Sunday, December 27, 2009

JIAMINI UTAFANIKIWA

MSOMAJI wangu, katika mfululizo wa makala hizi za Maisha Yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi.
Leo tutaangalia jinsi ambavyo kila mmoja anapaswa kujijengea uwezo wa kuweza kujiamini ili kupata mafanikio.
Kila mmoja anapaswa kutamani kuwa kiongozi yeye mwenyewe, ili aweze kujenga uwezo wa kuwa na maendeleo binafsi, pasipo kutamani maendeleo ya mtu mwingine.
Kwasababu hakuna mtu atakayemlazimisha mtu mwingine kupata mafanikio.
Lakini kwa upande mwingine, suala la mafanikio ni jambo linalotokana na muda uliopo, kujitoa na kufanyia kazi mambo mbalimbali mtu anayoyapanga.
Hivyo ujue wazi hakuna mtu atakayekulazimisha wewe kupata mafanikio, bali inakupasa kufanya bidii binafsi ili ufikie matarajio ya juu uliyojipangia.
Haya yakizingatiwa, kila mmoja atakuwa na ari ya kujisimamia, kufanya kazi kwa bidii katika mipango mbalimbali ya maendeleo ya ukuaji wa uchumi.
Sasa basi ili uweze kukua na kupata maendeleo, inakupasa kila jambo unalolipanga uweze kulitekeleza.
Ni vema kuanza kufanya jitihada binafsi za kupata maendeleo, pamoja na kufanya tathmini ya hapo ulipo na ulipotoka, taratibu utajikuta unapiga hatua siku baada ya siku.
Kwa kuwa, tayari unayo maabara iliyosheheni kila hitaji la mwanadamu, unayotakiwa kuichunguza na kuifanyia kazi, ni vema kujibidiisha ili uweze kukitumia kila kifaa kilichopo ndani yake, kwa ajili ya maendeleo.
Hakuna kikwazo chochote katika maabara hiyo, kinachoweza kukukwamisha, kama utajitambua kama wewe ni mhusika mkuu katika maabara hiyo ni wazi utapenda kujua kazi ya kila kifaa.
Kwa kuwa, ndani ya maabara hiyo, hakuna kitu cha kununua, kodi ya kulipa, wala ada ya aina yoyote ila unaweza kuitumia vile unavyopenda bila malipo yoyote.
Kama wewe ni msimamizi katika maabara yako mwenyewe, utapenda kufanya vile wanasayansi wengine wanavyofanya.
Unaweza kushangaa kwa nini watu wengi wana uelewa mdogo wa kufikia mafanikio, wakati wanazungukwa na wenye mafanikio makubwa.
Hii ni kwa sababu watu wengi hawafuatilii mambo yanayofanywa na wengine ili kufikia malengo makubwa.
Hivyo basi, Mtunzi David Sachwartz, nia yake ni kukusaidia kwa kuchunguza na kuangalia undani wa mambo yanayofanywa na wengine ambao wameweza kufanikiwa.
Kuna uchaguzi wa aina mbili wa kukusaidia ili uweze kufanikiwa; mojawapo ukiwa ni kupenda kujifunza kwa kuchunguza kila kitu unachokiona na kuamini kuwa kinaweza kukupatia maendeleo.
Pia unaweza kuchagua mifano ya watu wawili ambao unaweza kuwatumia kwa ajili ya kujifunzia katika kupata mafanikio yako.
Unatakiwa kuwachagua watu ambao mmoja wao, amefanikiwa na mwingine ambaye hajafikia mafanikio, ambao unawajua vema.
Anza kufuatilia kila jambo wanalolifanya, utapata somo litalokufumbua macho.
Kila unachojifunza kwa watu hao, kinakuwezesha kupiga hatua zaidi, lengo lako likiwa ni kuangalia kanuni za kufikia mafanikio. Pia kwa kutumia mifano ya watu hao, ndivyo utakavyopata mbinu mpya za kukabiliana na changamoto za maisha kufikia mafanikio.
Ni jambo la kufurahisha unapokuwa na ujasiri, na kufanikiwa kila unachopanga, kujiangalia unavyokuwa siku baada ya siku na mwezi baada ya mwezi.
Makala hii imeandikwa kwa msaada wa kitabu cha ‘The Magic of Thinking Big’, mtunzi wake ni David Schwartz.
Tukutane Alhamisi ijayo.

0 Maoni:

Twitter Facebook