Monday, December 8, 2014

Kipozi: Uhuru wa habari si upotoshaji



Na Mwandishi Wetu
MKUU wa Wilaya ya Bagamoyo ambaye pia ni mwanahabari, Ahmed Kipozi amesema kuwa uhuru wa vyombo vya habari maana yake si upotoshaji wa habari.
Kipozi ambaye pia ni mtangazaji mkongwe enzi za iliyokuwa redio Tanzania, televisheni ya ITV pamoja na redio Uhuru, alisema hayo katika mkutano mkuu wa Watangazaji kwa mwaka huu, ulioandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Jijini Dar es Salaam.
Alisema hivi sasa sekta ya habari imekuwa, na kwamba utangazaji unabeba utaifa na uzalendo hivyo lugha zinazotumika kwa miaka ya sasa zimebadilika tofauti na ilivyokuwa zamani.
“Uhuru wa habari maana yake si upotoshaji, lugha, nidhamu ya utangazaji vimebadilika. Ukumbuke kuwa mtangazaji unapotangaza unajibeba mwenyewe pia unabeba taifa,” alisema Kipozi.
Aliongeza kuwa, hivi sasa watangazaji wengi wanaweza kutangaza lakini hawafikishi ujumbe uliokusudiwa tofauti na ilivyokuwa miaka ile ya zamani.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TCRA Profesa John Nkoma alisema kuwa mabadiliko makubwa ambayo yametokea katika karne hii ni utangazaji wa kutumia teknolojia ya kidijiti.
Na kwamba mfumo huo wa kidijiti umeleta mabadiliko makubwa kwenye maisha ya kila siku kwa sasa unaweza kupata matangazo ya televisheni mahali popote kwa kutumia vifaa mbalimbali kama vile kompyuta, simu za mkononi na kompyuta ndogo za mkononi kwa kupitia mfumo wa intaneti.
Aliongeza kuwa kwa kipindi c ha miaka 20 iliyopita sekta ya utangazaji imekuwa kwa kiwango cha haraka hadi kufikia mwaka huu kuna vituo vya televisheni 28 na redio 94.
mwisho

watumiaji wa simu kudhibitiwa

Na Mwandishi Wetu
WAZIRI wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia Profesa Makame Mbarawa ameagiza wataalamu  kutayarisha mwongozo kwa ajili ya kampuni za simu, utakaoelekeza jinsi ya kutuma meseji katika kipindi cha kuelekea uchaguzi mkuu mwakani.
Mbarawa alisema jana alipokuwa akifungua mkutano wa kuadhimisha siku ya  Teknolojia ya Habari na Mawasiliano ya Jumuiya ya Mawasiliano Afrika, Jijini Dar es Salaam, ulioandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
Waziri Mbarawa alisema, mwakani ni kipindi cha uchaguzi hivyo kuna baadhi ya watu wamekuwa wakitumia simu kutuma meseji ambazo zinaweza kuhatarisha usalama wa raia.
“Watu wanatuma meseji hizo, nimeshawaagiza wataalamu kutoka wizarani na TCRA kwa ajili ya kuandaa mwongozo huo kwa ajili ya kutuma meseji kwa sababu teknolojia imekuwa, watu wanaweza kuitumia vibaya,” alisema.
Vile vile alivitaka vyombo vya habari vitumike kuwaelimisha wananchi vizuri kuhusu masuala ya uchaguzi kwa kutahadharisha kuwa mwongozo walioupata usiwe kwenye makaratasi tu bali wautekeleze.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TCRA Profesa John Nkoma alisema kuwa, hivi sasa Tanzania imepiga hatua kubwa kwa kuwa wanaotumia kadi za simu ni milioni 28, mtandao wa mawasiliano ni milioni tisa ikiwa na pamoja na ukuaji wa huduma za simu ambazo zimewezesha kutuma na kupokea fedha.
Pia alisema serikali imewekeza dola milioni 200 katika mkongo wa taifa kwa ajili ya maboresho kwenye upande wa utangazaji.
mwisho

