Friday, December 19, 2008

FAHAMU NJIA SAHIHI YA KUKOSOA ILI MTU ASIKUCHUKIE

KARIBUNI wapenzi wasomaji katika safu hii inayokujia kila Alhamisi. Ninamshukuru kila mmoja aliyekuwa mstari wa mbele katika kufuatilia mada mbalimbali. Wapo waliotoa ushauri, pongezi, lakini pale nilipokosolewa nilikubali kwani nia ni kuelimisha.
Leo tutaangalia mifano mbalimbali katika maisha yetu tunayoweza kuitumia pale tunapotaka kumkosoa mtu yeyote aliyefanya jambo kwa makusudi au kwa kutokujua bila kumfanya ajisikie vibaya.
Kwa kuanza, tumuangalie mkurugenzi mmoja aliyekuwa na viwanda mbalimbali vya kutengeneza nguo. Lakini siku moja aliamua kufanya ziara ya ghafla katika kiwanda chake kimoja.
Alipofika kiwandani aliwakuta baadhi ya wafanyakazi wake wakivuta sigara karibu kabisa na kibao kinachokataza uvutaji sigara sehemu hiyo.
Mkurugenzi huyo akakisogelea kibao hicho na kuwaonyesha wafanyakazi hao huku akiwauliza, ‘hamjasoma hapa?’ Wafanyakazi wote wakataharuki, wakashindwa kujieleza.
“Vijana ningefurahi kama mngevuta sigara nje ya eneo hili au niseme hata nje ya kiwanda.” Wafanyakazi hao walielewa kwamba bosi wao anatambua kuwa wamevunja sheria, lakini walimfurahia kwa sababu hakuzungumza nao kwa ukali, bali alizungumza kwa upendo na kuwafanya wajisikie kwamba wao ni wa muhimu katika kiwanda kile.
Hilo lilikuwa ni fundisho kubwa kwao, kwani tokea hapo hawakurudia kosa hilo tena. Hivyo unaposhughulika na watu mbalimbali jaribu kuwa na busara katika kuwaeleza jambo.
Mfano mwingine ni kwa ofisa mmoja aliyejulikana kwa jina la Robby. Alikuwa na biashara zake na kila siku alikuwa akitembelea mojawapo ya biashara hizo.
Ilifika siku moja akaenda kwenye ghala lake la vinywaji na kumwona mteja amekaa anasubiri huduma, lakini kulikuwa hakuna mtu wa kumhudumia kwa kipindi hicho.
Aligundua kuwa kwa wakati huo, wafanyakazi wake hawakuwa tayari kumsikiliza mteja huyo, bali walikuwa wamekaa kaunta, wakicheka na kuzungumza habari zao zinazowahusu bila kujali kuwa eneo lile ni eneo la kazi.
Robby hakuzungumza lolote, taratibu akanyata kando ya kaunta na kumhudumia mteja yule mwenyewe na kukabidhi pesa kwa wauzaji hao wakati alipokuwa anaondoka.
Hapo tunaona kwamba Robby alitumia njia ya busara ya kuishi na wafanyakazi wale. Angeweza kutumia ukali au kuchukua hatua ya kuwafuta kazi mara moja, lakini kwa kuwa alikuwa ni mtu mwenye hekima na busara, aliamua kumhudumia mteja yule aliyemkuta na hilo lilikuwa fundisho kubwa kwa wafanyakazi wake.
Aliwapa somo kwa njia ya vitendo kwamba kazi si mahali pa mchezo, bali panahitaji kuheshimiwa na kumheshimu kila anayehitaji huduma.
Vilevile tunaona kwamba viongozi wa umma mara nyingi wamekuwa wakipingwa kutokana na kutokuonekana katika majimbo yao. Mara zote wanasongwa na kazi, wamekuwa katika hali ya ulinzi muda wote na wasaidizi wao ambao hawapendi watu wawabugudhi mabosi, kwa kuruhusu wageni wazungumze nao.
Lakini kuna mbunge mmoja ambaye mara zote amekuwa akiwaasa wafanyakazi wake kuwaruhusu watu wamuone. Amekuwa akisema kwamba sera zake zipo wazi kwa kila mmoja, lakini wasaidizi wake wamekuwa wagumu kumuelewa, na kuendelea kuwazuia wananchi wasiweze kumuona kwa urahisi ili waeleze matatizo yao yanayowakabili.
Baada ya kuona somo hilo halieleweki kwa wasaidizi wake, mbunge huyo mwishoni alipata suluhu kwa kuamua kuondoa mlango wa ofisi yake. Kitendo hicho kilitoa ujumbe kwa urahisi kwa wasaidizi wake, kwamba mbunge huyo yuko wazi na yuko tayari kumsikiliza kila mmoja.
Hapo inamaanisha kwamba si lazima kila mara ukawa unazungumza na watu ambao hawakuelewi, wakati mwingine unaweza kuzungumza kwa vitendo, utaeleweka.
Kwa kawaida unapobadilisha maneno mawili au matatu inaweza kuleta tofauti kati ya kushindwa na mafanikio katika kuwabadilisha watu wasiweze kuwa na uchungu.
Unapotumia njia ya busara katika kumrekebisha mtu aliyekosa, inamfanya mtu yule asiyekuwa na uvumilivu katika kuwasahihisha wengine kwa kuwakosoa katika njia ya uwazi, kujifunza kitu.
Mfano mwingine upo kwa familia mmoja, iliyokuwa inakarabati nyumba yao, kwa kutumia mafundi ujenzi, familia hiyo ilifikia mahala ikaamua kuwashawishi mafundi kufanya usafi mara tu wamalizapo kazi yao.
Kwa siku za mwanzoni mwa ujenzi huo, mama mwenye nyumba alipokuwa akirudi nyumbani baada ya kazi, alibaini kuwa eneo la nyumbani kwake lilikuwa chafu, lenye kuonekana vipande vya mbao na uchafu mwingine. Mama huyo hakutaka kuzungumza na mafundi hao, kwa sababu walikuwa wamefanya kazi nzuri.
Kwa hiyo baada ya mafundi hao, kuondoka, yeye na watoto wake waliokota vipande hivyo vya mbao na kusafisha eneo hilo la ujenzi. siku iliyofuata alimwita kiongozi wa mafundi waliokuwa wakijenga na kumwambia kuwa, “Nimefurahishwa na jinsi mlivyoacha eneo hili jana usiku, lilikuwa zuri na safi, na halikuweza kuleta usumbufu kwa jirani.” Tangu siku ile na kuendelea, wafanyakazi wale baada ya kazi walikuwa wakikusanya takataka zote na kuacha eneo lile safi. Na kiongozi yule alikuwa akihakikisha kama wafanyakazi wake wameacha eneo walilofanyia kazi likiwa safi.
Katika mfano mwingine tunaweza kuuona kwa askari. Kati ya eneo linalotatanisha askari wanapokuwa kwenye mafunzo yao ni suala la ukataji wa nywele. Kwa kuwa wengi wao wanajiona kwamba kama bado ni raia wa kawaida, na ghafla wanajikuta wanatakiwa kukata nywele zao na kuwa fupi.
Kiongozi wao mmoja alilibaini hilo, na kusema kuwa awali kabla ya kugundua njia ya kutatua tatizo hilo, alikuwa akiwatisha askari hao bila mafanikio.
Lakini alipobaini tatizo lake, siku hiyo akaanza kwa kuwaambia maaskari hao: “Ndugu zangu, nyie ni viongozi. Na mnakuwa viongozi bora pale mnapofundisha kwa mifano. Mnatakiwa kuwa mfano ili wengine wafuate. Je, mwajua masharti ya jeshi kuhusu kukata nywele? Ninakwenda kukata nywele zangu leo, ingawa bado ni fupi kuliko baadhi yenu. Mnaweza kujiangalia wenyewe kwenye kioo, na mwone kama mnapaswa kukata nywele ili muwe mfano bora, tutapanga muda kwenu wa kwenda kwa kinyozi.”
Matokeo yake yakawa mazuri, kwani maaskari hao wanafunzi walijiangalia kwenye kioo na kwenda kwa kinyozi mchana ule na wakawa wamepokea masharti hayo ya kuwa na nywele fupi.

