Wednesday, April 29, 2009

BOSI WAKO ANAPOKUVUNJA MOYO USIKATE TAMAA

KWA mara nyingine tena, ninapenda kuwakaribisha wasomaji wangu katika safu hii inayokujia kila alhamisi, ili uweze kuelimika kwa kupata mawazo mbalimbali.
Leo tutaenda kuangalia njia mbadala za kufanya baada ya kukumbana na misukosuko mbalimbali kutoka kwa bosi, mkuu wa kitengo au mkurugenzi wako.
Watu wengi wamekuwa wakivunjika moyo na wengine wao kuamua kuacha kazi eti kwa sababu bosi wake hampendi, lakini ikumbukwe kuwa hiyo siyo suluhu kwako kwani kuna hatua mbalimbali za kufuata kabla ya kuchukua uamuzi wako ulioukusudia.
Je umeshoka? Umekata tamaa? Huna furaha? au Hupati hamasa katika kazi yako? Pia inawezekana kwamba mawasiliano yako na bosi wako yanakufanya uwe mnyonge, kwa kuwa ni mwonevu, mkatili na mkandamizaji. Anaingilia faragha yako, anakudhibiti, mchokonoaji au kukuona huna maana.
Lakini bosi huyo huyo hupata sifa kupitia kazi zako nzuri unazozifanya, kwa kuwa hakujali wala kukuthamini, kamwe hawezi kukupa habari nzuri kuhusu utendaji wako. Badala yake anakutia katika msukosuko kikazi, pia anashindwa kukusaidia ili uweze kukamilisha kazi yako.
Huyo ni bosi ambaye siye mtendaji mzuri, mara zote hupenda kuchongea wafanyakazi wake na kuwatafutia sababu ya kuwapa onyo. Kutokana na hali hiyo anakuwa ni bosi mwenye upungufu katika kazi yake, hana sifa ya kuwa kiongozi bora. Uwepo wa mameneja au mabosi kama hao ni mkubwa na hiyo ndiyo changamoto kubwa waliyonayo waajiri wengi. Haijalishi ni tabia gani mbaya ya bosi wako, unapojua hali hiyo usikate tamaa endelea kufanya kazi yako kwa bidii na utayaona matokeo.
Sasa basi, unapokabiliana na hali kama hiyo, anza kufanya kampeni ya kufanya bosi wako atambue kuwa yeye ni kikwazo katika utendaji wako.
Kumbuka kuwa mabosi wengi hawatambui kuwa kushindwa kutoa maelekezo au kukupa taarifa za utendaji wako inamfanya yeye kuonekana kuwa hawezi kuongoza. Mara nyingine anaweza kufikiri kuwa ana mamlaka zaidi ya wafanyakazi wake. Kwani bosi au meneja ambaye amekuwa akitoa maelekezo mengi ambayo hushindwa kuyasimamia, hujihisi kuwa hayuko salama.
Mara nyingine hali hiyo hutokea kwa kuwa bosi huyo amekuwa hana elimu ya kuwa bosi, au ni makusudi yake tu. Matokeo yake wafanyakazi mara zote humcheka na kumdharau kutokana na tabia yake mbaya.
Huyo bosi ambaye si mtetezi wa wafanyakazi wake au mbaguzi kwa baadhi ya wafanyakazi, hawezi kuona thamani yako. Hata kama utatumia muda wako wa mapumziko na kuongeza bidii katika kazi.
Hivyo njia ambazo unaweza kuzifanya ili bosi wako ajue kuwa umebaini hali hiyo, ni vema kumfuata na kuzungumza naye, na umwambie unahitaji kwake kupata maelekezo, kuhusu utendaji wako na msaada wake.
Kuwa mpole na ulenge kwenye hitaji lako, ili bosi huyo aweze kujijua na kuamua kubadilika.
Muulize ni jinsi gani unaweza kumsaidia kufikia malengo yake. Hakikisha unamsikiliza vizuri na kutoa msaada unaohitajika.
Tafuta busara nyingine kutoka kwa mabosi wengine au watu wenye ujuzi wao, ili uwe na elimu nzuri ya kuzungumza na bosi huyo, na kuongeza nafasi ya ujuzi wako.
Kama utachukua hatua hizi na hazijafanya kazi, nenda kwa bosi aliye juu ya huyo na kuomba msaada. Au unaweza kwenda kwa mkuu anayehusika na masuala ya wafanyakazi kabla hujafika kwa mkurugenzi mtendaji, uzungumzae naye na kupata ushauri zaidi. Uelewe wazi kuwa bosi wako wa awali hatakusamehe, hivyo hakikisha unafanya kile unachoweza, kabla hujafikisha jambo hilo juu zaidi.
Endapo hutaweza kupata msaada kutoka kwa mabosi wako uliowaeleza, ya kutatua tabia mbaya za bosi wako, iwe ni siri kwako, na kuamua kufanya maamuzi mengine ya busara ambayo yataleta matokea mazuri kwako.
Kama hakuna mabadiliko yoyote, pamoja na jitihada zako binafsi, na kuona kuwa tatizo ni kwamba hawakuamini, unganeni wafanyakazi wote ambao wamepatwa na tatizo hilo, muende tena kwa bosi wa juu zaidi ili aweze kuliangalia tatizo hilo na kulishughulikia kwa ukubwa wake.
Kama unafikiri tatizo ni kwamba bosi wako hawezi au hataki kubadilika, omba uhamisho katika kitengo kingine katika ofisi hiyo hiyo.
Endapo uhamisho wako hautakubalika, anza kutafuta kazi nyingine. Ni vema kutafuta kazi hiyo kwa siri, lakini ukiwa na matumaini kuwa ipo siku moja utaondoka eneo hilo.
Hivyo basi ni muhimu kwa watendaji waliopewa madaraka ya kuwaongoza wengine kuwa makini katika mawasiliano na wafanyakazi wao, pia wapende kujifunza kwa kusoma na kutoka kwa viongozi wengine waliofanikiwa zaidi.

Wengi wa mabosi wa aina hiyo ni wale ambao elimu yao ya darasani huwa ni ndogo hivyo wanakuwa hawana mpanuko wa mawazo, na mara nyingi husababisha makundi katika ofisi.

Japo pia wapo mabosi ambao wamekwenda shule, ila kunyanyasa inakuwa ni tabia yao ambayo pia wakiambiwa wanaweza kuibadili.

Kwa upande wa wafanyakazi wanaokabiliana na hali hiyo ngumu, wasichoke kumwomba Mungu kwani yeye ndiye muweza wa mambo yote, pia wajitahidi kupata elimu zaidi ili wawe na uwezo wa kufanya kazi yoyote iliyo mbele yao.

0713 331455/0733 331455
www.lngowi.blogspot.com
lcyngowi@yahoo.com

0 Maoni:

Twitter Facebook