Chuo Kikuu chatoa zawadi kwa wanafunzi

Na Mwandishi Wetu
CHUO Kikuu Ardhi (ARU) kimewazawadia wanafuzi 130 wa masomo mbalimbali zawadi zenye thamani ya zaidi ya shilingi mil. 60 kutokana na ufaulu mzuri katika masomo yao.
Zawadi hizo ni fedha taslimu, mashine za upimaji ardhi na laptop katika hafla fupi iliyofanyika chuoni hapo Jijini Dar es Salaam.
Akikabidhi zawadi hizo, Makamu Mkuu wa chuo hicho Idrissa Mshoro alisema kuwa wanafunzi wa kike wameendelea kufanya vizuri katika masomo yao ambapo wamefikia wastani wa asilimia 40 dhidi ya asilimia 30 kwa wanaume.
Alisema miongoni mwa wanafunzi waliopata zawadi hizo hawakuwa na sifa za kujiunga katika chuo hicho mpaka walipopewa kozi fupi ambapo baada ya usaili walifaulu.
Profesa Mshoro alisema kuwa waliamua kuwa na mfumo huo baada ya kuona wanafunzi wengi wanataka kujiunga na chuo hicho kwa ajili ya elimu ya juu lakini alama zao walizopata katika shule walizokuwa wanasoma haziwawezesha kujiunga.
Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Taaluma chuoni hapo, Gabriel Kassenga alisema kuwa matokeo ya mwaka huu yameendelea kufuta dhana kuwa wanawake sio wazuri katika masomo ya sayansi.
“Wameonyesha uwezo mkubwa kwa kutwaa zawadi nyingi kuliko wanaume na hiyo ni dalili kuwa sayansi sio ya wanaume pekee” aisema na kuongeza kuwa hata mwaka jana wanawake waliongoza kwa kupata tuzo nyingi za kitaaluma kuliko wanaume.
Mwisho………………

ARU kudahili wanafunzi zaidi ya 7000

Na mwandishi wetu 
Chuo Kikuu Ardhi (ARU) kinatarajia kudahili wanafunzi 7700 ifikapo 2016/17.
Mwenyekiti wa Baraka la Chuo Kiki Ardhi Tabitha Siwale alisema hayo kwenye mahafali ya nane yaliyofanyika jijini Dar es Salaam. 
Alisema ili mpango huo utekelezwe chuo hakina budi kuongeza idadi ya wahadhiri na wafanyakazi wengine, kupanua miundombinu pamoja na kuongeza vifaa vya kujifunzia na kufundishia. 
"Chuo bado kinakabiliwa na changa moto mbalimbali zikiwemo idadi ya wahadhiri, uchakavu wa miundombinu, upungufu wa vyumba vya miha dhara, maabara, malazi kwa wanafunzi na nyumba za wafanyakazi, "alisema. 
Siwale alisema ili mpango huo utekelezwe zinahitajika shilingi bil 44 katika miaka mitatu ijayo. 
Kwa upande wake Makamu Mkuu Wa ARU, Profesa Idrissa Mshoro alisema kuwa katika mahafali hiyo wanafunzi 964 walihitimu ikilinganishwa na 483 wa mwaka jana. 
Alisema mafanikio hayo yanatokana na ongezeko la udahiliwa wanafunzi ambalo lilianza kukua kwa kasi zaidi mwaka 2010/11. 
Alisema ili kufikia malengo waliojiwekea mwaka wa masomo 2015/16 wanatarajia kuongeza udahili na kufikia 7741. 
Mwisho

