Wednesday, July 23, 2008

WAZA MAMBO MAZURI


KARIBUNI wapenzi wasomaji katika safu ya ‘Maisha Yetu’. Kwa zaidi ya mwaka sasa nimeandika mambo mbalimbali yanayohusu mafanikio, jinsi ya kuishi na watu mbalimbali, kujua tabia za watu, kujijua mwenyewe na jinsi ya kupambana na maisha katika hali yoyote.
Kwa kweli safu yetu imepongezwa sana na tulipokosea tulikubali ushauri kutoka kwa wasomaji wetu. Naamini mtaendelea kutuungana mkono kwa kusoma na kuendelea kutoa ushauri wa kuboresha safu hii.
Wiki iliyopita niliishia sehemu inayosema; kumbuka unapoanza kuwa na hofu ya vitu vilivyopita ni kama unajaribu kupanda mazao yako kwenye vumbi.
Maana yake ni kwamba yale yaliyopita usiyasumbukie, bali ugange yajayo. Ukiendelea kuyasumbukia, utajisababishia mikunjo katika paji la uso wako na vidonda vya tumbo.
Hivyo, endapo una tatizo la kukumbuka mambo yaliyopita, iambie nafsi yako kwamba huishi kwa ajili ya mambo hayo. Badala yake unaweza kuwa na mipango mizuri zaidi kwa ajili ya maisha yako.
Unaweza kujishughulisha kwa kuandaa mashindano mbalimbali kama vile muziki, soka au uchoraji. Lengo ni kujishughulisha kila mara ili usiwe na nafasi ya kufikiria mambo yaliyopita ambayo yamekusababishia hasara na hofu maishani mwako.
“Miaka michache iliyopita nilitakiwa kujibu swali moja ambalo lilikuwa likiuliza, je, ni somo gani kubwa ambalo nimejifunza.
“…Jibu lake lilikuwa ni jepesi kwamba somo nililowahi kujifunza na kulifurahia ni juu ya umuhimu wa vile tunavyofikiri.
“Kwani endapo mimi ningejua kile unachokifikiri ningejua wewe ni nani na wewe ungejua kile ninachofikiri, ungejua mimi ni nani - kwani mawazo yetu yanatufanya tujue sisi ni nani”.
Sasa tunaweza kujua matatizo makubwa tunayokuwa nayo mimi na wewe, kwamba tatizo tunalohangaika nalo ni jinsi ya kuchagua mawazo sahihi. Kama tutafanikiwa katika hili, tutakuwa kwenye njia sahihi ya kutatua mawazo yetu yote.
Ni ukweli usiopingika kuwa endapo unafikiria mawazo ya furaha utakuwa na furaha maishani mwako, vile vile endapo unafikiria mawazo ya umaskini, utakuwa hivyo.
Kama unawaza mawazo ya hofu, utaishi kwa hofu. Iwapo mawazo yako ni kuumwa, kuna uwezekano wa kupata maradhi. Kama unafikiria kushindwa, utashindwa kweli kwenye mipango yako.
Kama unatabika na kujionea huruma, kila mmoja atakuepuka na kujitenga nawe. Huko vile unavyofikiri, bali kile unachofikiri, ndivyo kilivyo.
Mtu mmoja alikuwa na maisha mazuri, lakini ghafla alifilisika, ingawa mtu huyo alijikuta na madeni makubwa, alijishughulisha hakuwa na hofu kwa kuwa alijua endapo ataruhusu hali hiyo imvunje moyo, atakosa kuthaminiwa, pamoja na mdai wake.
Hivyo alijipa matumaini kwa kuwaza mambo ya mafanikio, mawazo ya kutia moyo na kukataa kuiruhusu hali ya kushindwa.
Hali hiyo ilimfanya atulize akili yake na kupanga mambo ya mafanikio katika maisha yake. Alijitathmini na kuangalia upungufu uliokuwapo hadi hali ile ikamtokea, alimwomba Mungu, pia alijitahidi kufanya kazi yoyote iliyokuwa mbele yake kwa malengo.
Tuangalie mfano uliotolewa na Mwalimu John uliomhusu mwanafunzi wake ambaye alivunjika moyo kutokana na hofu iliyomwandama.
Kwa maelezo ya Mwalimu John, mwanafunzi huyo alikuwa wazi kwake hivyo alimweleza kuwa hali ya wasiwasi ilikuwa ikimtesa kwa muda mrefu.
Hivyo, alikuwa na wasiwasi wa kila kitu, alikuwa na hofu kutokana na wembamba aliokuwa nao, kwamba alihofia kupata fedha za kuoa, alihofu kumpoteza msichana aliyetaka kufunga naye ndoa.
Alihisi kuwa kamwe hatakaa aishi maisha mazuri, alikuwa na hofu kuwa atapata vidonda vya tumbo. Kutokana na hali hiyo, aliamua kuacha kazi.
