Sunday, December 27, 2009

ONDOA HOFU, KUWA JASIRI

KARIBU msomaji wa safu hii ya maisha yetu inayokujia kila siku ya Alhamisi.
Leo tutaangalia jinsi ya kuwa na ujasiri na kuondoa hofu katika maisha yako.
Hofu si jambo zuri katika maisha, lakini ni ukweli usiopingika kuwa, kila mtu hupatwa na hofu kutokana na jambo fulani analokutana nalo.
Hofu hiyo hukaa nayo kwa dakika chache kabla ya kutoweka. Lakini wapo wengine hukaa nayo kwa siku nzima. Kutegemea ni jinsi gani unavyoidhibiti hofu hiyo.
Watu wengi hukabiliwa na hali ya wasiwasi, kutokutulia, kudharauliwa, kuchanganyikiwa au mambo yake kutokuwa katika mpangilio mzuri, pamoja na kuwa na mawazo hasi.
Hali hiyo, isipodhibitiwa kwa haraka huleta usumbufu katika maisha yake. Hivyo ni vema kujijengea hali ya ujasiri na kuondoa hofu, katika jambo lolote lile unalolifanya.
Kwa mfano, kama umeamua kulima ekari tano, utimize lengo lako, usiwe tayari kukatishwa tamaa na maneno kutoka kwa wengine, kuwa hakutakuwa na mvua, ama ardhi haina rutuba nzuri, ng’ang’ana pale ulipojiwekea malengo yako.
Ama umedhamiria kufungua duka eneo fulani, wapo watakaokuunga mkono, pia wapo watakaokukatisha tamaa, cha msingi, fanya kile ulichokusudia kukifanya, mradi kiko kwenye mpangilio wako na umekifanyia maandalizi ya kutosha.
Fahamu kuwa, biashara yoyote haiwafuati wateja, bali wateja ndio wanaoifuata. Hivyo ubunifu wako ndiyo utakaokufanya usonge mbele na kukabiliana na changamoto katika biashara hiyo.
Kamwe usiingize hofu katika uamuzi wako, kutokana na maneno ya watu wengine ya kukuvunja moyo.
Hivyo utaona hofu ni adui namba moja wa maendeleo yako. Pia hurudisha nyuma maendeleo ya watu, kwa kuwazuia kufanya mambo yatakayowafanya wasonge mbele.
Pia humfanya mtu augue, husababisha matatizo ya kimaumbile, hufupisha maisha na hukunyamazisha pale unapotaka kuzungumza. Hivyo ni vizuri ukaondoa hali ya hofu katika maisha yako.
Hofu hukuletea hali ya mashaka, ambayo hukufanya usiwe na uamuzi sahihi. Inakuondolea hali ya kujiamini, ya kuweza kujitathmini kwa nini unakuwa na hali ngumu ya kiuchumi.
Ukweli ni kwamba, hofu ina nguvu katika maisha ya mwanadamu. Kwa njia moja ama nyingine hali hiyo inazuia watu kupata kile wanachokihitaji katika maisha.
Hofu kwa jinsi yoyote ile ni athari za saikolojia. Unaweza kuitibu hali hiyo kama vile unavyotibu magonjwa katika mwili wako.
Kwanza, kuwa na maandalizi wewe mwenyewe ya kuondoa hali hiyo, kwa kuwa na hali ya kujiamini. Kwa kuwa, hakuna yeyote aliyezaliwa katika hali hiyo ya kujiamini, bali wameishinda hali hiyo.
Hata pale unapokabiliwa na hali ngumu katika maisha, usikate tamaa, chukua hatua madhubuti ya kupambana na hali hiyo, njia itaonekana kwako.
Inakupasa kuondoa hali ya hofu uliyonayo ili uweze kupiga hatua zaidi.
Endapo unakabiliwa na hali ya hofu ya kupoteza wateja wako muhimu kulingana na ushindani ulionao, fanya kazi mara mbili zaidi ili kutoa huduma bora zaidi, weka vitu vile vinavyowafanya wateja wako wakukimbie, utafanikiwa.
Ama unakabiliwa na hofu ya kupata ajali wakati ukiendesha gari, ni vema kuwa makini na kuvaa ujasiri ili kuondoa hofu kwa abiria wengine waliopo kwenye gari.
Yamkini unaweza kujikuta unakabiliwa na hofu ya watu wengine hufikiri ama kusema nini juu yako. Inakupasa kuweka mipango yako vizuri na kuikamilisha kama ulivyoipanga ili kutimiza kile ulichokikusudia.
Katika kutibu hali hiyo, iondoe hofu uliyonayo, pamoja na kuchukua hatua madhubuti za kuondoa hali hiyo.
Kadiri unavyoshindwa kuwa na ujasiri, ndivyo unavyoshindwa kujisimamia katika mipango yako.
Akili yako ni kama benki, kila siku unawaza mambo mapya unayoyahifadhi katika benki yako.
Mawazo hayo unapoyaweka katika benki ya akili yako, yanakuwa na kukaa katika kumbukumbu zako.
Pale unapokabiliana na tatizo, unaangalia katika benki yako na kupata jibu sahihi. Benki yako itatoa majibu na kusambaza taarifa mbalimbali zinazohusiana na hali unayokabiliana nayo.
Lakini ili benki yako iwe na manufaa kwako, inakupasa uweke mawazo mazuri yenye kukupatia maendeleo.
Iwapo unakula, ama unaendesha gari wakati ukiwa mwenyewe, ni wakati wako mzuri wa kuhifadhi mawazo mazuri katika benki yako. Pia kabla ya kulala, ni vema kuweka mawazo mazuri katika benki yako.
Waza kuwa na maisha mazuri, familia nzuri, afya njema, elimu nzuri na hali ya kupata mahitaji yote katika utoshelevu.
Pia katika benki yako, unatakiwa kuchukua mawazo mazuri tu. endapo utachukua mawazo mabaya, yatakuletea usumbufu au hali ya kuchanganyikiwa.
Tukutane wiki ijayo.
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa kitabu cha The Magic of Thinking Big, kilichotungwa na David Schwartz.

0 Maoni:

Twitter Facebook