NJIA SAHIHI YA KUSHUGHULIKA NA MALALAMIKO

WATU wengi wamejaribu kuwashawishi wengine jinsi wanavyofikiri kufanya kwa kuzungumzia zaidi kuhusu mambo yao. Waache na wengine wazungumze.
Kwani wanajua zaidi kuhusu shughuli zao na matatizo kuliko unavyodhani. Kwa hiyo ni vema uendelee kuwauliza maswali ili waweze kukwambia mambo machache wanayoyajua.
Watu wengi hujikuta wakiingilia kati pale ambapo hawakubaliani na mazungumzo ya mwingine. Lakini wewe usifanye hivyo. Ni hatari. Hawatakusikiliza wakati bado wana mawazo yao mengi ya kueleza.
Hivyo ni vema kusikiliza kwa utulivu na kuweka kumbukumbu kile kinachozungumzwa. Kuwa mtulivu katika hilo. Watie moyo kuelezea mawazo yao yote.
Je, unafikiri utaratibu huo ni mzuri? Hebu tumuangalie mfanyabiashara. Kulikuwa na mfanyabiashara moja ambaye alikuwa akitafuta soko kwa ajili ya biashara yake, kabla ya kumwona mhusika mkuu wa ofisi aliyokuwa anakwenda, alipata tatizo la kukaukiwa na sauti yake.
Alipopata nafasi ya kuonana na Mkurugenzi huyo wa kampuni aliyokwenda, aliandika kwenye karatasi kumweleza kuwa sauti yake imekauka na kumuuliza kama wanaweza kuendelea katika hali hiyo aliyonayo na mhusika yule akamwambia kwamba wanaweza kuendelea na mazungumzo yao.
Hivyo, alitoa nyaraka mbalimbali za uthibitisho wa bidhaa zake, ambapo Mkurugenzi yule alipokuwa akizipitia alikuwa akitabasamu kwa kuonyesha kuwa anakubaliana na bidhaa hizo.
Alimpongeza mfanyabiashara huyo kwa kuwa na bidhaa nzuri na kuamua kusaini naye mkataba. Baada ya kutiliana saini, mfanyabiashara alisema tangu aanze biashara yake hiyo hajawahi kupata kazi yenye mkataba wa fedha nyingi kama ulivyo huo.
“Ninajua kuwa ningepoteza mkataba huu kama sauti yangu isingekauka, kwa sababu nilikuwa na mawazo tofauti katika mazungumzo yote tuliyoyafanya.
“Nimegundua kuwa kukauka sauti kwangu kwa bahati mbaya, kumenipatia utajiri mkubwa, hivyo wakati mwingine ni vyema kuwaacha watu wengine wazungumze,” anasema mfanyabiashara huyo.
Kuwaacha watu wengine wazungumze kunasaidia katika mazingira ya familia pia kwenye biashara. Mfano mwingine ni wa mama mmoja na mtoto wake Lilly ambao walikuwa hawana mahusiano mazuri.
Lily alikuwa ni mtoto mkimya asiyependa kuzungumza, lakini alikuwa hana uhusiano mzuri na mama yake wakati wa ukuaji wake, kwa kuwa mama yake alikuwa akimtishia na kumwadhibu pasipo sababu za msingi.
Kutokana na adhabu hizo mtoto huyo alikuwa akimwangalia tu mama yake, na mama huyo alipokuwa akimgombeza mtoto huyo alimwangalia tu na kuondoka eneo hilo.
Siku moja mama huyo aliwaambia wenzake kuwa mtoto wake amemshinda hivyo amenawa mikono juu yake. ” Mtoto huyu amenishinda amekuwa akiondoka nyumbani na kwenda kwa rafiki yake wa kike bila kuaga, lakini aliporudi nilikosa nguvu ya kumwadhibu tena, nilimwangalia kwa huzuni na kumuuliza kwa nini Lilly unafanya hivi?,” anasema mama huyo.
Kwa maelezo ya mama huyo, mtoto wake alimwangalia kwa upole na kumuuliza, “Je ni kweli unataka kujua?,” mama huyo anasema kwanza alimwangalia mtoto wake na kuanza kupatwa na wasiwasi, baada ya muda wasiwasi huo ukatoweka. Hakuwa tayari kumsikiliza, japo amekuwa mara nyingi akimwambia mtoto huyo kufanya kile na kile.
Mama huyo anasema wakati mtoto Lilly alipokuwa anamweleza mawazo na hisia zake, aliingilia kati na kutoa mamlaka nyingi kumzuia asiendelee kuzungumza.
Lakini mama anasema aliaza kutambua kuwa mtoto huyo alimhitaji, si kwamba awe kama mama ambaye anajiona ni bosi, lakini mwenye ujasiri na hayo ndiyo matokeo ya kumchanganya katika makuzi yake. Na mtoto huyo alipokuwa akijaribu kuzungumza na mama yake, mama huyo hakuwa tayari kumsikiliza.
Baada ya kukaa na kutathmini mama huyo alijiona kuwa ana makosa katika malezi ya mtoto wake, kwani mtoto huyo alihitaji kusikilizwa na kuheshimiwa mawazo yake. Tokea siku hiyo mama huyo alimwacha mtoto wake kumweleza hisia zake na aliweza kumsikiliza.
“Tangu wakati huo na kuendelea nimekuwa nikimwacha mtoto wangu azungumze kile anachotaka. Ananishirikisha mambo yake na uhusiano wetu umeanza kuwa mzuri, amerudi kuwa mtu wenye ushirikiano,” anasema mama huyo.
Hivyo, ni jambo zuri kwa wazazi kuwa karibu na watoto wao, kujua nini wanapenda, upungufu wao na jinsi gani anaweza kumrekebisha kwa hekima pasipo kutumia jazba wala kujionyesha kuwa yeye ni bosi hivyo mtoto anapaswa kumsikiliza kwa kila jambo.
Malezi bora ni pale wazazi na watoto wanapoelezana jambo kwa uwazi, hekima na kusikilizana hata kufikia mwisho wa jambo lenyewe. Ni vema kutoa nafasi kwa wengine nao waweze kutoa mawazo yao.

