaya acha kufanya mambo mema kwa wengine.
Unaweza kufanya tathmini katika maisha yako.
Kumbuka Mungu ni mzuri katika maisha yako, na ameyatengeneza maisha yako kwamba hatakuangusha wala kukuacha mpweke. Atakupa mambo mazuri katika mabaya unayokutana nayo.
Ushike vilivyo mwenendo huu mwema. Kumbuka Mungu ana nguvu kuliko wote, yeye ni mwanzo wa maisha yetu, anapanga mipango yetu yote, analeta mambo mazuri katika hatua mbaya uliyofikia, anasamehe, yupo nasi hakuna kinachomshinda yeye. Tarajia mambo mema kutoka kwake nawe utayapata.
Kumbuka furaha inaondoa huzuni katika maisha tunayoishi. Unapokuwa nayo uwezo wa kujiamini unakuwepo katika maisha yetu.
Tabia yako ya zamani haiwezi kufa kwa haraka, lakini tabia mpya inakuja kutokana na bidii yako ya kutaka kubadili mfumo wa maisha yako.
Penda kufikiria mawazo mazuri kila mara utapata marafiki wazuri wenye fikra kama zako.
Utapata marafiki wenye mawazo mazuri na ambao watakusaidia katika mambo mbalimbali ya maisha unayoyapitia. Fikiri vyema ili upate matokeo mazuri.
Tukutane wiki ijayo.
lcyngowi@yahoo.com0713 331455/ 0733 331455

0 Maoni:

Twitter Facebook