Friday, August 28, 2009

MSONGO KATIKA SEHEMU ZA KAZI (3)

KARIBUNI wapenzi wasomaji katika siku nyingine ambayo Mwenyezi Mungu ametujalia kuiona.

Leo tutaendelea kuangalia mada kuhusu msongo katika sehemu za kazi.

Wengi wetu tumekuwa tukikabiliana na hali ya msongo katika vipindi mbalimbali vya maisha, kuanzia kipindi cha utoto hadi uzee.

Hali hiyo humpata mtu anayefanya kazi, mzazi katika kipindi cha kulea watoto wake na katika vipindi mbalimbali vya maisha.

Ila humjia kila mmoja kwa jinsi yake.

Mafanikio yetu katika maisha na thamani ya maisha, inategemea ni jinsi gani tunavyokabiliana na hali hiyo.

Tunahitaji kuelewa msongo ni kitu gani na kujifunza jinsi ya kukabiliana na hali hiyo.

Mtaalamu mmoja aliwahi kuelezea fani saba ambazo haziepukiki katika suala la msongo, ambazo ni fani ya ualimu, uuguzi, umeneja, ustawi wa jamii, udereva, upolisi na ofisa magereza.

Je, umejiona katika kundi lolote hapo juu? Usijali kuhusu hilo, cha msingi ni kujua unafanya nini na jinsi gani ya kujiepusha na msongo katika kazi yako.

Pia inawezekana wewe ni miongoni mwa watu zaidi ya 200,000 ambao hupatwa na maradhi yanayotokana na hali ya msongo katika kazi zao, kila mwezi na kulazimika kupumzika nyumbani ili kuondoa hali hiyo.

Pia yawezekana kwamba, wewe ni miongoni mwa asilimia 27 ya watu wanaolalamikia mazingira ya kazi zao, ama kati ya asilimia 19 ambao hawana mazingira bora ya kufanyia kazi, au asilimia 17 ya wale ambao ofisi zao haziko katika muundo wa kisasa hivyo kufanya kazi zao kuwa ngumu, kwa kuwa hakuna mwanga au hewa ya kutosha.

Pia yawezekana umo miongoni mwa asilimia 14 ya wale wafanyakazi ambao hawana nafasi ya kutosha ya kukutana na wenzao, kutokana na kazi kuwa nyingi, asilimia 13 ya wale ambao hawajaridhika na eneo ambalo ofisi yao ipo, asilimia 12 ya wale wasio na vifaa vya kisasa ofisini kwao, asilimia 5 ya wale wanaolalamika kuhusu kukosa uhuru wa kuvuta sigara ama mazingira wanayofanyia kazi hayana uhuru wa kumfanya avute sigara na asilimia nne wanakosa ushirikiano na wafanyakazi wengine.

Je, hofu kuhusu kazi yako inaongezeka bila kupata suluhu? Uamuzi wako wa mwisho ni kubadili kazi na kuchukua tahadhari kwa hatari unazoweza kukabiliana nazo katika kazi hiyo mpya.

Lakini lazima uchukue tahadhari, kwa sababu ni gharama.

Pia utaona kuwa, mpangilio mbaya wa kazi zako unaweza kukusababishia maradhi.

Utawala mzuri huwafanya wafanyakazi kuwa na afya bora, hivyo uzalishaji unakuwa mzuri pia.

Utafiti mwingine uliofanywa kwa wafanyakazi 600, asilimia 60 kati ya hao wamewalalamikia watengenezaji wa barabara kuwa wanachangia msongo katika maisha yao, kutokana na kusababisha foleni wawapo barabarani, asilimia 40 wamesema kuwa, malengo waliyojiwekea hawajaweza kuyafikia hivyo yanawasababishia hali hiyo.

Wengine walisema kuwa, hali ya hofu na wasiwasi wanayoipata wanasababishiwa na rafiki zao, ama kutoelewana kwa wafanyakazi ndani ya ofisi.

Pia katika ofisi nyingi, suala la mapumziko limekuwa ni kitendawili, wafanyakazi hawapati mapumziko wawapo kazini, hali inayosababisha hofu, wasiwasi na hasira za mara kwa mara.

Ni wafanyakazi wachache wanaoweza kupata muda wa mapumziko na kwenda kupata chakula cha mchana, wengine kutokana na muda kuwa mdogo kwa ajili ya kazi nyingi hujikuta wakipitisha mchana bila kula chakula.

Vile vile haijalishi wewe ni nani, unaweza kukabiliwa na msongo katika mazingira ya ofisi.

Tuangalie mfano wa sekretari, ambao wamekuwa wakisumbuliwa na hali ya hofu na wasiwasi katika kazi zao.

Hivyo msongo mkubwa huwakabili kutokana na kazi zao za kila siku wanazozifanya.

Sekretari hupatwa na msongo pale anapokuwa ana kazi nyingi mara simu inaita au wageni wanafika na kuuliza habari mbalimbali zinazomhusu bosi wake, ilhali kipindi hicho anahangaika akamilishe kazi ya bosi wake anayoisubiri ili aanze kikao.

Vile vile hupatwa na msongo pale mashine yake ya kutolea ‘photocopy’ inapokwamisha karatasi au kukwama ama inaposhindwa kufanya kazi kwa kipindi hicho anachohitaji kuitumia huku akiwa anakabiliwa na kazi nyingine.

Wakati huo huo, kunakuwapo na watu wanaosubiri kuweka ahadi ya kuongea na bosi wake, ambao hawako kwenye ratiba ya siku hiyo.

Vile vile hukabiliwa na msongo pale anapopata kazi nyingine ya dharura ilhali alishajiandaa kwenda nyumbani.

Mbali na hali ya msongo wa kawaida, wanayokabiliana nayo katika shughuli zao za kiofisi, kwa upande mwingine hulalamika kupewa kazi za dharura na mabosi wao, wakati hakuna posho.

Wanapewa kazi zinazopoteza nguvu zao na kuwafanya washindwe kuwasiliana na watu wengine, pia wapo wanaolalamikia masuala ya ngono.

Hayo yote yanajumuisha mazingira mabovu ya ofisi, muundo mbaya wa viti vya ofisi ambavyo havimpi starehe mtumiaji na badala yake vinamfanya achoke na kuchukia mazingira ya ofisi anayofanyia kazi.

Hivyo unapoona una dalili ya kuchoka, ama kuumwa mara kwa mara, ni vema kuangalia afya yako ilhali isiwe mbaya zaidi.

Utafiti uliofanywa katika nchi za wenzetu mwaka 2003, ulibaini kuwa, asilimia 35 ya mabosi wamekuwa wakikubali majukumu mbalimbali ya ofisi zao ili kuwafanya wafanyakazi wao, wasipate msongo ama kupunguza hali hiyo kabisa.

Tukutane wiki ijayo

0 Maoni:

Twitter Facebook