Friday, December 19, 2008

JARIBU KUWA JASIRI KUKIRI KOSA

KARIBUNI wapenzi wasomaji katika safu hii ya Maisha Yetu inayokujia kila Alhamisi. Safu hii imekuwa ikielimisha, ikikosoa na hata kutoa muongozo wa maisha ya kila siku.
Leo katika safu hii tutaangalia jinsi unavyoweza kujiepusha usiwe na maadui katika maeneo mbalimbali uliyopo. Kuna wakati unaweza kuona umeelemewa na mawazo pasipo kukumbana na tatizo lolote, lakini mtu anapokuambia umekosea, hilo linaweza kukufanya uwe na huzuni katika moyo wako.
Hivyo basi, unaweza kumueleza mtu kwamba amekosea kwa kumwangalia, kumwambia au kutumia ishara kama njia ya kumshawishi mtu akuelewe kama vile unavyoweza kuzungumza kwa maneno.
Elewa kuwa utapomwambia mtu ana makosa, unafikiri utamfanya akuamini? Hapana. Hiyo si njia sahihi, kwani unaweza kulitatua tatizo hilo kwa busara, maarifa, hekima na staha. Ukitumia njia za busara itamuwezesha yule mwenye tatizo kujutia makosa yake, japo haitamfanya kubadili mtazamo wake.
Unapojishughulisha na mtu yeyote huku ukitaka kufanikiwa, kamwe usianze kwa kueleza: “Ninakwenda kuhakikisha jambo hili na hili kwako” kufanya hivyo si jambo zuri, hiyo ni sawa kusema “Mimi ni bora kuliko wewe”.
Badala ya kutumia njia hiyo ni vyema kumueleza mtu unayetaka kumchunguza, mambo ambayo unafikiri yatabadili fikra zake, na kuweza kumsaidia.
Hiyo ni changamoto kwa kila mmoja kwani inaweza kuleta kutokuelewana na kumfanya yule uliyekusudia kumuonyesha kuwa wewe ni bora kuliko yeye, kupambana nawe kabla hujaamua kuanza. Kwa mtazamo huo, ni vigumu kubadili fikra za watu, ambao unadhani kuwa, wanaenda kinyume.
Hivyo ni busara unapotaka kwenda kuthibitisha jambo lolote, usilifanye kwa uwazi kila mmoja akatambua unalotaka kulifanya. “Fanya kwa werevu, ustadi, asiwepo yeyote atakayeweza kuhisi kwamba kuna jambo unalifanya”. Ili usije kujijengea uadui usiokuwa na lazima.
Mtu mmoja aliweza kumwambia mtoto wake kwamba awe na busara kuliko watu wengine kama anaweza, lakini asiwe mwepesi wa kuzungumza na kuwaeleza udhaifu wao ulipo.
“Ni kweli, ni vyema ukaiambia nafsi yako kuwa huwezi kuwa bora kuliko mwingine, kwa hiyo inakupasa kutokuwahukumu”.
Endapo mtu atakwambia maneno ambayo unafikiri si sahihi, nawe unajua hivyo, si vema kusema “Vizuri, sasa, tazama. Ninafikiri kuwa lakini ninaweza kuwa nimekosea mara kwa mara na kama nimekosea, nataka kujiweka sawa, tuweze kuujua ukweli”.
Huo ni muujiza, unasema “ninaweza kuwa nimekosea, imenitokea mara kwa mara, acha tujue ukweli,”. Hakuna mtu yeyote chini ya mbingu au chini ya ardhi atakayekubaliana na maneno hayo.
Kuna baadhi ya watu wamekuwa wakitumia maneno hayo pale wanapokumbana na misukosuko ya wateja au wafanyakazi wenzao. Kutokana na misukosuko hiyo ya mara kwa mara hupatwa na hasira anapokuwa na wakati mgumu wa kushughulika na matatizo ya wateja wake, hali inayomsababishia hasira, kukosana na watu na kutokukubalika.
Lakini unapokuwa jasiri na kukabiliana na hali hiyo kwa kuwaambia watu unaoshughulika nao, kuwa upo tayari kurekebisha upungufu unaoonekana kwao, na kusema kuwa uko tayari kushughulikia matatizo hayo, utakuwa na imani kwa wateja hao.
Unapokuwa jasiri wa namna hiyo inapunguza hasira kwa wale unaowatumikia na wataondoa hisia walizokuwa nazo juu yako na kampuni yako, ni vyema kuwa makini unaposhughulikia jambo lolote.
Ni vyema kuonyesha heshima kwa wateja, wafanyakazi wote bila kubagua, kwa kuwashauri na kuwajali itasaidia kuendelea kuwa shujaa katika ushindani wa biashara uliyonayo.
Kamwe hutaingia matatizoni pale utakapokubali kuwa umekosea, kwani itakuondolea maswali, kukupa moyo na itakufanya kuwa wazi pamoja na kupata uelewa mkubwa kuliko ulivyokuwa awali.
Unapokuwa umekosea ni vyema kukiri makosa hayo na endapo utakiri kwa unyenyekevu, utawafanya na wengine wajivune kupitia wewe.

0 Maoni:

Twitter Facebook