Sunday, December 27, 2009

KUBALI TATIZO LAKO ULITATUE

MPENZI msomaji, nakukaribisha tena katika safu hii ya Maisha Yetu. Leo tutaangalia njia mbalimbali za kukusaidia unapopatwa na matatizo.
Mara nyingi mtu anapopatwa na matatizo hubabaika na kujikuta hana msaada wowote.
Mtu huyo huwa anashindwa kujikubali kama yupo salama na lipo tumaini jipya baada ya matatizo hayo anayokabiliana nayo.
Ni watu wachache wanaojikubali kuwa wana matatizo na kutafuta njia ya kukabiliana nayo.
Wengi walio na misukosuko hukosa furaha na kujiona kuwa ni wanyonge, waliokataliwa na jamii inayowazunguka.
Hali hiyo huwafanya afya zao kuzorota na kukabiliwa na magonjwa mbalimbali kama ya moyo na vidonda vya tumbo.
Kutokana na hali hiyo inayomkabili mtu huyo, jamii, ndugu na hata marafiki zake huwa mbali naye na kuacha kutoa ushirikiano wa karibu kwake.
Ni vizuri kuelewa kuwa, kila mmoja wetu ana matatizo, hivyo njia ya kuyatatua anayo yeye mwenyewe.
Unaporuhusu hali ya kukata tamaa kujengeka katika maisha yako, ndipo unapoona kuwa matatizo hayatatuliki na ni mzigo mkubwa usiobebeka.
Pili inakupasa kujua kuwa, matatizo ni kitu kisichoepukika katika maisha, japo yanaumiza sana kwa wakati huo.
Lakini faida yake ni kwamba yanakujenga sana imani yako na hata kuwajua watu wa kweli kwako, iwe ndugu ama marafiki.
Na huu ndiyo wakati muafaka wa kujenga maisha yako na kuimarisha ujasiri. Hakuna mtu mwenye akili na jasiri kama mtu mwenye matatizo, kwani fikra zake siku zote ni kutatua hali hiyo inayomkabili. Wakati wale wasio na matatizo hujibweteka kiakili hata kiafya.
Tatu, ni vema kuelewa kuwa njia ya kutatua matatizo yako unayo mwenyewe na lipo tumaini.
Hetu tuangalie mfano wa mtu anayekabiliwa na matatizo ya kuuguliwa na mtoto, baba mzazi na wakati huo huo anakuwa na madeni yaliyomwelemea na kumfanya ashindwe kuelewa anaanzia wapi.
Kumbuka kipindi kama hiki wapo baadhi ya ndugu na marafiki wanaokucheka, wakisubiri waone mwisho wa kushindwa kwako.
Njia sahihi za kufuata ni kuepuka sana kuwa karibu na watu kama hao. Kama unadaiwa na unakwenda kumueleza mtu asiye na madeni akusaidie shida yako, hatakuwa na moyo, atakucheka na wengine hufika mbali kwa kukutangaza.
Ni vizuri ukawa na watu walio na utayari wa kukusaidia, pata muda mzuri wa kupumzika ukiwa peke yako ili uwe na akili tulivu, utafakari uanze na tatizo lipi ili kukabiliana na hali uliyo nayo.
Si vizuri kumwambia kila mtu matatizo yako, kwani walio wengi hawawezi kukuzungumzia mambo mema kwa kuwa midomo yao imejaa hila.
Uwaone viongozi wako wa dini kwa ajili ya ushauri zaidi.
Pia kila unapokutana na watu wa aina mbalimbali jifunze kuongea nao vizuri na penda kuongelea zaidi mafanikio yako kuliko matatizo.
Hii inasaidia wale wasiopenda mafanikio yako, wasijue undani wako ulivyo.
Siku zote za maisha yako uwe na ndoto za mafanikio, hii itakufanya siku moja uketi pamoja na wakuu wa nchi. Kubali kupokea baraka kutoka kwa wengine na uwe mtu wa shukrani. Hiyo ni siri tosha ya kuondoa matatizo.
Tumia muda wako vizuri kupanga mambo ya kimaendeleo. Pia fanya mazoezi ya viungo na si kunywa pombe ukidhani kuwa utatuliza mawazo.
Kumbuka watu waliokabiliana na matatizo makubwa ndio walioweza kufikia mafanikio makubwa kiroho, kiuchumi na kisiasa, kwa kuwa wanazikubali changamoto katika maisha.

USIKUBALI KUKATISHWA TAMAA

MSOMAJI, katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi. Leo tutaangalia jinsi ya kutokufuata mawazo ya wale wanaotaka kukurudisha nyuma kimaendeleo.
Miongoni mwa jamii tunazoishi, huwa kuna baadhi ya watu ambao hufurahia wenzao wanaposhindwa kutimiza malengo waliojiwekea.
Ama huwa na tabia ya kuwakatisha tamaa wanaopenda kujikwamua kutoka katika hatua moja na kuelekea hatua nyingine.
Watu hao mara zote huwakatisha tamaa wenzao kwa jambo fulani, kwa kuwaambia kuwa, wasijaribu kulifanya kwa kuwa hawatafanikiwa.
Kumbe watu hao, ilitakiwa kuwatia moyo wale wanaotaka kujikwamua kiuchumi kwa kuwaambia kuwa, wajaribu kufanya jambo walilolikusudia.
“Mawazo ya watu kama hao wasiopenda mafanikio ya wengine mara zote ni sumu ya maendeleo”.
Hivyo unapokutana na watu kama hao, unachotakiwa kukifanya, ni kujiwekea mazingira ya kujikinga pale wanapokujia na kutaka kukulisha sumu hiyo.
Lakini kwa upande mwingine, wewe unayependa kupiga hatua kimaisha, unaweza kuyapokea mawazo ya wale wanaowakatisha tamaa wenzao, kama ni njia mojawapo ya kukutoa hapo ulipo na kupiga hatua zaidi.
Kamwe usiruhusu watu hao wasiopenda maendeleo yako kukukatisha tamaa kiasi cha kuharibu ratiba na mipango yako ya kimaendeleo uliyojiwekea.
Kwa kuwa, watu wa namna hiyo wapo kila mahali, na kazi yao ni kuharibu mipango mizuri ya maendeleo ya wengine.
Huweza kutumia wengine kuyabeza mafanikio yako, kukucheka, na pengine huweza kukukopa baadhi ya bidhaa zako na kukuletea usumbufu katika malipo, ili mradi wewe uchukie na kuamua kuacha kufanya biashara uliyoianza.
Hizo ni changamoto zilizopo katika maisha yetu ya kila siku cha msingi, ni kusonga mbele na kufanya kile ulichokusudia bila kuangalia wengine wanasemaje juu yako ya kukurudisha nyuma.
Wapinzani wa maendeleo ya wengine wapo kila mahali. Wengi wao ni wavivu hivyo wanashindwa kukabiliana na ugumu wa maisha, hupenda kuwakatisha tamaa wengine ambao wamekuwa wakikabiliana na changamoto mbalimbali katika kufikia mafanikio wanayoyataka.
Usifanye makosa katika malengo yako. Kwa kuwa hata katika eneo lako la kazi, iwe ni ofisini ama kwenye biashara wapo wanaokukatisha tamaa ya kuendelea na mipango yako.
Kwa kuwa, katika hali halisi tumetofautiana kifikra na kimaendeleo. Miongoni mwetu wapo wale wenye mipango ya kupenda kupiga hatua kila wakati za kimaisha, na wapo wale ambao hupenda kuangalia wengine wanafanya nini na kuwabeza.
Katika hilo, usikate tamaa. Piga hatua zaidi katika kufanikisha malengo yako kwa kuwa na mkakati wa kujiwekea kanuni ya kutafuta ushauri kutoka kwa watu wenye mafanikio zaidi yako.
Ukijijengea tabia ya kuuliza maswali pale unaposhindwa, ni sawa na kutibu ugonjwa wa kansa unaokusumbua.
Vile vile ujue kuwa, katika maisha mafanikio yako pia yanategemea msaada wa kimawazo kutoka kwa wengine.
Huwezi ukawa na mipango yako mwenyewe na mawazo yako mwenyewe ukafanikiwa bila kuomba ushauri kwa wengine walio mbali zaidi yako kimaendeleo, wale unaoweza kuonana nao na kuongea nao bila matatizo.
Changamoto za mafanikioKufanya kazi kwa bidii kunaleta mafanikio. Bila kufanya kazi kwa bidii ni vigumu kupata mafanikio katika maisha.
Njia mojawapo ya kufikia mafanikio hayo ni kuainisha malengo yako unayotaka kuyafikia.
Tukutane Alhamisi ijayo.

IMANI HULETA MAFANIKIO

NAKUKARIBISHA, katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, zinazokujia kila Alhamisi.
Ili kuwa mtu wa mafanikio ni vema kutumia mbinu ya kufikiri kwa ubunifu kile unachotaka kukifanya.
Ni vizuri kuwa na imani, unaweza kufanya jambo lako na likafanikiwa, kwani unapoamini litafanikiwa, akili yako itazidi kutafuta njia ya kulifanikisha zaidi.
Kuamini kuwa unaweza kufanya jambo kubwa, kunafungua njia ya mafanikio. Kamwe usiseme ama kufikiri kuwa huwezi kufanya jambo fulani katika maisha yako, badala yake, jaribu kufanya kile unachofikiri kuwa huwezi.
Usiruhusu mambo ya mila na desturi ama utamaduni uliouzoea kutawala akili yako.
Kuwa mtu wa kupokea mambo na mawazo mapya kila wakati, kisha uyafanyie kazi.
Kila wakati jaribu njia mpya katika kufanikisha mambo yako, pamoja na kuwa mfuatiliaji wa shughuli zako unazozifanya.
Iulize nafsi yako, inakupasa kufanya nini ili kuweza kufanya vizuri zaidi? Wakati unajiuliza swali hilo, unakuwa tayari umeshapata jibu, cha msingi ni kulifanyia kazi jibu hilo ulilolipata bila kuchelewa.
Pia jiulize ni kwa vipi unaweza kufanya vizuri zaidi? Pia ni vema ukawa na mazoea ya kusikiliza na kuuliza kwa wengine, kuhusu mambo unayotaka kuyafanya kwani utapata mawazo mengi usiyoyajua kutoka kwa wengine.
Yapanue mawazo yako, kwa kujichanganya na watu mbalimbali wakiwamo wenye ujuzi wanaoweza kukupa mawazo na njia mpya za kufanya mambo.
Moja ya kanuni ya mtu anayependa au mwenye mafanikio ni kuwa na muonekano mzuri mbele ya jamii, kuanzia anavyozungumza hadi mavazi yake.
Unaweza usikubaliane nami, lakini ukweli ni kuwa, kama wewe ni mfanyabiashara wa nguo, jinsi unavyokuwa mtanashati mbele za watu, ndivyo watakavyopenda kuja katika duka lako na kununua bidhaa zako hizo.
Lakini, kama utakuwa haujijali kwa upande wa mavazi, halafu ukawa mfanyabiashara wa bidhaa hiyo, utapata wateja wale wasiokujua na wanaokujua wachache.
Utanashati unavutia biashara yako, si tu kwa biashara ya nguo, bali hata katika shughuli zako nyingine unazozifanya, uwe ni mwanasheria, mwalimu ama mpishi wa chakula, vile unavyoonekana ndivyo unavyozidi kuimarisha biashara yako.
Kumbuka watu wanakutathmini kutokana na muonekana ulio nao.
Hebu tuangalie mfano huu kuwa, mtu anafanya biashara ya nyanya, anazipanga mafungu mafungu na kuziuza.
Mwingine anafanya biashara hiyo hiyo, na kuziweka nyanya zile katika mfuko wenye kuonyesha bidhaa iliyopo ndani yake na kufunga vizuri.
Biashara hizo zikiwa katika eneo moja, watu wengi watanunua zile zilizofungwa vizuri kwenye mfuko wakiamini kuwa ni salama zaidi.
Mfano huo ni sawa na muonekana ama utanashati wako kwa watu katika shughuli yoyote ile unayoifanya.
Uvaaji mzuri na wa heshima kwenye jamii, unakufanya uheshimike na kuaminika kuwa unaweza kufanya mambo makubwa unayoyapanga.
Ni vizuri kuboresha mawazo yako kila siku, kama watu maarufu wanavyokuwa.
Kuboresha mawazo, kufikiri na utendaji wako kutakuletea mafanikio katika mipango yako yote.
Hivyo ni vema, kula vizuri ili uweze kufikiri vizuri katika mambo unayoyafanya.
Endapo hautakula mlo kamili, akili yako haitakuwa na uwezo wa kufikiri vizuri, utabakia kuwa mtu wa kushindwa.
Kama mtu anakula vizuri, anajilinda na magonjwa mbalimbali, mwili wake unakuwa na afya pamoja na akili yake kuwaza mambo makubwa.
Akili yako huwezi kuilisha chakula unachokula, bali chakula chake ni mazingira yanayokuzunguka.
Mtu yeyote anayetembea katika nchi ama mikoa mbalimbali, huwa na mazingira ya tofauti, kila anapokwenda hujifunza kitu kitakachomsaidia.
Mazingira ya eneo ulilopo yanaifanya akili yako ifikiri zaidi ufanye kitu gani cha mafanikio katika eneo hilo ulilopo kitachokupatia maendeleo.
Ukubwa wa jinsi unavyowaza, malengo yako, mazingira yako au vile unavyoonekana, ni kutokana na mazingira uliyopo.
Unapokuwa na watu wenye mawazo ya kuchelewa kufanikisha mambo, nawe utakuwa mtu wa kuchelewa kufikia malengo uliyojiwekea.
Kwa maana nyingine, kushirikiana na watu wenye mawazo makubwa kunakufanya uwaze mambo makubwa ya maendeleo.
Pia kukaa karibu na watu wenye malengo ama maono ya mafanikio, kunakufanya nawe uwe katika hali hiyo.
Katika jamii tunayoishi, kumekuwa na watu wenye tabia zilizogawanyika katika makundi matatu.
Kundi la kwanza, ni la watu wale ambao wameona kuwa hawawezi kufanya jambo likafanikiwa kabisa.
Wamekuwa na ujuzi na kukubali ujuzi huo katika eneo moja, yaani wameridhika na hali hiyo.
Kama, Mungu amekupa ujuzi wako mzuri na ukabahatika kupata kazi sehemu nzuri, pamoja na kufanya kazi ile, utumie ujuzi wako katika maeneo mengine.
Unaweza kufungua ofisi yako na kuanzisha kitu chako mwenyewe huku ukiendelea na kazi yako.
Kamwe usijikatishe tamaa kwa kuona kuwa huwezi kufanya hivyo, kudhani kuwa, wewe umeumbwa kwa ajili ya kufanya kazi za wengine tu.
Kuna watu wenye malengo makubwa na waliopanga kuyatimiza lakini kutokana na ushindani uliopo hufika mahali na kushindwa kuendelea na mikakati waliyojiwekea.
Tunaweza kusema, wamekata tamaa na kuacha kuyafanyia kazi malengo yao, mwishoni hupoteza mwelekeo kabisa.
Kundi hili, wamejijengea tabia ya hofu, hofu ya kushindwa kutimiza malengo yao, hofu ya ulinzi, hofu katika jamii inayomzunguka na kupoteza kila wanalicho nacho.
Kundi la watu hawa, kamwe hawatafanikiwa kwani wameshajiweka kwenye kundi la kushindwa ingawa lina watu wenye akili, vipaji walivyojaliwa na Mwenyezi Mungu.
Kundi la tatu ni la watu wale ambao hawako tayari kukatishwa tamaa, hawa ni asilimia ndogo sana katika jamii.
Kundi hili pamoja na kukatishwa tamaa, katika mipango yao, wamekuwa wakijitahidi kufanya jitihada mbalimbali ili wajikwamue katika hali hiyo waliyonayo na kuwa katika hatua nyingine.
Mara zote hupumua mafanikio katika maisha yao. Kundi hili pia lina furaha kwa kuwa limeshakamilisha baadhi ya malengo waliyojiwekea.
Wamekuwa wakipitia changamoto mbalimbali, lakini wamezishinda, wamekuwa wakiangalia siku mpya ikianza na jambo jipya.
Ni ukweli usiopingika kuwa, kila mmoja wetu anapenda kuwa katika kundi la tatu, ambalo kila mwaka wanapata mafanikio, wanaofanya mambo mbalimbali na matokeo yake yanaonekana.
Tukutane Alhamisi ijayo.
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa kitabu cha 'The Magic of Thinking Big,’ kilichotungwa na David Schwartz pamoja na mitandao mbalimbali.