NHC kutatua matatizo ya wananchi



Na Mwandishi Wetu
MKURUGENZI Mkuu wa Shirika la Nyumba  nchini (NHC), Nehemia Mchechu, amesema kuwa wanaiangalia miradi waliyonayo ni jinsi gani inaweza kutatua matatizo waliyonayo wananchi.
Mchechu alisema hayo jjijini Dar es Salaam, alipokuwa akizungumza katika mjadala ulioandaliwa na Chuo Kikuu Ardhi (ARU), wakati akiwasilisha mada yake.
Alisema NHC inaangalia ni jinsi gani watengeneze vitovu vya miji ambavyo kutakuwa na makazi ya watu, biashara mbalimbali pamoja na ofisi ili kumpunguzia mwananchi usumbufu wa kutembea muda mrefu.
“Je NHC katika miradi yao wanafanya nini ili wananchi waishi vizuri? Tunachoangalia miradi yetu tuliyonayo ni jinsi gani inaweza kutatua matatizo na kurahisisha huduma kwa wananchi,” alisema Mchechu.
Mchechu alisema kuna miradi Kawe ‘apartment’ iliyopo Dar es Salaam ambayo itawezesha watu kupata mahitaji yote kwa pamoja.
“Ukimfanya mtu akaishi na kufanya kazi karibu na ofisi, ataongeza kipato na kupunguza matumizi kwa kuwa hatasafiri tena mwendo mrefu kwa ajili ya kuwahi kazini, pia itafanya awe na afya bora kwa kupunguza msongo unaotokana na foleni,” alisema Mkurugenzi huyo.
Naye Profesa Lusugga Kironde ambaye anashughulika na masuala ya Maendeleo ya Ardhi na Uthamini (ARU),alisema kuwa siku hizi watu wanakuja mjini kuishi siyo kuondoka tofauti na zamani, hivyo wanaangalia masuala ya kazi, makazi na jinsi wanavyojitambua ili kuwezesha waishi vizuri.
Pia alishangazwa na kitendo cha kuvunja majengo ya zamani na kuwekwa mapya kwa kuwa kinadhoofisha fursa za utalii.
mwisho



 NHC kupunguza matatizo ya wananchi

Na Mwandishi Wetu
MKURUGENZI Mkuu wa Shirika la Nyumba  nchini (NHC), Nehemia Mchechu, amesema kuwa wanaiangalia miradi waliyonayo ni jinsi gani inaweza kutatua matatizo waliyonayo wananchi.
Mchechu alisema hayo jjijini Dar es Salaam, alipokuwa akizungumza katika mjadala ulioandaliwa na Chuo Kikuu Ardhi (ARU), wakati akiwasilisha mada yake.
Alisema NHC inaangalia ni jinsi gani watengeneze vitovu vya miji ambavyo kutakuwa na makazi ya watu, biashara mbalimbali pamoja na ofisi ili kumpunguzia mwananchi usumbufu wa kutembea muda mrefu.
“Je NHC katika miradi yao wanafanya nini ili wananchi waishi vizuri? Tunachoangalia miradi yetu tuliyonayo ni jinsi gani inaweza kutatua matatizo na kurahisisha huduma kwa wananchi,” alisema Mchechu.
Mchechu alisema kuna miradi Kawe ‘apartment’ iliyopo Dar es Salaam ambayo itawezesha watu kupata mahitaji yote kwa pamoja.
“Ukimfanya mtu akaishi na kufanya kazi karibu na ofisi, ataongeza kipato na kupunguza matumizi kwa kuwa hatasafiri tena mwendo mrefu kwa ajili ya kuwahi kazini, pia itafanya awe na afya bora kwa kupunguza msongo unaotokana na foleni,” alisema Mkurugenzi huyo.
Naye Profesa Lusugga Kironde ambaye anashughulika na masuala ya Maendeleo ya Ardhi na Uthamini (ARU),alisema kuwa siku hizi watu wanakuja mjini kuishi siyo kuondoka tofauti na zamani, hivyo wanaangalia masuala ya kazi, makazi na jinsi wanavyojitambua ili kuwezesha waishi vizuri.
Pia alishangazwa na kitendo cha kuvunja majengo ya zamani na kuwekwa mapya kwa kuwa kinadhoofisha fursa za utalii.
mwisho