Mwanafunzi huyo alisema baada ya kujitathmini alijiona ana kasoro, hivyo alimwomba Mungu ampe nguvu ya kufanya shughuli zake na kuondoa hofu hiyo aliyokuwa nayo.
“Hali hiyo ilikuwa ikinitokea mara kwa mara, hivyo sikuweza kuieleza hata familia yangu,” anasema mwanafunzi huyo. Anasema hakuweza kuidhibiti hali hiyo, kwani alikuwa amejaa hofu.
Kutokana na hali hiyo, alijiepusha na kila mtu. Lakini ufumbuzi ulipatikana baada ya kumwomba Mungu ampe nguvu ya kuikabili hali hiyo na kujishughulisha.
Baada ya kuigundua hali hiyo, ilimbidi abadilike kwa kuondoa mawazo yaliyokuwa yakimsumbua. Alipoamua kukondokana na hali hiyo, alijikuta ameirudia kazi yake aliyokuwa ameiacha, miezi minne baadaye alimwoa binti aliyefikiri kuwa angemkosa kutokana na hofu aliyokuwa nayo, hivyo kujikuta anaishi maisha yenye furaha.
Kumbuka unapokuwa katika hali ya kukata tama, unajikuta huwezi kuendelea wala kuwa na mafanikio yoyote katika maisha yako. Unapoikataa hali hiyo maisha yanakuwa mazuri na kuwa kama ni rafiki yako.
Kumbuka amani tuliyonayo na furaha tunayopata haitegemei wapi tulipo au nini tulichonacho ama sisi ni kina nani, lakini ni kutokana na mawazo tunayoyawaza.
Ni vizuri kuitafuta furaha kwa gharama yoyote ili kuondoa hofu na wasiwasi inayokuandama. Iambie nafsi yako kwa leo utakuwa na furaha. Kumbuka furaha inatoka ndani, si jambo linalotoka nje. Pia uhudumie mwili wako kwa mazoezi na kuupamba, usiudharau.
Pia jifunze kuwa na mawazo yenye nguvu ambayo yatakufanya ujifunze mambo kwa ajili ya manufaa. Usiiruhusu akili yako iwaze masuala yasiyo na nguvu yatakayokufanya ujione huna maana. Jizoeze kusoma vijaridia vya kukuwezesha kuwa na jitihada katika shughuli zako, pamoja na akili.
Anza kuwa na ratiba katika maisha yako ya kila siku, kwa kuandika kwenye kijitabu yale mambo unayotarajia kuyafanya kila saa, si lazima ufuate kama ratiba ilivyo, lakini ni vizuri kuwa na ratiba.
Pia ni vizuri kujipa muda wa kutulia na kupumzika, pamoja na kumwomba Mungu. Iambie nafsi yako kwa siku hiyo hautakuwa na hofu, ila furaha na kufurahia vitu vizuri na kuwapenda wengine.
Tukutane Alhamisi ijayo.
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa mtandaohttp://www.lngowi.blogspot.com/lcyngowi@yahoo.com0713 – 331 455 au0733 – 331 455

ONDOA WASIWASI KATIKA MAISHA USONGE MBELE


KARIBUNI wapenzi wasomaji wa safu hii inayowajia kwa lengo la kufundisha na kubadili maisha yetu. Pia safu hii huweza kumtoa mtu katika hali fulani aliyokuwa nayo na kumweka katika hali nyingine.
Wiki iliyopita tuliishia sehemu iliyoeleza, unapokuwa kwenye wakati mgumu, kama unaweza kuiondoa hali hiyo ni vizuri, lakini kama huwezi usiipe nafasi moyoni mwako.
Endapo utaipa nafasi hali hiyo, itarudisha nyuma maendeleo yako kwa kuwa kila utakapotaka kupiga hatua, hofu ya kufa au kuugua na kuacha mali zako hukujia.
Katika vipindi mbalimbali mtu anavyopitia, amekuwa akikutana na hali isiyo nzuri kutokana na mzunguko wa dunia.
Hivyo, unapojikuta katika hali hiyo, una uamuzi wa kuikubali hali iliyokupata kuwa haiwezi kubadilika na kuwa tayari kukabiliana nayo, endapo hautaikubali hali hiyo utaishia kuwa na hofu kila wakati.
Leo, tutaangalia jinsi ya kukabiliana na hali inayokupata mara tu biashara yako inapokwenda mrama. Unapokutana na hali hiyo ni vema kuweka tamko la kusitisha hasara uliyoipata, kwamba huko tayari kukubali hasara hiyo iendelee, kwani utajitahidi kuweka mikakati zaidi ya kuiboresha na kuomba ushauri wa kimaendeleo kwa wafanyabiashara waliofanikiwa.