BUNI NJIA ZA MAFANIKIO

MSOMAJI wangu, katika mfululizo wa makala hii ya maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi.
Leo tutaangalia ujasiri unavyomfanya mtu kubuni njia mbalimbali za mafanikio.
Kila mmoja anapenda kuwa na mafanikio katika maisha yake, lakini mafanikio hayaji tu bila kufanya juhudi ama jitihada za dhati.
Mojawapo ya njia inayoweza kukutoa hapo ulipo na kukupeleka katika hatua nyingine nzuri zaidi ni ubunifu.
Mtu yeyote anayependa kuwa na mafanikio maishani, inambidi awe mbunifu katika nyanja mbalimbali ili kama yeye ni mfanyabiashara aweze kuteka soko kubwa.
Unaweza kuwa mbunifu katika fani yoyote ile uliyonayo, ama kipaji ulichopewa na Mungu, kitakachokufanya uwe mtu tofauti katika maisha yako.
Kama wewe ni mwalimu ambaye ni mbunifu wa kufundisha, maisha yako yatakuwa mazuri kwa sababu utasifika kwenye shule yako na sifa zako zitafika mbali hadi shule nyingine.
Hali hiyo itakufanya utafutwe na shule nyingi, hivyo ni uamuzi wako kuchagua uende wapi.
Ama utatafutwa na wanafunzi kutoka shule mbalimbali uweze kuwasaidia katika masomo yao ili waweze kufaulu mtihani, hapo wewe si yule wa zamani bali umekuwa mtu mwingine wa tofauti, kutokana na ubunifu wako.
Kama wewe, una ofisi ya ushonaji na ukawa mbunifu mzuri wa mavazi, sifa zako zitafika mbali zaidi na watu wengi watakutafuta kwa ajili ya kuwabunia mavazi yao.
Tayari utakuwa umeshajijengea jina, cha msingi ni kuongeza jitihada ili wale wateja wako usiwapoteze.
Kama wewe ni mbunifu wa kupika chakula ama vitafunwa mbalimbali, utajulikana mtaani, kwenye ofisi ama kampuni mbalimbali na hata kutafutwa na watu kwa ajili ya shughuli zao za sherehe.
Hiyo ni mifano michache sana, ambayo unaweza kujifunza. Si hiyo tu, bali unaweza kutumia uhandisi wako kwa kujenga nyumba nzuri, ukatumia uandishi wako kwa kuandika habari nzuri, ukatumia udaktari wako kutoa ushauri na kutibu vizuri wagonjwa unaowaoona.
Tumia akili yako uliyopewa na Mungu, kwa kuwa mbunifu ili uweze kuwa na maisha mazuri.
Binafsi ninaamini kuwa kila mmoja Mungu amempa kipaji ama akili kwa ajili ya kuwa mbunifu.
Tatizo lililopo kwa watu wengi ni kukata tamaa. Wengi wamekuwa wakikatishwa tamaa na ndugu, jamaa ama marafiki zao.
Na mara nyingi, wanaweza kufanya jambo na lisifanikiwe kama walivyofikiri matokeo yake, badala ya kutafuta ufumbuzi kwa nini hali hiyo imetokea, hukata tamaa na kuamini kuwa hawezi kufanya jambo lolote likafanikiwa labda aajiriwe tu.
Inabidi tubadilike kimtazamo, kiakili na kifikra ili kila mmoja afurahie maisha yake aliyopangiwa na Mwenyezi Mungu hapa duniani.
Hivyo, endapo unaamini jambo fulani haliwezekani, ndivyo itakavyokuwa.
Lakini endapo unaamini kuwa jambo fulani linawezekana, akili yako italifanyia kazi na kutafuta njia ya kulifanikisha.
Kuamini kuwa unaweza kufanya jambo, kunakufungulia milango zaidi ya kuwa mbunifu katika shughuli na maisha yako.
Akili yako, itafungua njia ya mafanikio kama utaitumia vema.
Na pia, kama unataka kuona njia ya kukutoa hapo ulipo, ondoa ukuta wa kuona kuwa haiwezekani, ndipo mafanikio yako yatakapoonekana.
Mafanikio makubwa yanakwenda kwa mtu anayefikiri kuwa na maisha ya viwango kwa ajili yake na wengine.
Ni vizuri pia kuboresha biashara zako ama shughuli zako unazozifanya kwa ajili ya kukupatia riziki, ili wengine waweze kufurahia huduma zako na kukutafuta.
Pia unaweza kujijengea tabia ya kuwa na mazoea ya kufikiri mbinu mbalimbali za maendeleo kwa dakika 10 kila siku, kabla hujaanza kazi yoyote.
Zoezi hilo, ni rahisi na kama utalizingatia utaona matokeo yake mazuri, ni vema kulizingatia.
Kwa upande mwingine, utagundua kuwa, watu wote waliofanikiwa, hupenda kujishughulisha, si wavivu.
Penda kujiuliza unatakiwa kufanya nini ili uzalishe zaidi? Ama uwe na maisha bora zaidi? Majibu ya maswali hayo ndiyo yatakayokufanya uongeze bidii zaidi.
Na kwamba, ili uweze kuzalisha kitu chochote, unatakiwa uwe na malighafi.
Katika kufikia uamuzi makini, malighafi ni mawazo na mapendekezo ya watu wengine.
Kuwa makini, usipende sana kuhitimisha jambo lako, kwa mawazo ya wengine. Kwani mawazo ya wengine yanakusaidia kuchekecha mawazo yako mwenyewe kwa kuwa akili yako ina ubunifu.
Ili ufanikiwe katika kampuni yako ama kiwanda chako, inakupasa ufanye utafiti wa kujua ubora wa bidhaa zako kwa wengine.
Uliza maswali kuhusu ubora wa bidhaa zako, ukubwa wake, bei yake ama mwonekano wake kwa jamii uko vipi ili uweze kufanya maboresho pale inapotakiwa.
Kuwasikiliza wengine, kunakufanya kukuwezesha kuboresha pale penye upungufu.
Tukutane wiki ijayo.
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa kitabu cha ‘The Magic of Thinking Big’, kilichotungwa na David Schwartz pamoja na mitandao mbalimbali.

JINSI YA KUPANGA MALENGO YAKO

MSOMAJI wangu, nakukaribisha tena katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, zinzokujia kila Alhamisi.
Leo tutaangalia jinsi unavyoweza kupanga malengo makubwa katika maisha yako.
Watu wengi hushindwa kufikia malengo makubwa kwa kuwa, mara zote hujikatisha tamaa kuwa hawawezi kufanya jambo kubwa la kimaendeleo, kabla ya kujaribu kulifanya.
Tabia ya baadhi ya watu hao wanaokuwa na malengo madogo katika mazingira wanayoishi, ina maanisha eneo hilo hakuna ushindani wa kimaendeleo, ama wao wenyewe hawana jitihada za dhati za kupiga hatua zaidi mbele.
Lakini ikimbukwe kuwa, katika kutafuta mafanikio hayo ili uwe na maisha bora, usimwangalie mtu jinsi alivyo, kwamba ana urefu gani, ana pesa kiasi gani, digrii aliyonayo ama kuangalia historia ya maisha yake, bali hupimwa kwa uwezo wa kufikiri kwake.
Watu wengi wanaofikiria kuwa na malengo makubwa ya mafanikio, katika maisha yao ni kutokana na matarajio waliyonayo.
Inakupasa kila mara ujitahidi kupanua mawazo yako na kubuni mbinu mpya za kukutoa hapo ulipo na kukuweka katika hatua nyingine nzuri zaidi kimaendeleo.
Hivyo utambue kuwa, unapotaka kufanya mambo makubwa inakupasa ujijue wewe ni nani na una thamani gani.
Kwa maelezo mengine usijishushe hadhi yako kwa kuona kuwa huwezi kufanya mambo makubwa ya kimaendeleo ambayo yatakutoa hapo ulipo na kukuweka katika hatua nyingine nzuri zaidi.
Tuangalie mfano wa kijana mmoja aliyeshindwa kupiga hatua mbele baada ya kujishusha hadhi yake na kujiona hawezi.
Kijana huyo, aliona tangazo la kazi katika gazeti. Kazi aliyokuwa anapenda kuifanya na pia ameisomea.
Lakini hakufanya jitihada za dhati za kuomba nafasi ile, kwa kuwa alijiona hawezi kuipata hata kama angeomba.
Aliona kuliko ajitaabishe ni heri aache kuomba nafasi hiyo. Mfano huo si mzuri kwa mtu anayetaka kupiga hatua kimaisha.
Usijishushe hadhi yako ama usikatishwe tamaa kwa hali yoyote ile. Ni vema kujaribu kile unachokipenda na unachokihitaji katika maisha yako, kuliko kuacha kujaribu kwa kuogopa kuwa hautafanikiwa.
Kwani matokeo huja baadaye, hata utakaposhindwa, utakuwa na nguvu ya kujaribu tena sehemu nyingine.
Wengi wetu, tumekuwa tukijikatisha tamaa katika shughuli mbalimbali tuzifanyazo ama tunazotaka kuzifanya.
Yawezekana umeanzisha biashara kwa lengo la kukuinua kiuchumi, lakini matokeo yake, biashara hiyo haiendi kama vile ulivyotarajia.
Jambo la msingi, inakupasa kukaa chini na kujitathmini, kuangalia ni sehemu gani unayokosea.
Ama kuangalia, kama una washindani wengi katika eneo hilo, ili uweze kufanya vizuri zaidi yao, kwa kuweka vitu vingi tofauti na kuboresha eneo la biashara yako.
Kuwa mbunifu katika biashara yako kutakupa wateja wengi, na utafanikiwa zaidi. Cha msingi usikate tamaa katika kufikia malengo unayoyakusudia.
Kutokana na hali ya kujikatisha tamaa, miongoni mwa watu wengi, wanasaikolojia mbalimbali wamekuwa wakishauri ni vema, watu wajijue vile walivyo ili waweze kujirekebisha pale penye upungufu na kusonga mbele kimaisha.
Hali ya kujikatisha tamaa ni mbaya sana, ni sawa na ugonjwa usiopona katika mwili wako. Ili kuutibu ugonjwa huo, inakupasa ujielewe wewe ni nani, na una upungufu gani, pamoja na kukubali mabadiliko.
Tatizo kubwa lililopo kwa watu wengi, hawajui kuwa, wao wana uwezo mkubwa tofauti na wanavyojifikiria.
Hivyo ni vema kuweka mawazo yako kwenye kipimo halisi, uyachuje na kuchukua yale yaliyo na thamani.
Penda kufikiri mambo makubwa. Usijishushe hadhi yako kwa kujiwekea au kufikiri malengo madogo. Anza sasa kuwaza mambo makubwa ili uwe mtu mwenye ndoto njema ya maendeleo.
Kutokana na hali hiyo ya watu kujikatisha tamaa, wale ambao wamewahi kufanya biashara na kufilisika, wengi wao wamekuwa wakisema kuwa hawatarudia tena kufanya biashara hiyo.
Lakini kumbe, haikuwapasa kukata tamaa, bali kujipa moyo, na kuelewa kuwa pamoja na hali hiyo ya kushindwa inawapasa kujaribu tena.
Kamwe usikate tamaa katika jambo lolote unaloliwaza ama kulifanya. Kwa kuwa, upo msemo mmoja unaosema, penye nia pana njia.
Tukutane wiki ijayo.
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa kitabu cha ‘The Magic of Thinking Big’, kilichotungwa na David Schwartz pamoja na mitandao mbalimbali.

ONDOA HOFU, KUWA JASIRI

KARIBU msomaji wa safu hii ya maisha yetu inayokujia kila siku ya Alhamisi.
Leo tutaangalia jinsi ya kuwa na ujasiri na kuondoa hofu katika maisha yako.
Hofu si jambo zuri katika maisha, lakini ni ukweli usiopingika kuwa, kila mtu hupatwa na hofu kutokana na jambo fulani analokutana nalo.
Hofu hiyo hukaa nayo kwa dakika chache kabla ya kutoweka. Lakini wapo wengine hukaa nayo kwa siku nzima. Kutegemea ni jinsi gani unavyoidhibiti hofu hiyo.
Watu wengi hukabiliwa na hali ya wasiwasi, kutokutulia, kudharauliwa, kuchanganyikiwa au mambo yake kutokuwa katika mpangilio mzuri, pamoja na kuwa na mawazo hasi.
Hali hiyo, isipodhibitiwa kwa haraka huleta usumbufu katika maisha yake. Hivyo ni vema kujijengea hali ya ujasiri na kuondoa hofu, katika jambo lolote lile unalolifanya.
Kwa mfano, kama umeamua kulima ekari tano, utimize lengo lako, usiwe tayari kukatishwa tamaa na maneno kutoka kwa wengine, kuwa hakutakuwa na mvua, ama ardhi haina rutuba nzuri, ng’ang’ana pale ulipojiwekea malengo yako.
Ama umedhamiria kufungua duka eneo fulani, wapo watakaokuunga mkono, pia wapo watakaokukatisha tamaa, cha msingi, fanya kile ulichokusudia kukifanya, mradi kiko kwenye mpangilio wako na umekifanyia maandalizi ya kutosha.
Fahamu kuwa, biashara yoyote haiwafuati wateja, bali wateja ndio wanaoifuata. Hivyo ubunifu wako ndiyo utakaokufanya usonge mbele na kukabiliana na changamoto katika biashara hiyo.
Kamwe usiingize hofu katika uamuzi wako, kutokana na maneno ya watu wengine ya kukuvunja moyo.
Hivyo utaona hofu ni adui namba moja wa maendeleo yako. Pia hurudisha nyuma maendeleo ya watu, kwa kuwazuia kufanya mambo yatakayowafanya wasonge mbele.
Pia humfanya mtu augue, husababisha matatizo ya kimaumbile, hufupisha maisha na hukunyamazisha pale unapotaka kuzungumza. Hivyo ni vizuri ukaondoa hali ya hofu katika maisha yako.
Hofu hukuletea hali ya mashaka, ambayo hukufanya usiwe na uamuzi sahihi. Inakuondolea hali ya kujiamini, ya kuweza kujitathmini kwa nini unakuwa na hali ngumu ya kiuchumi.
Ukweli ni kwamba, hofu ina nguvu katika maisha ya mwanadamu. Kwa njia moja ama nyingine hali hiyo inazuia watu kupata kile wanachokihitaji katika maisha.
Hofu kwa jinsi yoyote ile ni athari za saikolojia. Unaweza kuitibu hali hiyo kama vile unavyotibu magonjwa katika mwili wako.
Kwanza, kuwa na maandalizi wewe mwenyewe ya kuondoa hali hiyo, kwa kuwa na hali ya kujiamini. Kwa kuwa, hakuna yeyote aliyezaliwa katika hali hiyo ya kujiamini, bali wameishinda hali hiyo.
Hata pale unapokabiliwa na hali ngumu katika maisha, usikate tamaa, chukua hatua madhubuti ya kupambana na hali hiyo, njia itaonekana kwako.
Inakupasa kuondoa hali ya hofu uliyonayo ili uweze kupiga hatua zaidi.
Endapo unakabiliwa na hali ya hofu ya kupoteza wateja wako muhimu kulingana na ushindani ulionao, fanya kazi mara mbili zaidi ili kutoa huduma bora zaidi, weka vitu vile vinavyowafanya wateja wako wakukimbie, utafanikiwa.
Ama unakabiliwa na hofu ya kupata ajali wakati ukiendesha gari, ni vema kuwa makini na kuvaa ujasiri ili kuondoa hofu kwa abiria wengine waliopo kwenye gari.
Yamkini unaweza kujikuta unakabiliwa na hofu ya watu wengine hufikiri ama kusema nini juu yako. Inakupasa kuweka mipango yako vizuri na kuikamilisha kama ulivyoipanga ili kutimiza kile ulichokikusudia.
Katika kutibu hali hiyo, iondoe hofu uliyonayo, pamoja na kuchukua hatua madhubuti za kuondoa hali hiyo.
Kadiri unavyoshindwa kuwa na ujasiri, ndivyo unavyoshindwa kujisimamia katika mipango yako.
Akili yako ni kama benki, kila siku unawaza mambo mapya unayoyahifadhi katika benki yako.
Mawazo hayo unapoyaweka katika benki ya akili yako, yanakuwa na kukaa katika kumbukumbu zako.
Pale unapokabiliana na tatizo, unaangalia katika benki yako na kupata jibu sahihi. Benki yako itatoa majibu na kusambaza taarifa mbalimbali zinazohusiana na hali unayokabiliana nayo.
Lakini ili benki yako iwe na manufaa kwako, inakupasa uweke mawazo mazuri yenye kukupatia maendeleo.
Iwapo unakula, ama unaendesha gari wakati ukiwa mwenyewe, ni wakati wako mzuri wa kuhifadhi mawazo mazuri katika benki yako. Pia kabla ya kulala, ni vema kuweka mawazo mazuri katika benki yako.
Waza kuwa na maisha mazuri, familia nzuri, afya njema, elimu nzuri na hali ya kupata mahitaji yote katika utoshelevu.
Pia katika benki yako, unatakiwa kuchukua mawazo mazuri tu. endapo utachukua mawazo mabaya, yatakuletea usumbufu au hali ya kuchanganyikiwa.
Tukutane wiki ijayo.
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa kitabu cha The Magic of Thinking Big, kilichotungwa na David Schwartz.