Tuesday, October 28, 2014

TCRA KUTOA MWONGOZO KWA WATANGAZAJI KWENYE UCHAGUZI


MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imeandaa rasimu ya mwongozo utakaofuatwa na vituo vya utangazaji katika kipindi cha uchaguzi wa serikali za mitaa, wabunge na raisi lengo likiwa kuweka usawa na uwazi katika kipindi cha uchaguzi, wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi kufanyika.
Mwenyekiti wa Kamati ya Maudhui ya mamlaka hiyo Margaret Munyagi alisema hayo katika mkutano wa kupokea maoni ya wadau juu ya utaratibu wa kuandaa na kurusha vipindi vinavyohusu vyama vya siasa wakati wa uchaguzi.
Alisema kuingia kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa nchini 1993, kulienda sambamba na kuanzishwa kwa vituo binafsi vya utangazaji, hivyo ongezeko la vituo hivyo limekuwa ni kichocheo cha kukuza demokrasia, kuboresha amani, kudumisha umoja na mshikamano wa taifa.
“Kama mnavyojua nchi yetu inategemea kuingia kwenye kipindi cha uchaguzi wa serikali za mitaa, wabunge na rais ifikapo 2015. Uchaguzi ni mchakato muhimu sana katika kukuza na kuimarisha demokrasia ya n chi husika,” alisema.
Munyagi alisema kuwa, vipindi vinavyotangaza masuala ya uchaguzi vinahitaji umakini mkubwa pamoja na uwepo wa mizani katika muda wanaopewa vyama vya siasa, kuwepo kwa uwazi, kufuata sheria na kanuni husika.
Alisisitiza kuwa, kukamilika kwa mwongozo huo kutawasaidia watangazaji na waandaaji wa vipindi kuepuka kufanya makosa ambayo kama yasipodhibitiwa yanaweza kusababisha uchochezi na kuleta mifarakano miongoni mwa jamii.
Alisema, tofauti na mategemeo hayo baadhi ya vyombo vya utangazaji vimekuwa vikikiuka sheria na kanuni kwa kuwa maudhui yanayotangazwa hayazingatii maadili ya kitanzania badala yake vimechangia kuharibu utamaduni wetu.
Pia vingine vimesahau madhumuni ya kuanzishwa kwao na wajibu wao katika jamii, hivyo kujiingiza katika masuala ya uchochezi pamoja na uvunjifu wa amani na utulivu.
Awali Mkurugenzi wa Utangazaji TCRA, Habbi Gunze alisema kuwa mpaka sasa kuna vituo vya redio 95, pamoja na  vya televisheni 28 nchini, hivyo ni bora vikapata mwongozo maalum wa namna ya kuandika habari za uchaguzi.


mwisho

Friday, March 14, 2014

JENGA MAZINGIRA MAZURI KAZINI


 KUNA vitu mbalimbali ambavyo kiongozi au meneja anaweza kuvifanya ili kuweka mazingira ya kazi yako yawe katika hali nzuri na kujenga hali ya umoja, mshikamano na furaha miongoni mwa wafanyakazi.
 
Miongoni mwa vitu hivyo ni kiongozi au meneja huyo kujenga kuaminiwa na wale anaowaongoza. Kujenga uaminifu ni jambo muhimu kwa wale wote wanaomhusu katika eneo la kazi.
 
Kiongozi unatakiwa kuaminiwa kwa kile unachokizungumza kwamba utakifanya. Ni njia ya kuwaonyesha wafanyakazi kuwa kila unachokifanya ni kwa ukamilifu sio ubabaishaji, ni jukumu lako.
 
Pia kuwaonyesha wale unaowaongoza kuwa unatarajia kupata mambo kama hayo unayostahili kuwafanyia kutoka kwao.
 
Endapo maneno yako unayoyazungumza na tabia yako vinakwenda sambamba hapo utaaminiwa sana . Inaweza kuchukua muda fulani kwa wafanyakazi wako kuelewa kuwa, kile unachokizungumza ndicho unachokitenda.
 
Lakini kinyume cha hapo utaonekana kuwa mbabaishaji, kama maneno yako hayataendana na matendo yako hutaaminiwa. Siri ni kwamba, inachukua muda mrefu kujenga kuaminika lakini muda mfupi kuondoa uaminifu huo endapo utaenda tofauti na unayoyazungumza.
 
Pale unapoondoa uaminifu wako kwa wale unaowaongoza, itachukua muda mrefu kujenga kuaminiwa tena, pia kamwe hautaaminiwa kama ilivyokuwa mwanzo.
 