Tumwangalie mfanyabiashara John Robert, aliyekuwa amepewa fedha na rafiki zake kiasi cha dola 200,000 za Kimarekani, ili kuwekeza katika soko la hisa.
Baada ya kupewa fedha hizo na kuzifanyia biashara, Robert alifikiri kuwa angepata faida ambayo ingemfanya awe na maendeleo zaidi katika maisha yake, lakini kwa bahati mbaya ilikuwa kinyume na matarajio yake.
Awali, alipoanza biashara hiyo alipata faida ambayo ilimfanya asiwe mbunifu katika biashara yake, lakini matokeo yake ni kwamba baada ya muda mfupi alifilisika.
Mfanyabiashara huyo, baada ya kufilisika alipata hofu kutokana na fedha alizopewa kwa ajili ya kufanyabiashara.
“Sikujali kupoteza pesa zangu mwenyewe,” alisema mfanyabiashara huyo na kwamba kipindi hicho kilikuwa kigumu kwake, kutokana na kupoteza pesa za rafiki zake.
Lakini, mara baada ya kufanikiwa kuishinda hofu iliyokuwa ikimkabili, alijikuta amepata ujasiri mpya na kwenda kuwakabili tena rafiki zake na kuwaeleza kilichomsibu.
Pamoja na maelezo hayo, marafiki wale hawakuonyesha mshangao katika jambo hilo, bali walilichukulia kuwa la kawaida. Lakini kwa upande wake ilionekana halitatibika.
“Nilijua nilikuwa nafanya biashara katika mtindo wa 'pata potea' nikitarajia zaidi bahati na mawazo ya watu. Nilikuwa nikishiriki katika soko la hisa kwa kusikia,” alisema.
Kwa maelezo ya Robert, alianza kufikiria makosa yake na kufanya uamuzi kabla ya kuamua kurudi kwenye soko kwa mara nyingine, alijaribu kutafuta chanzo cha jambo hilo, pia alifikiri na kuamua kuja na mwongozo mpya wa mafanikio.
Baada ya hali hiyo kumtokea, alitafuta ushauri kutoka kwa rafiki zake, kwa kuwauliza ni jinsi gani wameweza kufanikiwa na kuendesha biashara zao, ambazo zinakwenda vizuri.
Mmoja wa marafiki zake, aliyeendesha biashara yake vizuri alimweleza akiweka tamko la kusitisha hasara katika hofu yake kwenye majukumu aliyojipangia.
Hivyo, mtu yeyote anaweza kuondoa tabia ya hofu aliyonayo. Hivyo popote unaposhawishika kuweka pesa zako baada ya kupoteza, ni vizuri kutulia na kujiuliza maswali yafuatayo.
Ni kwa kiasi gani umekuwa na hofu kuhusu jambo fulani juu yako? Ni kwa jinsi gani utaepuka kupata hasara katika hofu inayokukabili na kusahau? Ni kwa jinsi gani utaepuka kupata hasara katika wasiwasi na kusahau?
Kumbuka unapoanza kuwa na hofu ya vitu vilivyopita na kufanyika ni kama unakuwa ukijaribu kupanda mazao yako kwenye vumbi. Maana yake ni kwamba yale yaliyopita usiyasumbukie, bali ugange yajayo. Ukiendelea kuyasumbukia utajisababishia mikunjo katika paji la uso wako na vidonda vya tumbo.
Hivyo, endapo una tatizo la kukumbuka mambo yaliyopita, iambie nafsi yako kwamba huishi kwa ajili ya mambo hayo. Badala yake unaweza kuwa na mipango mizuri zaidi kwa ajili ya maisha yako. Unaweza kujishughulisha kwa kuandaa mashindano mbalimbali kama vile muziki, ngumi au uchoraji.
Lengo ni kuwa unajishughulisha kila mara ili usiwe na nafasi ya kufikiria mambo yaliyopita ambayo yamekusababishia hasara na hofu maishani mwako.
Tukutane Alhamisi ijayo.
Makala hii ni kwa msaada wa mtandao wa mtanadao na kitabu cha Ondoa wasiwasi anza maisha mapya’.
http://www.lngowi.blogspot.com/ lcyngowi@yahoo.com0713 331455 OR 0733 331455

KUBALIANA NA HALI USIYOWEZA KUIBADILI

KARIBUNI wapenzi wasomaji katika Safu ya Maisha Yetu, ambayo huelimisha, huadilisha na kubadilisha mambo mbalimbali tunayokabiliana nayo katika maisha yetu ya kila siku.
Wiki iliyopita tulimwona Steven baada ya kufiwa na watoto wake wawili mfululizo aliishi kwa hofu na kukata tamaa kwa muda mrefu, lakini siku moja mtoto wake wa kiume (5) alimwomba baba yake amtengenezee boti, ambayo ilimchukua muda mrefu kuimaliza.
