Friday, December 19, 2008

TAFUTA NJIA SAHIHI YA KUTATUA MIGOGORO

JINSI jamii inavyokuwa na mfumo wa aina fulani ya maisha, kuna kila uwezekano wa kujenga mizizi inayoweza kusababisha mikwaruzano mbalimbali.
Ni vema kuelewa kuwa, kila jamii ina mfumo wake, hivyo wengine kuona kuwa, hawatendewi haki kama wenzao, hali ambayo itaweza kuchangia kutokuelewana au migongano.
Hali hiyo ya kutokuelewana hutokea hasa pale kiongozi wa nchi, wilaya, kijiji, mtaa, kwenye maeneo ya kazi au katika shughuli yoyote inayowashirikisha watu wengi, kiongozi huyo, anaposhindwa kuwawakilisha wote kwa usawa.
hali hiyo huwa hutokea kwa kiongozi yeyote ambaye hayuko makini katika utendaji wake, kwani kila mwanadamu ana mahitaji muhimu, hupenda kuwa salama na kutambulika. Sasa basi, ikiwa mahitaji yake hayafikii malengo iliyokusudia, husababisha maamuzi mabovu kutolewa, amani kutoweka na pengine kutokuelewana. Kuna vyanzo mbalimbali vinavyosababisha migongano katika jamii tunayoishi, ambavyo huweza kuwa vya kisiasa au kujamii. Mara nyingi tunaona kuwa kutokuelewana hutokea pale watu wanapokosa kuelewana katika jambo linalofanana. Endapo kunakosekana usawa katika mojawapo ya mambo, kwa mfano, utofauti wa kipato unaosababisha mifarakano kutokana na rasilimali za nchi kama vile ardhi na maji. Pia tunaona hali ya kutokuelewana huibuka pale watu wanapokuwa hawana furaha kutokana na watawala wanaowaongoza.
Mara nyingi tumeshuhudia kuwa migongano ya mara kwa mara hutokea wakati kikundi fulani kinapotaka kuwa huru kutokana na utawala uliopo madarakani, madai yao yanaposhindwa kuwasilishwa serikalini, serikali inapowadharau, kutowaheshimu wananchi wake au kuwapatia mahitaji yao ya muhimu.Migongano mingine yaweza kusababishwa na masuala ya dini na siasa. Wakati mwingine husababishwa na kikundi cha dini au siasa kilichohujumiwa. Hata hivyo, migongano yoyote inaibuka wakati watu wanapoumizwa.
Ingawa mara nyingi migongano hiyo huonekana ni kinyume, inaweza kufikiwa muafaka kama utatuzi utapatikana. Pia katika maeneo ya kazi mara nyingi kumekuwa na mifarakano ya mahitaji. Wafanyakazi wanapozidiana katika rasilimali na kutambuliwa kazini, migongano hutokea.
Kwa mfano, utakuta kuwa mkuu wa idara amekuwa akiwapendelea baadhi ya wafanyakazi kwa kuwapa motisha zaidi, hali inayowavunja moyo wafanyakazi wengine na kusababisha migongano. Pia ufahari au jinsi ya kuishi na watu maeneo ya kazi huleta kutokuelewana kama tu hutajishusha na kuishi maisha ya kawaida katika jamii inayokuzunguka. Kumbuka kila mtu ana tabia zake binafsi, kunakuwa na tofauti katika kuwafikia watu na matatizo yao. Kama kiongozi jihusishe nao kuelewa mitindo yao ya maisha na jifunze jinsi ya kuepuka migongano inayoweza kusababishwa na hali hiyo.Kwa mfano, inapotokea mfanyakazi mmoja akawa anafanya kazi katika mazingira bora na mazuri wakati mfanyakazi mwingine anafanya kazi katika mazingira yasiyoridhisha, na ilhali wapo katika kampuni au shirika moja, wafanyakazi hao wawili ni rahisi kukorofishana na kutokuelewana, kwa vile mmoja wao ataona kuwa hatendewi haki kwa hilo.
Matatizo mengine huchangiwa pale mtu asipoweza kufikia lengo alilokusudia kutokana na kutowezeshwa na mwajiri wake. Mfano katika suala la vitendea kazi, hali inayochangia kuchelewa kutekeleza majukumu yake.
Wakati mwingine mwajiri wako anaweza kukulaumu kutokana na kuchelewa kufanya kazi zako kwa ufanisi, kumbe ucheleweshwaji huo, huchangiwa na mwajiri huyo, kwa kutoona umuhimu wa kuweka vitendea kazi vya kutosha, hali inayoleta mvutano baina ya wafanyakazi wenyewe wakigombea vitendea kazi vichache vilivyopo.Na wakati mwingine idara mojawapo hupewa vitendea kazi na nyingine kukosa. Hiyo huleta hali ya mvutano na kutokuelewana katika maeneo ya kazi.
