Sunday, December 27, 2009

BUNI NJIA ZA MAFANIKIO

MSOMAJI wangu, katika mfululizo wa makala hii ya maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi.
Leo tutaangalia ujasiri unavyomfanya mtu kubuni njia mbalimbali za mafanikio.
Kila mmoja anapenda kuwa na mafanikio katika maisha yake, lakini mafanikio hayaji tu bila kufanya juhudi ama jitihada za dhati.
Mojawapo ya njia inayoweza kukutoa hapo ulipo na kukupeleka katika hatua nyingine nzuri zaidi ni ubunifu.
Mtu yeyote anayependa kuwa na mafanikio maishani, inambidi awe mbunifu katika nyanja mbalimbali ili kama yeye ni mfanyabiashara aweze kuteka soko kubwa.
Unaweza kuwa mbunifu katika fani yoyote ile uliyonayo, ama kipaji ulichopewa na Mungu, kitakachokufanya uwe mtu tofauti katika maisha yako.
Kama wewe ni mwalimu ambaye ni mbunifu wa kufundisha, maisha yako yatakuwa mazuri kwa sababu utasifika kwenye shule yako na sifa zako zitafika mbali hadi shule nyingine.
Hali hiyo itakufanya utafutwe na shule nyingi, hivyo ni uamuzi wako kuchagua uende wapi.
Ama utatafutwa na wanafunzi kutoka shule mbalimbali uweze kuwasaidia katika masomo yao ili waweze kufaulu mtihani, hapo wewe si yule wa zamani bali umekuwa mtu mwingine wa tofauti, kutokana na ubunifu wako.
Kama wewe, una ofisi ya ushonaji na ukawa mbunifu mzuri wa mavazi, sifa zako zitafika mbali zaidi na watu wengi watakutafuta kwa ajili ya kuwabunia mavazi yao.
Tayari utakuwa umeshajijengea jina, cha msingi ni kuongeza jitihada ili wale wateja wako usiwapoteze.
Kama wewe ni mbunifu wa kupika chakula ama vitafunwa mbalimbali, utajulikana mtaani, kwenye ofisi ama kampuni mbalimbali na hata kutafutwa na watu kwa ajili ya shughuli zao za sherehe.
Hiyo ni mifano michache sana, ambayo unaweza kujifunza. Si hiyo tu, bali unaweza kutumia uhandisi wako kwa kujenga nyumba nzuri, ukatumia uandishi wako kwa kuandika habari nzuri, ukatumia udaktari wako kutoa ushauri na kutibu vizuri wagonjwa unaowaoona.
Tumia akili yako uliyopewa na Mungu, kwa kuwa mbunifu ili uweze kuwa na maisha mazuri.
Binafsi ninaamini kuwa kila mmoja Mungu amempa kipaji ama akili kwa ajili ya kuwa mbunifu.
Tatizo lililopo kwa watu wengi ni kukata tamaa. Wengi wamekuwa wakikatishwa tamaa na ndugu, jamaa ama marafiki zao.
Na mara nyingi, wanaweza kufanya jambo na lisifanikiwe kama walivyofikiri matokeo yake, badala ya kutafuta ufumbuzi kwa nini hali hiyo imetokea, hukata tamaa na kuamini kuwa hawezi kufanya jambo lolote likafanikiwa labda aajiriwe tu.
Inabidi tubadilike kimtazamo, kiakili na kifikra ili kila mmoja afurahie maisha yake aliyopangiwa na Mwenyezi Mungu hapa duniani.
Hivyo, endapo unaamini jambo fulani haliwezekani, ndivyo itakavyokuwa.
Lakini endapo unaamini kuwa jambo fulani linawezekana, akili yako italifanyia kazi na kutafuta njia ya kulifanikisha.
Kuamini kuwa unaweza kufanya jambo, kunakufungulia milango zaidi ya kuwa mbunifu katika shughuli na maisha yako.
Akili yako, itafungua njia ya mafanikio kama utaitumia vema.
Na pia, kama unataka kuona njia ya kukutoa hapo ulipo, ondoa ukuta wa kuona kuwa haiwezekani, ndipo mafanikio yako yatakapoonekana.
Mafanikio makubwa yanakwenda kwa mtu anayefikiri kuwa na maisha ya viwango kwa ajili yake na wengine.
Ni vizuri pia kuboresha biashara zako ama shughuli zako unazozifanya kwa ajili ya kukupatia riziki, ili wengine waweze kufurahia huduma zako na kukutafuta.
Pia unaweza kujijengea tabia ya kuwa na mazoea ya kufikiri mbinu mbalimbali za maendeleo kwa dakika 10 kila siku, kabla hujaanza kazi yoyote.
Zoezi hilo, ni rahisi na kama utalizingatia utaona matokeo yake mazuri, ni vema kulizingatia.
Kwa upande mwingine, utagundua kuwa, watu wote waliofanikiwa, hupenda kujishughulisha, si wavivu.
Penda kujiuliza unatakiwa kufanya nini ili uzalishe zaidi? Ama uwe na maisha bora zaidi? Majibu ya maswali hayo ndiyo yatakayokufanya uongeze bidii zaidi.
Na kwamba, ili uweze kuzalisha kitu chochote, unatakiwa uwe na malighafi.
Katika kufikia uamuzi makini, malighafi ni mawazo na mapendekezo ya watu wengine.
Kuwa makini, usipende sana kuhitimisha jambo lako, kwa mawazo ya wengine. Kwani mawazo ya wengine yanakusaidia kuchekecha mawazo yako mwenyewe kwa kuwa akili yako ina ubunifu.
Ili ufanikiwe katika kampuni yako ama kiwanda chako, inakupasa ufanye utafiti wa kujua ubora wa bidhaa zako kwa wengine.
Uliza maswali kuhusu ubora wa bidhaa zako, ukubwa wake, bei yake ama mwonekano wake kwa jamii uko vipi ili uweze kufanya maboresho pale inapotakiwa.
Kuwasikiliza wengine, kunakufanya kukuwezesha kuboresha pale penye upungufu.
Tukutane wiki ijayo.
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa kitabu cha ‘The Magic of Thinking Big’, kilichotungwa na David Schwartz pamoja na mitandao mbalimbali.

0 Maoni:

Twitter Facebook