KAMA UMEKOSEA KUBALI KOSA

KARIBUNI wapenzi wasomaji katika safu hii. Tunamshukuru Mungu kwa kutufikisha tena Alhamisi ya kwanza ya Desemba. Nafikiri kupitia safu hii umepata elimu na maarifa mbalimbali. Leo, tutaangalia jinsi inavyokupasa kukubali kosa endapo utakosea.
Katika maisha yetu ya kila siku, ni vema kutambua kuwa unaweza kukosea kwa kufanya jambo makusudi au kwa kutokukusudia. Hivyo basi, endapo utakosea jambo, ni vizuri kukiri kosa pasipo kubisha hiyo ndiyo njia sahihi ya kuishi katika ulimwengu huu.
Iwapo umetenda kosa lolote, ukaulizwa na kukiri kukosea, ni rahisi kwa mtu anayekuuliza kuelewa kwamba umetambua kosa lako na kulijutia, hivyo hautarudia tena, tofauti kama ungekataa na kusema hujakosea.
Asilimia kubwa ya watu wanapokosea hunyamaza hadi wanapoulizwa. Lakini njia nzuri, unapokosea kujitambua mara moja na kukiri kosa kabla hujaulizwa, hiyo itamfanya yeyote kufikiria njia ya kukusamehe kama umemkosea.
Kijana mmoja aliyekuwa kiongozi katika idara yake, alisema kuna wakati hakutoa stahili ya fedha kwa wafanyakazi wake kiasi kwamba jambo hilo lilimgharimu na kuonekana hawezi kuongoza wenzake.
Alilitambua hilo mapema kabla bosi wake hajamuuliza, alimfuata na kumueleza kilichotokea, alikiri kuwa hali hiyo ameisababisha yeye.
Kijana huyo aliingia ofisini kwa bosi wake na kumueleza juu ya jambo hilo na kukiri kuwa amekosea. Kwa maelezo ya kijana huyo, baada ya kukiri kwa bosi wake kwamba jambo hilo ni yeye alilisababisha, anasema bosi wake alimwangalia na kumwambia “Sawa, ni kosa lako, lakini inakubidi kurekebisha jambo hilo.
“Makosa huwa yanarekebishika, kila mmoja anakosea,” anasema. Kijana anabainisha kwamba baada ya kuambiwa hivyo na bosi wake, alipata nguvu mpya na kufarijika zaidi, tangu siku hiyo bosi wake alimwamini kwa kila jambo.
Mtu asiye na busara, mara nyingi hujaribu kujitetea anapofanya makosa badala ya kukiri na kujirekebisha. Hali hii ipo kwa watu wengi katika maisha yetu ya kila siku. Wengi wetu hufanya makosa, badala ya kukiri huamua kukaa kimya mambo yanapoharibika ndiyo hukumbuka kuomba msamaha.
Mara nyingine mtu wa aina hiyo hupoteza uaminifu kwa wenzake na hata kufukuzwa kazi, kwa tabia ya kutokuwa tayari kukiri kosa. Hebu tuangalie mfano wa mwalimu aliyekuwa hana uhusiano mzuri na mtoto wake. Siku moja katika kipindi chake asubuhi, aliwaeleza wanafunzi wake jinsi alivyotofautiana na mtoto wake, hata kushindwa kuwaona wajukuu zake.
Mzazi huyo alihisi kuwa, kijana wake anapaswa kuwaheshimu babu zake, kukubali kila jambo atakaloambiwa liwe zuri au baya, kwamba hapaswi kuwa na maamuzi yake.
Mwisho, mwalimu alilieleza darasa lake kuwa amekuwa akiwaza tatizo hilo na kuona kuwa kuna umuhimu wa kumuomba mtoto wake msamaha. Anaeleza, mwanafalsafa anasema kama umekosea ni vema kukiri kosa haraka; kwa msisitizo. “Kwangu ilichukua muda mrefu kukiri kwa haraka, lakini nimeweza kukubali katika hali ya kumaanisha”.
Inawezekana niliona aibu kumuomba msamaha kijana mdogo, lakini nilikuwa nimekosea na lilikuwa ni jukumu langu kufanya hivyo.
Baada ya kusema hayo darasa lake lilishangilia kwa kupiga makofi, na kumpongeza. Kipindi kilichofuata mwalimu huyo aliwaeleza wanafunzi wake jinsi alivyokwenda nyumbani kwa mtoto wake, kuomba na kupewa msamaha, kwa sasa wamejenga uhusiano mpya na mtoto wake, mkwewe na watoto wao.
Hivyo basi, tumekuwa tukishuhudia watu mbalimbali wenye uwezo wa kukabiliana na watu ambao walikuwa ni maadui na kujenga urafiki mpya.
Je, waweza kusemaje kwa mtu anayekutendea jambo kama hilo? Pale tunapokuwa sahihi tuchukuliane na watu kwa upendo, tunapokosea, tukubali makosa yetu, hali hii itazidisha upendo kuliko kubakia kila wakati unajitetea

JARIBU KUWA JASIRI KUKIRI KOSA

KARIBUNI wapenzi wasomaji katika safu hii ya Maisha Yetu inayokujia kila Alhamisi. Safu hii imekuwa ikielimisha, ikikosoa na hata kutoa muongozo wa maisha ya kila siku.
Leo katika safu hii tutaangalia jinsi unavyoweza kujiepusha usiwe na maadui katika maeneo mbalimbali uliyopo. Kuna wakati unaweza kuona umeelemewa na mawazo pasipo kukumbana na tatizo lolote, lakini mtu anapokuambia umekosea, hilo linaweza kukufanya uwe na huzuni katika moyo wako.
Hivyo basi, unaweza kumueleza mtu kwamba amekosea kwa kumwangalia, kumwambia au kutumia ishara kama njia ya kumshawishi mtu akuelewe kama vile unavyoweza kuzungumza kwa maneno.
Elewa kuwa utapomwambia mtu ana makosa, unafikiri utamfanya akuamini? Hapana. Hiyo si njia sahihi, kwani unaweza kulitatua tatizo hilo kwa busara, maarifa, hekima na staha. Ukitumia njia za busara itamuwezesha yule mwenye tatizo kujutia makosa yake, japo haitamfanya kubadili mtazamo wake.
Unapojishughulisha na mtu yeyote huku ukitaka kufanikiwa, kamwe usianze kwa kueleza: “Ninakwenda kuhakikisha jambo hili na hili kwako” kufanya hivyo si jambo zuri, hiyo ni sawa kusema “Mimi ni bora kuliko wewe”.
Badala ya kutumia njia hiyo ni vyema kumueleza mtu unayetaka kumchunguza, mambo ambayo unafikiri yatabadili fikra zake, na kuweza kumsaidia.
Hiyo ni changamoto kwa kila mmoja kwani inaweza kuleta kutokuelewana na kumfanya yule uliyekusudia kumuonyesha kuwa wewe ni bora kuliko yeye, kupambana nawe kabla hujaamua kuanza. Kwa mtazamo huo, ni vigumu kubadili fikra za watu, ambao unadhani kuwa, wanaenda kinyume.
Hivyo ni busara unapotaka kwenda kuthibitisha jambo lolote, usilifanye kwa uwazi kila mmoja akatambua unalotaka kulifanya. “Fanya kwa werevu, ustadi, asiwepo yeyote atakayeweza kuhisi kwamba kuna jambo unalifanya”. Ili usije kujijengea uadui usiokuwa na lazima.
Mtu mmoja aliweza kumwambia mtoto wake kwamba awe na busara kuliko watu wengine kama anaweza, lakini asiwe mwepesi wa kuzungumza na kuwaeleza udhaifu wao ulipo.
“Ni kweli, ni vyema ukaiambia nafsi yako kuwa huwezi kuwa bora kuliko mwingine, kwa hiyo inakupasa kutokuwahukumu”.
Endapo mtu atakwambia maneno ambayo unafikiri si sahihi, nawe unajua hivyo, si vema kusema “Vizuri, sasa, tazama. Ninafikiri kuwa lakini ninaweza kuwa nimekosea mara kwa mara na kama nimekosea, nataka kujiweka sawa, tuweze kuujua ukweli”.
Huo ni muujiza, unasema “ninaweza kuwa nimekosea, imenitokea mara kwa mara, acha tujue ukweli,”. Hakuna mtu yeyote chini ya mbingu au chini ya ardhi atakayekubaliana na maneno hayo.
Kuna baadhi ya watu wamekuwa wakitumia maneno hayo pale wanapokumbana na misukosuko ya wateja au wafanyakazi wenzao. Kutokana na misukosuko hiyo ya mara kwa mara hupatwa na hasira anapokuwa na wakati mgumu wa kushughulika na matatizo ya wateja wake, hali inayomsababishia hasira, kukosana na watu na kutokukubalika.
Lakini unapokuwa jasiri na kukabiliana na hali hiyo kwa kuwaambia watu unaoshughulika nao, kuwa upo tayari kurekebisha upungufu unaoonekana kwao, na kusema kuwa uko tayari kushughulikia matatizo hayo, utakuwa na imani kwa wateja hao.
Unapokuwa jasiri wa namna hiyo inapunguza hasira kwa wale unaowatumikia na wataondoa hisia walizokuwa nazo juu yako na kampuni yako, ni vyema kuwa makini unaposhughulikia jambo lolote.
Ni vyema kuonyesha heshima kwa wateja, wafanyakazi wote bila kubagua, kwa kuwashauri na kuwajali itasaidia kuendelea kuwa shujaa katika ushindani wa biashara uliyonayo.
Kamwe hutaingia matatizoni pale utakapokubali kuwa umekosea, kwani itakuondolea maswali, kukupa moyo na itakufanya kuwa wazi pamoja na kupata uelewa mkubwa kuliko ulivyokuwa awali.
Unapokuwa umekosea ni vyema kukiri makosa hayo na endapo utakiri kwa unyenyekevu, utawafanya na wengine wajivune kupitia wewe.

