Wednesday, April 8, 2009

MALENGO NI MUHIMU KATIKA MAISHA

KARIBUNI wapenzi wasomaji wa safu hii ya Maisha Yetu. Leo ni siku nyingine mpya tunayoangalia ili tufanikiwe katika maisha yatupasa kufanya mambo gani.
Kama unataka kufanikiwa katika maisha yako, inakupasa uwe wazi kwa kile unachohitaji kukifanya. Kwa mfano, unaweza kumuuliza kijana mdogo anatarajia kuwa nani katika maisha yake, hapo utapata jibu kutoka kwake. Kijana huyo anaweza kukwambia, anataka kuwa mwana anga, rubani, daktari, muigizaji au askari. Watoto hueleza kwa uwazi kile wanachohitaji.
Kwa upande mwingine swali hilo hilo ukimuuliza mtu mzima kile anachokitarajia katika maisha yake, mara nyingi huwa hayuko wazi kuelezea matarajio yake ni yapi. Hapa inaonyesha kuwa watu wengi wanashindwa kufikia matarajio waliyonayo kwa kuwa hawana malengo thabiti ya maisha yao.
Ni nini unachokihitaji katika maisha yako? Je, unakijua? Umeweka wazi malengo yako kwa kipindi hiki? Katika maisha ni muhimu kujua kile unachotaka kukifanya na kuandika malengo katika kutimiza kile unachokihitaji. Ni vema kuandika, kuwa wazi kwa kile unachotaka kukifanya.
Fahamu kile unachotaka kufanya katika kutengeneza maisha yako, vitu unavyotarajia kuvikamilisha kama ni afya njema, ndoa yenye mafanikio, amani, kazi nzuri, nyumba mpya, safari ya kwenda nje ya nchi au pesa nzuri.
Kila jambo huwa na mpangilio, ili ufikie maisha mazuri inakupasa uwe na malengo na kujituma katika kazi. Kama unajua ni nini unachohitaji na kuwa na malengo sahihi, utakuwa na bidii katika shughuli zako. Kwa kuwa unapokuwa na mipango katika maisha yako, kunakufanya kusonga mbele.
Kumbuka kuwa mafanikio huja kutokana na malengo, kinyume na hapo utashindwa. Malengo ni kiongozi katika safari yako ya maisha, tofauti na hapo safari hiyo itakuwa na vikwazo vingi. Unapokuwa na biashara yako, ni vema ukawa na ripoti inayoonyesha maendeleo yako ya kila siku. Usivunjike moyo kama malengo yako hayatafanikiwa.
Songa mbele. Ona kama kushindwa ni kwa muda tu, hivyo yakupasa uongeze bidii. Kila jambo linakwenda kwa mzunguko. Jipe moyo kwa kujua kuwa, uwezo na utayari ulionao unaondoa vikwazo vyovyote vinavyo kukwamisha.
Kwa upande mwingine unapopata wazo lolote la maendeleo usilidharau, kwani linaweza kukutoa hapo ulipo na kukufanya kuwa na mafanikio zaidi.
Wazo linapokujia katika akili yako,liandike, lifikirie kwa umakini, likuze zaidi, kuwa na shauku nalo, halafu chukua hatua kuhusiana na wazo hilo.
Wazo unalolipata ni kitu cha thamani kinachoweza kukuzwa na kuendelezwa na kuchukua hatua ili kiwe kitu halisi.
Ni kama vile kupanda mbegu, ambazo hukua na kuleta mazao mazuri. Mawazo ni mbegu, ambayo yakitumiwa vizuri yataleta matokeo mazuri. Ni jinsi gani unaweza kupata wazo la kukuinua kimaisha? Mawazo hupatikana kwa kuangalia, kuuliza, kufikiri, kuangalia matatizo unayokabiliana nayo na kutafuta njia ya kuyatatua.
Pamoja na kusoma vijarida vinavyoweza kukupatia mawazo mapya na maendeleo, kujadiliana na wengine. Jifunze kuwa na utaratibu wa kuandika kila wazo linakujia na kulipanua zaidi.
Mara nyingi mawazo huja yenyewe. Yanaweza kukujia kwa kusoma magazeti, unapokuwa kwenye matembezi, unapotembelea madukani, unapoangalia picha na kuwasikiliza watangazaji wa vipindi mbalimbali vya kwenye redio au televisheni.
Unaweza kupata mawazo toka kwenye vyanzo mbalimbali, inakupasa uchukue mawazo mazuri pekee yatayokuletea mafanikio katika maisha yako.

0 Maoni:

Twitter Facebook