Kwa hiyo, ni muhimu yale unayoyazungumza ukayatendea kazi ili kuendelea kujenga uaminifu wako kwa wafanyakazi.
 
Hata kama uko katika mazingira ambayo siyo mazuri, kama wewe ni mwaminifu itarahisisha mambo katika utendaji wako. Kile unachokizungumza na kile unachokifanya kinakueleza wewe ni nani.
 
 
Hata kama hawatapendezwa na kile unachokisema. Kama utakizungumza kwa uaminifu, ukarimu  na umakini utaheshimika na kuaminiwa.
 
Uaminifu wa wafanyakazi wako utazingatia jinsi unavyojenga hali ya kujiamini na uwazi katika mazungumzo yako.
 
Pia wanataka kujua kama wanazungumza nawe kuhusu mambo muhimu au taarifa zitachukuliwa katika hali ya usiri mkubwa.
 
Siri ni jambo la muhimu katika mazingira ya kazi, haitakiwi kutoa siri ya mtu kw amwingine isipokuwa umeizungumza katika hali chanya.
 
Pia  matatizo mengine yanayowakuta wafanyakazi wako yanatakiwa yahifadhiwe kati yako na mwajiri pamoja na kiongozi wako, kama itawezekana.
 
Kiongozi mzuri hawezi kuzungumza mtazamo mbaya juu ya timu yake anayofanya nayo kazi.
 
Pia kiongozi mzuri anapaswa kuwasiliana kwa upole na uwazi na wafanyakazi wake. Ili kujenga mazingira mazuri kazini kila mfanyakazi anahitaji kuheshimiwa. Hili linafanyika kupitia kuwasikiliza kila mmoja na kumheshimu kwa kile anachozungumza.
 
Kwa kufanya hivyo unaonyesha kuwa unajali na kumheshimu kila mmoja. Jambo moja muhimu ni kuweka uwazi kwa wafanyakazi wako ili wawe huru nawe katika kuzungumza maono na malengo ya kampuni waliyonayo.
 
Baada ya kuwasikiliza wafanyakazi wako yale waliyonayo pia nawe chukua muda wa kuwaeleza maono na mipango uliyonayo. Eleza jinsi unavyoona jinsi ya kufanya kazi kama timu kwa kuwa kila mtu  ni sawa anastahili heshima, kuliko kufanya kazi kwa matabaka.
 
Kila mtu ni sawa kwa kuwa kila kazi ina umuhimu sawa katika kufanikisha maono ya kampuni. Pia zungumza nao kuhusu maadili, miiko ya kazi pamoja na uthamani wake.
 
Kuzungumza kuhusu maadili ya kazi kutaonyesha mfano wa matarajio unayotaka kuyaona katika utendaji wa wafanyakazi wako na tabia zao. Hiyo ni pamoja na kujivunia kazi unayoifanya, kumjali kila mmoja kutokana na utendaji wake, pia kutumia kazi yako kama njia mojawapo ya kuendelea kujifunza.
 
mwisho

Monday, March 3, 2014

WIVU HULETA MAFARAKANO KAZINI

Mafanikio huzaa mafanikio, lakini kwa bahati mbaya huleta wivu.

WAKATI unapokuwa na mafanikio katika kampuni ama eneo la kazi, unaweza kujikuta una marafiki wengi, pamoja na maadui wachache.

Hawa maadui mara nyingi wamekuwa wakijaribu kukuangusha ama kukufanya ushindwe katika kazi zako ama kukupa ushirikiano mdogo.

Wakati mwingine maadui hao huweza kutafuta namna ya kukukwamisha kwa kukufanyia visa mbalimbali ikiwemo wivu, fitina, ukorofi lengo likiwa ni kukukwamisha kimaendeleo na hata katika taaluma yako ama shughuli inayokukupatia kipato, pia wanaweza kukuwekea mitego ili ushindwe.

Hao wafanyakazi ambao wana wivu nawe au wasiopenda ufanikiwe katika kazi yako, ni rahisi kuwatambua kwa kukushusha thamani ama kukunenea maneno ya kushindwa kwa wengine na kukulinganisha na watu hata ambao hawana uwezo ulionao kuwa wapo juu yako kiutendaji ili mradi tu watimize lengo lao.