JINSI UNAVYOWEZA KUJENGA URAFIKI

KILA mmoja hapa duniani ana jukumu la kuwa kiongozi mahali popote alipo - iwe nyumbani, kazini ama shuleni - ili kuwawezesha wengine kufanya kazi kwa kufuata kanuni na sheria zilizopo.
Mfano wewe ni kiongozi katika kampuni, shirika au ofisi yoyote, ni jukumu lako kuwaangalia wafanyakazi wenzako kama wanafanyakazi zao kwa kufuata sheria na taratibu za kazi zilizopo.
Kama utashindwa kuwasimamia vizuri, ikatokea mmoja wao akapatwa na madhara, jukumu hilo utalibeba wewe kama kiongozi wao. Hivyo basi, kama wewe ni kiongozi katika kampuni ya uhandisi ni vyema kuhakikisha kuwa wafanyakazi unaowasimamia wanatimiza wajibu wao, kwa kuvaa kofia za kufanyia kazi wakati wote wawapo kazini.
Inawezekana wakati mwingine wafanyakazi hao wakafanya mazoea na kuacha kuvaa kofia hizo au wakadharau kufuata sheria unazowaelekeza kama kiongozi wao, na kuamua kuzivunja unapoondoka katika eneo hilo la kazi na kufanya vile wapendavyo.
Kama utagundua kwamba maelekezo unayoyatoa kwa wafanyakazi hao hayatekelezeki ni vyema kujaribu njia nyingine ya kuwafikishia ujumbe huo, ili waweze kufanyakazi zao kwa kufuata sheria zilizopo, kuepuka na madhara yanayoweza kuwapata.
Ikitokea utawakuta wafanyakazi hawajavaa kofia wakiwa kazini, ni vema kutumia mbinu na kuanza kuwauliza, wanajisikiaje pale wanapovaa kofia hizo, je, wanakuwa huru au haziwakai vizuri ili uweze kujua tatizo lipo wapi.
Unapopata majibu kutoka kwao, ni vema kuwakumbusha kwa upole, umuhimu wa kofia hizo za kazi wanazopaswa kuvaa, kwamba zimetengenezwa kwa ajili yao wanapokuwa kazini tu, ili kuwakinga na hatari, endapo vitu vizito vitadondoka kwa bahati mbaya wawapo kazini.
Utakapofanya hivyo itakuwa rahisi kwa wafanyakazi hao kuelewa umuhimu huo na kuutekeleza, tofauti kama ungetumia sauti ya ukali na kuamrisha. Huo ni mfano mojawapo wa kujishughulisha na watu wanaokuzunguka katika mazingira mbalimbali. Unapokuwa mwenye busara na hekima katika kuzungumza, unakubalika na wale wanaokuzunguka kinyume cha hapo hata upige mbiu hautasikilizwa.
Ni vema kukumbuka kuwa, unapojishughulisha na watu, unajishughulisha na viumbe vyenye hisia, hivyo uamuzi mkali utasababisha hisia mbalimbali kwao.
Kiongozi asiye na busara anaweza kutumia muda wake mwingi kukosoa, kulaumu na kulalamika. Hivyo ndivyo wafanyavyo viongozi wote wasiotumia nafasi yao vizuri. Lakini ni vyema kiongozi akawa na tabia ya kujitawala na kuwa mwelewa, mwenye busara na kusamehe.
Kumbuka kuwa kuna siri kubwa ya kushughulika na watu. Pia kuna njia moja ya kumfanya yeyote kufanya chochote anachotaka, itategemea ni jinsi gani utakavyozungumza naye.
Unaweza kumlazimisha mtoto wako afanye kile unachotaka kwa kumchapa au kumtishia. Unaweza ukawalazimisha wafanyakazi wako kukupa ushirikiano, pale unapowatishia kuwafukuza. Lakini kumbuka hiyo siyo njia nzuri ya kujishughulisha na watu wanaokuzunguka.
Kuna msemo unaosema kama hutakuwa na uso wa tabasamu, huwezi kuuza duka. Tabasamu lako ndio mwongozo wa kufanya mambo mema. Pia inatoa mwanga wa maisha kwa wote wanaokutazama.
Hivyo endapo utakutana na watu wenye matatizo mbalimbali yanayowafanya wachukie wakati wote au kukunja nyuso zao kwa kukosa furaha, kumbuka tabasamu yako pekee ndiyo itakuwa dawa kwa wote walioumizwa.
Kwani watu hao hufikia hatua ya kukata tamaa baada ya kupata mashinikizo mbalimbali kutoka kwa mabosi, wateja, walimu, wazazi au watoto wao, tabasamu pekee ndilo linaloweza kuwasaidia kujua kwamba huo si mwisho wa maisha bali kuna furaha katika dunia.
Katika maisha tunayoishi ni vema ukajifunza njia mbalimbali za kuishi na watu ambazo zitakujengea heshima popote utakapokuwa. Njia hizo ni kupenda kujua majina ya kila unayekutana naye, kujitahidi kumwita kwa jina lake kila unapomwona.
Utakapofanya hivyo utajijengea heshima kwa jamii inayokuzunguka iwe ni nyumbani, shuleni na hata ofisini. Baadhi ya watu wamekuwa na tabia nzuri ambazo hupendwa na jamii. Tabia hizi ni pamoja na kutumia muda wao na kumsikiliza kila anayezungumza naye bila kumpinga.
Hali hii humfanya kupata njia sahihi ya kumsaidia mtu huyo endapo anahitaji msaada, ushauri au mara nyingine kumwelekeza. Baada ya kutumia muda wake kusikiliza kwa makini, huzungumza kwa sauti ya upole na unyenyekevu, akionyesha hisia za kweli. Mtu wa aina hii hukubalika na watu wengi, kwa kuwa hutoa muda wake kumsikiliza hata mtu asiye na busara au mropokaji.
Kama kiongozi alikuwa na tabia ya kujisifu, kukatisha mazungumzo wakati wa chini yake anapomweleza shida zake, kutokuwa msikivu, kuingilia mazungumzo yasiyomuhusu na mengune yanayofanana na hayo, basi ajue kuwa ameshajijengea mpaka kati yake na wa chini yake.
Ni kweli watu wa namna hii wanaudhi. “Watu ambao huzungumza mambo yao tu, na wale ambao hufikiria mambo yao tu, wanakuwa hawana maana, tena hawajaelimika,” Dk. Nich Muron, anasema.
Hivyo basi kama unapenda kuwa mzungumzaji mzuri uwe msikilizaji mzuri, unayevutia na unayevutiwa na mazungumzo ya wengine. Penda kuuliza maswali ambayo wengine watafurahia kuyajibu. Watie moyo kuzungumzia mambo yao na mafanikio yao.
Ni muhimu kukumbuka kwamba wakati unapoanza mazungumzo ni vyema kuwa msikilizaji mzuri, uwatie moyo wengine wazungumzie mafanikio yao kuliko kubaki unajisifu wewe mwenyewe.

