Friday, August 28, 2009

HOFU HUSAIDIA KUEPUKA HATARI

KARIBU mpenzi msomaji katika safu ya Maisha Yetu inayokujia kila Alhamisi. Leo tutaangalia mbinu za kuwa jasiri katika uamuzi wako unaoufanya.

Katika maisha yetu ya kila siku, tunaona kwamba mbinu za kuwa jasiri ni nzuri katika kukabiliana na hatari iliyo mbele yako. Lakini kwa wakati mwingine, mtu anapokuwa na hali ya hofu inamsaidia kutokana na sababu iliyopo.

Ama tunaweza kusema unapokuwa na hofu, hali hiyo inakusaidia kwa kusudi maalumu. Ila kuna baadhi ya watu ambao hufikiri kuwa, si vizuri mtu kuwa na woga ama hofu. Lakini hii si kweli.

Kwani hali ya hofu husaidia, ni ishara katika ubongo wako kwamba pale huenda pakawa na hatari. Zipo sababu nzuri zinazopasa kuwa na hofu, kwa kuwa hofu inayozungumza ndani yetu ni vema kuilinda mwenyewe.

Kutokana na hofu unapokumbana na jambo, unajikuta hufikiri cha kufanya kwa wakati huo, ila unajikuta unaondoka katika eneo hilo kwa haraka.

Pia kuna baadhi ya watu wamejijengea tabia kama ya watoto wadogo ya kutokuwa na woga katika maisha yao. Lakini wakumbuke hali hiyo mara nyingine huwaletea matatizo.

Kwa mfano watoto wanapokuwa sio waoga, huwa na sehemu ya kuegemea ambayo ni wazazi wao. Wanakuwa hawana woga wa kuruka katika maeneo hatarishi, wakijiona kuwa wako salama.

Hivyo, kama watu wazima watafanya michezo ya kitoto watajikuta wakipoteza maisha kutokana na hatari mbalimbali kama vile ajali za barabarani au ugomvi.

Woga maana yake unatuepusha na hatari zilizoko mbele yetu. Hofu ipo ili kuwakinga watu wasipoteze vitu vyao vya thamani, kama vile pesa. Watu ambao hawana hofu ya kupoteza fedha zao, huzifanyia kazi zisizo na faida na baadaye kusababisha hasara kwao.

Pia hofu, humfanya mtu aliyepewa jukumu la kusimamia jambo fulani, kujiandaa mapema ili asiharibikiwe. Hebu fikiria mtu hana hofu anapohojiwa kwenye mhadhara kuhusu jambo fulani huku akiwa hana upeo nalo, pia hajajiandaa. Matokeo yake katika mjadala huo huonekana mjinga. Hivyo hofu humfanya mtu kuwa makini, pamoja na kuwa na maandalizi mazuri.

Unapaswa kuwa na hofu ili kuweza kujiandaa na hatari zilizo mbele yako, kama za kimaumbile, kifedha ama kijamii. Kama mvua zisiponyesha ina maana kutakuwa na njaa. Hivyo taifa lolote lililo makini hutafuta njia mbadala ya kukabiliana na hali hiyo.

Hii ni kutokana na hofu huenda siku za mbeleni, wananchi wakakosa chakula na kupata utapiamlo ama kufariki dunia. Lakini pia, ukumbuke kuwa, hali hiyo ikizidi inaingilia uhuru wa maisha yako. Watu wengi wamejikuta wakiwa na hali ya hofu ama woga kupita kiasi. Hali ambayo si nzuri kwao.

Kwa sababu hofu ni hisia zinazofanya damu yako ichemke, na mara nyingi unajikuta unahamaki kwa kusema kuwa ‘aah! Ngoja nitoke eneo hili ni la hatari’.

Na kama hali hiyo itakuwa inakutokea mara kwa mara, linakuwa sasa ni tatizo ambalo unatakiwa kulitatua. Kwa kawaida kila mmoja anakuwa na kiwango kidogo cha hofu isiyo ya kawaida.

Kwa mfano unakuta daraja kubwa linajengwa na kuanza kupatwa na hofu kwamba daraja hilo litabomoka. Huhisi hivyo hata kama inaonekana kuwa kwa hali ya kawaida si rahisi kwa daraja hilo kubomoka. Hilo ni tatizo linalohitaji ufumbuzi.

Wengine wanakuwa na woga wa kufanya mazoezi mbalimbali ya darasani, matokeo yake wanakwepa kabisa ama kufanya vibaya. Bahati nzuri ni kwamba kuna njia muafaka ya kuondoa hali hiyo, kwa kutathmini tatizo lililopo.

Kama vile, kuwa na mbinu ya ujasiri, ili kuweza kukabiliana na hali hiyo, kwa kuangalia ukubwa wa tatizo. Kwa mfano; mwanafunzi anatarajia kufanya mtihani wake, ambao una maswali 100; amejiandaa vizuri. Japo mwanafunzi anakuwa na hofu ya kushindwa kwa baadhi ya maswali, lakini kwa kuwa alishajiandaaa vizuri atakuwa katika nafasi nzuri.

Nini cha kufanya kuhusu hofu na hatari iliyopo. Cha msingi ni kuangalia ukubwa wa hali hiyo na kuitatua kabla. Kwa mfano, mtu anayehofu kuwa malipo yake yatapunguzwa. Hataogopa kwa hilo, bali atakuwa na hofu kwa kuwa hakutegemea hali hiyo.

Ili kukabiliana na hali hiyo ni vema kutafuta kazi nyingine itayomlipa zaidi, kwa kufanya hivyo atakuwa amelikabili tatizo hilo. Kuna mambo tunayoweza kuyafanya ya kuondoa hali hiyo ya hatari, iwe kubwa ama ndogo. Kuna mambo matatu ya kufanya tunayoweza kuyachagua.

Mojawapo ni homoni zinazoshtua mfumo wa damu, wakati upatwa na jambo linalokutia hofu. Homoni hizo zinasaidia kama mtu anataka kukimbia ama kujikinga na jambo.

Zinafanya mwili kuwa na utayari wa jambo lolote. Pia ni vizuri kujiepusha ama kuondoka katika sehemu inayoweza kuwa na hatari. Maana yake ni kwamba kama upo kwenye eneo hilo la hatari, yakupasa kuondoka mara moja.

Kwa kufanya hivyo, utakuwa umefanya uamuzi wa busara. Vema kujijengea uwezo na kuwa tayari katika kupambana na jambo la hatari. Hilo litakuwezesha kukabiliana na jambo lolote kwa urahisi.

Mfano kama wewe ni mwimbaji mzuri yakupasa ujiandae vema. Pia kufanya majaribio kunafanya kazi yako iwe nzuri yenye kiwango cha kuridhisha. Inamaanisha kuwa, unaiandaa akili yako kuimba mbele ya watu katika tamasha.

Hebu fikiria kuwa una hofu ya kuendesha gari, ni vema kukaa mbali na usukani. Kujijengea uwezo na maandalizi kunakufanya uwe mwangalifu na kumwangalia mwingine wakati anapoendesha. Hukufanya ujifunze mengi kupitia kwa mwingine, mwishoni hofu hiyo itaondoka.

Tukutane wiki ijayo.

0 Maoni:

Twitter Facebook