Sunday, December 27, 2009

JINSI YA KUPANGA MALENGO YAKO

MSOMAJI wangu, nakukaribisha tena katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, zinzokujia kila Alhamisi.
Leo tutaangalia jinsi unavyoweza kupanga malengo makubwa katika maisha yako.
Watu wengi hushindwa kufikia malengo makubwa kwa kuwa, mara zote hujikatisha tamaa kuwa hawawezi kufanya jambo kubwa la kimaendeleo, kabla ya kujaribu kulifanya.
Tabia ya baadhi ya watu hao wanaokuwa na malengo madogo katika mazingira wanayoishi, ina maanisha eneo hilo hakuna ushindani wa kimaendeleo, ama wao wenyewe hawana jitihada za dhati za kupiga hatua zaidi mbele.
Lakini ikimbukwe kuwa, katika kutafuta mafanikio hayo ili uwe na maisha bora, usimwangalie mtu jinsi alivyo, kwamba ana urefu gani, ana pesa kiasi gani, digrii aliyonayo ama kuangalia historia ya maisha yake, bali hupimwa kwa uwezo wa kufikiri kwake.
Watu wengi wanaofikiria kuwa na malengo makubwa ya mafanikio, katika maisha yao ni kutokana na matarajio waliyonayo.
Inakupasa kila mara ujitahidi kupanua mawazo yako na kubuni mbinu mpya za kukutoa hapo ulipo na kukuweka katika hatua nyingine nzuri zaidi kimaendeleo.
Hivyo utambue kuwa, unapotaka kufanya mambo makubwa inakupasa ujijue wewe ni nani na una thamani gani.
Kwa maelezo mengine usijishushe hadhi yako kwa kuona kuwa huwezi kufanya mambo makubwa ya kimaendeleo ambayo yatakutoa hapo ulipo na kukuweka katika hatua nyingine nzuri zaidi.
Tuangalie mfano wa kijana mmoja aliyeshindwa kupiga hatua mbele baada ya kujishusha hadhi yake na kujiona hawezi.
Kijana huyo, aliona tangazo la kazi katika gazeti. Kazi aliyokuwa anapenda kuifanya na pia ameisomea.
Lakini hakufanya jitihada za dhati za kuomba nafasi ile, kwa kuwa alijiona hawezi kuipata hata kama angeomba.
Aliona kuliko ajitaabishe ni heri aache kuomba nafasi hiyo. Mfano huo si mzuri kwa mtu anayetaka kupiga hatua kimaisha.
Usijishushe hadhi yako ama usikatishwe tamaa kwa hali yoyote ile. Ni vema kujaribu kile unachokipenda na unachokihitaji katika maisha yako, kuliko kuacha kujaribu kwa kuogopa kuwa hautafanikiwa.
Kwani matokeo huja baadaye, hata utakaposhindwa, utakuwa na nguvu ya kujaribu tena sehemu nyingine.
Wengi wetu, tumekuwa tukijikatisha tamaa katika shughuli mbalimbali tuzifanyazo ama tunazotaka kuzifanya.
Yawezekana umeanzisha biashara kwa lengo la kukuinua kiuchumi, lakini matokeo yake, biashara hiyo haiendi kama vile ulivyotarajia.
Jambo la msingi, inakupasa kukaa chini na kujitathmini, kuangalia ni sehemu gani unayokosea.
Ama kuangalia, kama una washindani wengi katika eneo hilo, ili uweze kufanya vizuri zaidi yao, kwa kuweka vitu vingi tofauti na kuboresha eneo la biashara yako.
Kuwa mbunifu katika biashara yako kutakupa wateja wengi, na utafanikiwa zaidi. Cha msingi usikate tamaa katika kufikia malengo unayoyakusudia.
Kutokana na hali ya kujikatisha tamaa, miongoni mwa watu wengi, wanasaikolojia mbalimbali wamekuwa wakishauri ni vema, watu wajijue vile walivyo ili waweze kujirekebisha pale penye upungufu na kusonga mbele kimaisha.
Hali ya kujikatisha tamaa ni mbaya sana, ni sawa na ugonjwa usiopona katika mwili wako. Ili kuutibu ugonjwa huo, inakupasa ujielewe wewe ni nani, na una upungufu gani, pamoja na kukubali mabadiliko.
Tatizo kubwa lililopo kwa watu wengi, hawajui kuwa, wao wana uwezo mkubwa tofauti na wanavyojifikiria.
Hivyo ni vema kuweka mawazo yako kwenye kipimo halisi, uyachuje na kuchukua yale yaliyo na thamani.
Penda kufikiri mambo makubwa. Usijishushe hadhi yako kwa kujiwekea au kufikiri malengo madogo. Anza sasa kuwaza mambo makubwa ili uwe mtu mwenye ndoto njema ya maendeleo.
Kutokana na hali hiyo ya watu kujikatisha tamaa, wale ambao wamewahi kufanya biashara na kufilisika, wengi wao wamekuwa wakisema kuwa hawatarudia tena kufanya biashara hiyo.
Lakini kumbe, haikuwapasa kukata tamaa, bali kujipa moyo, na kuelewa kuwa pamoja na hali hiyo ya kushindwa inawapasa kujaribu tena.
Kamwe usikate tamaa katika jambo lolote unaloliwaza ama kulifanya. Kwa kuwa, upo msemo mmoja unaosema, penye nia pana njia.
Tukutane wiki ijayo.
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa kitabu cha ‘The Magic of Thinking Big’, kilichotungwa na David Schwartz pamoja na mitandao mbalimbali.

2 Maoni:

This comment has been removed by the author.
Twitter Facebook