Kwa maelezo ya Steven, kutengeneza boti hiyo kulichukua muda wa saa tatu, lakini ilipokwisha aligundua muda huo alioutumia katika kazi aliyokuwa akiifanya, uliweza kumpumzisha akili yake na kumpa amani ambayo aliipoteza kwa muda mrefu baada ya kufiwa na watoto wake.
Tokea hapo, aligundua kuwa ni vizuri mtu ajishughulishe katika kipindi kigumu anachopitia kama vile kufiwa na mke, mume, wazazi au watoto. Kwa kuwa mtu anapojishughulisha hukosa muda wa kufikiri hali ile iliyompata huko nyuma na badala yake anafiki kile anachokifanya kwa wakati huo.
Leo tutakwenda kumwangalia George ambaye anasema alipokuwa mtoto alikuwa na wasiwasi. Kwa maelezo yake, kila ilipofikia kipindi cha radi na ngurumo alikuwa akipatwa na hofu kuwa huenda mwanga wa radi utamuua.
Vilevile katika kipindi kigumu cha kutokuwa na mazao shambani mwao, alikuwa akihofu huenda watakosa chakula cha kutosha, na kuwasababisha wakae na njaa.
Hofu yake haikuishia hapo, bali aliendelea kuwaza kuwa endapo atakufa atakwenda motoni. Alikuwa akimwogopa kijana ambaye alimtishia kuwa angemkata masikio yake na kuwaogopa wasichana kuwa wangemcheka endapo angeongea nao. Wasiwasi wake ni kwamba hakuna msichana yeyote atakayekubali kuolewa naye.
Yote hiyo ni hali ya wasiwasi aliyokuwa nayo kijana huyo na kumfanya aishi kwa hofu muda mrefu, mpaka pale alipokuwa mkubwa na kugundua asilimia 90 ya vitu alivyokuwa akiviogopa havikumtokea.
Hivyo unaweza kuona, hofu inapoumbika katika maisha yako inasababisha shida kubwa na kurudisha nyuma maendeleo yako kwa kuwa kila ukitaka kupiga hatua unakuwa na hofu kuwa huenda ukafariki au kuugua.
Hivyo wasiwasi ni mbaya sana. George anasema hali hiyo ilikuwa ikimtesa katika kipindi cha ujana, lakini kadiri alivyokuwa anakuwa aliipuuza kwa kuwa ilimtesa.
Endapo unasumbuliwa na hali hiyo, jitahidi kuiondoa kwa gharama yoyote ili isikuletee uharibifu siku za usoni. Mara nyingi mwishoni mwa wiki, watu wengi hupenda kwenda matembezi mbalimbali kama madukani, sokoni au kutembelea ndugu, jamaa na marafiki.
Safari hiyo itakuwa nzuri kama mtu huyo atatuliza akili yake katika matembezi anayoyafanya. Lakini kinyume chake kama utakuwa haujaishinda huko uliko, utaanza kuwa na wasiwasi labda umeacha pasi inawaka au nyumba yako inaungua.
Unaweza kuwa na wasiwasi, kwamba msichana unayeishi naye ametoroka na kuwaacha watoto wako peke yao au hofu yako wamegongwa na gari na kufariki wakati wakiendesha baiskeli zao.
Hali hiyo itakuondolea raha ya matembezi hivyo usipoidhibiti itakuletea matatizo katika familia na hata ndoa yako. Unapokuwa na hali ya hofu ni vema ukaupumzisha mwili na kufikiri njia ya kuondokana na hali hiyo.
Ni vema ukakubaliana na hali ile ambayo huwezi kuibadili au kuizuia. Unapokutana na jambo linalokuumiza, ni vema ukakubaliana nalo. Mfano unaweza kupata ajali na kukatika vidole vya mguu wa kushoto, kabla ya hapo ulikuwa ukiuona mguu wako ukiwa na vidole vyote vitano, usipokubali hali hiyo, siku zote utakuwa mtu wa hofu na kukata tamaa. Hivyo ni vizuri kukubaliana na hali ile ambayo huwezi kuizuia au kuiepuka.
Katika vipindi mbalimbali tunavyopitia, tumekuwa tukikutana na hali isiyo nzuri katika maisha yetu, na hivyo ndivyo ilivyo. Tuna uamuzi, tunaweza kukubali hali hiyo kuwa haiwezi kubadilika na kuwa tayari kukabiliana nayo, au kutokubaliana na hali hiyo, ambapo mwisho wake ni kuwa na wasiwasi kila wakati.
“Kukubaliana na kile kilichokutokea ni hatua ya kwanza ya kukabiliana na jambo lolote lililo gumu,” anasema Godfrey Johnson. Usiiruhusu nafsi yako kukata tamaa hadi kushindwa kufanya jambo la maendeleo katika maisha yako. Isifikie hatua ukaona kuwa hakuna faida ya kuishi kutokana na misukosuko inayokukabili.