JIAMINI UTAFANIKIWA

MSOMAJI wangu, katika mfululizo wa makala hizi za Maisha Yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi.
Leo tutaangalia jinsi ambavyo kila mmoja anapaswa kujijengea uwezo wa kuweza kujiamini ili kupata mafanikio.
Kila mmoja anapaswa kutamani kuwa kiongozi yeye mwenyewe, ili aweze kujenga uwezo wa kuwa na maendeleo binafsi, pasipo kutamani maendeleo ya mtu mwingine.
Kwasababu hakuna mtu atakayemlazimisha mtu mwingine kupata mafanikio.
Lakini kwa upande mwingine, suala la mafanikio ni jambo linalotokana na muda uliopo, kujitoa na kufanyia kazi mambo mbalimbali mtu anayoyapanga.
Hivyo ujue wazi hakuna mtu atakayekulazimisha wewe kupata mafanikio, bali inakupasa kufanya bidii binafsi ili ufikie matarajio ya juu uliyojipangia.
Haya yakizingatiwa, kila mmoja atakuwa na ari ya kujisimamia, kufanya kazi kwa bidii katika mipango mbalimbali ya maendeleo ya ukuaji wa uchumi.
Sasa basi ili uweze kukua na kupata maendeleo, inakupasa kila jambo unalolipanga uweze kulitekeleza.
Ni vema kuanza kufanya jitihada binafsi za kupata maendeleo, pamoja na kufanya tathmini ya hapo ulipo na ulipotoka, taratibu utajikuta unapiga hatua siku baada ya siku.
Kwa kuwa, tayari unayo maabara iliyosheheni kila hitaji la mwanadamu, unayotakiwa kuichunguza na kuifanyia kazi, ni vema kujibidiisha ili uweze kukitumia kila kifaa kilichopo ndani yake, kwa ajili ya maendeleo.
Hakuna kikwazo chochote katika maabara hiyo, kinachoweza kukukwamisha, kama utajitambua kama wewe ni mhusika mkuu katika maabara hiyo ni wazi utapenda kujua kazi ya kila kifaa.
Kwa kuwa, ndani ya maabara hiyo, hakuna kitu cha kununua, kodi ya kulipa, wala ada ya aina yoyote ila unaweza kuitumia vile unavyopenda bila malipo yoyote.
Kama wewe ni msimamizi katika maabara yako mwenyewe, utapenda kufanya vile wanasayansi wengine wanavyofanya.
Unaweza kushangaa kwa nini watu wengi wana uelewa mdogo wa kufikia mafanikio, wakati wanazungukwa na wenye mafanikio makubwa.
Hii ni kwa sababu watu wengi hawafuatilii mambo yanayofanywa na wengine ili kufikia malengo makubwa.
Hivyo basi, Mtunzi David Sachwartz, nia yake ni kukusaidia kwa kuchunguza na kuangalia undani wa mambo yanayofanywa na wengine ambao wameweza kufanikiwa.
Kuna uchaguzi wa aina mbili wa kukusaidia ili uweze kufanikiwa; mojawapo ukiwa ni kupenda kujifunza kwa kuchunguza kila kitu unachokiona na kuamini kuwa kinaweza kukupatia maendeleo.
Pia unaweza kuchagua mifano ya watu wawili ambao unaweza kuwatumia kwa ajili ya kujifunzia katika kupata mafanikio yako.
Unatakiwa kuwachagua watu ambao mmoja wao, amefanikiwa na mwingine ambaye hajafikia mafanikio, ambao unawajua vema.
Anza kufuatilia kila jambo wanalolifanya, utapata somo litalokufumbua macho.
Kila unachojifunza kwa watu hao, kinakuwezesha kupiga hatua zaidi, lengo lako likiwa ni kuangalia kanuni za kufikia mafanikio. Pia kwa kutumia mifano ya watu hao, ndivyo utakavyopata mbinu mpya za kukabiliana na changamoto za maisha kufikia mafanikio.
Ni jambo la kufurahisha unapokuwa na ujasiri, na kufanikiwa kila unachopanga, kujiangalia unavyokuwa siku baada ya siku na mwezi baada ya mwezi.
Makala hii imeandikwa kwa msaada wa kitabu cha ‘The Magic of Thinking Big’, mtunzi wake ni David Schwartz.
Tukutane Alhamisi ijayo.

HUU NDIO UGONJWA WA KUSHINDWA KUFIKIA MALENGO

MSOMAJI wangu, katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila alhamisi.
Leo tutaangalia jinsi ya kukabiliana na ugonjwa wa kushindwa kufikia malengo.
Kila mmoja tayari ana vifaa vya kutosha katika maabara yake ambayo anaweza kuitumia kwa ajili ya kazi na kujifunza.
Maabara ambayo ina kila kitu kinachokuzunguka katika dunia hii. Ambamo hutapata vikwazo, kwa kuwa kila utakachojifunza utajiona kama wewe ni mtaalamu.
Ukiweza kuitumia vizuri maabara hiyo, itakuwezesha kumaliza matatizo yako ya kifamilia kama vile, kulipia kodi ya nyumba, kulipia ada za shule na mambo mengine yanayofanana na hayo. Hivyo unaweza kuitumia maabara hiyo kwa uhuru zaidi jinsi unavyopenda.
Kwa upande mwingine, unaweza kuwaza jinsi ya kuwa na malengo makubwa katika maisha, kwa kupenda kujifunza kwa wengine waliofanikiwa.
Lakini angalizo lililopo, unatakiwa kujifunza kutoka kwa wengine kwa uangalifu. Pale unapopata jambo linalokufaa lifanyie kazi.
Unapoendelea kujifunza kutoka kwa wengine, utaona kuwa, watu wasiokuwa na mafanikio wanataabika katika akili zao kwa ugonjwa wa kufikiri.
Kila mtu asiyefikia malengo ya mafanikio amekuwa na ugonjwa huo kwa kiwango kikubwa.
Na mara zote mtu mwenye malengo makubwa hupenda kujiuliza ni kwanini hapo alipofikia hajafanikiwa, kwa nini hana kitu fulani au kwanini hawezi kufanya jambo fulani, ili aweze kupiga hatua zaidi ya hapo alipo.
Kama ugonjwa mwingine wowote unavyompata mtu, ugonjwa wa kufikiri unakuwa mbaya sana endapo hautatibiwa vizuri.
Muathirika wa ugonjwa huu, anakuwa akiwaza mambo mengi, kama vile ‘najaribu kufanya jambo hili na lile lakini sipati mafanikio’ na kuendelea kuwaza: “ Je, ni afya mbaya niliyonayo” au ni ukosefu wa elimu? Umri mkubwa? Umri mdogo? Bahati mbaya? Ama kutokuwa na bahati ya maisha? Mke? Ama jinsi nilivyolelewa na familia yangu?”
Hivyo mtu huyo aliyeathirika na ugonjwa huo, asipojigundua ataendelea na hali hiyo katika maisha yake.
Ili kukabiliana na hali hiyo, ni vizuri kujizoeza kuwa na mawazo chanya yenye mafanikio, ambayo ndiyo tiba ya ugonjwa wa kushindwa.
watu wenye ugonjwa wa kushindwa huwa na visingizio mbalimbali kama vile ‘afya yangu siyo nzuri’. Hiyo hufanya kila siku anapopata changamoto ya maisha badala ya kutoka hapo alipo, kuwa na jambo lolote la utetezi fulani.
Anakuwa na afya mbaya katika aina tofauti tofauti, ambacho ndicho kisingizio chake anaposhindwa kufanya jambo linalompatia maendeleo.
Wapo watu wengine wamekuwa wakisingizia wana matatizo ya moyo, na wamekwenda kwa daktari zaidi ya mara nne, na kila wanapokwenda ugonjwa hauonekani.
Kuendelea kueleza kuwa, una ugonjwa wa moyo, mwisho wa siku tatizo hilo litakupata kweli. Kinachotakiwa ni kuishinda hali hiyo na kusonga mbele katika kupata maendeleo yako katika maisha, bila kujali unasumbuliwa na kitu gani.
Sasa basi yapo mambo manne ambayo yanaweza kukupa afya njema na kuondokana na hiyo hali inayokufanya ukate tamaa, ama kufikiria kuwa huwezi kila jambo lililopo mbele yako.
Kwanza usikubali kuizungumzia afya yako. Kadiri unavyozungumzia kuhusu ugonjwa unaokusumbua, hata kama ni wa kawaida, ndivyo utakavyozidi kukusumbua.
Kuzungumzia kuhusu afya yako kama ni mbaya ni kama unaweka mbolea kwenye mbegu zilizopandwa.
Kuzungumzia afya yako ni tabia mbaya. Inachosha wengine. Watu waliofanikiwa wana tabia ya kutokuzungumiza afya zao zinapokuwa mbaya.
Pili usiwe na hofu juu ya afya yako. Fanya kile unachokusudia ili kufikia malengo mazuri.
Tatu, jione kuwa afya yako ni njema haina kasoro. Na pia endelea kujikumbusha kuwa, maisha yapo kwa ajili ya kuyafurahia. Usipoteze. Wala usiishi kwa kufikiri juu ya kulazwa hospitali.
Vile vile usipende kuchunguza kwa nini mipango unayoipanga haifanikiwi, bali ichekeche akili yako kuelekea njia ya mafanikio.
Tukutane wiki ijayo.

AKILI YAKO NI KIWANDA CHA MAFANIKO

MSOMAJI wangu, katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi. Leo tunazungumzia ili ufanikiwe unatakiwa ufanye nini.
Ni ukweli usiopingika kuwa, ili ufanikiwe katika maisha yako, inakubidi ufanye jitihada ya dhati. Kwa kujiuliza ni wapi uliposhindwa, ili uweze kuongeza bidii.
Vile vile, ni vema kuangalia udhaifu wako ulipo, ili uweze kurekebisha pale unapokosea katika kufikia mafanikio unayoyataka.
Watu wengi hupenda kuwa na mafanikio makubwa, lakini hawaonyeshi jitihada za dhati za kuwatoa pale walipo na kuwasogeza mbele.
Mara zote hukata tamaa kwa kuwaza mambo ambayo huwarudisha nyuma, hawako tayari kukubaliana na ukweli kuwa wanaweza kufanya jambo lolote ili kufikia malengo makubwa, cha msingi kinachotakiwa ni jitihada.
Hivyo basi, ni vizuri kuiambia nafsi yako, kuwa wewe unaweza kufanya jambo fulani kubwa litalokutoa hapo ulipo na kukufikisha sehemu nyingine yenye mafanikio zaidi.
Watu wengi hawaamini kuwa, Mungu amewabariki kwa kuwapa utajiri mwingi katika maisha yao, kwa kuwa, hawajui akili, nguvu, vipaji mbalimbali walivyonavyo ni utajiri tosha Mungu aliowapa katika maisha yao.
Ni vema kujiamini kuwa unaweza kufanya jambo kubwa katika maisha. Jitihada katika jambo lolote linakuleta mafanikio, kwa kukutoa katika hatua moja na kukupeleka katika hatua nyingine.
Vinginevyo utabakia kila siku ukiiambia nafsi yako, kwa nini wengine wanafanikiwa na wewe unabaki katika hali ile ile.
Jione kuwa wewe ni mtu wa thamani na ni mtu wa daraja la kwanza. Pia jenga hali ya kujiamini katika kila jambo unalotaka kulifanya.
Jiamini wewe mwenyewe na mambo mazuri yatatokea kwako, usiwe na hali ya hofu katika mambo uyafanyayo.
Akili yako ni kiwanda cha fikra. Ni kiwanda kilicho na shughuli nyingi. Hivyo itumie kwa busara upate mafanikio mengi.
Utakapoitumia akili yako vizuri utajikuta kila siku unapiga hatua zaidi. Kamwe usiiruhusu akili yako kuwaza kushindwa.
Unapodhamiria kufanya jambo fulani amini kuwa utafanikiwa. Wasiwasi utakufanya ushindwe katika kila unalotaka kulifanya.
Inuka, mlango wa mafanikio uko wazi na ujiweke kwenye kumbukumbu sasa kwamba unajiunga na kundi ambalo linakubali mabadiliko katika maisha.
Na hatua ya kwanza katika maisha yako, ambayo huwezi kuiepuka, amini kuwa unaweza kufanikiwa.
Je, ni jinsi gani, unaweza kuwa katika hali ya kujiamini kwamba unaweza kufanya jambo lolote na ukafanikiwa?
Ni pale tu utapofikiri kuhusu mafanikio yako na siyo kushindwa, uwapo kazini kwako ama nyumbani.
Hata pale utakapoona unapokabiliwa na hali ngumu, jiambie kuwa utashinda. Na kama upo ushindani kati yako na mtu mwingine, fikiri kuwa, una uwezo wa kushinda na si kushindwa.
Na nafasi ya kushinda inapoonekana, fikiri kuwa unaweza na si kwamba huwezi. Akili yako mara zote ifikiri kuwa unaweza kufanya jambo la mafanikio katika maisha.
Hali ya kuwaza mafanikio inakufanya katika akili yako uweke mikakati ya kukufanya upige hatua zaidi. Kinyume na hapo, utakaporuhusu akili yako kuwaza hali ya kushindwa, kamwe hautapiga hatua yoyote, kila mara utabakia pale pale.
Jambo jingine jikumbushe kwamba wewe ni bora kuliko unavyodhani. Watu wenye mafanikio si kwamba wana nguvu zaidi ya wengine.
Wala mafanikio si suala la kuona mtu fulani ana bahati, bali ni hali inayoweza kujengwa na mtu mwenyewe kwa kuongeza bidii.
Panda kuwaza mambo makubwa, ukubwa wa mafanikio yako unategemea jinsi unavyowaza. Kama unawaza malengo madogo, utarajie kupata mafanikio madogo.
Unapofikiri malengo makubwa, unakuwa na mafanikio makubwa pia.
Kumbuka hili, mawazo na malengo makubwa, mara zote yanarahisisha mambo yako na kukufanya usipate vikwazo vingi, tofauti na unavyowaza malengo madogo.
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa kitabu cha ‘The Magic of Thinking Big’ kilichotungwa na David Schwartz.
Tukutane alhamisi ijayo.