Kila utakachofanya kwa watu wa aina hii kwao kitakuwa ni gumzo, ama kukushusha thamani hata kama wakiwa wanaujua ukweli halisi juu yako kuhusu utendaji wako wa kazi.

Maadui wa aina hii hutumia fursa ya kuzungumza maneno mabaya au ya kukuvunja moyo pale utakapofanya kosa ama kushindwa jambo. Hawa ni hatari kwa kuwa wanajihesabia haki ama watenda mema wao wenyewe.

Jinsi ya kushughulika na watu wa aina hii katika eneo lako la kazi, kuna njia mbili. Njia ya kwanza ni kuwa kimya na kupuuzia kila wanalokufanyia na ya pili ni kuzungumzia jitihada zao kama zipo.

Katika mazingira kama hayo, inakubidi uwe jasiri na unayejiamini usimamie kile unachokiamini. Pia uwe mnyenyekevu katika kazi yako, toa kile ulichonacho kwa wengine kwa kuwafundisha mbinu mbalimbali za kuweza kufikia mafanikio.

Jitahidi kujiweka katika hali ya kawaida katika mazingira unayofanyia kazi, kuwa na amani na maadui zako, fanya mabadiliko ya kweli katika moyo wako.

Kutokana na umuhimu wa fani yako, epuka migogoro ama migongano isiyokuwa na lazima katika eneo lako la kazi.

Utakapofanya hivyo utapata heshima kutoka kwa wafanyakazi wengine.

Hata kama kwa upande wako umekosea katika eneo Fulani, ni wakati mzuri sasa wa kujirekebisha kutokana na makosa yaliyopita.

Kwa kufanya hivyo watu wataona mabadiliko yako, pia kuwa mtu wa kukubali kubadilika pale unapokosolewa.

Endapo utatambua kuwa wenzako ama msaidizi wako kazini hana furaha nawe, unaweza kuondoa ama kuzuia wivu wake kwako.

Inabidi kuwa mkimya, mtulivu lakini si kwa kiwango ambacho mchango wako utashindwa kuonekana.

Pia wapongeze wenzako katika mafanikio yao. Jitahidi kutokuwa na wivu, endapo nawe utakuwa na wivu kwa wengine, utakuwa huna tofauti na hao wenye wivu katika ofisi yako.

Kama utakuwa hauko imara kuondoa wivu miongoni mwa wafanyakazi, nawe utalazimika kuwa na tabia hiyo katika eneo lako la kazi.

Wakati wote uwapo katika eneo lako la kazi fanya kazi kwa bidii, simamia kile unachokiamini kamwe usijiingize katika makundi ya masengenyo ambayo yanatokea eneo ulilopo.

Kushughulika na watu wa aina hii mara nyingi inakuwa ni vigumu kwa kuwa, wako kwenye mazingira ambayo unataka kuyaepuka. Ni vizuri kufanya jitihada ili kuwa timu moja na kukatama mazingira ya wivu kwa kuwa hali hiyo ikiachwa italeta tatizo.

Mwisho.

Saturday, February 22, 2014

KWA NINI WATU WANAWAKATISHA TAMAA WENGINE?

FRANK John anasema, amekuwa akipata ujumbe mbalimbali kupitia simu ama barua pepe yake zikieleza kuwa kuna baadhi ya watu wamekuwa wakiwakatisha tamaa wengine wasifikie malengo ama mafanikio waliojiwekea.
 
Anasema sababu aliyoipata wakati anasoma ujumbe hizo ni kwamba baadhi ya wale wanaokatishwa tamaa wanawaamini hao wanaowakatisha tamaa.
 
Si vibaya kuwazungumzia hao wanaokukatisha tamaa, lakini pale unapoanza kujiuliza maswali baada ya kuzungumza nao jua kwamba uko kwenye hatari kubwa.
 
Njia inayoweza kukusaidia ambayo haitakudhuru kutokana na watu wa aina hiyo ni kutaka ujue kwa nini watu wanawavunja moyo ama kuwakatisha tamaa wengine.
 