Watu wengine wanapokumbana na hali ngumu katika maisha yao hufikia hatua ya kuidharau kazi anayoifanya na hata kujitenga na marafiki zake. Isifikie hatua ukaachilia kila jambo ulilokuwa ukilifanya kutokana na hali hiyo.
“Nilipopata habari za kunitia hofu niliacha kazi yangu, na kwenda mbali ambako nilijificha nikalia kwa uchungu,” alisema Mary. Kwa maelezo yake alikumbuka wakati alipofiwa na mama yake mzazi alitumiwa ujumbe ambao ulisema kuwa; “Jipe moyo kwa yale yaliyokupata. Zuia huzuni zako kwa tabasamu na kuinuka.”
Alisema maneno hayo alipoyatafakari kwa mara nyingine yalimwinua na kumtia nguvu mpya. Alisahau tabu na huzuni zote zilizomkabili. Baada ya kupata faraja hiyo, aliondoka na kurudi kazini kwake kuendelea na kazi, kwa kuwa, aliikataa hali ile iliyokuwa ikimsononesha, kwa kuiambia nafsi yake kuwa, “imetokea. Siwezi kuibadili hali hiyo.”
Hivyo ni vema kila unapokabiliana na hali hiyo, kukubali kuuchosha mwili wako kwa kuanza masomo ya jioni, kujifunza mambo mapya na kuwa na marafiki wapya. Baada ya kufanikiwa kufanya hivyo utaishi maisha mapya ya furaha yasiyo na huzuni, kwa kuwa hautairuhusu nafsi yako kukumbuka yaliyopita.
Hivyo ni kawaida, mazingira pekee hayawezi kutufanya tuwe na furaha au kutokuwa nayo. Ni kwa jinsi gani tunakabiliana nayo inategemea hisia zetu. Tuangalie mfano wa kijana mmoja ambaye alizoea kusema kuwa, hawezi kuwa na wasiwasi hata kama atapoteza fedha zote alizonazo kwa sababu haoni atakachopata endapo atairuhusu hali hiyo zaidi ya kujipa maumivu.
Ila alisema kitakachofuata baada ya hapo, ni kufanya kzi kwa bidii vile atakavyoweza, na matokeo yake atayaacha mikononi mwa Mungu. Unapokuwa katika wakati mgumu, kama unaweza kuiondoa hali hiyo ni vizuri, kama huwezi usiipe nafasi katika moyo wako hali hiyo.
Makala hii ni kwa msaada wa mtandao wa intanenti na kitabu kijulikanacho kama ‘Ondoa wasiwasi anza maisha mapya’.
Tukutane alhamisi ijayo
www.lngowi.blogspot.comlcyngowi@yahoo.com0713 331455 or 0733 331455

KUJISHUGHULISHA NI NJIA YA KUONDOA HOFU, WASIWASI



NI vizuri ukakabiliana na hali ya wasiwasi inayokusumbua na kuanza siku mpya. Wasiwasi mara nyingi unasababisha uso wako kuharibika, kukunjika, kupatwa na chunusi, vipele vidogo vidogo, ngozi kukunjamana, nywele kubadilika rangi na wakati mwingine kukatika.
Unaweza kuona hali hiyo kuwa ni ya kawaida, lakini sivyo unavyofikiri, hivyo unaweza kukabiliana nayo kwa kuondoa hali hiyo ya hofu na wasiwasi.
Je, unapenda maisha? Je, unapenda kuishi maisha marefu na kufurahia afya bora? Unatakiwa kuwa na amani ndani ya moyo wako ambayo itakuwezesha kuishi kwa kujiamini.
Tuangalie mfano wa kijana Dave, ambaye alihakikishiwa na daktari wake kuwa ana ugonjwa wa kansa, hivyo tangu wakati huo alijiona kama anakufa taratibu kutokana na ugonjwa huo uliompata.
Kwa kuwa alikuwa bado kijana, hakupenda kufa mapema, hivyo kila mara akawa anasumbuliwa na hofu ya kifo. Hivyo aliamua kumpigia simu daktari wake na kumweleza hali aliyonayo na jinsi anavyojisikia kutokana na hali hiyo.
Daktari yule alimweleza wazi kijana Dave, kwamba, kama ataendelea kuwa na hofu, atakufa, cha msingi akubaliane na hali ile aliyokuwa nayo ya ugonjwa bila kuwa na wasiwasi.
“Ni kweli umepatwa na hali mbaya, cha msingi ikubali hali hiyo,” alisema daktari yule na kumsisitiza zaidi kwa kumwambia aiondoe hali ya hofu aliyonayo.
Tangu hapo Dave aliikubali hali ile na kuiambia nafsi yake hana haja ya kuwa na wasiwasi tena, wala kulia, pia yuko tayari kukabiliana na hali yoyote katika maisha.