TAFUTA NJIA SAHIHI YA KUTATUA MIGOGORO

JINSI jamii inavyokuwa na mfumo wa aina fulani ya maisha, kuna kila uwezekano wa kujenga mizizi inayoweza kusababisha mikwaruzano mbalimbali.
Ni vema kuelewa kuwa, kila jamii ina mfumo wake, hivyo wengine kuona kuwa, hawatendewi haki kama wenzao, hali ambayo itaweza kuchangia kutokuelewana au migongano.
Hali hiyo ya kutokuelewana hutokea hasa pale kiongozi wa nchi, wilaya, kijiji, mtaa, kwenye maeneo ya kazi au katika shughuli yoyote inayowashirikisha watu wengi, kiongozi huyo, anaposhindwa kuwawakilisha wote kwa usawa.
hali hiyo huwa hutokea kwa kiongozi yeyote ambaye hayuko makini katika utendaji wake, kwani kila mwanadamu ana mahitaji muhimu, hupenda kuwa salama na kutambulika. Sasa basi, ikiwa mahitaji yake hayafikii malengo iliyokusudia, husababisha maamuzi mabovu kutolewa, amani kutoweka na pengine kutokuelewana. Kuna vyanzo mbalimbali vinavyosababisha migongano katika jamii tunayoishi, ambavyo huweza kuwa vya kisiasa au kujamii. Mara nyingi tunaona kuwa kutokuelewana hutokea pale watu wanapokosa kuelewana katika jambo linalofanana. Endapo kunakosekana usawa katika mojawapo ya mambo, kwa mfano, utofauti wa kipato unaosababisha mifarakano kutokana na rasilimali za nchi kama vile ardhi na maji. Pia tunaona hali ya kutokuelewana huibuka pale watu wanapokuwa hawana furaha kutokana na watawala wanaowaongoza.
Mara nyingi tumeshuhudia kuwa migongano ya mara kwa mara hutokea wakati kikundi fulani kinapotaka kuwa huru kutokana na utawala uliopo madarakani, madai yao yanaposhindwa kuwasilishwa serikalini, serikali inapowadharau, kutowaheshimu wananchi wake au kuwapatia mahitaji yao ya muhimu.Migongano mingine yaweza kusababishwa na masuala ya dini na siasa. Wakati mwingine husababishwa na kikundi cha dini au siasa kilichohujumiwa. Hata hivyo, migongano yoyote inaibuka wakati watu wanapoumizwa.
Ingawa mara nyingi migongano hiyo huonekana ni kinyume, inaweza kufikiwa muafaka kama utatuzi utapatikana. Pia katika maeneo ya kazi mara nyingi kumekuwa na mifarakano ya mahitaji. Wafanyakazi wanapozidiana katika rasilimali na kutambuliwa kazini, migongano hutokea.
Kwa mfano, utakuta kuwa mkuu wa idara amekuwa akiwapendelea baadhi ya wafanyakazi kwa kuwapa motisha zaidi, hali inayowavunja moyo wafanyakazi wengine na kusababisha migongano. Pia ufahari au jinsi ya kuishi na watu maeneo ya kazi huleta kutokuelewana kama tu hutajishusha na kuishi maisha ya kawaida katika jamii inayokuzunguka. Kumbuka kila mtu ana tabia zake binafsi, kunakuwa na tofauti katika kuwafikia watu na matatizo yao. Kama kiongozi jihusishe nao kuelewa mitindo yao ya maisha na jifunze jinsi ya kuepuka migongano inayoweza kusababishwa na hali hiyo.Kwa mfano, inapotokea mfanyakazi mmoja akawa anafanya kazi katika mazingira bora na mazuri wakati mfanyakazi mwingine anafanya kazi katika mazingira yasiyoridhisha, na ilhali wapo katika kampuni au shirika moja, wafanyakazi hao wawili ni rahisi kukorofishana na kutokuelewana, kwa vile mmoja wao ataona kuwa hatendewi haki kwa hilo.
Matatizo mengine huchangiwa pale mtu asipoweza kufikia lengo alilokusudia kutokana na kutowezeshwa na mwajiri wake. Mfano katika suala la vitendea kazi, hali inayochangia kuchelewa kutekeleza majukumu yake.
Wakati mwingine mwajiri wako anaweza kukulaumu kutokana na kuchelewa kufanya kazi zako kwa ufanisi, kumbe ucheleweshwaji huo, huchangiwa na mwajiri huyo, kwa kutoona umuhimu wa kuweka vitendea kazi vya kutosha, hali inayoleta mvutano baina ya wafanyakazi wenyewe wakigombea vitendea kazi vichache vilivyopo.Na wakati mwingine idara mojawapo hupewa vitendea kazi na nyingine kukosa. Hiyo huleta hali ya mvutano na kutokuelewana katika maeneo ya kazi.
Shinikizo kutoka kwa viongozi wa kazi huchangia migongano. Kwa kuwa inaweza kutokea watu wawili au zaidi katika kitengo kimoja wanapokuwa na majukumu tofauti yanayotakiwa na bosi wao kwa wakati mmoja.Kwa mfano, kiongozi wa kazi anapotaka taarifa kamili ikamilike saa tisa alasiri - muda anaotakiwa mfanyakazi mwingine kukamilisha taarifa yake - ambapo wote kwa pamoja wanahitaji kutumia mashine moja kwa kuwa mashine nyingine ni mbovu, kipi ni suluhu? Matokeo yake mgongano unatokea.
Migongano mingine husababishwa na hali ya upendeleo kwa baadhi ya wafanyakazi. Utakuta bosi bila uficho wowote anaonyesha hali ya kuwathamini baadhi ya wafanyakazi na kuwadharau wengine. Ubaguzi katika maeneo ya kazi unasababisha minong’ono, tuhuma, na hatimaye migongano. Hivyo ili kuondoa hali hiyo, kiongozi mkuu wa kampuni anatakiwa kuwa thabiti katika kuhakikisha kampuni yake haiwi na mgawanyiko wowote na kuwafanya wafanyakazi wake wafanye kazi zao kama timu moja imara.Mingine husababishwa na sera mpya ambazo hazikutarajiwa. Popote sera za kampuni zinapobadilika, kutokuelewana kunatokea, wafanyakazi wanahitaji kufahamishwa sheria na sera za kampuni, pale mabadiliko mapya yanapotokea hawatakiwi kubahatisha. Vinginevyo vitu visivyotarajiwa vitatokea kama kupeana taarifa potofu.Njia mbalimbali zinazoweza kumsaidia mkurugenzi wa kampuni, mkuu wa idara au yeyote mwenye dhamana ya kuwaongoza wenzake, jinsi ya kutatua migogoro katika maeneo ya kazi, ni pale atakapotambua na kusuluhisha kwa umakini mkubwa.Kwani baadhi ya migogoro ikitatuliwa kwa umakini matokeo yake, hujenga mahusiano bora zaidi tofauti na ilivyokuwa mwanzo. Ukumbuke kuwa migongano katika sehemu za kazi ni sehemu ya maisha na haiepukiki, lakini ni jinsi gani tunaishughulikia inapotokea kama bosi bila kuathiri biashara na shughuli za uzalishaji katika kampuni yako. Kama viongozi kunakuwepo na majukumu imara ya kusuluhisha migogoro kwa haraka. Viongozi wa kisasa hawatakiwi kuwa ‘wanyapara’, bali wawe viongozi wanaodhihirisha fani zao, heshima na usawa katika mazingira yoyote na zaidi wanaposhughulikia migongano.
Kwanza yampasa kiongozi atathmini chanzo cha tatizo. Mafanikio ya kutatua tatizo la kutokuelewana kwa kikundi au jamii yanatokana na kuelewa chanzo halisi cha mgongano huo. Ni muhimu sana kuangalia mgogoro kutokana na mtazamo wa kila mmoja unaomhusu. Kutokuelewa chanzo cha tatizo kutafanya utatuaji wa tatizo hilo kuchukua muda mrefu kutambua aliyehusika na sababu za kuhusika kwake, na sababu zinazofanya tatizo hilo kuwa gumu. Kutegemeana na hali ya tatizo lilivyo, unaweza kuzungumza ‘chemba’ na kila mmoja aliyehusika katika mgongano huo au unaweza kuzungumza nao wote kama kikundi. Kusikiliza ni silaha mojawapo muhimu itakayoweza kukusaidia na kulielewa tatizo. Pia katika utatuaji wa tatizo unatakiwa kuwa makini na kujua kwa undani chanzo. Kuwa mkweli katika kulishughulikia tatizo. Kusikiliza kwa umakini kutakuwezesha kutoa mawazo yasiyopendelea upande wowote na kukuwezesha kutatua tatizo. Mruhusu kila mmoja kuwa mhusika katika hatua hizo na hakikisha uko wazi, mkweli na kutenda kwa usawa kama unavyozungumza na mtu binafsi. Ainisha njia bora zaidi ya kutatua matatizo. Mara unapokuwa na vielelezo vya uhakika mbele yako ni kazi yako kuongoza kikundi katika kufikia suluhu au kuainisha njia bora ya utatuzi. Mafanikio ya utatuzi wa matatizo mbalimbali mara zote inahusisha pande zote katika kutathmini tatizo na kipindi cha kutafuta utatuzi. Muulize mtu binafsi kama anaweza kutoa mawazo ya jinsi ya kutatua tatizo. Kama hawatakuwa na uwezo wa kufanya hivyo, unaweza kutumia njia bora ya kutatua tatizo. Malengo yako ni kuhakikisha unapatikana mwafaka wa usawa na utatuzi wa tatizo lililokuwepo ambalo litaleta utatuzi thabiti katika kampuni yako au kwa mtu binafsi.
Wakati mwingine linapotokea tatizo, chukua muda na kujiuliza maswali yafuatayo: Nini kinachosababisha migongano katika kampuni yako? Kwa nini wewe au mwingine anahitaji vitendea kazi? Je, mtindo wa mfanyakazi fulani ni tofauti na mtindo wako uliouzowea?0713 3314550733
lcyngowi@yahoo.com, www.lngowi.blogspot.com

