Wednesday, July 23, 2008

ONDOA WASIWASI KATIKA MAISHA USONGE MBELE


KARIBUNI wapenzi wasomaji wa safu hii inayowajia kwa lengo la kufundisha na kubadili maisha yetu. Pia safu hii huweza kumtoa mtu katika hali fulani aliyokuwa nayo na kumweka katika hali nyingine.
Wiki iliyopita tuliishia sehemu iliyoeleza, unapokuwa kwenye wakati mgumu, kama unaweza kuiondoa hali hiyo ni vizuri, lakini kama huwezi usiipe nafasi moyoni mwako.
Endapo utaipa nafasi hali hiyo, itarudisha nyuma maendeleo yako kwa kuwa kila utakapotaka kupiga hatua, hofu ya kufa au kuugua na kuacha mali zako hukujia.
Katika vipindi mbalimbali mtu anavyopitia, amekuwa akikutana na hali isiyo nzuri kutokana na mzunguko wa dunia.
Hivyo, unapojikuta katika hali hiyo, una uamuzi wa kuikubali hali iliyokupata kuwa haiwezi kubadilika na kuwa tayari kukabiliana nayo, endapo hautaikubali hali hiyo utaishia kuwa na hofu kila wakati.
Leo, tutaangalia jinsi ya kukabiliana na hali inayokupata mara tu biashara yako inapokwenda mrama. Unapokutana na hali hiyo ni vema kuweka tamko la kusitisha hasara uliyoipata, kwamba huko tayari kukubali hasara hiyo iendelee, kwani utajitahidi kuweka mikakati zaidi ya kuiboresha na kuomba ushauri wa kimaendeleo kwa wafanyabiashara waliofanikiwa.
Tumwangalie mfanyabiashara John Robert, aliyekuwa amepewa fedha na rafiki zake kiasi cha dola 200,000 za Kimarekani, ili kuwekeza katika soko la hisa.
Baada ya kupewa fedha hizo na kuzifanyia biashara, Robert alifikiri kuwa angepata faida ambayo ingemfanya awe na maendeleo zaidi katika maisha yake, lakini kwa bahati mbaya ilikuwa kinyume na matarajio yake.
Awali, alipoanza biashara hiyo alipata faida ambayo ilimfanya asiwe mbunifu katika biashara yake, lakini matokeo yake ni kwamba baada ya muda mfupi alifilisika.
Mfanyabiashara huyo, baada ya kufilisika alipata hofu kutokana na fedha alizopewa kwa ajili ya kufanyabiashara.
“Sikujali kupoteza pesa zangu mwenyewe,” alisema mfanyabiashara huyo na kwamba kipindi hicho kilikuwa kigumu kwake, kutokana na kupoteza pesa za rafiki zake.
Lakini, mara baada ya kufanikiwa kuishinda hofu iliyokuwa ikimkabili, alijikuta amepata ujasiri mpya na kwenda kuwakabili tena rafiki zake na kuwaeleza kilichomsibu.
Pamoja na maelezo hayo, marafiki wale hawakuonyesha mshangao katika jambo hilo, bali walilichukulia kuwa la kawaida. Lakini kwa upande wake ilionekana halitatibika.
“Nilijua nilikuwa nafanya biashara katika mtindo wa 'pata potea' nikitarajia zaidi bahati na mawazo ya watu. Nilikuwa nikishiriki katika soko la hisa kwa kusikia,” alisema.
Kwa maelezo ya Robert, alianza kufikiria makosa yake na kufanya uamuzi kabla ya kuamua kurudi kwenye soko kwa mara nyingine, alijaribu kutafuta chanzo cha jambo hilo, pia alifikiri na kuamua kuja na mwongozo mpya wa mafanikio.
Baada ya hali hiyo kumtokea, alitafuta ushauri kutoka kwa rafiki zake, kwa kuwauliza ni jinsi gani wameweza kufanikiwa na kuendesha biashara zao, ambazo zinakwenda vizuri.
Mmoja wa marafiki zake, aliyeendesha biashara yake vizuri alimweleza akiweka tamko la kusitisha hasara katika hofu yake kwenye majukumu aliyojipangia.
Hivyo, mtu yeyote anaweza kuondoa tabia ya hofu aliyonayo. Hivyo popote unaposhawishika kuweka pesa zako baada ya kupoteza, ni vizuri kutulia na kujiuliza maswali yafuatayo.
Ni kwa kiasi gani umekuwa na hofu kuhusu jambo fulani juu yako? Ni kwa jinsi gani utaepuka kupata hasara katika hofu inayokukabili na kusahau? Ni kwa jinsi gani utaepuka kupata hasara katika wasiwasi na kusahau?
Kumbuka unapoanza kuwa na hofu ya vitu vilivyopita na kufanyika ni kama unakuwa ukijaribu kupanda mazao yako kwenye vumbi. Maana yake ni kwamba yale yaliyopita usiyasumbukie, bali ugange yajayo. Ukiendelea kuyasumbukia utajisababishia mikunjo katika paji la uso wako na vidonda vya tumbo.
Hivyo, endapo una tatizo la kukumbuka mambo yaliyopita, iambie nafsi yako kwamba huishi kwa ajili ya mambo hayo. Badala yake unaweza kuwa na mipango mizuri zaidi kwa ajili ya maisha yako. Unaweza kujishughulisha kwa kuandaa mashindano mbalimbali kama vile muziki, ngumi au uchoraji.
Lengo ni kuwa unajishughulisha kila mara ili usiwe na nafasi ya kufikiria mambo yaliyopita ambayo yamekusababishia hasara na hofu maishani mwako.
Tukutane Alhamisi ijayo.
Makala hii ni kwa msaada wa mtandao wa mtanadao na kitabu cha Ondoa wasiwasi anza maisha mapya’.
http://www.lngowi.blogspot.com/ lcyngowi@yahoo.com0713 331455 OR 0733 331455

0 Maoni:

Twitter Facebook