“Sitaki kuwa na mawazo kuwa nina kansa, bali ninaamini kuwa akili yenye uchangamfu inausaidia mwili kupigana na magonjwa,” alisema Dave na hapo aliendelea kuwa na afya njema, na kusema kuwa anaufurahia msemo unaosema, ‘kubaliana na ukweli, ondoa wasiwasi, halafu fanyia kazi hali hiyo’.
Ni jinsi gani ya kuchanganua na kutatua matatizo yanayosababisha wasiwasi? Kwanza yakupasa upate uhakika wa jambo linalokusumbua, ulichanganue na kufikia uamuzi ambao utaufanyia kazi.
Unafikiri ni kwanini ni muhimu kupata uhakika? Ni kwa sababu kama una uhakika wa lile unalotaka kulitatua haitakuwa rahisi kupata utatuzi wa busara, kwani bila uhakika yote utakayoyafanya yatakuchanganya zaidi.
Unapoamua kutafuta utatuzi wa tatizo lako kamwe usigeuke nyuma na kuangalia hali uliyokuwa nayo awali, ambayo inaweza kukusababishia hofu nyingine. Pia tuangalie ni jinsi gani unaweza kuondoa hofu inayokukabili katika biashara zako.
Dk. Jarome anasema kuwa, kwa miaka 15 amekuwa akitumia nusu ya muda wake wa kufanya biashara zake kwenye mikutano, kujadili matatizo. Kwamba biashara hiyo inaweza kufanywa hivi au vile au kutokufikia muafaka. Anaeleza mara zote amekuwa akipata wasiwasi yeye na wenzake, kwenye viti walivyokalia vinavyozunguka, kutembea kwenye korido, kujadili na kuangalia ukubwa wa tatizo. Na inapofika usiku tayari amekuwa amechoka.
Anasema anategemea hali hiyo ya kuwa na mambo mengi yanayomkabili itakuwa inaendelea katika maisha yake yote. Anasisitiza amekuwa akifanya hivyo miaka 15 iliyopita, kamwe haitatokea kwake njia nyingine ya kufanya hivyo.
“Hapa kuna siri,” anasema Jarome. “Kwanza nimeacha utaratibu niliokuwa nimejiwekea katika mikutano kwa miaka 15 iliyopita.” Anasema aliamua kubadilisha mfumo huo na kuwashirikisha wengine kwa kuwauliza watafanya nini ili kutatua matatizo.
Pili, anasema alitengeneza sheria mpya ya kwamba kila mmoja atakayetaka kupeleka tatizo kwake, lazima ajiandae na kuandaa taarifa ambayo itampatia majibu katika maswali manne ambayo ni kutaka kujua tatizo haswa ni nini, chanzo chake, njia zinazowezekana kutatua tatizo hilo na njia za kutatua tatizo zitakazofikiwa. Hiyo ndiyo changamoto ya kuondoa wasiwasi kwa asilimia 50.
Ni jinsi gani ya kuondoa hali ya wasiwasi inayokukabili kabla haijakuondoa wewe? Tuangalie mfano wa Steven ambaye alikuwa jasiri na kuwaeleza wenzake aliokuwa akisoma nao kwenye chuo kimoja, jinsi ambavyo alikumbana na msiba mara mbili katika familia yake. Kwa maelezo ya Steven, mara ya kwanza alimpoteza mtoto wake wa miaka mitano ambaye alikuwa ni binti, mtoto aliyempenda mno.
Anasema yeye na mke wake walifikiri kuwa hawataweza kustahimili hali hiyo, lakini Steven anasema, miezi kumi baadaye, Mungu aliwapa mtoto mwingine wa kike ambaye alifariki baada ya siku tano.
Steven alisema yeye na mkewe hawakuwahi kupitia kipindi kigumu kama hicho katika maisha yao. “Sikuweza kuchukuliana na hali hiyo, sikuweza kulala, sikuweza kula, sikuweza kupumzika wala kuburudika. Mishipa yangu ilikuwa ikitetemeka na hali ya kujiamini ikaniaondoka,” anasema baba huyo.
Mwishoni alienda kwa madaktari ambao walimshauri wamchome sindano ya usingizi au atafute matembezi ya mbali kwa ajili ya kupumzisha akili. Anasema alijaribu vyote lakini havikuweza kumsaidia.
Anasema hali hiyo iliendelea kumtesa kwa muda mrefu, akaeleza kuwa kwa yeyote aliyewahi kupooza kutokana na jambo baya lililompata ataelewa ni nini anachokisema.
Lakini anamshukuru Mungu kwa kuwa, alikuwa na mtoto mmoja aliyebakia wa kiume wa miaka mitano. Ambaye alimpa ufumbuzi wa tatizo lake. Siku moja mchana alipokuwa amekaa anajisikitikia, mtoto huyo alimwuliza baba yake kama anaweza kumtengenezea boti.
