Wednesday, April 8, 2009

ZUIA HASIRA, HISIA ZINAZOKULETEA MAUMIVU

NI siku nyingine njema ambayo Mwenyezi Mungu ametujalia kuiona tena. Tunayo kila sababu ya kumshukuru kwa pumzi na uhai aliotupa.
Mwanadamu yeyote aliyeumbwa na Mwenyezi Mungu ana hisia mbalimbali ambazo humfanya kuwa hivyo alivyo. Mojawapo ya hisia hizo ni hasira. Lakini ni vema kujitambua na kuitawala hasira yako kabla haijakutawala.
Hivyo basi, kama hupatwi na hasira, ni lazima utakuwa na tatizo. Pia ni vema kutambua kuwa kupatwa na hasira ni hali ya kawaida. Ni suala la hisia za muhimu kwa afya yako. Tatizo linakuwepo pale mtu anaposhindwa kuzuia hasira yake na kuchukua hatua na kuanza kupigana au kugombana na watu pasipo sababu ya msingi.
Hasira isiyo na mipaka inasababisha vurugu zinazoleta uharibifu. Ni sawa na ugonjwa, usipoizuia hasira inaweza kukudhuru na kukukereketa moyoni kwa njia ya fundo, husuda, chuki.
Wakati haya yanatokea, njia pekee ya kuondoa hasira ni msamaha. Kuwa tayari kusamehe na kusahau. Safisha akili na moyo wako. Rudisha chuki kwenye upendo.
Unaporuhusu furaha moyoni mwako unapata afya. Kwa kuwa inakufanya uwe na afya bora. Watu wenye furaha wana afya na watu wenye afya wana furaha.
Vile vile, kicheko ni dawa kubwa, Pia ni afya. Inaondoa hali ya kukata tamaa. Madaktari wanasema ndiyo dawa pekee ya dunia. Inakuletea furaha, amani na utulivu katika akili yako na mwili.
Unaweza kuepuka magonjwa ya akili kwa kujifunza kuwa na furaha pamoja na kucheka.
Pia jambo lingine la kuzingatia, ni kwamba usile chakula wakati una hasira, vinginevyo hakitafanya kazi mwilini au kitakusababishia vidonda vya tumbo.
Ni desturi kwamba, kabla hujakaa na kuanza kula unanawa mikono, vile vile ni vema kusafisha akili yako na kuondoa hasira uliyokuwa nayo, uchungu, uhasama na mawazo mabaya. Endapo unakula ukiwa na hisia hizo, chakula unachokula kinakuwa hakina ladha, pia hakitaweza kufanya kazi vizuri mwilini.
Safisha akili yako vizuri na uondoe mawazo yote mabaya. Kama umekasirishwa na mtu, au jambo lolote au una matatizo sahau wakati unapokula chakula. Kwa kufanya hivyo utafurahia chakula unachokula.
Ni jinsi gani unaweza kuzuia vidonda vya tumbo visikupate? Kwanza utambue kuwa vidonda vya tumbo humpata mtu mmoja kati ya watu kumi. Mara nyingi husababishwa na wasiwasi, hasira, uchungu, uchovu na utumiaji wa sigara pamoja na vinywaji vikali.
Kamwe usiache matatizo yako yakakuzidi, yaachilie kwa kuzungumza na watu unaofikiri kuwa wanaweza kukusaidia. Wakati unapojisikia vibaya, jisogeze taratibu baada ya kuacha kile ulichokuwa ukikifanya ili upate muda wa kupumzika.
Punguza matatizo yako kwa kujishughulisha, usiende nayo nyumbani. Kama utapenda kuwa na furaha na amani moyoni mwako itakufanya usipate vidonda vya tumbo. Kumbuka hali ya furaha ya mara kwa mara inakuondolea hali uliyonayo ya huzuni, majonzi au hasira na kukufanya uwe na afya bora.
Njia nyingine inayoweza kukufanya uepuke kupata maradhi ya moyo ni kuondoa wasiwasi na kula vyakula ambavyo havina mafuta mengi. Wataalamu wa afya wanaamini kuwa maradhi ya moyo yanaweza kuzuilika kuanzia kipindi cha ujana.
Pia wanaamini kuwa vyakula vya mafuta, shinikizo la damu, kukosa mazoezi, uvutaji wa sigara, ulevi, msongo wa mawazo na uchovu unasababisha ugonjwa huo.
Ili kujiepusha ni vema kupata muda mzuri wa kupumzika, kufanya mazoezi, kuondoa hofu, kutokuvuta sigara, kutokunywa pombe, jitahidi kutokuwa na uzito utakaozidi pamoja na kuangalia afya yako mara kwa mara.

0 Maoni:

Twitter Facebook