Sunday, December 27, 2009

AKILI YAKO NI KIWANDA CHA MAFANIKO

MSOMAJI wangu, katika mfululizo wa makala hizi za maisha yetu, nimedhamiria kukuletea kitu kipya kila Alhamisi. Leo tunazungumzia ili ufanikiwe unatakiwa ufanye nini.
Ni ukweli usiopingika kuwa, ili ufanikiwe katika maisha yako, inakubidi ufanye jitihada ya dhati. Kwa kujiuliza ni wapi uliposhindwa, ili uweze kuongeza bidii.
Vile vile, ni vema kuangalia udhaifu wako ulipo, ili uweze kurekebisha pale unapokosea katika kufikia mafanikio unayoyataka.
Watu wengi hupenda kuwa na mafanikio makubwa, lakini hawaonyeshi jitihada za dhati za kuwatoa pale walipo na kuwasogeza mbele.
Mara zote hukata tamaa kwa kuwaza mambo ambayo huwarudisha nyuma, hawako tayari kukubaliana na ukweli kuwa wanaweza kufanya jambo lolote ili kufikia malengo makubwa, cha msingi kinachotakiwa ni jitihada.
Hivyo basi, ni vizuri kuiambia nafsi yako, kuwa wewe unaweza kufanya jambo fulani kubwa litalokutoa hapo ulipo na kukufikisha sehemu nyingine yenye mafanikio zaidi.
Watu wengi hawaamini kuwa, Mungu amewabariki kwa kuwapa utajiri mwingi katika maisha yao, kwa kuwa, hawajui akili, nguvu, vipaji mbalimbali walivyonavyo ni utajiri tosha Mungu aliowapa katika maisha yao.
Ni vema kujiamini kuwa unaweza kufanya jambo kubwa katika maisha. Jitihada katika jambo lolote linakuleta mafanikio, kwa kukutoa katika hatua moja na kukupeleka katika hatua nyingine.
Vinginevyo utabakia kila siku ukiiambia nafsi yako, kwa nini wengine wanafanikiwa na wewe unabaki katika hali ile ile.
Jione kuwa wewe ni mtu wa thamani na ni mtu wa daraja la kwanza. Pia jenga hali ya kujiamini katika kila jambo unalotaka kulifanya.
Jiamini wewe mwenyewe na mambo mazuri yatatokea kwako, usiwe na hali ya hofu katika mambo uyafanyayo.
Akili yako ni kiwanda cha fikra. Ni kiwanda kilicho na shughuli nyingi. Hivyo itumie kwa busara upate mafanikio mengi.
Utakapoitumia akili yako vizuri utajikuta kila siku unapiga hatua zaidi. Kamwe usiiruhusu akili yako kuwaza kushindwa.
Unapodhamiria kufanya jambo fulani amini kuwa utafanikiwa. Wasiwasi utakufanya ushindwe katika kila unalotaka kulifanya.
Inuka, mlango wa mafanikio uko wazi na ujiweke kwenye kumbukumbu sasa kwamba unajiunga na kundi ambalo linakubali mabadiliko katika maisha.
Na hatua ya kwanza katika maisha yako, ambayo huwezi kuiepuka, amini kuwa unaweza kufanikiwa.
Je, ni jinsi gani, unaweza kuwa katika hali ya kujiamini kwamba unaweza kufanya jambo lolote na ukafanikiwa?
Ni pale tu utapofikiri kuhusu mafanikio yako na siyo kushindwa, uwapo kazini kwako ama nyumbani.
Hata pale utakapoona unapokabiliwa na hali ngumu, jiambie kuwa utashinda. Na kama upo ushindani kati yako na mtu mwingine, fikiri kuwa, una uwezo wa kushinda na si kushindwa.
Na nafasi ya kushinda inapoonekana, fikiri kuwa unaweza na si kwamba huwezi. Akili yako mara zote ifikiri kuwa unaweza kufanya jambo la mafanikio katika maisha.
Hali ya kuwaza mafanikio inakufanya katika akili yako uweke mikakati ya kukufanya upige hatua zaidi. Kinyume na hapo, utakaporuhusu akili yako kuwaza hali ya kushindwa, kamwe hautapiga hatua yoyote, kila mara utabakia pale pale.
Jambo jingine jikumbushe kwamba wewe ni bora kuliko unavyodhani. Watu wenye mafanikio si kwamba wana nguvu zaidi ya wengine.
Wala mafanikio si suala la kuona mtu fulani ana bahati, bali ni hali inayoweza kujengwa na mtu mwenyewe kwa kuongeza bidii.
Panda kuwaza mambo makubwa, ukubwa wa mafanikio yako unategemea jinsi unavyowaza. Kama unawaza malengo madogo, utarajie kupata mafanikio madogo.
Unapofikiri malengo makubwa, unakuwa na mafanikio makubwa pia.
Kumbuka hili, mawazo na malengo makubwa, mara zote yanarahisisha mambo yako na kukufanya usipate vikwazo vingi, tofauti na unavyowaza malengo madogo.
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa kitabu cha ‘The Magic of Thinking Big’ kilichotungwa na David Schwartz.
Tukutane alhamisi ijayo.

0 Maoni:

Twitter Facebook