AMINI KUWA UNAWEZA KUFANIKIWA

MSOMAJI wangu, katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi. Leo tutaangalia jinsi ya kuwa na malengo makubwa katika maisha.
Kufikiria mambo makubwa katika maisha, kunakuwezesha kuishi maisha mazuri, yenye furaha, utimilifu, kipato kizuri, marafiki na heshima.
Mafanikio maana yake ni kupata mahitaji unayohitaji, kustawi katika maisha, kuwa na nyumba nzuri, kupata safari, kuwa na vitu vipya, fedha zinazotosheleza mahitaji, pamoja na kuwapa watoto wako mahitaji ya muhimu.
Vile vile kwa maelezo mengine mafanikio ni kupandishwa cheo kazini kwako, kuendelea kuwa karibu na watu katika biashara zako na maisha yako kwa ujumla.
Pia kwa maelezo mengine, ni kujiheshimu, kuendelea kuwa na furaha pamoja na kutosheka katika maisha, kuwa na uwezo wa kufanya zaidi kwa wote wanaokutegemea.
Maana yake nyingine ni kushinda ama kufaulu katika maisha.
Kila mwanadamu anapenda kuwa na mafanikio katika maisha yake, hakuna hata mmoja anayefurahia hali ya kutokupiga hatua katika maisha, pia hakuna anayependa kuwa nyuma katika maisha haya tunayoishi.
Hivyo ni vizuri kupenda kujenga imani ya kujiamini kuwa unaweza kufanya jambo fulani ulilokusudia na kufanikiwa.
Kwa kuwa, mtu yeyote anapoweka nia kuwa anaweza jambo fulani, anafanikiwa. Lakini kinyume cha hapo, kamwe hatafanikiwa, atabakia katika hatua ile ile kila siku, ilhali wengine wakiwa wanasonga mbele.
Kila siku ulimwenguni, vijana wanaomaliza vyuo huanza kazi mpya. Kila mmoja anafikiria kuwa siku moja atafurahia mafanikio yatayompandisha juu kwa kumtoa hapo alipo na kumpa nafasi nyingine nzuri zaidi.
Lakini wengi wa vijana hao, hawafikirii kwamba ipo siku wanaweza kufika mbali zaidi ya hapo walipo. Matokeo yake, hawafiki mbali kwa kuwa hawana imani ya kuwatoa hapo walipo.
Matokeo yake, hubakia kuwa watu wa kawaida katika maisha yao.
Lakini kuna baadhi ya vijana wachache, wanaoamini kuwa, katika kipindi kifupi, tokea waanze kazi, watakuwa wameshasonga mbele zaidi.
Wanakuwa wanawaza kufika mbali zaidi na kuamini hivyo kunatokana na imani yao hiyo na kufikia pale walipokusudia.
Vijana hao huwa wajanja kwa kuwatazama wale waliowatangulia, upungufu wao na kufikiria jinsi ya kufanya vizuri zaidi.
Huwa wanawatazama wale waliofanikiwa kwamba wanakabilianaje na vikwazo mbalimbali na kufanya maamuzi ya busara.
Wanakuwa watu wanaokusudia kuwa na mafanikio, hivyo wanafanya jitihada mbalimbali ili kufikia walipokusudia.
Mara nyingi katika maisha yetu ya kawaida, unakuta mtu anakuwa anapenda kufika mbali katika maisha lakini anakatishwa tamaa na wengine.
Cha msingi, unapaswa kufanya kile ulichokusudia. Usiwe mwepesi wa kukata tamaa katika maisha yako. Na matokeo yake utayaona.
Unapokuwa na imani ya kufanya jambo fulani, kamwe usikate tamaa, kinachokupasa ni kufikiri mbinu ya kukutoa hapo ulipo na kusonga mbele.
Unapokuwa jasiri kufanya jambo fulani, kunawafanya na wengine wakuamini kuwa unaweza.
Hivyo unapoamini kuwa unaweza kufanya jambo fulani, utafanikiwa. Kwa wale wasiokuwa na imani ya kufanikiwa hata wanapofanya jambo hukwama njiani, kwa kuwa tokea awali walishaona hawataweza.
Unapokuwa na imani kuwa huwezi kufanya jambo fulani, ama kuwa na wasiwasi wa kufanya jambo, akili yako inapata sababu ya kukubaliana na kile unachokiamini.
Hofu, wasiwasi, kutokuamini kuwa unaweza, vinakufanya ushindwe kufikia malengo uliyojiwekea.
Hivyo ni vema kuwa na mawazo ya ushindi ili uweze kufanikiwa.
Imani ni kipimo chako katika maisha ambacho kitakuongoza. Kama unaamini kuwa kamwe hautakuwa tajiri, hali huwa hivyo hivyo.
Kama unaamini hutaweza kufanya mambo makubwa katika maisha, ndivyo itakavyokuwa. Kama unajiona kuwa wewe si wa muhimu, utaendelea kuonekana hivyo hivyo.
Kwa mtu anayewaza mambo makubwa, anakuwa anaamini kuwa atakuwa na utajiri, ndivyo inavyokuwa kwake.
Anaamini kuwa ataweza kufanya shughuli ngumu ambazo zitaMfikisha mahali pazuri na ndivyo inavyokuwa.
Kila kitu anachokifanya, jinsi anavyochukuliana na watu, tabia yake, mawazo yake, vyote vinamweka katika nafasi nzuri ya kuwa na mafanikio zaidi. Na kuonekana ni mtu wa maana.
Mtu ni bidhaa ya mawazo yake mwenyewe kwa kuamini na kufikiri mambo makubwa.
Tukutane Alhamisi ijayo.

KUWA NA MAWASILIANO MAZURI KAZINI KWAKO

MSOMAJI, katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi. Leo tutaangalia jinsi gani unaweza kuwa na mawasiliano mazuri katika ofisi unayofanyia kazi.
Ni ukweli usiopingika kuwa, wale wote wanaofanya kazi maofisini, hutumia muda mwingi zaidi wakiwa ofisini kuliko nyumbani.
Hivyo ni muhimu kufurahia kazi ile unayoifanya na kuwa karibu na wale wote unaofanya nao kazi kwa muda huo, kwa sababu, wakati mwingine kazi tuzifanyazo husababisha msongo, hivyo kama unapata msaada kutoka kwa wenzako, inakusaidia kuondoa hali hiyo.
Lakini kwa upande mwingine, unaweza ukajikuta kuwa bila sababu ya msingi unapata upinzani katika shughuli zako unazozifanya kutoka kwa wafanyakazi wenzako.
Na kwamba, pasipo sababu ya msingi unakuta watu wanakutendea matendo yanayokuudhi, unachotakiwa kukifanya ni kuwasamehe.
Unaweza ukawa mwema kwao, lakini wakakudharau, endelea kuwa mwema kwao.
Unaweza ukawa mpole, wakatumia nafasi hiyo kukuhadaa, endelea kuwa mpole kwao.
Ukiwa katika shughuli zako, unaweza ukaamua kutafuta furaha lakini wengine wakakuonea wivu, usivunjike moyo, endelea kuwa na furaha hiyo unayoitafuta.
Au unaweza kujikuta kuwa, mambo mazuri unayoyafanya leo, kesho yanaweza yakawa yamesahauliwa, Endelea kufanya vile vile bila kupunguza.
Pamoja na upinzani unaoweza kukutana nao katika ofisi yako, elewa kuwa na mawasiliano ni muhimu katika eneo lolote la kazi.
Kuzungumza na kusikiliza wasimamizi wako na wafanyakazi wenzako ni muhimu, si tu kwa ajili ya mafanikio yako, bali kwa ajili ya mafanikio ya kampuni yako pia.
Jifunze njia sahihi za kuwasiliana na wafanyakazi wenzako kwa njia mbalimbali, pia weka mazingira bora ya kazi kwa kila mmoja.
Penda kujifunza kusikiliza kwa makini, kusikiliza mtu ni jambo la muhimu sana, ni zaidi ya kuzungumza.
Kwa kuwa, kusikiliza kunakufanya kuwaelewa wafanyakazi wenzako, mawazo na thamani yao.
Kuwa na tabia ya kumsikiliza mwenzako na uliza maswali ili uwe na uhakika wa kile anachokizungumza na matarajio yake.
Pili, watendee wenzako vile unavyotaka wakutendee wewe. Kila mmoja mheshimu jinsi alivyo. Usimwingilie anapofanya shughuli zake, usimbughudhi na wala usigombane naye kuhusiana na vifaa vya ofisini.
Unapohitaji kufanya jambo mwombe na ukimaliza mshukuru, usisite kumpa sifa zake pale anapostahili.
Kuwa mwangalifu na ishara za mwili unazotaka kuzitumia. Kamwe hata kama hupendi kusikiliza jambo unaloambiwa na mfanyakazi mwenzako, epuka kushika shika mikono yako, kugonga gonga miguu yako au kuzungusha macho yako.
Kwa kufanya hivyo itaonyesha dhahiri kwamba hauna utayari wa kumsikiliza mtu huyo, na kufanya mawasiliano yenu kuwa magumu kwa siku zinazofuata.
Kuwa na muonekano wa tofauti katika shughuli zako. Pokea simu unazopigiwa, jibu barua pepe unazotumiwa na fanya kazi zako kwa wakati. Utaheshimika na jaribu kujenga mahusiano mazuri na baada ya muda nao watakuwa wema kwako.
Makala hii imeandikwa kwa msaada wa mashirika ya habari.
Tukutane Alhamisi ijayo.

Friday, August 28, 2009

SAHAU MAUMIVU ULIYONAYO UPATE FURAHA

WIKI iliyopita tuliangalia jinsi ya kudhibiti hisia zetu ili tuendelee kuwa na furaha, imeonekana kuwa watu wengi wameshindwa kudhibiti hisia walizokuwa nazo na kujikuta wako katika hali ya kukata tamaa, pamoja na kuvunjika moyo.

Katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi. Leo tutaangalia jinsi inavyokupasa uyaachie mambo yanayokusumbua, ili uishi kwa furaha. Tutaangalia jinsi ya kuachana na mambo mbalimbali tunayokutana nayo katika maisha ili kuweza kupata amani na utulivu katika mioyo yetu.

Kumbuka kuwa kama una tabia ya kuachana na ya maumivu na huzuni unayokabiliana nayo, utakuwa na maisha mazuri, lakini kinyume cha hapo, utaendelea kuwa mtu asiyekuwa na furaha siku zote.

Na pia ufahamu kuwa, kila mmoja wetu hukabiliana na changamoto mbalimbali katika sehemu fulani ya maisha yake, kama vile, hali ya huzuni au kukataliwa lakini njia nzuri ya kuishi vizuri ni kuwa jasiri katika kuikabili hali hiyo.

Japo wapo watu wengine hudhani, kwa kuwa wao ni washika dini sana, hali ya huzuni, kuhangaika, kukata tamaa haitawapata, la hasha! Kila mmoja anapatwa na hali hiyo, ila ni uamuzi wako kuchagua ni jinsi gani unapenda uwe, kuwa na furaha ama kutokuwa nayo.

Pia ukiangalia watu wengi ambao hawana furaha, hukabiliwa na magonjwa mbalimbali. Huweza kuwatambua kwa kuwaangalia muonekano wao kiafya, vile vile hupatwa na maradhi kama shinikizo la moyo, moyo kudunda kwa nguvu, kupooza na hata wakati mwingine kuugua kansa ambayo huzalishwa na hali ya msongo wa mawazo.

Kwa upande mwingine wa maisha haya tunayoyaishi, ujue kuwa nayo yana kanuni zake, kama unataka watu wakutendee mambo mema, nawe pia watendee yaliyo mema, kwa kila jambo unalotenda.

Kwa kila tendo jema, kuna mwitiko ulio mzuri, kinyume cha hapo hutabaki kuumia na kukosa furaha maishani. Wema wako unaowatendea wengine, ndivyo hivyo nawe utapokea katika maisha yako kutoka kwao.

Tiba ya kuishi maisha ya furaha ni hii ‘kuwa mzuri, kuwa mwema, usiwe mbinafsi. Watendee wengine vile unavyopenda wakutendee wewe’.

Kama kweli umedhamiria kupata furaha ya kutosha maishani, tumia kanuni hiyo ya maisha na kuifanyia kazi.

Kama unataka kuwa rafiki wa watu, nao wawe rafiki zako. Kuwa rafiki kwao na kama umezungukwa na watu wasio wazuri kwako, wabadili wawe watu wazuri kwa kuonyesha wema wako kwao, haijalishi jinsi watakavyokuchukulia.

Je, unadhani utawabadilishaje ili wawe watu wazuri? Ni kwa kushirikiana nao katika mambo yaliyo mema na kuwajali. Inawezekana wanaweza wasikukubali kirahisi, lakini jitahidi kuwa mwema kwao, bila kujali wanachokisema wala kukinong’ona.

Hebu tuangalie mfano wa mama mmoja, aliyekuwa ameolewa lakini hakuwa na furaha na mumewe, kwa kuwa kila alichokifanya mumewe huyo alikikosoa.

Mwanamke huyo aliamua kutafuta msaada kwa kiongozi wake wa dini na kumweleza kuhusu mumewe kwamba kila aliporudi nyumbani alikuwa na hasira na kukosoa kila jambo aliloliona limefanyika.

Lakini mama huyo, alipoomba ushauri, aliambiwa kuwa, inawezekana yeye ndiye chanzo cha yote kabla ya kumsema mumewe, ni vema akajiangalie yeye kwanza, jambo alilokubaliana nalo na kulifanyia kazi, baada ya muda, mumewe alibadilika. Furaha ikatawala nyumbani kwao.

Mwanamke huyo alisema, aliamua kubadilika kwa kumjali mumewe na kuwa karibu naye, bila kujali vile alivyokuwa akimtenda na kwamba kila mumewe huyo aliporudi nyumbani, na kuanza kukosoa kama alivyozoea, kwa kuwa mwanamke alikubali kubadilika, alijitahidi kumhudumia kwa upendo, kumpatia chakula, juisi na kumpa maneno matamu, bila kujali jinsi alivyokuwa akifoka kwa hasira.

Alisema aliendelea kuwa karibu na mumewe kila siku na mwishoni mumewe huyo alibadilika tabia yake ile aliyokuwa nayo. Kama unataka kuyabadili mazingira magumu unayokutana nayo, ni vema ukaanza kubadilika wewe kwanza.

Fikiri juu ya hili. Je, ni jambo gani linalotufanya kuwatendea watu mambo mema? Ni kwa kuwa, nasi tunapenda kutendewa mambo mema pia? Kamwe tusiruhusu hali ya chuki na hasira katika maisha tunayoyaishi. Mbaya zaidi hali ya hasira zilizofichika ndani vinginevyo utapata maumivu na majeraha yaliyofichika ambayo yanahitaji kuponywa.

Majeraha hayo yaliyofichika hukusababishia hasira, ugomvi ama hali yoyote ambayo hupendi utendewe na mtu mwingine. Baadhi ya dalili zinazomfanya mtu aonekana kama ana majeraha yaliyofichika ni maneno yake, mwonekano na vitendo vyake.

Sasa basi njia ya kukabiliana na maumivu ya ndani uliyonayo ni kuyasahau na kutokumbuka mambo uliyowahi kutendewa. Watu wengi wanakosa furaha ya kweli, kwa kuwa wamekuwa wakikumbuka jinsi walivyotendewa na baba au mama yake, alipokuwa mdogo, mke au mme wake alivyomtendea siku za nyuma, kwa kuwa wanashindwa kusamehe, miaka inapita huku maumivu hayo yakiwa yanaendelea.

