Friday, December 19, 2008

KAMA UMEKOSEA KUBALI KOSA

KARIBUNI wapenzi wasomaji katika safu hii. Tunamshukuru Mungu kwa kutufikisha tena Alhamisi ya kwanza ya Desemba. Nafikiri kupitia safu hii umepata elimu na maarifa mbalimbali. Leo, tutaangalia jinsi inavyokupasa kukubali kosa endapo utakosea.
Katika maisha yetu ya kila siku, ni vema kutambua kuwa unaweza kukosea kwa kufanya jambo makusudi au kwa kutokukusudia. Hivyo basi, endapo utakosea jambo, ni vizuri kukiri kosa pasipo kubisha hiyo ndiyo njia sahihi ya kuishi katika ulimwengu huu.
Iwapo umetenda kosa lolote, ukaulizwa na kukiri kukosea, ni rahisi kwa mtu anayekuuliza kuelewa kwamba umetambua kosa lako na kulijutia, hivyo hautarudia tena, tofauti kama ungekataa na kusema hujakosea.
Asilimia kubwa ya watu wanapokosea hunyamaza hadi wanapoulizwa. Lakini njia nzuri, unapokosea kujitambua mara moja na kukiri kosa kabla hujaulizwa, hiyo itamfanya yeyote kufikiria njia ya kukusamehe kama umemkosea.
Kijana mmoja aliyekuwa kiongozi katika idara yake, alisema kuna wakati hakutoa stahili ya fedha kwa wafanyakazi wake kiasi kwamba jambo hilo lilimgharimu na kuonekana hawezi kuongoza wenzake.
Alilitambua hilo mapema kabla bosi wake hajamuuliza, alimfuata na kumueleza kilichotokea, alikiri kuwa hali hiyo ameisababisha yeye.
Kijana huyo aliingia ofisini kwa bosi wake na kumueleza juu ya jambo hilo na kukiri kuwa amekosea. Kwa maelezo ya kijana huyo, baada ya kukiri kwa bosi wake kwamba jambo hilo ni yeye alilisababisha, anasema bosi wake alimwangalia na kumwambia “Sawa, ni kosa lako, lakini inakubidi kurekebisha jambo hilo.
“Makosa huwa yanarekebishika, kila mmoja anakosea,” anasema. Kijana anabainisha kwamba baada ya kuambiwa hivyo na bosi wake, alipata nguvu mpya na kufarijika zaidi, tangu siku hiyo bosi wake alimwamini kwa kila jambo.
Mtu asiye na busara, mara nyingi hujaribu kujitetea anapofanya makosa badala ya kukiri na kujirekebisha. Hali hii ipo kwa watu wengi katika maisha yetu ya kila siku. Wengi wetu hufanya makosa, badala ya kukiri huamua kukaa kimya mambo yanapoharibika ndiyo hukumbuka kuomba msamaha.
Mara nyingine mtu wa aina hiyo hupoteza uaminifu kwa wenzake na hata kufukuzwa kazi, kwa tabia ya kutokuwa tayari kukiri kosa. Hebu tuangalie mfano wa mwalimu aliyekuwa hana uhusiano mzuri na mtoto wake. Siku moja katika kipindi chake asubuhi, aliwaeleza wanafunzi wake jinsi alivyotofautiana na mtoto wake, hata kushindwa kuwaona wajukuu zake.
Mzazi huyo alihisi kuwa, kijana wake anapaswa kuwaheshimu babu zake, kukubali kila jambo atakaloambiwa liwe zuri au baya, kwamba hapaswi kuwa na maamuzi yake.
Mwisho, mwalimu alilieleza darasa lake kuwa amekuwa akiwaza tatizo hilo na kuona kuwa kuna umuhimu wa kumuomba mtoto wake msamaha. Anaeleza, mwanafalsafa anasema kama umekosea ni vema kukiri kosa haraka; kwa msisitizo. “Kwangu ilichukua muda mrefu kukiri kwa haraka, lakini nimeweza kukubali katika hali ya kumaanisha”.
Inawezekana niliona aibu kumuomba msamaha kijana mdogo, lakini nilikuwa nimekosea na lilikuwa ni jukumu langu kufanya hivyo.
Baada ya kusema hayo darasa lake lilishangilia kwa kupiga makofi, na kumpongeza. Kipindi kilichofuata mwalimu huyo aliwaeleza wanafunzi wake jinsi alivyokwenda nyumbani kwa mtoto wake, kuomba na kupewa msamaha, kwa sasa wamejenga uhusiano mpya na mtoto wake, mkwewe na watoto wao.
Hivyo basi, tumekuwa tukishuhudia watu mbalimbali wenye uwezo wa kukabiliana na watu ambao walikuwa ni maadui na kujenga urafiki mpya.
Je, waweza kusemaje kwa mtu anayekutendea jambo kama hilo? Pale tunapokuwa sahihi tuchukuliane na watu kwa upendo, tunapokosea, tukubali makosa yetu, hali hii itazidisha upendo kuliko kubakia kila wakati unajitetea

0 Maoni:

Twitter Facebook