“Ukweli ni kwamba nilikuwa sijisikii kutengeneza boti hiyo, nilikuwa sijisikii kufanya jambo lolote lile,” alisema na kuongeza kuwa ilimbidi afanye hivyo kwa kuwa mtoto wake huyo huwa abadili msimamo wa kile anachokitaka, hivyo ilimbidi amtengenezee.
Anasema kutengeneza boti hiyo ya kuchezea ilimchukua muda wa saa tatu. Lakini ilipokwisha, aligundua muda huo alioutumia uliweza kumpumzisha akili yake na kumpa amani aliyokuwa nayo kwa muda mrefu.
Hivyo amegundua kuwa unapokuwa na shughuli za kufanya kipindi ambacho umekuwa katika wakati mgumu uliokufanya uwe na wasiwasi, hofu au hali ya kukata tamaa, zinakufanya mtu uwe na nguvu mpya kwa kuwa hupati muda wa kufikiri yaliyopita, bali jinsi ya kufanya kazi hiyo ili ikamilike. Hivyo alifikia uamuzi wa kujishughulisha ili hali aliyokuwa nayo isimrudie tena.
Makala hii imetafsiriwa kutoka kwenye kitabu kijulikanacho kama ‘Ondoa wasiwasi anza maisha mapya’, pamoja msaada wa intaneti.
Tukutane wiki ijayo
lcyngowi@yahoo.com0713 331455 or 0733 331455

ONDOA WASIWASI ANZA MAISHA MAPYA

MWANAFUNZI aliyekuwa akichukua masomo ya udaktari, alikuwa na wasiwasi wa jinsi ya kufaulu mitihani yake ya mwisho ya kumaliza chuo. Na hata atakapomaliza masomo yake na kufaulu atapelekwa wapi kufanya kazi aliyoisomea na jinsi gani ataweza kumudu maisha.
Wakati akitafakari hayo, alijikuta anasoma maneno machache ambayo yalibadilisha mtazamo wake huo, na kumfanya kuwa daktari mmoja maarufu katika kizazi chake, na hata alipofariki kurasa 1,466 ziliandikwa kwa ajili ya kueleza wasifu wake.Maneno hayo ni - “Kazi yetu si kuona kwa upeo mdogo kilicho mbali, bali ni kufanya kile tulichonacho mkononi”.
Hata hivyo, mwanafunzi huyo aliamini kuwa njia inayowezekana kuandaa mambo ya kesho ni kufikiri kwa ufahamu wote, pamoja na kuwa na shauku ya kufanya kazi ya leo vizuri zaidi.
Aligundua kuwa hiyo ndiyo njia pekee inayowezekana mtu anayoweza kuiandaa kwa ajili ya maisha.
Mfano mwingine ni kwa mwanamke mmoja ambaye baada ya kufiwa na mume wake, alianza kujiona mpweke na kuvunjika moyo. Siku moja alipokuwa akitoka shuleni alikokuwa akifundisha, alianza kufikiri na kujisemea moyoni mwake kuwa shule aliyopo ni ya kimaskini, pia barabara anayopita wakati wa kwenda na kurudi nyumbani kwake ni mbaya, hivyo aliamua kuchukua uamuzi wa kujinyonga.
Alifikia hatua hiyo baada ya kuona kila kitu kwake hakiwezekani. “Sioni faida ya kuishi. Ninaamka kila asubuhi, kukabiliana na maisha. Nina hofu ya kila kitu, hofu ya kutoweza kumudu kuliendesha gari langu, hofu ya kushindwa kulipa kodi ya nyumba, hofu ya kutokuwa na chakula cha kutosha. Nina hofu ya afya yangu nami sina fedha ya kumwona daktari.
"Yote hayo yalimfanya kufikiria kujinyonga. Siku moja alisoma kifungu kimoja kilichomuinua kutoka katika ile hali iliyokuwa inamkabili na kumpa moyo wa kuendelea kuishi. Kifungu alichosoma kilisema: "Kila siku ni maisha mapya kwa mtu mwenye busara."
Alikiandika kifungu kile na kukibandika kwenye kioo cha gari yake alipoweza kukiona kila mara alipokuwa akiendesha.
Aligundua kuwa kuishi si jambo gumu kama alivyofikiria awali, alijifunza kusahau yaliyopita na kutokufikiria mambo ya kesho. Kila siku alijisemea moyoni mwake kuwa, ‘leo ni siku mpya’.
Alifanikiwa kuishinda hofu iliyokuwa ikimkabili ya upweke aliyojitakia. Tangu hapo akawa mtu wa furaha, mwenye mafanikio na anayependa kuishi.
