Wednesday, December 12, 2012

Ugumu wa Maisha wawatatiza vijana


NAMSHUKURU Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kukutana nawe tena katika safu hii inayokujia kila Alhamisi.

Katika miaka ya hivi karibuni vijana wengi wenye umri wa kujitegemea wamekuwa wakiishi na wazazi wao kwa kuogopa kupanga kutokana na changamoto mbalimbali zilizopo.

Kuendelea kuishi na wazazi baada ya kuhitimu chuo, ni jambo linalorudisha nyuma fikra za kijana au anakuwa na mawazo ya kudumaa.

Ukweli ni kwamba, vijana wa kiume wenye umri miaka 25 na 34 siku hizi wamekuwa wakirudi nyumbani kwa wazazi wao kwa ajili ya kuangalia video na michezo mbalimbali katika nyumba za wazazi wao.

Vijana hao wamekuwa wakiukataa ukweli halisi kuwa wamekwishakuwa wakubwa na wanapaswa kujitegemea.

Vijana wa aina hiyo wamekuwa wavivu, hawapendi kujishughulisha katika shughuli mbalimbali, wengi wao wakiwa wanaringia utajiri au mali za wazazi wao. Bila kufikiri ni jinsi gani wazazi hao wamezipata hizo mali.

Mazingira ya utamaduni wa kisasa nayo yamechangia kuwaathiri vijana hao, ongezeko la idadi ya vijana hao kurudi nyumbani kwa wazazi kumesababishwa na sababu mbalimbali.

Sababu mojawapo ni gharama kubwa za elimu ya juu. Unakuta kipindi cha likizo kijana anaamua kurudi nyumbani kwa wazazi wake ili kukwepa gharama za kuishi hosteli kipindi kile cha likizo.

Ikizingatiwa kuwa bodi ya mikopo imekuwa ikitoa kiasi kidogo cha mikopo hata pale mwanafunzi anapomaliza anajikuta bado ana deni liko mbele yake.

Ukosefu wa ajira kwa vijana hao kuanzia miaka ya 1970, kipato kwa vijana hao kimekuwa kikishuka, na soko la ajira limekuwa ni la ushindani mkubwa. Jambo hili limefanya mambo yawe mabaya.

Vile vile ongezeko la mahitaji katika elimu. Katika miaka ya nyuma mtu aliweza kupata kazi akiwa na cheti kidato cha sita tu.

Lakini hivi sasa soko la ajira linahitaji angalau awe na digrii, ila kikwazo kipo pale shule inapokuwa ya gharama ili kufikia malengo ambayo mtu amejipangia, hivyo inachukua muda mrefu kwa kijana kuweza kujitegemea kiuchumi.

Hivi sasa mtu anatumia zaidi ya nusu ya kipato chake kwa ajili ya gharama za nyumba.

Kutokana na gharama hizo,vijana kuwa na maeneo yao ya kuishi inakuwa ni vigumu.

Miaka ya zamani wazazi walikuwa na muda mzuri wa kukaa na watoto wao, lakini katika miaka ya hivi karibuni wazazi wamekuwa wakitumia muda mwingi wawapo maofisini hivyo kijana anapokuwa na umri wa kujitegemea, wazazi wake huona fahari kuendelea kuishi naye nyumbani.

Hivyo kwa mazingira hayo utaona ni kwa jinsi gani vijana wa siku hizi wamekuwa ni wavivu na wasiopenda kujituma.

Hivyo basi kutokana na mazingira haya, si busara kwa vijana waliofikisha umri wa kutengana na wazazi wao kuwaambia waondoke.

Kwa changamoto hizo utakuwa na sababu maalumu ya kwanini unarudi nyumbani na kuishi na wazazi wako.

Kwa miaka ya zamani vijana wengi walikuwa wakipenda kuficha mambo yao, lakini siku hizi mambo yamebadilika, vijana wanakuwa wazi katika kila jambo kwa wazazi wao ndio maana wanaendelea kuishi nyumbani.

Vijana wa zamani walikuwa wakiondoka nyumbani kwa kuwa walikuwa hawataki mambo yao yajulikane na kila mtu.

Imeandikwa kwa msaada wa mashirika ya habari.

0 Maoni:

Twitter Facebook