Friday, December 19, 2008

JINSI UNAVYOWEZA KUJENGA URAFIKI

KILA mmoja hapa duniani ana jukumu la kuwa kiongozi mahali popote alipo - iwe nyumbani, kazini ama shuleni - ili kuwawezesha wengine kufanya kazi kwa kufuata kanuni na sheria zilizopo.
Mfano wewe ni kiongozi katika kampuni, shirika au ofisi yoyote, ni jukumu lako kuwaangalia wafanyakazi wenzako kama wanafanyakazi zao kwa kufuata sheria na taratibu za kazi zilizopo.
Kama utashindwa kuwasimamia vizuri, ikatokea mmoja wao akapatwa na madhara, jukumu hilo utalibeba wewe kama kiongozi wao. Hivyo basi, kama wewe ni kiongozi katika kampuni ya uhandisi ni vyema kuhakikisha kuwa wafanyakazi unaowasimamia wanatimiza wajibu wao, kwa kuvaa kofia za kufanyia kazi wakati wote wawapo kazini.
Inawezekana wakati mwingine wafanyakazi hao wakafanya mazoea na kuacha kuvaa kofia hizo au wakadharau kufuata sheria unazowaelekeza kama kiongozi wao, na kuamua kuzivunja unapoondoka katika eneo hilo la kazi na kufanya vile wapendavyo.
Kama utagundua kwamba maelekezo unayoyatoa kwa wafanyakazi hao hayatekelezeki ni vyema kujaribu njia nyingine ya kuwafikishia ujumbe huo, ili waweze kufanyakazi zao kwa kufuata sheria zilizopo, kuepuka na madhara yanayoweza kuwapata.
Ikitokea utawakuta wafanyakazi hawajavaa kofia wakiwa kazini, ni vema kutumia mbinu na kuanza kuwauliza, wanajisikiaje pale wanapovaa kofia hizo, je, wanakuwa huru au haziwakai vizuri ili uweze kujua tatizo lipo wapi.
Unapopata majibu kutoka kwao, ni vema kuwakumbusha kwa upole, umuhimu wa kofia hizo za kazi wanazopaswa kuvaa, kwamba zimetengenezwa kwa ajili yao wanapokuwa kazini tu, ili kuwakinga na hatari, endapo vitu vizito vitadondoka kwa bahati mbaya wawapo kazini.
Utakapofanya hivyo itakuwa rahisi kwa wafanyakazi hao kuelewa umuhimu huo na kuutekeleza, tofauti kama ungetumia sauti ya ukali na kuamrisha. Huo ni mfano mojawapo wa kujishughulisha na watu wanaokuzunguka katika mazingira mbalimbali. Unapokuwa mwenye busara na hekima katika kuzungumza, unakubalika na wale wanaokuzunguka kinyume cha hapo hata upige mbiu hautasikilizwa.
Ni vema kukumbuka kuwa, unapojishughulisha na watu, unajishughulisha na viumbe vyenye hisia, hivyo uamuzi mkali utasababisha hisia mbalimbali kwao.
Kiongozi asiye na busara anaweza kutumia muda wake mwingi kukosoa, kulaumu na kulalamika. Hivyo ndivyo wafanyavyo viongozi wote wasiotumia nafasi yao vizuri. Lakini ni vyema kiongozi akawa na tabia ya kujitawala na kuwa mwelewa, mwenye busara na kusamehe.
Kumbuka kuwa kuna siri kubwa ya kushughulika na watu. Pia kuna njia moja ya kumfanya yeyote kufanya chochote anachotaka, itategemea ni jinsi gani utakavyozungumza naye.
Unaweza kumlazimisha mtoto wako afanye kile unachotaka kwa kumchapa au kumtishia. Unaweza ukawalazimisha wafanyakazi wako kukupa ushirikiano, pale unapowatishia kuwafukuza. Lakini kumbuka hiyo siyo njia nzuri ya kujishughulisha na watu wanaokuzunguka.
Kuna msemo unaosema kama hutakuwa na uso wa tabasamu, huwezi kuuza duka. Tabasamu lako ndio mwongozo wa kufanya mambo mema. Pia inatoa mwanga wa maisha kwa wote wanaokutazama.
Hivyo endapo utakutana na watu wenye matatizo mbalimbali yanayowafanya wachukie wakati wote au kukunja nyuso zao kwa kukosa furaha, kumbuka tabasamu yako pekee ndiyo itakuwa dawa kwa wote walioumizwa.
Kwani watu hao hufikia hatua ya kukata tamaa baada ya kupata mashinikizo mbalimbali kutoka kwa mabosi, wateja, walimu, wazazi au watoto wao, tabasamu pekee ndilo linaloweza kuwasaidia kujua kwamba huo si mwisho wa maisha bali kuna furaha katika dunia.
Katika maisha tunayoishi ni vema ukajifunza njia mbalimbali za kuishi na watu ambazo zitakujengea heshima popote utakapokuwa. Njia hizo ni kupenda kujua majina ya kila unayekutana naye, kujitahidi kumwita kwa jina lake kila unapomwona.
Utakapofanya hivyo utajijengea heshima kwa jamii inayokuzunguka iwe ni nyumbani, shuleni na hata ofisini. Baadhi ya watu wamekuwa na tabia nzuri ambazo hupendwa na jamii. Tabia hizi ni pamoja na kutumia muda wao na kumsikiliza kila anayezungumza naye bila kumpinga.
Hali hii humfanya kupata njia sahihi ya kumsaidia mtu huyo endapo anahitaji msaada, ushauri au mara nyingine kumwelekeza. Baada ya kutumia muda wake kusikiliza kwa makini, huzungumza kwa sauti ya upole na unyenyekevu, akionyesha hisia za kweli. Mtu wa aina hii hukubalika na watu wengi, kwa kuwa hutoa muda wake kumsikiliza hata mtu asiye na busara au mropokaji.
Kama kiongozi alikuwa na tabia ya kujisifu, kukatisha mazungumzo wakati wa chini yake anapomweleza shida zake, kutokuwa msikivu, kuingilia mazungumzo yasiyomuhusu na mengune yanayofanana na hayo, basi ajue kuwa ameshajijengea mpaka kati yake na wa chini yake.
Ni kweli watu wa namna hii wanaudhi. “Watu ambao huzungumza mambo yao tu, na wale ambao hufikiria mambo yao tu, wanakuwa hawana maana, tena hawajaelimika,” Dk. Nich Muron, anasema.
Hivyo basi kama unapenda kuwa mzungumzaji mzuri uwe msikilizaji mzuri, unayevutia na unayevutiwa na mazungumzo ya wengine. Penda kuuliza maswali ambayo wengine watafurahia kuyajibu. Watie moyo kuzungumzia mambo yao na mafanikio yao.
Ni muhimu kukumbuka kwamba wakati unapoanza mazungumzo ni vyema kuwa msikilizaji mzuri, uwatie moyo wengine wazungumzie mafanikio yao kuliko kubaki unajisifu wewe mwenyewe.

0 Maoni:

Twitter Facebook