ZAWADI SI LAZIMA IWE PESA

KARIBUNI wapenzi wasomaji katika safu hii ya Maisha Yetu kila Alhamisi. Leo tutakwenda kuangalia jinsi unavyoweza kuonyesha zawadi ya upendo kwa watu, hata kama huna fedha.
Kila mtu anapenda kupendwa, yakupasa kuwa na rafiki wa karibu atakayekushirikisha katika mambo mbalimbali unayokabiliana nayo.
Hivyo ni vema kuwa na rafiki mzuri na kuonyesha upendo wako kwake, kwa sababu wakati mwingine unajikuta hata familia yako inakuwa mbali nawe, hivyo kipindi hicho unakuwa unahitaji mtu wa kuongea naye.
Pia ni muhimu kuwa rafiki mzuri kwa sababu unajifunza ni jinsi gani ya kukutana na watu wapya na unajifunza kutokana na makosa yako.
Tafuta watu ambao unapenda wawe rafiki zako, kwa kujitambulisha, kumwacha mtu mwingine kukueleza juu ya mambo anayoyapendelea.
Mwonyeshe mtu huyo kuwa unamwamini, mwache ajue kuwa ni sawa kupendana, mwache ajue kuwa uko pale kwa ajili yake na atakuwa rafiki yako wa kudumu.
Mara zote mfanye atabasamu hata kama ana huzuni. Pia mwache ajue kuwa upo tayari kusikiliza chochote atakachosema.
Je? Unawezaje kuonyesha upendo bila kutumia fedha? Wakati mwingine tunajitahidi kwa bidii kutafuta zawadi ambayo ni sahihi tunayofikiria kuwa ina maana kwa yule unayempelekea.
Au, tunaishikilia zawadi hiyo, tukifikiria kama kuna sababu maalumu ya kutoa zawadi hiyo. Ninakutia moyo kutoa zawadi yako kwa uhuru na iwe ni mara kwa mara, kumbuka kuwa utoaji ni shughuli ambayo inamnufaisha mtu kila mara anapofanya hivyo.
Tuangalie zawadi 10 ambazo zinafaa kwa siku ya kawaida na maalumu. Pia, ni zawadi ambazo mtu yeyote anaweza kutoa kwa sababu halazimishwi ila ni kwa nia ya kuleta ushirikiano.
Zawadi ya kwanza ni muda. Kumbuka kuutoa muda wako na kushirikiana na wenzako ni moja ya zawadi kubwa unayoweza kuitoa.
Kama unatoa dakika 10 kwa kupiga hadithi na mtoto wako, kupata chakula cha mchana na rafiki yako au kutumia muda wa mchana kwa shughuli za nyumbani, shambani au nyinginezo, ukiwa na mume au mke wako, unakuwa unajitolea nafsi yako na kujenga uhusiano mzuri kwa muda huo.
Zawadi nyingine ni kukiri kwa uaminifu. Tumekuwa tukisikia watu wachache wakisema kuwa wamepokea shukrani nyingi au pongezi nyingi.
Wote tunajisikia vizuri wakati tunapata taarifa nzuri na shukrani kwa vile tulivyo au tunayoyafanya.
Anza kuzingatia kuimarika katika hilo na kutoa sifa nzuri kwa wengine na kujenga tabia ya kukiri jambo zuri linalofanywa na wengine kwa kile unachokiona.
Nyingine ni Msamaha. Hii ni zawadi nzuri mno yenye nguvu. Wakati tunasamehe wengine, tunaacha kuwaadhibu. Tunawaruhusu ili wajisikie hatia au kuona aibu ili waweze kugundua makosa yao.
Msamaha pia ni zawadi ya kutuweka huru kutoka kwenye uzoefu ulioupata wakati ulipoumizwa moyo wako au maumivu katika matukio yaliyopita.
Vile vile upendo. Wakati unapotaka kuuonyesha upendo wako kwa wengine, usiwahukumu wengine, na uwaone kama ni watu wa muhimu kwako, watakatifu na wa thamani, hiyo ni zawadi kubwa.
Tunaposhiriki kwa uwazi upendo wetu na wengine inasaidia kuponya majeraha, kujenga uhusiano mzuri na kumsaidia mtu katika kupitia changamoto za maisha pia kuwa na maisha mapya ya uhakika.
Usiugawe usikivu wako. Ingawa tunatoa muda wetu kwa ajili ya wengine, akili zetu zinaweza kuwa popote kutokana na uzoefu.
Jiruhusu nafsi yako kuwa kwa mtu mwingine, kupanga naye shughuli nyingine, mawazo au ajenda mpaka utakapofikia malengo yako uliyokusudia.
Kama utafanya hivyo, watu watakuona unastahili kupata asilimia zote, kwa usikivu wako na kwa upande mwingine inawezekana ukawa hujafikia kiwango hicho ila kutokana na hali hiyo uliyojiwekea kwa watu.
Heshima. Mara kwa mara tunakuwa na shughuli nyingi au tunajishughulisha sana katika maisha yetu ambayo yamekuwa na matukio mfululizo ya kuvutia ambapo tunasahau kama kuna watu wengine wanaotuzunguka. Iache nafsi yako ipumue na kutoa heshima kwa watu ambao unakutana nao kila siku.
Yapo mambo madogo madogo ambayo yanaweza kufungua milango kwa watu wengine kuthamini mambo ambayo unawafanyia kama kumpa lifti kwenye gari yako, kumbebea gazeti lake mpaka mlangoni pake au kusimamisha gari lako mbele ya mtu unayemfahamu na kumpa lifti kipindi cha msongamano wa abiria kituoni.
Mambo yote hayo yataonyesha hali ya kujali kwa mtu ingawa wakati mwingine mtu hawezi kuelewa wema wako na kukushukuru.
Shtukiza. Zawadi za aina hii zinamfanya mtu kuwa mbunifu wa hali ya juu. Je, unataka kumpa dada yako kadi ambayo inasema unampenda? Unajisikiaje unapomtumia mumeo maua?
Je, ni kweli utamshtusha? Au labda umechagua kujitolea kumpa mfanyakazi mwenzako kigari cha kusukuma cha watoto ili aweze kufurahia jioni anapokuwa matembezi na rafiki zake?
Zawadi kama hizo zinakuwa tukio kubwa kwa yule unayempelekea katika siku yake ya kawaida kwa sababu hakutarajia kufanyiwa jambo kama hilo kwa siku hiyo.
Shukrani ni zawadi pekee kwa yule unayempa, kwani inasababisha mtu huyo kujua kuwa umekuwa makini kwa lile alilokufanyia. Kama ukiri wa dhati, na neno jingine ni kusema asante, linaonekana ni jambo ambalo si la kawaida.
Endapo utachagua kusema au kuandika shukrani zako, hii ni zawadi ambayo inakwenda ndani ya moyo wa mpewa shukrani.
Tabasamu katika dunia ya kisasa, mara nyingi tunaona tabasamu chache na nyuso zenye furaha ya kweli. Kinyume cha mwelekeo kwa kujivisha tabasamu kama sehemu yako ya kila siku.
Tabasamu linajulisha moyo mkunjufu, mapokezi na urafiki. Pia inafanya kuonekana kwa urahisi kwa wote wenye nyuso za tabasamu. Iache zawadi hii ya tabasamu itoe ujumbe. Mfano “Nina furaha uko hapa”.
Maombi ya kimya kimya. Wote tunakuwa na maombi ya ziada na ya baraka katika maisha yetu. Hata kama hufahamu, mtu mwingine anaweza kukubariki wakati unampa zawadi ya maombi yenye nguvu.
Kama unajua au la, mazingira ya mtu au dini yake, unaweza kuuliza kwa msaada au usikivu. Maombi rahisi unaweza kumwombea kwa kutumia “Mungu/Allah, ninakuomba umbariki mtu huyu na ukutane na mahitaji yake yoyote ambayo anayo katika maisha yake, asante”.
Tukutane Alhamisi ijayo!
0713 3314550733 331455www.lngowi.blogspot.comlcyngowi@yahoo.com