Usilaani. Kamwe usiruhusu maumivu yakakufanye mtu mwenye uchungu, jaribu kusahau, kumbuka kuwa, huwezi kusahau maumivu yaliyokupata kama utakuwa unayakumbuka kumbuka.

Tukutane Alhamisi ijayo.

HALI YA KURIDHIKA INAONGEZA FURAHA

KATIKA mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya, ambapo leo tutaangalia jinsi ya kudhibiti hisia zetu ili tuendelee kuwa na furaha.

Watu ambao hawawezi kudhibiti hisia zao wanajikuta wako katika hali ya kukata tamaa na kuvunjika moyo.

Lakini ukweli ni kwamba, inakupasa usikate tamaa mpaka kumwazia Mungu wako mambo mabaya, kutokana na wewe mwenyewe kushindwa kudhibiti hisia zako.

Hivyo ni vema kuwa imara katika hisia zako, bila kujali kama unapitia hali ya milima na mabonde, ili kutimiza malengo yako uliyojiwekea, kinyume cha hapo, utaendelea kuwa mtu usiyesonga mbele kutokana na hali ambayo umeiruhusu, ilhali ungeweza kuidhibiti.

Mfano mzuri ni kwa mtu aliyeelimika, kwa kuwa yuko tayari kufundishika, ambaye ni muelewa, hataabiki kwa kuonyesha kuwa anajua kila kitu, hata kama anajua.

Huwa na utayari wa kujifunza kila mara, ni msikivu. Na kama njia yake haiko sawa sawa, anakuwa tayari kubadilika, mtu wa namna hii, ni rahisi
kuwa na mafanikio ya haraka.

Pia mtu wa aina hii, endapo hajui jambo fulani, hukubali kuwa hajui na huwa tayari kukiri hivyo. Mtu wa aina hii, yuko tayari kusikiliza wengine, iwe ni mzee, kijana, mwenye busara ama mwenye uzoefu zaidi yake, humsikiliza.

Hakuna ubishi, kutoelimika ni jambo la hatari, hivyo ni busara kila mmoja akapenda kuelimika bila kujali umri alionao, kwa kuwa atapata busara zaidi na mafanikio ikiwa ni pamoja na kujisimamia katika maamuzi yake, kabla ya kufanya jambo linaloweza kumharibia kabisa.

Kamwe usikubali kujishusha thamani yako na kujiona wewe si kitu, kwamba huwezi kufanya jambo fulani, kwani huo si ubinadamu. Bali inakupasa kupiga moyo konde na kusonga mbele, hata kama kuna hali ngumu inayokukatiza, jaribu kukabiliana nayo.

Kujikubali ulivyo ni pamoja na kuwa tayari kukubali kuwa watu wengine pia wanaweza kukusaidia pamoja na kukupa uwezo wa kujiamini kuweza kukiri upungufu ulionao.

Kuwa wazi, kuwa mnyenyekevu, jisahihishe na penda kuelimika. Kwa kufanya hivyo, utaweza kuishi kwa furaha na amani.

Wengi wetu tumejikuta hatuna furaha katika maisha yetu, kwa kuwa tunajitaabisha na mambo mengi na kujikuta kila wakati wewe ni mtu wa shughuli na mipango mingi isiyokwisha.

Kwa maelezo mengine, tunashindwa kuwa na furaha kila siku, kutokana na hisia zetu kuzielekeza kwenye shughuli na matukio ya siku inayofuata.

Tumekuwa na shughuli nyingi katika mipango ya maisha, hali inayotufanya kushindwa kuwa na furaha kwa muda uliopo.

Ebu tuangalie mfano wa mtu mmoja ambaye mwanzoni alifikiri kuwa, endapo angekuwa na nyumba yake angekuwa na utajiri ambao ungempatia furaha, lakini hilo lilipotimia alihitaji kitu kingine zaidi.

Alijikuta akihitaji nyumba nyingine kubwa zaidi. Wakati ukafika, akapata nyumba nyingine, lakini alijikuta kila wakati akifurahia nyumba yake ya awali, hivyo ilimlazimu kwenda kwenye nyumba yake ya awali, mara kwa mara.

Ilifikia mahali akasema kila alivyozidi kujiridhisha kwa kupata kile alichokihitaji, ndivyo alivyokuwa hafurahii vitu alivyokuwa navyo na kutamani kupata vingine zaidi. Hapa tunaona ni vizuri kuwa na kiasi katika maisha tunayoyaishi.

Hapa tunajifunza nini? Mwanadamu yeyote kama hana tabia ya kuridhika, anakuwa anajiongezea hali ya kukata tamaa na hata kuishi kwa hofu, kwa kutokufikia malengo makubwa aliyojipangia.

Ni sawa na kuamka usiku wa manane na kwenda kwenye jokofu kulifungua lakini hujui ni nini hasa unachokihitaji.

Kwa kuwa hujui unachokihitaji, unajikuta ukigusa hiki, unajaribu na kingine lakini katika vitu vyote hivyo hakuna unachokisikia ni kitamu.

Mwisho unafunga jokofu lako na kurudi kulala, huku bado ukiwa na njaa, hujatosheka.

Tunaona wengi wetu tunafanana tabia zetu kwa kuwa na hisia zisizotimizika.

Ili tuwe na mafanikio, inabidi kufanya uchaguzi katika kila tunachokiwaza. Inatakiwa kuondokana na mawazo yatakayoturudisha nyuma, kuwa na mawazo mazuri, ndoto nzuri na kufanya kazi kwa bidii.

Tukutane Alhamisi ijayo.

IKUBALI HALI ULIYONAYO UPATE FURAHA

MSOMAJI, katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi.

Leo tutaangalia jinsi unavyoweza kupata furaha kwa kuikubali hali ya upungufu uliyonayo.

Si rahisi kwa mtu yeyote kukubali hali ya uhitaji aliyonayo, lakini kufanya hivyo ni jambo la muhimu.

Ni ukweli usiopingika kuwa, katika maeneo yote ya maisha tunayoyaishi, kanuni zake zinafanana.

Na kwamba, unakuwa na furaha pale tu unapokubali hali ile ya upungufu uliyonayo, kwa kuwa hapo ndipo kwenye hitaji lako.

Kama ni kweli kuwa kila mmoja wetu hajakamilika katika eneo fulani katika maisha, kwa nini basi unakuwa hauko tayari kuikubali hali hiyo?

Wengi wetu tumekuwa hatuko tayari kukubali hali ya upungufu tuliyonayo, kwa kuhofia kuwa jamii inayotuzunguka itatucheka, kututenga ama kudhalilika.

Lakini kinachotakiwa hapa, ni kutoogopa jambo lolote lile, liwe kutengwa, kukataliwa ama kudharauliwa.

Sasa ni jinsi gani hali hii ya kuwa na furaha inaweza kukubadili wewe na mimi? Ni pale tu utakapoonyesha unahitaji msaada ama una upungufu.

Kwa mfano unaweza kuhitaji msaada kwa mtu yeyote kwa kumuuliza maswali yafuatayo: "Nimepata tatizo, je, waweza kunisaidia?, "Sielewi jambo fulani unaweza kunielewesha?, "Sijakubaliana na wewe, je, tunaweza kuonana mahali na kujadili zaidi?", "Nimepata hasara, je, waweza kuniongoza cha kufanya?"

Maswali ya namna hiyo ndiyo mwanzo wa kukuweka huru katika maisha yako. Hivyo furaha inakuwepo kwa mtu yeyote yule anayejua kuwa, eneo fulani ana upungufu hivyo anaukubali na kuhitaji msaada kwa wengine.

Kama wewe hauko tayari kulikubali jambo linalokusumbua, usishangae usipoona kuwa, wengine hawakujali.

Hivyo suluhu ni kujiweka mbele, jaribu kuwa mtu fulani ambaye hukuwahi kuwa hivyo, pamoja na kujiweka maridadi wakati wote.

Na ukweli ni kwamba, katika hali ya kuumia uliyonayo, kuna mtu ambaye yuko tayari kukusaidia juu ya upungufu wako, endapo tu ataelewa tatizo lako na kuliachilia. Lakini kama utajionyesha kuwa huna matatizo, hakuna njia ambayo mtu yeyote ataweza kukusaidia.

Wakati wote kuna mtu ambaye yupo tayari kukusaidia. Na kwamba mtu yeyote husaidiwa pale atakapokubali kuwa ana uhitaji katika sehemu fulani.

Kuna mfano wa mtu mmoja ambaye alikuwa ni mtumwa wa ulevi kwa muda mrefu, aliteseka katika hali hiyo kwa kuwa hakuwa tayari kuikubali. Na pale alipoelezwa kuhusiana na athari zinazoweza kumpata, hakuwa tayari kupokea msaada.

Siku moja baada ya kulewa kupindukia na kugonga gari lake alilokuwa akiliendesha, kwa maneno yake mwenyewe alijikuta akisema kuwa: ''Nimeteseka kwa ulevi kwa muda mrefu, kwa kuwa nilikuwa nasema kuwa, ninaweza kuudhibiti unywaji wangu, nilikataa ukweli kuwa nilikuwa mlevi niliyepitiliza, ningepokea uponyaji endapo ningeonyesha ninahitaji msaada. Na sasa baada ya hali hii kunikuta ninahitaji msaada na kubadili maisha yangu."

Tokea siku hiyo, maisha ya mtu huyo yalibadilika kwa kuwa alijitambua na kuhitaji msaada.

Kwa upande mwingine, furaha ya kweli inapatikana pale ambapo unaacha hali ya kulaumu. Ama kumlaumu Mungu au kujilaumu mwenyewe.

Watu wengi wanapopata matatizo hujikuta wakimlaumu Mungu ama kujilaumu wenyewe, badala ya kutafuta njia ya kumtoa hapo alipo ili aweze kuwa huru.

Sasa basi endapo umefikia hatua ya kukata tamaa ya maisha, umekutana na kipindi kigumu, kamwe usimlaumu Mungu kwa kuwa kufanya hivyo hutapata jibu la tatizo ulilonalo.

Makosa mbalimbali ambayo mwanadamu huyafanya pindi awapo katika hali ngumu ni yale ya kuhukumu, yatokanayo na utashi, sababu, ubinafsi, ukaidi, upumbavu na mengineyo yafananayo na hayo. Yote hayo ni chanzo cha binadamu kinachomfanya awe maskini na kuteseka.

Ama wakati mwingine unakuta mtu analaumu kwa ugonjwa alionao, ilhali wakati mwingine yawezekana yeye mwenyewe ameshindwa kujilinda mpaka akapata magonjwa.

Kwani kwa upande mwingine tunaweza kusema kuwa, magonjwa mengi sisi wenyewe ndiyo tunayasababisha kwa kutokula vizuri, kutokulala vizuri, kutokufanya mazoezi vizuri, kutopumua vizuri, haya yote ni kutokana na mazingira yanayomzunguka binadamu. Hivyo tunaona mambo mengine ni sisi wenyewe tunajisababishia na Mungu si wa kulaumiwa.

Mengi ya magonjwa hayo, huwapata wanadamu kutokana na uelewa mdogo ama elimu waliyonayo juu ya athari zinazoweza kutokea endapo ulishindwa kufanya jambo fulani.

Vile vile si vizuri kujilaumu wewe mwenyewe kutokana na hali inayokukabili, kwani kwa kufanya hivyo hutaweza kutatua tatizo linalokusumbua wala kuibadili hali hiyo.

Unaweza kupata hali ya kufiwa na mtoto, mzazi ama mume wako mpenzi, hali itakayokufanya ujitenge na wenzako, uache kujichanganya na kufanya mambo mengine ya kukusaidia, kutokana na hali iliyokukuta endapo hautakuwa makini na kuendelea na shughuli zako za kila siku, utajikuta hali yako kimaisha na kiuchumi inazidi kudidimia.

Katika hali kama hiyo, ndugu ama rafiki zako hawataweza kuyainua maisha yako siku zote, watakusaidia kwa sehemu tu, lakini itabidi nawe unyanyuke na kutoka katika hali ile ya kutokuwa na furaha na kujichanganya ili uweze kusukuma gurudumu hili la maendeleo.

Tukutane Alhamisi ijayo

TATUA TATIZO LINALOKUSUMBUA ILI UWE NA FURAHA

MSOMAJI wangu, katika mfululizo wa makala hizi za Maisha Yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi. Leo tutaangalia jinsi ya kuwa na furaha katika maisha yetu ya kila siku.

Hebu tuangalie mfano huu. Mwanamke mmoja alikuwa anahojiwa na mwandishi wa habari kwenye runinga na ghafla aliulizwa swali kama ‘anadhani ni watu gani siku hizi wana furaha’.

Kwa taharuki bila utulivu, mwanamke yule alikurupuka na kujibu lile swali kuwa kila mtu ana matatizo mengi, akimaanisha kuwa hakuna mtu yeyote aliye na furaha.

Hii inaonyesha dhahiri kuwa mwanamke yule kwa muda ule hakutarajiwa kuulizwa swali kama lile. Na aliulizwa bila kupewa nafasi ya kuwa na maandalizi. Na kwa muda huo, alikuwa ni mtu aliyejawa na mawazo.

Lakini ukweli ni kwamba furaha huwa ipo tu, bila kujali kama mtu ana matatizo ama hana. Inawezekana kabisa kila mmoja akawa na matatizo, lakini si kwamba kila moja hana furaha, kwani wapo watu wenye furaha lakini wana maisha duni, lakini wapo wengine hawana furaha ingawa ni matajiri wakubwa.

Tunaona kuwa kuna watu ambao wamejaaliwa kuwa na vitu vyenye thamani ya mabilioni ya fedha, lakini wamekuwa na matatizo ya kifedha. Utajiri wao upo kwenye mali walizowekeza.

Hupokea mshahara, lakini kiasi kikubwa kinakwenda kwenye madeni aliyonayo. Pia katika maisha haya tunayoyaishi kila mtu anakuwa na eneo fulani ambalo limekuwa likimkosesha furaha katika maisha yake. La msingi ni kuikabili hali hiyo na kutafuta ni jinsi gani utapata furaha na amani katika maisha.

Hata wewe inawezekana una hali hiyo katika shughuli zako uzifanyazo. Kama hilo unalikubali, hata kama una fedha nyingi bado kuna eneo utakuwa umekwama hivyo utakuwa huna furaha. Kila mmoja anapoanza maisha anakuwa na ndoto ya mafanikio. Inakubidi ujue ndoto ya shughuli unayotarajia kuifanya na jinsi ya kushikamana nayo.

Endapo ndoto za malengo yako zitatimia, ni lazima utakuwa na mafanikio makubwa. Na hapo ndipo furaha yako itakapotimilika. Pia wengine wana sononeko katika ufahamu wao. Hapa utaona kuwa kila mtu amebahatika kupewa eneo lake alitawale. Kwa maana kwamba, wapo wenye akili za darasani, wenye ushauri wa busara, wenye akili ya biashara na mambo mengine.

Utaona hapa kila mmoja, Mungu amemjalia kwa sehemu yake. Kwa hiyo kila mmoja ana eneo ambalo hakubahatika kuwa nalo. Hebu tuangalie mfano huu. Wanafunzi wawapo darasani, wapo wanaoelewa kwa haraka zaidi somo fulani kuliko wengine. Wengine ni wepesi katika hisabati, wengine histori na wengine Geography. Inategemeana na vile alivyojaliwa.

Hivyo kama mwanafunzi mzuri unapoona somo fulani linakupiga chenga huku wenzako wakiwa wanalielewa kwa urahisi, unaumia na kukosa furaha. Kinachotakiwa ni kutafuta njia ya kutatua hali hiyo ili uwe na furaha katika eneo hilo.

Kwa mfano, kuna kijana aliyekuwa haelewi somo la historia wakati mwalimu wake alipokuwa akifundisha darasani. Hivyo kila mara mwalimu huyo alipoingia darasani alikuwa akikosa furaha.