Zipo sababu zinazowafanya baadhi ya watu kuwakatisha tamaa wengine.
 
Kwanza watu hao hawawezi kufanya mambo unayotaka kuyafanya., mfano “ Kama ninaamini kuwa siwezi kufanikiwa lakini ninafikiri kuwa wengine wana bahati hiyo, ndiyo maana ninapokutana na mtu ninayeamini anamafanikio ninaanza kumvunja moyo ama kumkatisha tamaa kutokana na imani yangu potofu,”.
 
Pili mtu wa aina hiyo anatishiwa na wewe kwa kila unachokifanya hata kama ni cha kawaida ambacho kama angejaribu kukifanya naye angefanikiwa.
 
Baadhi ya watu wanahisi kushindwa kufanya jambo pale wanapomwona mtu anajaribu kufanya kitu fulani. Kama wakati wote mtu fulani anataka kuwa tajiri lakini hajishughulishi kufanya shughuli binafsi, huhisi kutishika pale anapoona wewe unachukua hatua ya kuanza jambo la mafanikio.
 
Kutokana na hali hiyo, mtu wa aina hiyo hujaribu kukukatisha tamaa ili usiweze kuwa bora kumzidi yeye.
 
Sababu nyingine mtu wa aina hiyo anakuwa na wivu. Amini ama usiamini. Rafiki yako wa karibu anaweza kujaribu kukuvunja moyo kutokana na wivu alionao kwako. Kama anajihisi ni mnyonge kwako kwa jambo fulani ama kuna mambo unayoyafanya ambayo yeye hawezi kuyafikia hujaribu kukurudisha nyuma kutokana na wivu alionao.
 
Jambo jingine ni woga. Kuna mtu mmoja alitaka kuchapisha kitabu chake cha kwanza , hivyo alimwendea mshapishaji kwa makubaliano maalum kuwa atammalizia fedha zake atakapokiuza kitabu kile, lakini mshapishaji yule alimvunja moyo kuwa huchapisha vitabu vya siasa tu kwa kuwa ndivyo vina biashara. Lakini baadaye mtu huyo aliweza kuchapisha vitabu hivyo na kwa haraka alifanikiwa kuuza zaidi ya nakala milioni moja.
 
Anasema aligundua kuwa, mchapishaji yule aliogopa kupata hasara kwa sababu alimwona kuwa ni kijana, pia alidhamiria kumuangusha asisonge mbele.
 
Sababu nyingine ni kuchukiwa. Kama mtu anakuchukia hataki kukuona ukiendelea katika jambo lolote na ndio maana atajaribu kukuvunja moyo pale anapopata nafasi. Kuwa makini na maadui wa aina hiyo.
 
Vile vile watu wa aina hiyo hawakupi taarifa sahihi. Watu wengi wanapenda kusema ‘sijui’ wanapoulizwa jambo fulani. Wanakuwa hawana elimu muhimu kuhusu kile unachokipanga kukifanya hivyo kurudisha nyuma kwa kusema hawajui.
 
Jambo lingine ni kwamba watu wa aina hii hawawezi kuiona picha halisi uliyonayo juu ya mipango yako. Baadhi yao watakukatisha tamaa kwa kuwa tu hawaelewi picha unayoipanga katika maisha yako.
 
Sasa basi ni jinsi gani unaweza kuwazuia watu wasikukatishe tamaa.
Kuna mambo mawili unahitaji kuyafanya ili kuzuia hali hiyo. jambo la kwanza ni kutokuzungumza kuhusu mipango yako isipokuwa kwa mtu yule ambaye unadhani kuwa anakupenda kwa dhati. Kama utafanya kinyume na hapo utakuwa ukivunjwa moyo na watu wa aina hiyo kila mara.
 
Jambo la pili ni kuonyesha kuwa jambo ulilokusudia kulifanya unalishikilia hilo hilo mpaka linafikia mwisho na mafaniko yake unayaona. Kutokana na sababu hiyo wale wanaokurudisha nyuma wataanza kukuamini na kile unachokisimamia ni sahihi.
 
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa mtandao.
 
mwisho

Twitter Facebook