USIIGE FANYA BIASHARA UNAYOIMUDU

HABARI wapenzi wasomaji wetu. Tunamshukuru Mungu kwa siku nyingine ya leo kutuamsha tukiwa wenye afya njema. Kama kawaida leo tutakwenda kuangalia Maisha Yetu ambayo huchapishwa kila Alhamisi.
Je, wajua kuwa bahati yako ipo mikononi mwako? Na kama utafanya bidii kwa kutumia mikono yako Mungu aliyokupa ni lazima utaiona.
Ninamaanisha kuwa mtu yeyote anayependa mafanikio na kuamua kupambana ili kufikia malengo yake, ni lazima atafanikiwa. Mafanikio hayo yatatokana na jitihada pamoja na bidii anayoionyesha mtu huyo.
Mtu yeyote ambaye hatataka kujikwamua kutoka katika hali ya dhiki aliyonayo, atabakia kuwa maskini na tegemezi. Utajiri wa watu wale wanaofanya jitihada na hata kufanikiwa hautamsaidia mtu ambaye hapendi kujishughulisha.
Kama hautapenda kujikwamua kutoka katika hali ya dhiki uliyonayo, kuendelea na ujinga wa kutotaka kujifunza ili kuondoka katika tabu yako, wenye akili watatumia juhudi na maarifa yao na kukuzidi katika hali ya kuwa na mafanikio.
Kama utakuwa mwenye upumbavu, busara za wengine hazitakuongoza. Kama utapoteza muda na pesa zako, uchumi wa wengine utafikia kikomo na kukufedhehesha.
Unapokuwa na mafanikio binafsi unakuwa na nguvu katika kufanikisha mambo mbalimbali unayotarajia, ndiyo maana kila mtu peke yake anafanya jitihada za kutaka kujikwamua kutoka kwenye umaskini.
Katika jamii tunayoishi, kila mmoja wetu ni mjasiriamali. Kila mmoja ni rais katika shirika lake. Hivyo atawajibika katika mafanikio na kushindwa ambako kutaweza kutokea katika ofisi yake.
Wewe na familia yako ni wadau katika shirika lako, na ni jukumu lako kuhakikisha kuwa thamani ya mahitaji ya biashara zako yanakuwepo kwa miaka yote.
Wakati unaendelea kuendesha biashara yako inayoendelea kukua, inawezekana kabisa kama utaamua kupunguza mahitaji makubwa uliyonayo, ili uweze kusimamia vizuri pesa ulizonazo, kusimamia vizuri suala la uzalishaji, mauzo na kufanya utafiti.
Pasipokuwa na mtaji wa kutosha, hakuna uzalishaji. Bila uzalishaji, biashara yako itakuwa haina kitu cha kuuza. Bila bidhaa, shirika lako litasimamisha uzalishaji. Na bila utafiti, washirika wako hawatakuwa na imani ya kuendelea kuwepo katika kampuni hiyo kwa siku zijazo.
Suala la kutumia akili yako ya kuzaliwa ni la muhimu sana. Utafiti unaonyesha kuwa mara nyingi mtu anayefanikiwa ni yule ambaye anatumia akili yake katika kumpatia faida.
Mfano, mtu alikopa pesa benki na kuweka dhamana kwa kutumia samani zake za nyumbani. Na alitumia akili yake kuwaza biashara atakayoifanya kutokana na mkopo ule. Alianzisha biashara ya kuuza nafaka kwa jumla na sasa hivi mtu huyo ana malori ambayo yanapeleka mizigo nje ya nchi.
Kufanikiwa kwa mtu huyo kusikufanye na wewe ukaanzisha biashara kama yake, kwani unaweza kukwama. Kinachotakiwa ni kuchekecha akili yako na kuamua kufanya biashara ambayo utaimudu.
Mafanikio katika biashara yako ya kifedha yanakuja kutokana na uongozi mzuri katika biashara yako unayoisimamia. Hakuna milango iliyo wazi katika suala la mafanikio, ni lazima ufanye utafiti, uweke malengo na kutimiza ndoto yako uliyoipanga. Japo kuna misuko suko mbalimbali katika kufikia mafanikio hayo.
Ukosefu wa nafasi isiwe sababu ya kutoa udhuru katika mipango yako inayoshindikana kutokana na kuwepo kwa vikwazo mbalimbali unavyoviruhusu wewe mwenyewe.
Kila maisha unayoyaishi yana nafasi nzuri ya mafanikio. George anasema tunaishi katika dunia ambayo wakati wote ina uwezekano wa kuwa na utajiri mwingi.
Maisha ni somo, na kila somo, linapokujia ni nafasi kwako ya kujifunza. Kila biashara unayoipitia ni nafasi kwako ya kujifunza. Unapowaza juu ya watu unaowafahamu waliofanikiwa, hiyo ni nafasi nzuri kwako ya kujifunza kutoka kwao.
Uwepo wako ni upendeleo wa pekee wa kukufanya uongeze bidii katika mipango yako, na pale unapopata bahati hiyo, nafasi yako ya mafanikio inakuja kwa haraka.
Watu wenye mafanikio, wavumbuzi na waasisi ni wale wenye ujasiri na wanaweza kusema, “Ndiyo, ninaweza! Njia ipo pale na nitaitafuta”. Wote hao ambao binafsi wameyakubali maisha na changamoto zake na kuzifanyia kazi changamoto hizo katika mafanikio.
Acha kulalamika kutokana na bahati mbaya uliyokumbana nayo au jambo baya lililokupata, amua kuwa na nafasi ya kubadilika.
Kuna kitu ambacho unaweza kukifanya vyema zaidi ya mtu mwingine. Ni nini hicho? Tafuta mpaka pale utakapopata eneo lako ambalo utafanya vizuri na kuzidi wengine. Halafu upange mipango yako ukinuia kuwa utafanikiwa.
Kamwe usipende kuwa mtu wa kushindwa ila wewe ndiye unayeweza kupata mafanikio. Inawezekana kabisa mtu aliyezaliwa katika familia maskini, akakua katika hali ya umaskini, akasoma kwa shida na matatizo mengi, hatimaye mtu huyo akaja kuwa tajiri mkubwa.
Mifano mingi tunayokutana nayo ni ya watu walioishi katika hali duni, kutokana na hali ile wakaamua kubadilika na kuwa watu tofauti katika dunia tunayoiishi na wengi wao wamefanikiwa, ni matajiri wanaishi maisha ya raha.
Watu hao mara zote wamekuwa wakiwausia watoto wao kuishi maisha ya kujituma na kufanya bidii ili watakapokua waweze kuwa na mafanikio, pia wasitegemee utajiri wa wazazi wao.
Kamwe usikate tamaa, wala kuvunjika moyo. Utavuna kesho kile ulichokipanda leo. Kila siku unatakiwa kujiuliza: “Siku hii ya leo kwangu ina maana gani?”
Utakapofanya maamuzi juu ya siku hiyo, utakuwa tayari kwa kutumia uzoefu ulionao wa kufanya jambo lile ambalo umelipanga.
Umepewa saa 24 kwa siku, siku saba kwa wiki, unatakiwa kuwajibika katika siku hizo. Uko huru kufanya kazi katika muda uliojipangia kutokana na uchaguzi wako.
Uamuzi wa mafanikio upo kwako, hivyo usivunjike moyo katika hatua unayoichukua ya kufanikisha malengo yako.
Tukutane alhamisi ijayo!
www.lngowi.blogspot.com, lcyngowi@yahoo.com, 0733 331455