Wakati huo, wenzake walikuwa wakilifurahia somo hilo kwa kuwa walikuwa wakilielewa vizuri pale mwalimu wao alipowafundisha.

Mwalimu wake aligundua hali hiyo kwamba kijana yule hana furaha kama wanafunzi wengine anapokuwa darasani. Na siku moja alimuuliza, ana tatizo gani ili aweze kumsaidia lakini kijana yule alimweleza kuwa hana tatizo.

Kwanza tunaona kuwa kijana yule alifanya kosa kwa kuwa hakuwa tayari kujieleza ili apate msaada kwa mwalimu wake. Hivyo ni ukweli usiopingika kuwa pale unapokuwa na tatizo na ukawa tayari kujieleza, unakuwa na amani na furaha moyoni, kwa kuwa unapata msaada zaidi. Kinyume cha hapo, unakosa furaha kila mara kipindi hicho kinapokaribia.

Kwa hiyo, tunaona kuwa mafanikio ya mwanafunzi yanapatikana pale anapokubali kuwa hawezi somo fulani, ili apatiwe msaada zaidi. Kwa upande mwingine, mtoto nyumbani anaweza kuwa na hali ya mfadhaiko na kushindwa kuwa na mawasiliano mazuri na wazazi wake, kutokana na jinsi ile wanavyomlea, kwamba wamekuwa wakali sana na hawamfundishi kwa upendo pale anapokosea.

Laiti mtoto yule angeweza kuwa wazi na kuwaambia wazazi wake hali aliyonayo inachangiwa na wao, angeweza kuwa na hali nzuri. Na ukawa mwanzo wa mahusiano mazuri kati yake na wazazi wake.

Vile vile kwa upande mwingine, ni vema wazazi wakawa wazi kwa watoto wao, pale wanapoona kuwa wamewakosea. Wawe tayari kukiri makosa hayo kwa watoto wao. Si vema mzazi akaonyesha kuwa yuko sahihi wakati wote hata kama amekosea. Ni vema kukiri kuwa jambo fulani limefanyika kimakosa.

Eneo jingine linalowanyima watu furaha ni upande wa hisia. Hapa utaona kuwa, watu wengi wamekuwa wakiugua maradhi mbalimbali, kutokana na hisia wanazokuwa nazo.

Wengine hufikia hatua ya kupungua uzito, kutokana na hali hiyo. Wengine kutokana na kupata msukosuko wa kimahusiano hufikia hatua hata ya kutaka kujiua.

Ni kweli kuwa katika maeneo yote ya maisha kanuni zinafanana. Hivyo unapokutana na tatizo ni vema kuikubali hali hiyo iliyokupata japo si jambo rahisi, ili urejeshe furaha yako uliyokuwa nayo. Na kwamba, furaha inapatikana pale tu unapokubali kuwa umepungukiwa hivyo unahitaji msaada.

Kuna swali moja la kujiuliza kwamba, kama kila mmoja kati yetu eneo fulani katika maisha ana uhitaji, kwanini basi tunakuwa wagumu kuikubali hali hiyo? Yawezekana ugumu unakuwepo kwa kuogopa kuwa, unaposema ukweli katika eneo fulani utakataliwa na jamii, rafiki ama familia.

Ama pia kukubali hali ile uliyonayo itakufanya upate aibu. La hasha, hiyo ndiyo njia sahihi ya maisha ya kujikubali na kuachana na mambo yale yanayokuumiza. Kinachotakiwa ni kujivika hali ya ujasiri bila kuogopa jambo lolote lile.

Furaha inakuja kwa mtu yule anayegundua eneo ambalo anahitaji msaada na kuwa wazi. Mafanikio yanakuja kwa mtu anayeomba kusaidia katika eneo lile aliloshindwa.

Tukutane alhamisi ijayo

FEDHA HAZIWEZI KUKUPA FURAHA

KARIBU mpenzi msomaji katika safu hii ya Maisha Yetu, inayokujia kila Alhamisi, lengo likiwa ni kujifunza mambo mbalimbali tunayoyapitia. Leo tutaangalia mambo yanayoweza kukupa furaha katika maisha.

Mara kwa mara waweza kufikiri kuwa kama ungekuwa na gari la aina fulani, nafsi yako ingeweza kufarijika. Kama ungeweza kumpata mtu mtakayeweza kuishi maisha ya ndoa katika raha na shida, ungekuwa na furaha, kama usingekuwa na hali ya msongo kutokana na ukosefu wa fedha, ungekuwa umejitosheleza.

Ni kweli unaweza kuwaza mengi zaidi ya hayo kwamba kama ungeweza kufanya jambo fulani ama kuwa na magari, nyumba, dhahabu na vitu vingine vya thamani, ungeweza kuwa na furaha, lakini hicho pia siyo kipimo halisi cha kuhitimisha furaha yako.

Sasa ni wapi ambako unaweza kuipata furaha, kama si kwenye utajiri, mazoezi, kukubalika ama kwenye mahusiano. Tunaona kuwa, ipo siri kwamba tabia yako ni muhimu kuliko hali halisi. Kinachotakiwa kufanya ni kuondoa mawazo hasi na kuwa na mawazo chanya.

Kuna mfano wa mtu mmoja aliyeona kuwa kama angekuwa na gari zuri la kifahari, furaha yake ingetimia. Kutokana na kupenda kuwa na gari, mara kwa mara alikuwa akiota kuwa na gari hilo.

Mtu huyo kila alipokuwa akijiwazia kama yupo kwenye usukani wa gari, alihisi ananusa harufu nzuri ndani ya gari. Na kwamba alihisi kama yupo barabarani analiendesha gari hilo.

Muda mfupi baadaye, alipandishwa cheo ofisini kwake na kujiona kuwa yale aliyoyatamani ameyapata. Na kwamba ataweza kujitosheleza kwa kile alichokihitaji. Baada ya kupata gari lile alilokuwa akilihitaji, alijikuta tena akitamani kila mwanamke aliyemuona, hali iliyofanya matumizi yake kuongezeka kuliko kipato kile alichokuwa akikipata.

Na kwamba wanawake aliowapenda hawakuwa na upendo wa dhati kwake, ila ni kwa kuwa walimuona anaendesha gari zuri la kifahari, kutarajia kupelekwa katika hoteli nzuri za kifahari, pamoja na kupewa zawadi nzuri za gharama.

Baada ya muda mchache alibaini kuwa, gari hilo badala ya kumpatia furaha, alipata maumivu, kwa sababu pesa yake ilitumika katika mambo ya kifahari zaidi. Taratibu alianza kufikiria gari lake na marafiki wapya aliowapata baada ya kuwa na gari, pamoja na kujiuliza kama kweli wanawake wale walikuwa wakimpenda kwa dhati ama walilipenda gari lake.

Furaha yake kuhusiana na gari lile ikaanza kutoweka, alianza kupata sononeko katika nafsi yake, pamoja na kuona gari lile kwamba ni mzigo. Hali hiyo ikamkatisha tamaa kwa yale aliyoyategemea, kwamba gari ndiyo utimilifu wa furaha katika maisha yake.

Ni vema kukumbuka kuwa vitu vinavyoonekana kwa macho haviwezi kuleta furaha ya kweli. Kwa sababu watu wanaotafuta furaha kwa kutumia fedha, ukuu walionao, utajiri ama mali walizowekeza, ni sawa na kuitafuta furaha hiyo kwa muda tu, na si ya kudumu. Kwa kuwa, siku zote fedha haziwezi kununua furaha.

Kuna mifano ya watu wengi ambao ni matajiri, lakini wamekuwa wakikabiliwa na matatizo mengi. Hawana furaha kama uliyo nayo wewe au mimi. Ni ukweli kwamba, fedha waliyonayo inawapa matatizo mengi na furaha kidogo.

Watu wengi mashuhuri wamekuwa wakiishi maisha ya kukata tamaa, matokeo yake, wengi wao huamua kujiua. Hivyo basi, furaha haipatikani kwenye utajiri, marafiki, kutumia dawa za kulevya ila ni katika kuituliza akili yako.

Tukiangalia katika maandiko matakatifu ndani ya Biblia, ambayo ndugu zetu Wakristo wanaiamini, yanasema kwamba heri wale walio maskini wa roho kwa maana ufalme wa Mungu ni wao, heri wale wenye huzuni kwa kuwa watarehemiwa. Heri wale wenye upole kwa kuwa watairithi nchi. Heri wale wenye njaa na kiu ya haki kwa kuwa watashibishwa. Heri wale wenye mioyo safi kwa kuwa watamuona Mungu. Heri wale wapatanishi kwa kuwa wataitwa wana wa Mungu.

Hivyo basi, neno heri lina maana ya furaha, hivyo bila kujali kama umeshinda ama umeshindwa, umefanikiwa ama hujafanikiwa, una furaha ama unatabika. Kwa hiyo mtu yeyote anayesoma maneno hayo na kuyarudiarudia moyoni mwake, anajikuta ni mwenye furaha wakati wote.


Tukutane Alhamisi ijayo.

HOFU HUSAIDIA KUEPUKA HATARI

KARIBU mpenzi msomaji katika safu ya Maisha Yetu inayokujia kila Alhamisi. Leo tutaangalia mbinu za kuwa jasiri katika uamuzi wako unaoufanya.

Katika maisha yetu ya kila siku, tunaona kwamba mbinu za kuwa jasiri ni nzuri katika kukabiliana na hatari iliyo mbele yako. Lakini kwa wakati mwingine, mtu anapokuwa na hali ya hofu inamsaidia kutokana na sababu iliyopo.

Ama tunaweza kusema unapokuwa na hofu, hali hiyo inakusaidia kwa kusudi maalumu. Ila kuna baadhi ya watu ambao hufikiri kuwa, si vizuri mtu kuwa na woga ama hofu. Lakini hii si kweli.

Kwani hali ya hofu husaidia, ni ishara katika ubongo wako kwamba pale huenda pakawa na hatari. Zipo sababu nzuri zinazopasa kuwa na hofu, kwa kuwa hofu inayozungumza ndani yetu ni vema kuilinda mwenyewe.

Kutokana na hofu unapokumbana na jambo, unajikuta hufikiri cha kufanya kwa wakati huo, ila unajikuta unaondoka katika eneo hilo kwa haraka.

Pia kuna baadhi ya watu wamejijengea tabia kama ya watoto wadogo ya kutokuwa na woga katika maisha yao. Lakini wakumbuke hali hiyo mara nyingine huwaletea matatizo.

Kwa mfano watoto wanapokuwa sio waoga, huwa na sehemu ya kuegemea ambayo ni wazazi wao. Wanakuwa hawana woga wa kuruka katika maeneo hatarishi, wakijiona kuwa wako salama.

Hivyo, kama watu wazima watafanya michezo ya kitoto watajikuta wakipoteza maisha kutokana na hatari mbalimbali kama vile ajali za barabarani au ugomvi.

Woga maana yake unatuepusha na hatari zilizoko mbele yetu. Hofu ipo ili kuwakinga watu wasipoteze vitu vyao vya thamani, kama vile pesa. Watu ambao hawana hofu ya kupoteza fedha zao, huzifanyia kazi zisizo na faida na baadaye kusababisha hasara kwao.

Pia hofu, humfanya mtu aliyepewa jukumu la kusimamia jambo fulani, kujiandaa mapema ili asiharibikiwe. Hebu fikiria mtu hana hofu anapohojiwa kwenye mhadhara kuhusu jambo fulani huku akiwa hana upeo nalo, pia hajajiandaa. Matokeo yake katika mjadala huo huonekana mjinga. Hivyo hofu humfanya mtu kuwa makini, pamoja na kuwa na maandalizi mazuri.

Unapaswa kuwa na hofu ili kuweza kujiandaa na hatari zilizo mbele yako, kama za kimaumbile, kifedha ama kijamii. Kama mvua zisiponyesha ina maana kutakuwa na njaa. Hivyo taifa lolote lililo makini hutafuta njia mbadala ya kukabiliana na hali hiyo.

Hii ni kutokana na hofu huenda siku za mbeleni, wananchi wakakosa chakula na kupata utapiamlo ama kufariki dunia. Lakini pia, ukumbuke kuwa, hali hiyo ikizidi inaingilia uhuru wa maisha yako. Watu wengi wamejikuta wakiwa na hali ya hofu ama woga kupita kiasi. Hali ambayo si nzuri kwao.

Kwa sababu hofu ni hisia zinazofanya damu yako ichemke, na mara nyingi unajikuta unahamaki kwa kusema kuwa ‘aah! Ngoja nitoke eneo hili ni la hatari’.

Na kama hali hiyo itakuwa inakutokea mara kwa mara, linakuwa sasa ni tatizo ambalo unatakiwa kulitatua. Kwa kawaida kila mmoja anakuwa na kiwango kidogo cha hofu isiyo ya kawaida.

Kwa mfano unakuta daraja kubwa linajengwa na kuanza kupatwa na hofu kwamba daraja hilo litabomoka. Huhisi hivyo hata kama inaonekana kuwa kwa hali ya kawaida si rahisi kwa daraja hilo kubomoka. Hilo ni tatizo linalohitaji ufumbuzi.

Wengine wanakuwa na woga wa kufanya mazoezi mbalimbali ya darasani, matokeo yake wanakwepa kabisa ama kufanya vibaya. Bahati nzuri ni kwamba kuna njia muafaka ya kuondoa hali hiyo, kwa kutathmini tatizo lililopo.

Kama vile, kuwa na mbinu ya ujasiri, ili kuweza kukabiliana na hali hiyo, kwa kuangalia ukubwa wa tatizo. Kwa mfano; mwanafunzi anatarajia kufanya mtihani wake, ambao una maswali 100; amejiandaa vizuri. Japo mwanafunzi anakuwa na hofu ya kushindwa kwa baadhi ya maswali, lakini kwa kuwa alishajiandaaa vizuri atakuwa katika nafasi nzuri.

Nini cha kufanya kuhusu hofu na hatari iliyopo. Cha msingi ni kuangalia ukubwa wa hali hiyo na kuitatua kabla. Kwa mfano, mtu anayehofu kuwa malipo yake yatapunguzwa. Hataogopa kwa hilo, bali atakuwa na hofu kwa kuwa hakutegemea hali hiyo.

Ili kukabiliana na hali hiyo ni vema kutafuta kazi nyingine itayomlipa zaidi, kwa kufanya hivyo atakuwa amelikabili tatizo hilo. Kuna mambo tunayoweza kuyafanya ya kuondoa hali hiyo ya hatari, iwe kubwa ama ndogo. Kuna mambo matatu ya kufanya tunayoweza kuyachagua.

Mojawapo ni homoni zinazoshtua mfumo wa damu, wakati upatwa na jambo linalokutia hofu. Homoni hizo zinasaidia kama mtu anataka kukimbia ama kujikinga na jambo.

Zinafanya mwili kuwa na utayari wa jambo lolote. Pia ni vizuri kujiepusha ama kuondoka katika sehemu inayoweza kuwa na hatari. Maana yake ni kwamba kama upo kwenye eneo hilo la hatari, yakupasa kuondoka mara moja.

Kwa kufanya hivyo, utakuwa umefanya uamuzi wa busara. Vema kujijengea uwezo na kuwa tayari katika kupambana na jambo la hatari. Hilo litakuwezesha kukabiliana na jambo lolote kwa urahisi.

Mfano kama wewe ni mwimbaji mzuri yakupasa ujiandae vema. Pia kufanya majaribio kunafanya kazi yako iwe nzuri yenye kiwango cha kuridhisha. Inamaanisha kuwa, unaiandaa akili yako kuimba mbele ya watu katika tamasha.

Hebu fikiria kuwa una hofu ya kuendesha gari, ni vema kukaa mbali na usukani. Kujijengea uwezo na maandalizi kunakufanya uwe mwangalifu na kumwangalia mwingine wakati anapoendesha. Hukufanya ujifunze mengi kupitia kwa mwingine, mwishoni hofu hiyo itaondoka.

