Sunday, December 27, 2009

AMINI KUWA UNAWEZA KUFANIKIWA

MSOMAJI wangu, katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi. Leo tutaangalia jinsi ya kuwa na malengo makubwa katika maisha.
Kufikiria mambo makubwa katika maisha, kunakuwezesha kuishi maisha mazuri, yenye furaha, utimilifu, kipato kizuri, marafiki na heshima.
Mafanikio maana yake ni kupata mahitaji unayohitaji, kustawi katika maisha, kuwa na nyumba nzuri, kupata safari, kuwa na vitu vipya, fedha zinazotosheleza mahitaji, pamoja na kuwapa watoto wako mahitaji ya muhimu.
Vile vile kwa maelezo mengine mafanikio ni kupandishwa cheo kazini kwako, kuendelea kuwa karibu na watu katika biashara zako na maisha yako kwa ujumla.
Pia kwa maelezo mengine, ni kujiheshimu, kuendelea kuwa na furaha pamoja na kutosheka katika maisha, kuwa na uwezo wa kufanya zaidi kwa wote wanaokutegemea.
Maana yake nyingine ni kushinda ama kufaulu katika maisha.
Kila mwanadamu anapenda kuwa na mafanikio katika maisha yake, hakuna hata mmoja anayefurahia hali ya kutokupiga hatua katika maisha, pia hakuna anayependa kuwa nyuma katika maisha haya tunayoishi.
Hivyo ni vizuri kupenda kujenga imani ya kujiamini kuwa unaweza kufanya jambo fulani ulilokusudia na kufanikiwa.
Kwa kuwa, mtu yeyote anapoweka nia kuwa anaweza jambo fulani, anafanikiwa. Lakini kinyume cha hapo, kamwe hatafanikiwa, atabakia katika hatua ile ile kila siku, ilhali wengine wakiwa wanasonga mbele.
Kila siku ulimwenguni, vijana wanaomaliza vyuo huanza kazi mpya. Kila mmoja anafikiria kuwa siku moja atafurahia mafanikio yatayompandisha juu kwa kumtoa hapo alipo na kumpa nafasi nyingine nzuri zaidi.
Lakini wengi wa vijana hao, hawafikirii kwamba ipo siku wanaweza kufika mbali zaidi ya hapo walipo. Matokeo yake, hawafiki mbali kwa kuwa hawana imani ya kuwatoa hapo walipo.
Matokeo yake, hubakia kuwa watu wa kawaida katika maisha yao.
Lakini kuna baadhi ya vijana wachache, wanaoamini kuwa, katika kipindi kifupi, tokea waanze kazi, watakuwa wameshasonga mbele zaidi.
Wanakuwa wanawaza kufika mbali zaidi na kuamini hivyo kunatokana na imani yao hiyo na kufikia pale walipokusudia.
Vijana hao huwa wajanja kwa kuwatazama wale waliowatangulia, upungufu wao na kufikiria jinsi ya kufanya vizuri zaidi.
Huwa wanawatazama wale waliofanikiwa kwamba wanakabilianaje na vikwazo mbalimbali na kufanya maamuzi ya busara.
Wanakuwa watu wanaokusudia kuwa na mafanikio, hivyo wanafanya jitihada mbalimbali ili kufikia walipokusudia.
Mara nyingi katika maisha yetu ya kawaida, unakuta mtu anakuwa anapenda kufika mbali katika maisha lakini anakatishwa tamaa na wengine.
Cha msingi, unapaswa kufanya kile ulichokusudia. Usiwe mwepesi wa kukata tamaa katika maisha yako. Na matokeo yake utayaona.
Unapokuwa na imani ya kufanya jambo fulani, kamwe usikate tamaa, kinachokupasa ni kufikiri mbinu ya kukutoa hapo ulipo na kusonga mbele.
Unapokuwa jasiri kufanya jambo fulani, kunawafanya na wengine wakuamini kuwa unaweza.
Hivyo unapoamini kuwa unaweza kufanya jambo fulani, utafanikiwa. Kwa wale wasiokuwa na imani ya kufanikiwa hata wanapofanya jambo hukwama njiani, kwa kuwa tokea awali walishaona hawataweza.
Unapokuwa na imani kuwa huwezi kufanya jambo fulani, ama kuwa na wasiwasi wa kufanya jambo, akili yako inapata sababu ya kukubaliana na kile unachokiamini.
Hofu, wasiwasi, kutokuamini kuwa unaweza, vinakufanya ushindwe kufikia malengo uliyojiwekea.
Hivyo ni vema kuwa na mawazo ya ushindi ili uweze kufanikiwa.
Imani ni kipimo chako katika maisha ambacho kitakuongoza. Kama unaamini kuwa kamwe hautakuwa tajiri, hali huwa hivyo hivyo.
Kama unaamini hutaweza kufanya mambo makubwa katika maisha, ndivyo itakavyokuwa. Kama unajiona kuwa wewe si wa muhimu, utaendelea kuonekana hivyo hivyo.
Kwa mtu anayewaza mambo makubwa, anakuwa anaamini kuwa atakuwa na utajiri, ndivyo inavyokuwa kwake.
Anaamini kuwa ataweza kufanya shughuli ngumu ambazo zitaMfikisha mahali pazuri na ndivyo inavyokuwa.
Kila kitu anachokifanya, jinsi anavyochukuliana na watu, tabia yake, mawazo yake, vyote vinamweka katika nafasi nzuri ya kuwa na mafanikio zaidi. Na kuonekana ni mtu wa maana.
Mtu ni bidhaa ya mawazo yake mwenyewe kwa kuamini na kufikiri mambo makubwa.
Tukutane Alhamisi ijayo.

0 Maoni:

Twitter Facebook