Wednesday, April 8, 2009

MPE MWENZA WAKO NAFASI YA KUZUNGUMZA

KARIBU mpenzi msomaji katika safu hii inayokujia kila Alhamisi, kwa lengo ya kukufanya wewe ujue mbinu mbalimbali zitazokufanya ufanikiwe katika maisha yako.
Katika maisha yako unayoishi, kamwe usiwadhalilishe wengine kwa jambo lolote lile.
Nasema hivyo kwa sababu rafiki yangu aliniambia kuwa hajawahi kujisikia vibaya kama siku moja aliyoalikwa kwenye chakula cha jioni na rafiki yake.
Alisema rafiki yake huyo, kila mara alikuwa akimdhalilisha mkewe alipokuwa akitaka kuchangia mada yoyote ambayo walikuwa wakiichangia.
“Mke wangu hana akili kwenye kichwa chake,” alisema mtu huyo aliyekuwa ameandaa chakula kwa ajili ya rafiki zake.
Baadhi ya wanaume wanafurahia kuwakosoa na kuwavunja moyo wake zao, au rafiki zao. Hali hiyo inaweza kuwafanya wakajisikia kana kwamba ni washindi kwa wakati huo, lakini sivyo walivyo, hiyo ni tabia mbaya inayoonyesha wazi mtu huyo alivyo.
Kunyamazisha uhuru wa kujieleza wa wengine ni kuonyesha hali ya ubinafsi, kutopevuka na dhambi, inafaa kuepukwa na watu wote wanaotamani kuwa na hali hiyo.
Ni vema kumpa nafasi mke wako ya kuzungumza neno lile analotaka kulizungumza. Mpe sifa mbele ya watu, muongoze katika mazungumzo na mpe moyo wa kuzungumza yale aliyonayo.
Pengine anaweza kusema jambo litakalowafanya wasonge mbele au kuwatahadharisha na mawazo mabaya yanayoweza kuwaingiza kwenye kuharibikiwa badala ya kusonga mbele.
Kumbuka kuwa kila mwanamke hupenda kuonyesha shukrani zake kwa mumewe. Mwache mke wako ajisikie wewe ndiye furaha yake zaidi sana mbele ya wengine.
Kwa kuwa ndoa inakuwa nzuri pale wawili wanaopendana wanapeana moyo badala ya kuvunjana moyo, hivyo utakaposhinda katika hilo, katika masuala yenu ya ndani mtaweza kuwa na ndoa yenye mafanikio kwa kupanga mipango mizuri ya familia, kinyume cha hapo hakutakuwa na maelewano, kwani kila mmoja anapenda kufarijiwa na kusikilizwa na mwenzake.
Katika hali hiyo kumbuka kuwa kila mmoja ni tajiri kulingana na vipaji mbalimbali Mungu alivyomjalia, ambavyo ni tofauti na wengine. Kila mmoja ana mambo yake mazuri aliyojaliwa na muumba, yawezekana ni busara, ushauri au mawazo mbalimbali ya kumtoa mtu kwenye hali ya umaskini na kumpa fikra ambazo zitamfanya afikirie mawazo ya kuwa na maendeleo.
Kila unachofikiri kinakuwa, kwani mtu mwenye mafanikio hufikiri njia za kuzidi kupata mafanikio, pia anakuwa na mawazo mapana ya kumpatia maendeleo.
Endapo mtu hutapenda kujishughulisha, wakati mwingine utajikuta ukipata magonjwa ya aina mbalimbali yanayotokana na hofu uliyonayo katika maisha yako.
Madaktari wengi hujua kuwa, asilimia 85 ya magonjwa yanayokupata yanatokana na msongo wa mawazo.
Wakati akili yako ina afya, moyo wako huwa na furaha. Wale wanaotaabika na magonjwa ya akili wanaweza kupata nafuu ya muda kutoka kwa daktari, lakini njia nzuri ni kuamua kukabiliana na hali ngumu ya maisha inayokupata kwa kufanya jitihada kwa mambo mazuri unayoyawaza ili uwe na maisha bora.
Shinda hofu ili utoke kwenye kifungo katika akili yako. Kwani hujazaliwa ili uwe mtu wa tabia ya hofu, ila uweze kukabiliana nayo. Mara nyingi wasiwasi ni ugonjwa unaoharibu maisha ya mwanadamu.
Magonjwa mengi ya hisia yanasababishwa na mtu kuchanganyikiwa kisaikolojia, woga na wasiwasi ambavyo huletwa na hofu na umaskini.
Mtu ambaye amejawa na hofu ni mfungwa katika akili yake. “Mateso mengi katika dunia hii kwa baadhi ya watu ni kufikiri,” anasema Luther.
Watu ambao hawajajifunza jinsi ya kufikiri wanaruhusu mawazo hasi yatakayokuwa muongozo wa maisha yao na baadaye kuwa waathirika wa pombe na dawa za kulevya.
Lakini uelewe kuwa, dawa za kulevya na pombe haviwezi kutatua tatizo. Hivyo basi unaweza kutoka kwenye kifungo cha hofu, wasiwasi, kuchanganyikiwa kwa kutumia akili yako kwa busara.

0 Maoni:

Twitter Facebook