Tukutane wiki ijayo.

ZUNGUMZA NA MTOTO WAKO ASIPATWE NA MSONGO

KARIBUNI wapenzi wasomaji katika siku nyingine ya leo, ambayo Mwenyezi Mungu ametujalia kuiona tena. Tunakwenda kuangalia hali ya msongo inayowakabili watoto pamoja na vijana wadogo.

Ni ukweli usiopingika kuwa hali ya msongo inakuwepo katika hatua zote za maisha ya binadamu. Tunaona watoto wengi wenye umri wa miaka mitano na kuendelea, wamekuwa wakiona vitu mbalimbali katika nyumba zao ambavyo hufanywa na wazazi wao.

Kwa mfano, kuna familia nyingine kila mara wazazi hugombana mbele ya watoto wao. Kama wazazi tuelewe, hali hiyo huleta hofu kwa mtoto na kuona kuwa baba au mama yake anaweza kumpiga wakati wowote. Wakati mwingine unakuta mzazi anaumwa na jino, maumivu anayoyapata anayaonyesha mbele ya mtoto wake, hali hiyo humjengea hofu.

Kwani kuanzia hapo, inawezekana kabisa, mtoto huyo akapatwa hali ya woga na hofu, juu ya meno yake. Hata pale atakapoumwa atalia na maumivu makali. Tukiachana na hofu hiyo, hofu nyingine kwa watoto ni pale wanapomuona daktari au hospitali.

Inawezekana kwa wakati huo, mtoto haumwi lakini, anapomuona daktari akiwa amebeba sindano au vifaa vya hospitali,akiwa anatembea maeneo ya shuleni ama sehemu yoyote, hata kama daktari hana mpango wa kuongea na mtoto huyo, mtoto hubadilika muda huo huo, wengine huanza kulia.

Hivyo, kwa haraka haraka utaona ni jinsi gani mtoto anakuwa hajaandaliwa kukabiliana na mazingira mbalimbali ili asikabiliwe na hali ya wasiwasi katika maisha yake. Kuna maeneo mawili ambayo watoto hupatwa na hali ya msongo katika maisha yao, ambayo dalili zake huonekana kwenye maumbile ama tabia zao.

Tukiangalia kwenye dalili za kimaumbile, ni kama vile kupatwa na gesi tumboni, kupatwa na hali ya ubaridi kwenye viganja vya mkono na unyayo.

Hali ya kukosa choo, kuharisha, kukaukiwa midomo, uso kubadilika, tumbo kuvurugika, mikono kutetemeka, kichwa kuuma, moyo kudunda pamoja na kutokwa na jasho.

Nyingine ni mtoto kuuma kucha zake, kuwa na hofu, uso kuwa na mafuta, hali ya kutetemeka, kupumua kwa shida, kutokwa na jasho mikononi na miguuni, meno kukakamaa, kukaza kwa misuli, kukaza kwa tumbo na macho kuwa mazito.

Kwa upande wa dalili za tabia ni kama vile, kupata ajali na kuanguka kwa kuelekea mbele, kupenda ugomvi, kujilinda, kuwa tegemezi, kushituka shituka, kuwa na hofu, kutopenda kuwasiliana na watu, kuumwa mara kwa mara na kuchoka, kujiamini kupita kiasi, kuwa na hisia zilizopitiliza, kutopenda kujishughulisha na kitu, kukosa nidhamu, utukutu, mwenye mambo ya kuficha ficha, kukata tamaa haraka na kutokuwa na ushirikiano.

Pia anakosa utulivu wa kusikiliza jambo, anakuwa na tatizo la mara kwa mara la kulala na kuota ndoto za kuzungumza kwa sauti, hupenda kuzungumza uongo ama kupotosha ukweli, anachukulia vitu kama si vya kwao, maendeleo yake ya shule hushuka, anakuwa na mwonekana mbaya pamoja na umaridadi wake kupungua, anakosa hamu ya kupenda kujua vitu bila sababu ya msingi, ana kuwa na mabadiliko katika ulaji wake wa chakula, anaweza kula chakula kidogo ama kingi sana.

Mzazi ama mlezi huweza kubaini mabadiliko hayo kwa mtoto, kama anakuwa na uhusiano wa karibu na mtoto huyo.

Pia ni vizuri pale unapobaini mabadiliko hayo, uendelee kuwa karibu zaidi na mtoto huyo. Ni vizuri kumuandalia mlo uliokamilika, wenye virutubisho vyote, mpe nafasi ya kufanya mazoezi na kupumzika, mtie moyo aweze kusaidia shughuli ndogo ndogo na kumpa vichekesho.

Pia ni vizuri kuwaruhusu watoto wazungumzie mambo yale yanayo wakosesha raha, kwani wakati mwingine watoto waliokuwa kidogo hali hiyo husababishwa na kujiingiza katika mahusiano baina ya watoto wa kike na kiume.

Kwa upande wa wale watoto wenye umri kati ya miaka 9 na 20; mara nyingine hupatwa na hali ya msongo kutokana na umri huo, kwani hudhani kuwa wanaweza kujitawala wenyewe kwa kila jambo, hujihusisha kwenye mahusiano yasiyofaa, na wanapoonywa hufikiria kuhama nyumbani na kuwaacha wazazi wao.

Kipindi hicho, wazazi nao hupatwa na msongo kutokana na kitendo cha watoto hao ambao kuwa na maamuzi yao wenyewe, hali inayowafanya waondoke nyumbani. Wazazi huwaza kwa kuona watoto bado wanahitaji msaada kutoka kwao.

Hivyo, ni jukumu la wazazi kutumia nafasi hiyo kuwaelimisha watoto wao, kuwa vile wanavyofikiri sivyo maisha yalivyo. Pia wazazi wanapogundua mabadiliko mbalimbali juu ya watoto wao, ni vema kuchukua hatua za haraka na kuwasaidia kuliko kuwaacha wakaharibikiwa.

Mara nyingi wazazi wanaowafuatilia watoto wao, hugundua mapema kuwa, watoto wameshuka kimasomo ama hawapendi kwenda shule, ama mtoto kwa kipindi hicho badala ya kuwaza kusoma anafikiria kuacha shule na kufanya kazi.

Watoto wengine hukatiza kozi wanazozisoma, si kwa sababu wamekuwa hawafanyi vizuri bali ni kutokana na kutaka kuwa na ushindani wa kupata maisha bora, wakati anakuwa hajamaliza hata masomo yake. Kwa upande wa watoto wa kike, hali hiyo huwafanya kupata mimba wasizozitarajia, ama kuwaza kujiua.

Wengine hujiingiza kwenye ulevi ama mihadarati. Lakini kwa kufanya hivyo hawawezi kupata suluhisho, hivyo ni vema watoto wanapokumbana na hali hiyo kuidharau na kuendelea na masomo yao, wakielewa kuwa kipindi hicho ni cha muda tu, la maana ni kuongeza bidii katika masomo.

Hivyo, ni vema kukaa na mtoto wako na kumfundisha mambo mbalimbali ili aweze kuendelea katika dunia hii iliyojaa misukosuko ya maisha. Penda kumsikiliza mtoto wako na kumshauri jambo zuri na baya. Pia mtie moyo kwa matarajio yaliyoko mbele yake kwamba akimaliza masomo yake ya msingi, atakwenda sekondari, halafu chuoni, baada ya chuo atapata kazi nzuri ili awe na ari ya kusoma.

Tukutane wiki ijayo.


WANAWAKE HUKABILIWA NA MSONGO KATIKA MAZINGIRA TOFAUTI

KARIBU mpenzi msomaji katika siku nyingine ambayo Mwenyezi Mungu ametujalia pumzi na uhai. Leo tutaangalia hali ya msongo inayowakabili wanawake.

Wanawake wengi duniani, wamekuwa wakikabiliwa na changamoto nyingi, hali inayowafanya kupatwa na hofu, wasiwasi pamoja na kutojiamini.

Changamoto nyingi huwakabili wanawake hao katika maeneo yao ya kazi, nyumbani na hata katika mazingira mbalimbali wanayokuwamo.

Kwa mfano, kuna msemo usemao kuwa, binadamu wote ni sawa, lakini ukifuatilia msemo huo utaona kuwa, mara nyingi baadhi ya wanaume hawataki kukubaliana na msemo huo, kwa maelezo kuwa, wanawake hawana uwezo wa kufanya kazi zile ambazo wao huzifanya kwa umakini na uhodari.

Kutokana na hali hiyo, ndiyo maana katika siku hizi za leo, wanawake nao wamekuwa wakihamasishana kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika serikali na kwenye ofisi mbalimbali, ili nao waonyeshe kuwa wanaweza kuongoza.

Pamoja na jitihada hizo, wanawake wamejikuta katika kipindi kigumu, pale wanaposhika nyadhifa mbalimbali, hujikuta wakidharauliwa ama kutokukubalika katika jamii, hata kama ana uwezo wa kuongoza, cha msingi ni kukabiliana na changamoto hizo, endapo unajiamini na kujiona kuwa una viwango vya kuwa kiongozi bora, na si bora kiongozi.

Wengine kwa fikra zao hudhani kuwa, wanawake hawawezi kuwa viongozi bora kwa sababu ya mwonekano wao, huamini kuwa, wanawake wengi hawajiamini.

Kutokana na changamoto hizo, wanawake wengi walio katika nafasi mbalimbali za uongozi hujikuta wakikabiliwa na hali ya msongo, inayomfanya kushusha kiwango chake cha utendaji na kuwapa nafasi nzuri wanaume kuamini kuwa wao pekee ndiyo wanaweza.

Lakini utafiti mwingine umebaini kuwa, wanawake wenye uwezo na elimu ya kuridhisha wamekuwa wakijiamini kuwa wanaweza, hali iliyowafanya kukubalika katika maeneo wanayoyaongoza.

Vile vile kwa suala la maumbile, wanawake wengi wamejikuta wakikabiliwa na hali ya woga, ama hofu ya kupoteza kazi. Wanawake hukabiliwa na changamoto ya kuona siku zao katika kila mwezi, hivyo wapo ambao huumwa sana hata kuwafanya walazwe hospitali ama kushindwa kwenda kazini kabisa.

Hali hiyo, huwafanya wakose amani, furaha ama hofu ya kwamba, huenda wakafukuzwa kazi.

Na wengine hujitahidi kwenda hivyo hivyo kazini lakini hujikuta wanapatwa na maumivu makali ya viungo, kichefuchefu, tumbo kuuma, macho kuwa mazito na hali ya kukata tamaa.

Katika hali kama hiyo, ni uhakika kuwa hataweza kuendelea na kazi zake hivyo itambidi arudi nyumbani na kwenda kupumzika.

Hivyo ni vema kwa kila mwanamke kujikubali katika hali hiyo aliyonayo, ili asiruhusu hali ya wasiwasi katika maisha yake, inayoweza kumwongezea maradhi mengine ya ziada.

Vile vile msongo huwapata baadhi ya wanawake, pale anapokaa muda mrefu bila kupata mtoto. Hivyo asipokuwa makini na kukabiliana na hali hiyo mwili wake utapatwa na maradhi mengine ambayo hakuyatarajia.

Vile vile hupatwa na msongo pale anapohisi maumivu makali kipindi cha kujifungua, ama kujifungua mtoto mwenye matatizo kiafya.

Pia kushindwa kuzaa kwa njia ya kawaida na kumfanya afanyiwe upasuaji, vitendo vya udhalilishwaji anapokuwa kwenye wodi ya wazazi wanaosubiri kujifungua, upungufu wa wakunga au kusikia kelele katika wodi hiyo.

Wengine hufikiria kuwa, waume zao hawatakuwa tayari kumfurahia mtoto aliyezaliwa, kutofurahia ndoa yake pamoja na kuruhusiwa kutoka hospitalini, huku akiwaza mtu wa kumsaidia anaporudi nyumbani kwake.

Hofu zote hizo zinazowakabili wanawake, huwafanya kutokujiamini na kuongeza msongo katika maisha yao.

Wengine hufikiri kuwa, endapo waume zao wangekuwepo wakati wanapojifungua, hofu hiyo ingewatoka.

Pia wanawake wengine hukabiliwa na hali ya hofu na wasiwasi, kipindi kile anachonyonyesha, hasa wakati wa usiku.

Vile vile wanawake hukabiliwa na hofu na wasiwasi pale wanapotengana ama kufiwa na waume zao, pia wanapopewa talaka.

Kutokana na matatizo hayo, hali yake ya kawaida huondoka na kama hatapata msaada wa haraka anaweza kupatwa na magonjwa mbalimbali yatakayodhoofisha afya yake.

Hata pale wanawake hao, wanapofiwa na watoto wao wachanga hukabiliwa na msongo. Utafiti uliowahi kufanywa ulibaini kuwa, baadhi ya wanawake wanapofiwa na watoto wao, hujiua ama hupata ajali kutokana na kuwa na mawazo mengi wakati wanapotembea.

Wengine hufariki dunia kwa maradhi ya moyo, kansa ama ugonjwa mwingine. Hivyo, ni vema kila mmoja akaigundua hali hiyo mapema na kuidhibiti, kwa kupata ushauri kutoka kwa daktari.

Wakati mwingine mwili wake hudhoofika kwa kuwa hapendi kula, ama huwa anachagua vyakula vya kula, ama jambo analolifikiri kwa kipindi hicho.

Hali hiyo huweza kudhoofisha mwili wake hata mifupa. Kwani mlo usio kamili ama kula bila kufuata mpangilio, kunaathiri uimara wa mifupa mwilini.

Pia wanawake wengi wanakabiliwa na suala la msongo kutokana na suala la kiuchumi, pale wanapoona wanashindwa kukabiliana na maisha hujikuta na hofu pamoja na wasiwasi, kwa kuwa, wengi wao hawapati msaada kutoka kwa waume zao.

Kutokana na hali hiyo wanayokabiliana nayo, wanawake wengine hujikuta wakijiingiza kwenye ulevi wa kupindukia kwa nia ya kuondoa mawazo, hali inayowafanya kushindwa kufanya kazi kwa bidii.

Tukutane Alhamisi ijayo

MSONGO KATIKA SEHEMU ZA KAZI (4)

NAWAKARIBISHA tena katika safu hii ya Maisha Yetu yenye lengo la kukufahamisha jinsi maisha yalivyo na yanavyopaswa kuwa.

Leo tunaendelea na mada yetu ya msongo katika maeneo ya kazi ili uweze kujua jinsi ya kukabiliana na hali hiyo mara unapokutana nayo.

Watafiti mbalimbali wamegundua kuwa, endapo bosi katika kampuni, atakuwa na hali ya msongo wa mawazo, ofisi, kampuni au shirika hilo litakuwa na mawasiliano mabaya.

Naye mwanasaikolojia mmoja anayeshughulika na masuala ya viwandani amewahi kuelezea jinsi meneja mzuri anavyopaswa kuwa.

Kwa maelezo ya mwanasaikolojia huyo, meneja mzuri anapaswa kuwa mshauri mzuri kwa wafanyakazi wake, ari ya kupenda kujituma, kupenda kufanya kazi na kushirikishana mambo mbalimbali na wafanyakazi wake.

Kwa maelezo ya mwanasaikolojia huyo, endapo bosi atakuwa karibu na wafanyakazi wake, ushauri mwingi utakaotoka kwa wafanyakazi hao, utampa mwanga wa kujua nini cha kufanya kwa kipindi hicho katika kuboresha ofisi.

Ndiyo maana katika ofisi nyingi ni rahisi kutambua sababu za meneja fulani kuwa mzuri, au wa kawaida ama mbaya katika utendaji wake, kutokana na jinsi anavyojishughulisha na watu wake.

Meneja mzuri ni yule anayependa kuwa karibu na wafanyakazi wake, kuwasikiliza na kufuatilia uzalishaji unavyokwenda katika kampuni.

Pia anakuwa mwadilifu katika utendaji wake, hatetereki katika malengo yake ya uzalishaji, pia huwasikiliza wafanyakazi wake wanapokuwa na mahitaji.

