Friday, August 28, 2009

WANAWAKE HUKABILIWA NA MSONGO KATIKA MAZINGIRA TOFAUTI

KARIBU mpenzi msomaji katika siku nyingine ambayo Mwenyezi Mungu ametujalia pumzi na uhai. Leo tutaangalia hali ya msongo inayowakabili wanawake.

Wanawake wengi duniani, wamekuwa wakikabiliwa na changamoto nyingi, hali inayowafanya kupatwa na hofu, wasiwasi pamoja na kutojiamini.

Changamoto nyingi huwakabili wanawake hao katika maeneo yao ya kazi, nyumbani na hata katika mazingira mbalimbali wanayokuwamo.

Kwa mfano, kuna msemo usemao kuwa, binadamu wote ni sawa, lakini ukifuatilia msemo huo utaona kuwa, mara nyingi baadhi ya wanaume hawataki kukubaliana na msemo huo, kwa maelezo kuwa, wanawake hawana uwezo wa kufanya kazi zile ambazo wao huzifanya kwa umakini na uhodari.

Kutokana na hali hiyo, ndiyo maana katika siku hizi za leo, wanawake nao wamekuwa wakihamasishana kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika serikali na kwenye ofisi mbalimbali, ili nao waonyeshe kuwa wanaweza kuongoza.

Pamoja na jitihada hizo, wanawake wamejikuta katika kipindi kigumu, pale wanaposhika nyadhifa mbalimbali, hujikuta wakidharauliwa ama kutokukubalika katika jamii, hata kama ana uwezo wa kuongoza, cha msingi ni kukabiliana na changamoto hizo, endapo unajiamini na kujiona kuwa una viwango vya kuwa kiongozi bora, na si bora kiongozi.

Wengine kwa fikra zao hudhani kuwa, wanawake hawawezi kuwa viongozi bora kwa sababu ya mwonekano wao, huamini kuwa, wanawake wengi hawajiamini.

Kutokana na changamoto hizo, wanawake wengi walio katika nafasi mbalimbali za uongozi hujikuta wakikabiliwa na hali ya msongo, inayomfanya kushusha kiwango chake cha utendaji na kuwapa nafasi nzuri wanaume kuamini kuwa wao pekee ndiyo wanaweza.

Lakini utafiti mwingine umebaini kuwa, wanawake wenye uwezo na elimu ya kuridhisha wamekuwa wakijiamini kuwa wanaweza, hali iliyowafanya kukubalika katika maeneo wanayoyaongoza.

Vile vile kwa suala la maumbile, wanawake wengi wamejikuta wakikabiliwa na hali ya woga, ama hofu ya kupoteza kazi. Wanawake hukabiliwa na changamoto ya kuona siku zao katika kila mwezi, hivyo wapo ambao huumwa sana hata kuwafanya walazwe hospitali ama kushindwa kwenda kazini kabisa.

Hali hiyo, huwafanya wakose amani, furaha ama hofu ya kwamba, huenda wakafukuzwa kazi.

Na wengine hujitahidi kwenda hivyo hivyo kazini lakini hujikuta wanapatwa na maumivu makali ya viungo, kichefuchefu, tumbo kuuma, macho kuwa mazito na hali ya kukata tamaa.

Katika hali kama hiyo, ni uhakika kuwa hataweza kuendelea na kazi zake hivyo itambidi arudi nyumbani na kwenda kupumzika.

Hivyo ni vema kwa kila mwanamke kujikubali katika hali hiyo aliyonayo, ili asiruhusu hali ya wasiwasi katika maisha yake, inayoweza kumwongezea maradhi mengine ya ziada.

Vile vile msongo huwapata baadhi ya wanawake, pale anapokaa muda mrefu bila kupata mtoto. Hivyo asipokuwa makini na kukabiliana na hali hiyo mwili wake utapatwa na maradhi mengine ambayo hakuyatarajia.

Vile vile hupatwa na msongo pale anapohisi maumivu makali kipindi cha kujifungua, ama kujifungua mtoto mwenye matatizo kiafya.

Pia kushindwa kuzaa kwa njia ya kawaida na kumfanya afanyiwe upasuaji, vitendo vya udhalilishwaji anapokuwa kwenye wodi ya wazazi wanaosubiri kujifungua, upungufu wa wakunga au kusikia kelele katika wodi hiyo.

Wengine hufikiria kuwa, waume zao hawatakuwa tayari kumfurahia mtoto aliyezaliwa, kutofurahia ndoa yake pamoja na kuruhusiwa kutoka hospitalini, huku akiwaza mtu wa kumsaidia anaporudi nyumbani kwake.

Hofu zote hizo zinazowakabili wanawake, huwafanya kutokujiamini na kuongeza msongo katika maisha yao.

Wengine hufikiri kuwa, endapo waume zao wangekuwepo wakati wanapojifungua, hofu hiyo ingewatoka.

Pia wanawake wengine hukabiliwa na hali ya hofu na wasiwasi, kipindi kile anachonyonyesha, hasa wakati wa usiku.

Vile vile wanawake hukabiliwa na hofu na wasiwasi pale wanapotengana ama kufiwa na waume zao, pia wanapopewa talaka.

Kutokana na matatizo hayo, hali yake ya kawaida huondoka na kama hatapata msaada wa haraka anaweza kupatwa na magonjwa mbalimbali yatakayodhoofisha afya yake.

Hata pale wanawake hao, wanapofiwa na watoto wao wachanga hukabiliwa na msongo. Utafiti uliowahi kufanywa ulibaini kuwa, baadhi ya wanawake wanapofiwa na watoto wao, hujiua ama hupata ajali kutokana na kuwa na mawazo mengi wakati wanapotembea.

Wengine hufariki dunia kwa maradhi ya moyo, kansa ama ugonjwa mwingine. Hivyo, ni vema kila mmoja akaigundua hali hiyo mapema na kuidhibiti, kwa kupata ushauri kutoka kwa daktari.

Wakati mwingine mwili wake hudhoofika kwa kuwa hapendi kula, ama huwa anachagua vyakula vya kula, ama jambo analolifikiri kwa kipindi hicho.

Hali hiyo huweza kudhoofisha mwili wake hata mifupa. Kwani mlo usio kamili ama kula bila kufuata mpangilio, kunaathiri uimara wa mifupa mwilini.

Pia wanawake wengi wanakabiliwa na suala la msongo kutokana na suala la kiuchumi, pale wanapoona wanashindwa kukabiliana na maisha hujikuta na hofu pamoja na wasiwasi, kwa kuwa, wengi wao hawapati msaada kutoka kwa waume zao.

Kutokana na hali hiyo wanayokabiliana nayo, wanawake wengine hujikuta wakijiingiza kwenye ulevi wa kupindukia kwa nia ya kuondoa mawazo, hali inayowafanya kushindwa kufanya kazi kwa bidii.

Tukutane Alhamisi ijayo

0 Maoni:

Twitter Facebook