Wednesday, April 29, 2009

TUNAWEZAJE KUEPUKA MIGONGANO?

KARIBUNI wapenzi wasomaji katika safu hii ya Maisha Yetu. Leo tutaangalia ni jinsi unavyoweza kuepuka migongano isiyokuwa ya lazima.
Ni jambo jema na la busara kuchagua nini cha kusema kuliko kusema kile unachochagua. Kwa kufanya hivyo utajiepusha na migogoro.
Mara kadhaa wanandoa wamekuwa wakitengana, marafiki kufarakana na wafanyakazi kukosa ushirikiano. Je, unafahamu ni nini kinasababisha hali hii ya huzuni? Sababu kubwa kuliko zote ni kutokuwa na mawasiliano mazuri. Tumeshashuhudia watu wazuri wakitengana kwa sababu ya kutokuelewana. Walifikiri walikuwa na mawasiliano, kumbe sivyo.
Tatizo ni kwamba watu wengi hawawezi kutofautisha kati ya kuzungumza na kuwasiliana, hali inayochangia migogoro. Mawasiliano yana sehemu mbili ya kuzungumza na kusikiliza. Mzizi wa neno mawasiliano maana yake ni kushirikishana. Ni jinsi gani tunaweza kushirikishana mawazo na hisia? ni mpaka pale wahusika katika mazungumzo watakaposikiliza kwa uelewa kama vile katika kuzungumza.
Ni jinsi gani tutakavyowaambia wapenzi wetu tunawapenda? Si kwa maneno, ni kwa kuwasikiliza kile wanachokisema. Tunasikia, lakini hatusikilizi, hatufyonzi ule ujumbe uliotolewa. Nini kinasababisha haya mawasiliano mabaya? Ni kwa kuwa tumetoka katika maeneo tofauti, uzoefu na historia tofauti. Jinsi tunavyoiangalia dunia na matukio mbalimbali tunatofautiana na kusababisha migongano.
Hasira inapopanda ni kwamba tumezungumza kile tulichochagua badala ya kuchagua kile cha kusema. Migongano hiyo husababisha kutokuelewana na hatimaye kutengana. Ukweli, kama tunashirikiana mawazo kwa pamoja, kutakuwa hakuna kutokukubaliana, bali kuishi kama vile dunia ilivyo.
Hatua ya kwanza itakayoondoa kutokuelewana ni kukubali kwamba wote hatufanani. Kwa sababu ya utofauti wa uasilia wetu na mawazo yetu. Yamkini, tunafanana katika hili, kwamba tunahitaji kueleweka na kukubalika.
Kuna wakati mwingine waweza kujihisi kutokukubaliana na fulani, ni vema kutulia na kujiuliza ni jinsi gani watu wanavyotofautiana na wewe. Unaweza kuelewa jambo lakini bado ukawa hukubaliani nalo. Kama mawazo yako ni tofauti, usipende wengine wakubaliane na mawazo yako.
Je, ni jinsi gani unaweza kuwafanya wengine wakubaliane nawe? Ni pale utakapowaheshimu. Unaweza kuwaeleza kuwa ‘siwezi kusema kuwa nakubaliana nanyi, lakini naheshimu kwa kuwa na mawazo tofauti,’ mara nyingi kutokuelewana kunaibuka kwa sababu tunaangalia maneno yanayozungumzwa badala ya kumwangalia mzungumzaji.
Viungo, joto, baridi, utajiri, umaskini, uhuru na amani, ingawa tunaelewa maneno haya tunayatafsiri tofauti. Kwa hiyo usiweke msisitizo kwenye maneno, lakini kwenye moyo wa mtu. Jaribu kumwelewa mtu na siyo maneno. Mara nyingine, licha ya jitihada zetu, migogoro hutokea. Kama ndivyo, hakuna haja ya kukata tamaa.
Jumla ya yote, migongano ni nafasi ya kukua. Tumia hali hiyo kujifunza pale ulipokosea na kujirekebisha. Kwa kuwa tunajifunza kutokana na makosa yetu, tunanafasi ya kusonga mbele.
Tutakapo mwelewa anayezungumza na kutoa nafasi ya kueleweka tutajiepusha na mengi. Pia, kila mmoja anapomwelewa mwenzake, hakuna haja ya kuombana msamaha. Kama tutafanikiwa kujiepusha kutokuelewana na migongano tunafikisha ujumbe wa amani.

0 Maoni:

Twitter Facebook