Friday, August 28, 2009

IKUBALI HALI ULIYONAYO UPATE FURAHA

MSOMAJI, katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi.

Leo tutaangalia jinsi unavyoweza kupata furaha kwa kuikubali hali ya upungufu uliyonayo.

Si rahisi kwa mtu yeyote kukubali hali ya uhitaji aliyonayo, lakini kufanya hivyo ni jambo la muhimu.

Ni ukweli usiopingika kuwa, katika maeneo yote ya maisha tunayoyaishi, kanuni zake zinafanana.

Na kwamba, unakuwa na furaha pale tu unapokubali hali ile ya upungufu uliyonayo, kwa kuwa hapo ndipo kwenye hitaji lako.

Kama ni kweli kuwa kila mmoja wetu hajakamilika katika eneo fulani katika maisha, kwa nini basi unakuwa hauko tayari kuikubali hali hiyo?

Wengi wetu tumekuwa hatuko tayari kukubali hali ya upungufu tuliyonayo, kwa kuhofia kuwa jamii inayotuzunguka itatucheka, kututenga ama kudhalilika.

Lakini kinachotakiwa hapa, ni kutoogopa jambo lolote lile, liwe kutengwa, kukataliwa ama kudharauliwa.

Sasa ni jinsi gani hali hii ya kuwa na furaha inaweza kukubadili wewe na mimi? Ni pale tu utakapoonyesha unahitaji msaada ama una upungufu.

Kwa mfano unaweza kuhitaji msaada kwa mtu yeyote kwa kumuuliza maswali yafuatayo: "Nimepata tatizo, je, waweza kunisaidia?, "Sielewi jambo fulani unaweza kunielewesha?, "Sijakubaliana na wewe, je, tunaweza kuonana mahali na kujadili zaidi?", "Nimepata hasara, je, waweza kuniongoza cha kufanya?"

Maswali ya namna hiyo ndiyo mwanzo wa kukuweka huru katika maisha yako. Hivyo furaha inakuwepo kwa mtu yeyote yule anayejua kuwa, eneo fulani ana upungufu hivyo anaukubali na kuhitaji msaada kwa wengine.

Kama wewe hauko tayari kulikubali jambo linalokusumbua, usishangae usipoona kuwa, wengine hawakujali.

Hivyo suluhu ni kujiweka mbele, jaribu kuwa mtu fulani ambaye hukuwahi kuwa hivyo, pamoja na kujiweka maridadi wakati wote.

Na ukweli ni kwamba, katika hali ya kuumia uliyonayo, kuna mtu ambaye yuko tayari kukusaidia juu ya upungufu wako, endapo tu ataelewa tatizo lako na kuliachilia. Lakini kama utajionyesha kuwa huna matatizo, hakuna njia ambayo mtu yeyote ataweza kukusaidia.

Wakati wote kuna mtu ambaye yupo tayari kukusaidia. Na kwamba mtu yeyote husaidiwa pale atakapokubali kuwa ana uhitaji katika sehemu fulani.

Kuna mfano wa mtu mmoja ambaye alikuwa ni mtumwa wa ulevi kwa muda mrefu, aliteseka katika hali hiyo kwa kuwa hakuwa tayari kuikubali. Na pale alipoelezwa kuhusiana na athari zinazoweza kumpata, hakuwa tayari kupokea msaada.

Siku moja baada ya kulewa kupindukia na kugonga gari lake alilokuwa akiliendesha, kwa maneno yake mwenyewe alijikuta akisema kuwa: ''Nimeteseka kwa ulevi kwa muda mrefu, kwa kuwa nilikuwa nasema kuwa, ninaweza kuudhibiti unywaji wangu, nilikataa ukweli kuwa nilikuwa mlevi niliyepitiliza, ningepokea uponyaji endapo ningeonyesha ninahitaji msaada. Na sasa baada ya hali hii kunikuta ninahitaji msaada na kubadili maisha yangu."

Tokea siku hiyo, maisha ya mtu huyo yalibadilika kwa kuwa alijitambua na kuhitaji msaada.

Kwa upande mwingine, furaha ya kweli inapatikana pale ambapo unaacha hali ya kulaumu. Ama kumlaumu Mungu au kujilaumu mwenyewe.

Watu wengi wanapopata matatizo hujikuta wakimlaumu Mungu ama kujilaumu wenyewe, badala ya kutafuta njia ya kumtoa hapo alipo ili aweze kuwa huru.

Sasa basi endapo umefikia hatua ya kukata tamaa ya maisha, umekutana na kipindi kigumu, kamwe usimlaumu Mungu kwa kuwa kufanya hivyo hutapata jibu la tatizo ulilonalo.

Makosa mbalimbali ambayo mwanadamu huyafanya pindi awapo katika hali ngumu ni yale ya kuhukumu, yatokanayo na utashi, sababu, ubinafsi, ukaidi, upumbavu na mengineyo yafananayo na hayo. Yote hayo ni chanzo cha binadamu kinachomfanya awe maskini na kuteseka.

Ama wakati mwingine unakuta mtu analaumu kwa ugonjwa alionao, ilhali wakati mwingine yawezekana yeye mwenyewe ameshindwa kujilinda mpaka akapata magonjwa.

Kwani kwa upande mwingine tunaweza kusema kuwa, magonjwa mengi sisi wenyewe ndiyo tunayasababisha kwa kutokula vizuri, kutokulala vizuri, kutokufanya mazoezi vizuri, kutopumua vizuri, haya yote ni kutokana na mazingira yanayomzunguka binadamu. Hivyo tunaona mambo mengine ni sisi wenyewe tunajisababishia na Mungu si wa kulaumiwa.

Mengi ya magonjwa hayo, huwapata wanadamu kutokana na uelewa mdogo ama elimu waliyonayo juu ya athari zinazoweza kutokea endapo ulishindwa kufanya jambo fulani.

Vile vile si vizuri kujilaumu wewe mwenyewe kutokana na hali inayokukabili, kwani kwa kufanya hivyo hutaweza kutatua tatizo linalokusumbua wala kuibadili hali hiyo.

Unaweza kupata hali ya kufiwa na mtoto, mzazi ama mume wako mpenzi, hali itakayokufanya ujitenge na wenzako, uache kujichanganya na kufanya mambo mengine ya kukusaidia, kutokana na hali iliyokukuta endapo hautakuwa makini na kuendelea na shughuli zako za kila siku, utajikuta hali yako kimaisha na kiuchumi inazidi kudidimia.

Katika hali kama hiyo, ndugu ama rafiki zako hawataweza kuyainua maisha yako siku zote, watakusaidia kwa sehemu tu, lakini itabidi nawe unyanyuke na kutoka katika hali ile ya kutokuwa na furaha na kujichanganya ili uweze kusukuma gurudumu hili la maendeleo.

Tukutane Alhamisi ijayo

0 Maoni:

Twitter Facebook