Shinikizo kutoka kwa viongozi wa kazi huchangia migongano. Kwa kuwa inaweza kutokea watu wawili au zaidi katika kitengo kimoja wanapokuwa na majukumu tofauti yanayotakiwa na bosi wao kwa wakati mmoja.Kwa mfano, kiongozi wa kazi anapotaka taarifa kamili ikamilike saa tisa alasiri - muda anaotakiwa mfanyakazi mwingine kukamilisha taarifa yake - ambapo wote kwa pamoja wanahitaji kutumia mashine moja kwa kuwa mashine nyingine ni mbovu, kipi ni suluhu? Matokeo yake mgongano unatokea.
Migongano mingine husababishwa na hali ya upendeleo kwa baadhi ya wafanyakazi. Utakuta bosi bila uficho wowote anaonyesha hali ya kuwathamini baadhi ya wafanyakazi na kuwadharau wengine. Ubaguzi katika maeneo ya kazi unasababisha minong’ono, tuhuma, na hatimaye migongano. Hivyo ili kuondoa hali hiyo, kiongozi mkuu wa kampuni anatakiwa kuwa thabiti katika kuhakikisha kampuni yake haiwi na mgawanyiko wowote na kuwafanya wafanyakazi wake wafanye kazi zao kama timu moja imara.Mingine husababishwa na sera mpya ambazo hazikutarajiwa. Popote sera za kampuni zinapobadilika, kutokuelewana kunatokea, wafanyakazi wanahitaji kufahamishwa sheria na sera za kampuni, pale mabadiliko mapya yanapotokea hawatakiwi kubahatisha. Vinginevyo vitu visivyotarajiwa vitatokea kama kupeana taarifa potofu.Njia mbalimbali zinazoweza kumsaidia mkurugenzi wa kampuni, mkuu wa idara au yeyote mwenye dhamana ya kuwaongoza wenzake, jinsi ya kutatua migogoro katika maeneo ya kazi, ni pale atakapotambua na kusuluhisha kwa umakini mkubwa.Kwani baadhi ya migogoro ikitatuliwa kwa umakini matokeo yake, hujenga mahusiano bora zaidi tofauti na ilivyokuwa mwanzo. Ukumbuke kuwa migongano katika sehemu za kazi ni sehemu ya maisha na haiepukiki, lakini ni jinsi gani tunaishughulikia inapotokea kama bosi bila kuathiri biashara na shughuli za uzalishaji katika kampuni yako. Kama viongozi kunakuwepo na majukumu imara ya kusuluhisha migogoro kwa haraka. Viongozi wa kisasa hawatakiwi kuwa ‘wanyapara’, bali wawe viongozi wanaodhihirisha fani zao, heshima na usawa katika mazingira yoyote na zaidi wanaposhughulikia migongano.
Kwanza yampasa kiongozi atathmini chanzo cha tatizo. Mafanikio ya kutatua tatizo la kutokuelewana kwa kikundi au jamii yanatokana na kuelewa chanzo halisi cha mgongano huo. Ni muhimu sana kuangalia mgogoro kutokana na mtazamo wa kila mmoja unaomhusu. Kutokuelewa chanzo cha tatizo kutafanya utatuaji wa tatizo hilo kuchukua muda mrefu kutambua aliyehusika na sababu za kuhusika kwake, na sababu zinazofanya tatizo hilo kuwa gumu. Kutegemeana na hali ya tatizo lilivyo, unaweza kuzungumza ‘chemba’ na kila mmoja aliyehusika katika mgongano huo au unaweza kuzungumza nao wote kama kikundi. Kusikiliza ni silaha mojawapo muhimu itakayoweza kukusaidia na kulielewa tatizo. Pia katika utatuaji wa tatizo unatakiwa kuwa makini na kujua kwa undani chanzo. Kuwa mkweli katika kulishughulikia tatizo. Kusikiliza kwa umakini kutakuwezesha kutoa mawazo yasiyopendelea upande wowote na kukuwezesha kutatua tatizo. Mruhusu kila mmoja kuwa mhusika katika hatua hizo na hakikisha uko wazi, mkweli na kutenda kwa usawa kama unavyozungumza na mtu binafsi. Ainisha njia bora zaidi ya kutatua matatizo. Mara unapokuwa na vielelezo vya uhakika mbele yako ni kazi yako kuongoza kikundi katika kufikia suluhu au kuainisha njia bora ya utatuzi. Mafanikio ya utatuzi wa matatizo mbalimbali mara zote inahusisha pande zote katika kutathmini tatizo na kipindi cha kutafuta utatuzi. Muulize mtu binafsi kama anaweza kutoa mawazo ya jinsi ya kutatua tatizo. Kama hawatakuwa na uwezo wa kufanya hivyo, unaweza kutumia njia bora ya kutatua tatizo. Malengo yako ni kuhakikisha unapatikana mwafaka wa usawa na utatuzi wa tatizo lililokuwepo ambalo litaleta utatuzi thabiti katika kampuni yako au kwa mtu binafsi.
Wakati mwingine linapotokea tatizo, chukua muda na kujiuliza maswali yafuatayo: Nini kinachosababisha migongano katika kampuni yako? Kwa nini wewe au mwingine anahitaji vitendea kazi? Je, mtindo wa mfanyakazi fulani ni tofauti na mtindo wako uliouzowea?0713 3314550733
lcyngowi@yahoo.com, www.lngowi.blogspot.com

0 Maoni:

Twitter Facebook