Bosi wa wastani katika utendaji wake, ni yule anayeangalia ufanisi wake pekee, bila kuona umuhimu wa wengine. Kama vile wanavyowajibika katika kazi zao.

Kwa upande wa bosi mbaya ni yule anayefanya kazi kwa kutumia vitabu, pamoja na kujenga hali ya kujilinda kila wakati.

Utafiti mwingine uliofanywa, ulionyesha kuwa, msongo katika kazi unawafanya watu wengi kutumia vileo na kujikuta wanashindwa kufikia malengo katika kazi zao, hali inayowafanya kufukuzwa kazi.

Wengine wanaokabiliwa na msongo, hutumia dawa za kulevya, hali inayowafanya kupatwa na magonjwa ya akili, kuathiri utendaji wao katika uzalishaji na kuhatarisha ajira walizonazo.

Utafiti mwingine unaonyesha kuwa, msongo mwingine kwa wafanyakazi huchangiwa na uamuzi unaofanywa na kampuni kwa kuwapunguza kazini wafanyakazi kutokana na sababu mbalimbali.

Hivyo basi, ni vyema kwa mameneja katika ofisi zao kuzungumza na kuwasikiliza wafanyakazi wao.

Pia wawe wanawauliza wafanyakazi hao kuchanganua mambo matatu yanayoweza kuboresha kampuni au ofisi hiyo na mambo matatu yatakayoweza kuzorotesha uzalishaji katika kampuni hiyo.

Bosi huyo apende kujua kama mazingira wanayofanyia kazi wafanyakazi wake, yanaridhisha.

Ni vema bosi kuwaheshimu watu aliowaajiri ama anaowasimamia katika kampuni hiyo na kuwajulisha kuwa yuko tayari kushughulikia taarifa yoyote itakayomfikia.

Ni vema wafanyakazi wakawa wanashirikishwa katika maamuzi yanayofanyika ili wajione nao ni sehemu ya ofisi hiyo.

Si mbaya wakaorodhesha matatizo mbalimbali yaliyowapata wafanyakazi na kuangalia jinsi ya kuyashughulikia.

Ni vizuri kiongozi huyo akawa anaongoza kwa vitendo. Asiwe mwepesi wa kuzungumza.

Hayo yote yatakapoweza kutekelezwa na mameneja ama waajiri wa kampuni, msongo katika eneo hilo la kazi hautawapata wafanyakazi wake.

Ugonjwa mbaya katika kampuni ni ile hali ya wafanyakazi kukosa ari ya kufanya kazi kutokana na msongo wanaokabiliana nao.

Hiyo ni pamoja na kupunguza ari ya kupenda kazi kwa wafanyakazi, utendaji mbovu na unaopunguza uzalishaji, kuongezeka kwa magonjwa miongoni mwa wafanyakazi, wafanyakazi kuchelewa kazini hali inayosababisha kampuni hiyo kutokufikia malengo iliyokusudia.

Vile vile baada ya kampuni kupunguza wafanyakazi, wale wanaobakia nao wanaendelea kupatwa na hali hiyo ya msongo kwa kuwa, kunakuwa na ongezeko kubwa la kazi hali itakayowafanya washindwe kupata muda wa kupumzika.

Tukutane alhamisi ijayo

MSONGO KATIKA SEHEMU ZA KAZI (3)

KARIBUNI wapenzi wasomaji katika siku nyingine ambayo Mwenyezi Mungu ametujalia kuiona.

Leo tutaendelea kuangalia mada kuhusu msongo katika sehemu za kazi.

Wengi wetu tumekuwa tukikabiliana na hali ya msongo katika vipindi mbalimbali vya maisha, kuanzia kipindi cha utoto hadi uzee.

Hali hiyo humpata mtu anayefanya kazi, mzazi katika kipindi cha kulea watoto wake na katika vipindi mbalimbali vya maisha.

Ila humjia kila mmoja kwa jinsi yake.

Mafanikio yetu katika maisha na thamani ya maisha, inategemea ni jinsi gani tunavyokabiliana na hali hiyo.

Tunahitaji kuelewa msongo ni kitu gani na kujifunza jinsi ya kukabiliana na hali hiyo.

Mtaalamu mmoja aliwahi kuelezea fani saba ambazo haziepukiki katika suala la msongo, ambazo ni fani ya ualimu, uuguzi, umeneja, ustawi wa jamii, udereva, upolisi na ofisa magereza.

Je, umejiona katika kundi lolote hapo juu? Usijali kuhusu hilo, cha msingi ni kujua unafanya nini na jinsi gani ya kujiepusha na msongo katika kazi yako.

Pia inawezekana wewe ni miongoni mwa watu zaidi ya 200,000 ambao hupatwa na maradhi yanayotokana na hali ya msongo katika kazi zao, kila mwezi na kulazimika kupumzika nyumbani ili kuondoa hali hiyo.

Pia yawezekana kwamba, wewe ni miongoni mwa asilimia 27 ya watu wanaolalamikia mazingira ya kazi zao, ama kati ya asilimia 19 ambao hawana mazingira bora ya kufanyia kazi, au asilimia 17 ya wale ambao ofisi zao haziko katika muundo wa kisasa hivyo kufanya kazi zao kuwa ngumu, kwa kuwa hakuna mwanga au hewa ya kutosha.

Pia yawezekana umo miongoni mwa asilimia 14 ya wale wafanyakazi ambao hawana nafasi ya kutosha ya kukutana na wenzao, kutokana na kazi kuwa nyingi, asilimia 13 ya wale ambao hawajaridhika na eneo ambalo ofisi yao ipo, asilimia 12 ya wale wasio na vifaa vya kisasa ofisini kwao, asilimia 5 ya wale wanaolalamika kuhusu kukosa uhuru wa kuvuta sigara ama mazingira wanayofanyia kazi hayana uhuru wa kumfanya avute sigara na asilimia nne wanakosa ushirikiano na wafanyakazi wengine.

Je, hofu kuhusu kazi yako inaongezeka bila kupata suluhu? Uamuzi wako wa mwisho ni kubadili kazi na kuchukua tahadhari kwa hatari unazoweza kukabiliana nazo katika kazi hiyo mpya.

Lakini lazima uchukue tahadhari, kwa sababu ni gharama.

Pia utaona kuwa, mpangilio mbaya wa kazi zako unaweza kukusababishia maradhi.

Utawala mzuri huwafanya wafanyakazi kuwa na afya bora, hivyo uzalishaji unakuwa mzuri pia.

Utafiti mwingine uliofanywa kwa wafanyakazi 600, asilimia 60 kati ya hao wamewalalamikia watengenezaji wa barabara kuwa wanachangia msongo katika maisha yao, kutokana na kusababisha foleni wawapo barabarani, asilimia 40 wamesema kuwa, malengo waliyojiwekea hawajaweza kuyafikia hivyo yanawasababishia hali hiyo.

Wengine walisema kuwa, hali ya hofu na wasiwasi wanayoipata wanasababishiwa na rafiki zao, ama kutoelewana kwa wafanyakazi ndani ya ofisi.

Pia katika ofisi nyingi, suala la mapumziko limekuwa ni kitendawili, wafanyakazi hawapati mapumziko wawapo kazini, hali inayosababisha hofu, wasiwasi na hasira za mara kwa mara.

Ni wafanyakazi wachache wanaoweza kupata muda wa mapumziko na kwenda kupata chakula cha mchana, wengine kutokana na muda kuwa mdogo kwa ajili ya kazi nyingi hujikuta wakipitisha mchana bila kula chakula.

Vile vile haijalishi wewe ni nani, unaweza kukabiliwa na msongo katika mazingira ya ofisi.

Tuangalie mfano wa sekretari, ambao wamekuwa wakisumbuliwa na hali ya hofu na wasiwasi katika kazi zao.

Hivyo msongo mkubwa huwakabili kutokana na kazi zao za kila siku wanazozifanya.

Sekretari hupatwa na msongo pale anapokuwa ana kazi nyingi mara simu inaita au wageni wanafika na kuuliza habari mbalimbali zinazomhusu bosi wake, ilhali kipindi hicho anahangaika akamilishe kazi ya bosi wake anayoisubiri ili aanze kikao.

Vile vile hupatwa na msongo pale mashine yake ya kutolea ‘photocopy’ inapokwamisha karatasi au kukwama ama inaposhindwa kufanya kazi kwa kipindi hicho anachohitaji kuitumia huku akiwa anakabiliwa na kazi nyingine.

Wakati huo huo, kunakuwapo na watu wanaosubiri kuweka ahadi ya kuongea na bosi wake, ambao hawako kwenye ratiba ya siku hiyo.

Vile vile hukabiliwa na msongo pale anapopata kazi nyingine ya dharura ilhali alishajiandaa kwenda nyumbani.

Mbali na hali ya msongo wa kawaida, wanayokabiliana nayo katika shughuli zao za kiofisi, kwa upande mwingine hulalamika kupewa kazi za dharura na mabosi wao, wakati hakuna posho.

Wanapewa kazi zinazopoteza nguvu zao na kuwafanya washindwe kuwasiliana na watu wengine, pia wapo wanaolalamikia masuala ya ngono.

Hayo yote yanajumuisha mazingira mabovu ya ofisi, muundo mbaya wa viti vya ofisi ambavyo havimpi starehe mtumiaji na badala yake vinamfanya achoke na kuchukia mazingira ya ofisi anayofanyia kazi.

Hivyo unapoona una dalili ya kuchoka, ama kuumwa mara kwa mara, ni vema kuangalia afya yako ilhali isiwe mbaya zaidi.

Utafiti uliofanywa katika nchi za wenzetu mwaka 2003, ulibaini kuwa, asilimia 35 ya mabosi wamekuwa wakikubali majukumu mbalimbali ya ofisi zao ili kuwafanya wafanyakazi wao, wasipate msongo ama kupunguza hali hiyo kabisa.

Tukutane wiki ijayo

MSONGO KATIKA SEHEMU ZA KAZI

KWA mara nyingine nawakaribisha tena katika safu hii ya Maisha Yetu, inayokujia kila Alhamisi, lengo likiwa ni kuelimisha.

Wiki iliyopita tulizungumzia kuhusu msongo katika maeneo ya kazi, tuliona sababu zinazosababisha mtu kupatwa na msongo katika eneo la kazi ni hofu, ongezeko la muda wa kazi, ilhali masilahi ni madogo na msisitizo wa kuongeza uzalishaji kazini wakati hakuna ongezeko la marupurupu yoyote.

Leo ni mwendelezo wa makala ile na tutaangalia jinsi ya kuondoa hali hiyo, ambayo kwanza inakubidi ujijali wewe mwenyewe.

Wakati msongo katika kazi yako unaingilia uwezo wako wa kufanya kazi, ni vema kujijali wewe mwenyewe, au kusimamia maisha yako mwenyewe, ni wakati wa kuchukua hatua.

Wakati unapodhamiria kujali mahitaji yako, unakuwa na nguvu ya kushinda hali hiyo ya msongo.

Vile vile unavyojihisi, unavyoweza kujizatiti, ndipo utakapoweza kusimamia kazi yako bila kuendelea kujisababishia msongo mwingine.

Kujijali mwenyewe hakujalishi maisha uliyonayo kama ni ya kifahari au la. Hata katika kufanya vitu vidogo vidogo vinaweza kuinua tena hali yako ya kuvunjika moyo na kukata tamaa, vitu hivyo vinaweza kukuongezea nguvu.

Fanya kitu kimoja kwa wakati na kufanya vile ulivyoamua maisha yako yawe, hapo utagundua kuwa kuna tofauti katika hali ile ya msongo uliyokuwa nayo, nyumbani hata kazini kwako.

Vile vile unaweza kuondoa hali hiyo kwa kuangalia picha mbalimbali. Kwa kufanya hivyo kunaweza kuinua tena hisia zako, kukuongezea nguvu, kukufanya uwe na matarajio ya baadaye na kutuliza akili na mwili wako.

Kwa kiasi kikubwa utaondoa hali iliyokuwa inakutesa. Pia kutengeneza chakula unachokipenda kutakufanya ujisikie vizuri.

Unapopangilia mlo wako, hata kama ni kidogo kutakufanya upate nguvu katika mwili wako na kujisikia vizuri.

Ili kuondokana na hali hiyo ni vema, kulala usingizi wa kutosha. Kwani hali hiyo inakufanya ukose usingizi.

Lakini hali ya kukosa usingizi, inaweza kukusababishia ukapatwa na maradhi mengine.

Unapolala na kukosa usingizi, hali hiyo inakuweka katika hatari ya kuwa na msongo zaidi. Lakini wakati unapokuwa umepata mapumziko mazuri, inakuwa ni rahisi kukabiliana na hali hiyo ya msongo.

Pia unaweza kuondoa hali hiyo kwa kutoa vipaumbele na kuwa na mpangilio katika kazi zako.

Wakati unazungukwa na hali ya msongo katika kazi na eneo lako la kazi, unaweza kukabiliana na hali hiyo kwa kuamua kuikubali hali hiyo ngumu inayokutesa na kujitahidi kukamilisha kazi zako kwa wakati.

Jitahidi kujitawala katika kazi zako wewe mwenyewe bila kusaidiwa na mtu, pamoja na kujenga mahusiano bora katika kazi.

Haya ni baadhi ya mapendekezo katika kupunguza hali hiyo kwa kutoa vipaumbele na kuwa na mpangilio katika majukumu yako.

Baadhi ya mambo yanayoweza kukuondolea hali hiyo

Ni vema kutengeneza ratiba. Changanua utaratibu wako wa kufanya kazi, majukumu, na shughuli za kila siku.

Kamwe usivuruge utaratibu uliojiwekea kwa kazi isiyokuwepo. Jaribu kutafuta uangalifu kati ya kazi, maisha ya familia, shughuli za kijamii na mambo binafsi na majukumu ya kila siku.

Kamwe usijiwekee ratiba zilizo nje ya uwezo wako. Epuka kuwa na ratiba ya mrundikano wa kazi katika siku moja.

Unapokuwa na ratiba ya kazi nyingi kwa siku moja, mara nyingi kazi hizo hufanywa chini ya viwango.

Ondoa kazi zile ambazo hazina umuhimu kwa siku hiyo katika ratiba yako.

Jaribu kuondoka mapema muda wa asubuhi. Dakika moja mpaka 15; zinaweza kufanya tofauti kwa kuweza kukamilisha kazi zako vizuri kwa siku hiyo na kukurahisishia utendaji wako wa siku hiyo.

Kamwe usijiongezee kiwango cha msongo unaokukabili kwa kuendelea kuchelewa ofisini.

Ni vema kuwa na ratiba ya kupumzika. Hakikisha unakuwa na muda mfupi wa kupumzika kwa ajili ya kuisafisha akili yako.

Pia ni vema kwenda mbali na meza yako unayofanyia kazi kwa ajili ya kupata chakula.

Na kwa kufanya hivyo kunaongeza ari yako ya kufanya kazi, kinyume cha hapo kutakufanya uwe na uzalishaji mdogo.

Mambo yanayoweza kukuondolea msongo katika kazi yako endapo wewe ndiyo mmiliki mkuu, ama mkurugenzi ni pale, unapotoa kipaumbele kwa kazi zilizopo.

Andika ratiba ya kazi unazoweza kuzifanya na uzifanye kulingana na umuhimu wake. Anza na kazi ile yenye umuhimu. Na kama una jambo la muhimu, ni vema kuamka mapema.

Kwa kuamka mapema, shughuli nyingine za siku hiyo zitakuwa na matokeo mazuri.

Ni vema kukabidhi majukumu yako kwa wengine. Huwezi kufanya kazi zote wewe mwenyewe, iwe nyumbani, shuleni au kazini.

Kama wapo watu wengine wanaoweza kufanya kazi hiyo, ni vema ukawashirikisha.

Hali hiyo itakupunguzia kuwa na msongo usio na lazima.

Twitter Facebook