KUJIAMINI KUNASTAWISHA MAISHA YAKO

UTAKUWA na tofauti gani katika maisha yako endapo utakuwa mtu wa kujiamini? Ni nini zaidi utakachokipata? Hilo ni swali ambalo sote tunaweza kujiuliza.
Ni ukweli usiopingika, kwamba hali ya kujiamini inasitawisha maisha yako. Hivyo unapokuwa na afya nzuri inakufanya ufikie malengo yako kwa urahisi zaidi.
Unapojiamini katika maisha yako na shughuli zako za kila siku, utaweza kuwasaidia na wengine ambao unawasiliana nao katika maeneo mbalimbali iwe ni nyumbani au kazini. Vile vile endapo unakutana na mambo ya kustaajabisha, ya kushtusha au ya mshangao huna haja ya kuogopa, kwa kuwa tayari umeshajijengea hali ya kujiamini, utaikabili hali hiyo kwa urahisi.
Ni vizuri kujijengea hali ya kujiamini katika maisha yako kwani watu wote walio na hali hiyo wamekuwa na viwango vya tofauti ambavyo kila moja anavifurahia. Kumbuka kuwa hali ya kujiamini na kuwa jasiri, ni muhimu sana katika kila hatua ya maisha yetu, hivyo watu wengi wanajitahidi kuitafuta.
Kwa mtazamo mwingine watu waliokosa hali ya kujiamini inakuwa ni vigumu kwao kupata mafanikio. Kwa upande mwingine, unaweza kushawishika na mtu anayezungumza kwa ufasaha, anayejibu maswali yake kwa kujiamini na anayekuwa tayari kukubali kwamba jambo fulani halifahamu.
Mtu huyo ni rahisi kujifunza jambo jipya ambalo litamwongezea mafanikio zaidi katika maisha yake kwa kuwa yuko tayari. Watu wanaojiamini huambukiza hali hiyo kwa wengine. Hadhira anayokutana nayo, wanachama wenzake, bosi wake, wateja wake na rafiki zake.
Kupata ujasiri wa wengine ni njia mojawapo ambayo mtu anayejiamini huitafuta kwa ajili ya kupata mafanikio zaidi. Habari njema ni kwamba hali hiyo unaweza kujifunza na kuijenga katika maisha yako.
Na endapo unafanya kazi kwa kujiamini au kuwajengea ujasiri watu wanaokuzunguka, unakuwa umefanya jambo jema. Mambo mengine yote yanakuwa sawa kutokana na kujiamini kwako, na yeyote anayejiamini huwa na mafanikio katika maisha yake tofauti na yule mtu ambaye hajiamini. Kiwango chako cha kujiamini kinaweza kuonekana katika njia nyingi. Mfano kutokana na tabia yako, lugha yako, jinsi unavyoongea, kile unachozungumza na mambo mengine mbalimbali. Unawezaje kujijengea hali ya kujiamini?
Ni kwa kufanya kazi ya kutoa ushauri katika mazingira ya kushughulika na watu wa aina mbalimbali, wenye tabia mbalimbali waliovunjika moyo na wanaohitaji msaada zaidi wa kukabiliana na ugumu wa maisha. Unapofanya kazi hiyo ya kutoa ushauri unatakiwa kujua njia sahihi ya kukabiliana na mtu mwenye msongo wa mawazo na kujua ni jinsi gani utaanza mazungumzo naye kutokana na hali aliyokuwa nayo.
“Wakati nilipokuwa naanza kuangalia jinsi ya kuwa na hali yangu mwenyewe ya kujiamini, nilijaribu kuangalia maeneo mbalimbali yatakayonifanya nijijengee uwezo wa kujiamini. Japo kwa mara ya kwanza ilikuwa ni vigumu, lakini ilichukua muda mrefu na niliweza kufanikiwa,” alisema John Robert.
Jambo jingine ambalo linaweza kukusaidia ni kupunguza kumbukumbu za maumivu yatokanayo na mambo yaliyopita katika maisha yako. Hivyo, kama unataka kusonga mbele usikumbuke mambo yaliyopita ambayo yatakurudisha nyuma. Japo ni vizuri kujifunza kutokana na mambo yaliyopita lakini huhitaji kuendelea kuwa na kumbukumbu zinazoumiza.
Ni vyema kama hautafikiria yaliyopita. Hivyo, unaweza ukawa umejifunza wewe mwenyewe mbinu za kujiamini, unapoamua kubadilika na kuwa jasiri, ni kwamba pale unapoanza, utaendelea kukua na kukua.
Unaweza kuendelea kuhisi kwamba pengine unaweza kujiamini zaidi, maisha yanaweza kuwa mazuri kutokana na hali hiyo. Hivyo, mwishoni unafikia ndoto zako kama vile kupata kazi kubwa, kuwa na mahusiano mazuri, kununua nyumba na mambo mengineyo. Unajisikia vizuri wewe mwenyewe na kuwa na furaha kutokana na kile unachokipata. Zipo njia mbalimbali zinazoweza kukufanya ujiamini. Baadhi ya njia hizo zinafanikiwa na nyingine zinashindwa kutokana na mtu mwenyewe.
Wakati mwingine unaweza kujisikia kuwa unahitaji msaada, mtu wa kuongea naye, au kutafuta njia rahisi na kutoa ushauri bila kulipa pesa nyingi. Ni njia ya muda mrefu kuweza kuwa na hali hiyo ya kujiamini lakini inaweza kuwa ni safari nzuri kwa sababu inabadilisha maisha yako. Pia inashangaza kwa sababu unaweza kunufaika zaidi katika kila hatua unavyoongea.
Je, uko tayari kujijengea hali ya kujiamini? Kwanza inakupasa kufanya shughuli mbalimbali ambazo zitakujengea uwezo huo.
“Fanya shughuli za kukujengea ujasiri kila siku na kuwa na mawazo yanayoipanua akili yako,” anasema Mike Bonny. Pia unaweza kujiuliza ni kwa kiasi gani una ujasiri? Hali hiyo inaweza kuwepo kutokana na afya katika akili yako. Kwa mfano, kama unajisikia uchovu muda wote, itakuwa ngumu kuwa jasiri.
Ujasiri katika kufikiri ni jinsi gani mawazo yako yanaweza kuyabadilisha maisha yako. Unapokuwa jasiri katika kufikiri ni sababu ya kuyabadili mawazo tunayoyawaza. Vilevile, ujasiri katika mahusiano mara nyingine unaweza kuona ni kitu cha kukupa changamoto.
Sasa basi, unaweza ukaangalia ulinganisho wa tabia ya kujiamini na ile ya kutojiamini. Ni hatua gani unazoweza kuzichukua kwako binafsi na kwa watu wanaokuzunguka? Unapokuwa mtu wa kujiamini unafanya kile unachofikiri ni sawa, ingawa wengine watakukosoa.
Pia utakuwa tayari kwa lolote ili uweze kupata vitu vizuri. Vile vile unakuwa ni mtu wa kukubali makosa yako na kujifunza. Mtu asiyejiamini anakuwa ameegemea upande wa wengine wanavyofikiri. Unabakia kukaa sehemu moja ukiogopa kushindwa na kukwepa kubahatisha au kuthubutu kufanya jambo fulani. Anakuwa mgumu kukubali kosa.
Kama ulivyoona katika mifano hiyo hapo, hali ya kutojiamini inakuletea uharibifu, bali inakujenga. Jifunze kujiamini, kuwa jasiri katika kila jambo unalolifanya, usitetereke utafanikiwa.
www.lngowi.blogspot.comlcyngowi@yahoo.com0713 331455 au 0733 331455

Twitter Facebook