Kuanzia hapo alisema kuwa hataogopa tena, bila kujali maisha yatakuwa ya aina gani kwake. Aligundua kuwa hataogopa maisha yajayo na ndiyo maana kila siku ni mpya kwa mtu mwenye busara.
Jinsi ya kuondoa hali hiyo ya wasiwasi
Kumbuka kuwa hali ya wasiwasi inakuondolea uwezo wa kufikiri. Kwani unapokuwa na hofu akili yako 'inaruka' na kufikiri hapa na kule na kila mahali, na unapoteza nguvu yote ya maamuzi. Hata hivyo, wakati unapojilazimisha kufikiria jambo linalokufanya upatwe na hali hiyo na kuikubali katika akili yako, unaiweka katika kupata muafaka wa jambo linalokukwaza.
Unapokuwa na wasiwasi unaweza kupata vidonda vya tumbo, pia uzito wako unaweza kupungua ghafla pamoja na kupata maradhi mbalimbali.Ili kuondokana na hali hiyo, inakupasa kuacha kufikiria na kujipa ujasiri katika kila jambo unalolifanya, pamoja na kuamua kufanikisha mipango yako ya baadaye. Pia unaposafiri maeneo mbalimbali inakusaidia kukutana na watu tofauti na kupata mawazo mapya ya maisha hivyo kujikuta unaondokana na hali uliyokuwa nayo.
Hali hiyo imekusababishia mambo gani
Hali hiyo humfanya mtu akawa mgonjwa na kuanza kuhisi dalili za tumbo kujaa, kuwa na vidonda vya tumbo, mapigo ya moyo kuongezeka, kuumwa na kichwa na mara nyingine kupatwa na hali kama ya kupooza.
"Magonjwa kama haya hutokea. Ninajua ninachokizungumza,” anasema Dk. Gober. "Kwa upande wangu nimesumbuliwa na vidonda vya tumbo kwa muda wa miaka 20.
“Hofu inasababisha wasiwasi. Pia wasiwasi huo, unakufanya uwe katika hali ya kutotulia na ya fadhaa, huathiri misuli ya tumbo lako, hubadili tumbo lako kutoka katika hali ya kawaida, ambayo mara nyingi huchangia kupata vidonda vya tumbo,”.
Naye Dk. Joseph Montague anasema huwezi kupata vidonda vya tumbo kutoka kwenye kile ulacho, bali unapata vidonda hivyo kutoka kwa kile kinachokutafuna.
Hofu, wasiwasi, chuki, ubinafsi na kutokuwa na uwezo wa kukabiliana na ukweli wa mambo katika ulimwengu huu, ni sababu kubwa za maumivu ya tumbo, pamoja na vidonda…vidonda vya tumbo vinaweza kukuua.
Pia utafiti uliofanywa umebaini kuwa wafanyabiashara wengi ambao hawajafikisha miaka 45 hupatwa na magonjwa ya moyo, vidonda vya tumbo na shinikizo la damu, kutokana na kuishi maisha ya wasiwasi.
Mtu anaweza kupata mafanikio katika biashara yake na kujisababishia matatizo makubwa ya afya yake. Itamsaidia nini kupata ulimwengu wote kwa utajiri na kupoteza afya yake? Hata kama amekuwa tajiri wa dunia inambidi alale katika kitanda kimoja kwa wakati na kula mlo mara tatu kwa siku, siyo kujishughulisha kupita kiasi na kusahau muda wake wa kula, pamoja na kulala.
Zaidi ya nusu ya wagonjwa wanaolazwa hospitalini huwa na matatizo yaliyosababishwa na hofu, wasiwasi, mshtuko, dukuduku na hali ya kutofanya lolote la maana. Mtu mmoja alisema kuwa kosa linalofanywa na wataalamu wanakuwa wanajitahidi kuponya mwili, badala ya kuangalia chanzo cha tatizo na kukishughulikia. Ingawa mwili na ufahamu ni mmoja na hautakiwi kutenganishwa.
Wasiwasi unaweza kukuweka kwenye kiti cha walemavu kutokana na ugonjwa wa viungo na ugonjwa wa baridi yabisi. Dk. Russell Cecil ameorodhesha vitu vinne vinavyochangia ugonjwa wa baridi yabisi kuwa ni: kuvunjika kwa ndoa, majanga ya kutokuwa na fedha pamoja na huzuni, upweke na wasiwasi pamoja na hali ya kutaka kupata faraja kuchukua muda mrefu tofauti na matarajio.
Tukutane wiki ijayo.
Makala hii imetafsiriwa kutoka kwenye kitabu kilichoandikwa na Dale Carnegie
lcyngowi@yahoo.com0713 3314550733 331455Mwisho

Thursday, July 10, 2008

Bill Gates


Wengine kufikia mfanikio kama aliyo nayo Bill Gates, huona ni ndoto na jambo lisilowezekana, kabisa, lakini amini inawezekana!

Twitter Facebook