Friday, August 28, 2009

SAHAU MAUMIVU ULIYONAYO UPATE FURAHA

WIKI iliyopita tuliangalia jinsi ya kudhibiti hisia zetu ili tuendelee kuwa na furaha, imeonekana kuwa watu wengi wameshindwa kudhibiti hisia walizokuwa nazo na kujikuta wako katika hali ya kukata tamaa, pamoja na kuvunjika moyo.

Katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi. Leo tutaangalia jinsi inavyokupasa uyaachie mambo yanayokusumbua, ili uishi kwa furaha. Tutaangalia jinsi ya kuachana na mambo mbalimbali tunayokutana nayo katika maisha ili kuweza kupata amani na utulivu katika mioyo yetu.

Kumbuka kuwa kama una tabia ya kuachana na ya maumivu na huzuni unayokabiliana nayo, utakuwa na maisha mazuri, lakini kinyume cha hapo, utaendelea kuwa mtu asiyekuwa na furaha siku zote.

Na pia ufahamu kuwa, kila mmoja wetu hukabiliana na changamoto mbalimbali katika sehemu fulani ya maisha yake, kama vile, hali ya huzuni au kukataliwa lakini njia nzuri ya kuishi vizuri ni kuwa jasiri katika kuikabili hali hiyo.

Japo wapo watu wengine hudhani, kwa kuwa wao ni washika dini sana, hali ya huzuni, kuhangaika, kukata tamaa haitawapata, la hasha! Kila mmoja anapatwa na hali hiyo, ila ni uamuzi wako kuchagua ni jinsi gani unapenda uwe, kuwa na furaha ama kutokuwa nayo.

Pia ukiangalia watu wengi ambao hawana furaha, hukabiliwa na magonjwa mbalimbali. Huweza kuwatambua kwa kuwaangalia muonekano wao kiafya, vile vile hupatwa na maradhi kama shinikizo la moyo, moyo kudunda kwa nguvu, kupooza na hata wakati mwingine kuugua kansa ambayo huzalishwa na hali ya msongo wa mawazo.

Kwa upande mwingine wa maisha haya tunayoyaishi, ujue kuwa nayo yana kanuni zake, kama unataka watu wakutendee mambo mema, nawe pia watendee yaliyo mema, kwa kila jambo unalotenda.

Kwa kila tendo jema, kuna mwitiko ulio mzuri, kinyume cha hapo hutabaki kuumia na kukosa furaha maishani. Wema wako unaowatendea wengine, ndivyo hivyo nawe utapokea katika maisha yako kutoka kwao.

Tiba ya kuishi maisha ya furaha ni hii ‘kuwa mzuri, kuwa mwema, usiwe mbinafsi. Watendee wengine vile unavyopenda wakutendee wewe’.

Kama kweli umedhamiria kupata furaha ya kutosha maishani, tumia kanuni hiyo ya maisha na kuifanyia kazi.

Kama unataka kuwa rafiki wa watu, nao wawe rafiki zako. Kuwa rafiki kwao na kama umezungukwa na watu wasio wazuri kwako, wabadili wawe watu wazuri kwa kuonyesha wema wako kwao, haijalishi jinsi watakavyokuchukulia.

Je, unadhani utawabadilishaje ili wawe watu wazuri? Ni kwa kushirikiana nao katika mambo yaliyo mema na kuwajali. Inawezekana wanaweza wasikukubali kirahisi, lakini jitahidi kuwa mwema kwao, bila kujali wanachokisema wala kukinong’ona.

Hebu tuangalie mfano wa mama mmoja, aliyekuwa ameolewa lakini hakuwa na furaha na mumewe, kwa kuwa kila alichokifanya mumewe huyo alikikosoa.

Mwanamke huyo aliamua kutafuta msaada kwa kiongozi wake wa dini na kumweleza kuhusu mumewe kwamba kila aliporudi nyumbani alikuwa na hasira na kukosoa kila jambo aliloliona limefanyika.

Lakini mama huyo, alipoomba ushauri, aliambiwa kuwa, inawezekana yeye ndiye chanzo cha yote kabla ya kumsema mumewe, ni vema akajiangalie yeye kwanza, jambo alilokubaliana nalo na kulifanyia kazi, baada ya muda, mumewe alibadilika. Furaha ikatawala nyumbani kwao.

Mwanamke huyo alisema, aliamua kubadilika kwa kumjali mumewe na kuwa karibu naye, bila kujali vile alivyokuwa akimtenda na kwamba kila mumewe huyo aliporudi nyumbani, na kuanza kukosoa kama alivyozoea, kwa kuwa mwanamke alikubali kubadilika, alijitahidi kumhudumia kwa upendo, kumpatia chakula, juisi na kumpa maneno matamu, bila kujali jinsi alivyokuwa akifoka kwa hasira.

Alisema aliendelea kuwa karibu na mumewe kila siku na mwishoni mumewe huyo alibadilika tabia yake ile aliyokuwa nayo. Kama unataka kuyabadili mazingira magumu unayokutana nayo, ni vema ukaanza kubadilika wewe kwanza.

Fikiri juu ya hili. Je, ni jambo gani linalotufanya kuwatendea watu mambo mema? Ni kwa kuwa, nasi tunapenda kutendewa mambo mema pia? Kamwe tusiruhusu hali ya chuki na hasira katika maisha tunayoyaishi. Mbaya zaidi hali ya hasira zilizofichika ndani vinginevyo utapata maumivu na majeraha yaliyofichika ambayo yanahitaji kuponywa.

Majeraha hayo yaliyofichika hukusababishia hasira, ugomvi ama hali yoyote ambayo hupendi utendewe na mtu mwingine. Baadhi ya dalili zinazomfanya mtu aonekana kama ana majeraha yaliyofichika ni maneno yake, mwonekano na vitendo vyake.

Sasa basi njia ya kukabiliana na maumivu ya ndani uliyonayo ni kuyasahau na kutokumbuka mambo uliyowahi kutendewa. Watu wengi wanakosa furaha ya kweli, kwa kuwa wamekuwa wakikumbuka jinsi walivyotendewa na baba au mama yake, alipokuwa mdogo, mke au mme wake alivyomtendea siku za nyuma, kwa kuwa wanashindwa kusamehe, miaka inapita huku maumivu hayo yakiwa yanaendelea.

Usilaani. Kamwe usiruhusu maumivu yakakufanye mtu mwenye uchungu, jaribu kusahau, kumbuka kuwa, huwezi kusahau maumivu yaliyokupata kama utakuwa unayakumbuka kumbuka.

Tukutane Alhamisi ijayo.

2 Maoni:

Nina nukuu "Tiba ya kuishi maisha ya furaha ni hii ‘kuwa mzuri, kuwa mwema, usiwe mbinafsi. Watendee wengine vile unavyopenda wakutendee wewe’" mwisho wa kunukuu. Nimekipenda kipengele hiki. Asante sana nimejifunza kitu au niseme mambo hapa darasa zuri sana.

kweli rafiki wa kweli kwako ni wewe mwenyewe ukiamua kusahau maumivu yako ukayaweka kando ndivo utakavyotengeneza urafiki mzuri na nafsi yako, basi na tusahau yaliyotuumiza ili kuweka nafasi wazi kwa yanayotufurahisha

Twitter Facebook