Wednesday, July 23, 2008

WAZA MAMBO MAZURI


KARIBUNI wapenzi wasomaji katika safu ya ‘Maisha Yetu’. Kwa zaidi ya mwaka sasa nimeandika mambo mbalimbali yanayohusu mafanikio, jinsi ya kuishi na watu mbalimbali, kujua tabia za watu, kujijua mwenyewe na jinsi ya kupambana na maisha katika hali yoyote.
Kwa kweli safu yetu imepongezwa sana na tulipokosea tulikubali ushauri kutoka kwa wasomaji wetu. Naamini mtaendelea kutuungana mkono kwa kusoma na kuendelea kutoa ushauri wa kuboresha safu hii.
Wiki iliyopita niliishia sehemu inayosema; kumbuka unapoanza kuwa na hofu ya vitu vilivyopita ni kama unajaribu kupanda mazao yako kwenye vumbi.
Maana yake ni kwamba yale yaliyopita usiyasumbukie, bali ugange yajayo. Ukiendelea kuyasumbukia, utajisababishia mikunjo katika paji la uso wako na vidonda vya tumbo.
Hivyo, endapo una tatizo la kukumbuka mambo yaliyopita, iambie nafsi yako kwamba huishi kwa ajili ya mambo hayo. Badala yake unaweza kuwa na mipango mizuri zaidi kwa ajili ya maisha yako.
Unaweza kujishughulisha kwa kuandaa mashindano mbalimbali kama vile muziki, soka au uchoraji. Lengo ni kujishughulisha kila mara ili usiwe na nafasi ya kufikiria mambo yaliyopita ambayo yamekusababishia hasara na hofu maishani mwako.
“Miaka michache iliyopita nilitakiwa kujibu swali moja ambalo lilikuwa likiuliza, je, ni somo gani kubwa ambalo nimejifunza.
“…Jibu lake lilikuwa ni jepesi kwamba somo nililowahi kujifunza na kulifurahia ni juu ya umuhimu wa vile tunavyofikiri.
“Kwani endapo mimi ningejua kile unachokifikiri ningejua wewe ni nani na wewe ungejua kile ninachofikiri, ungejua mimi ni nani - kwani mawazo yetu yanatufanya tujue sisi ni nani”.
Sasa tunaweza kujua matatizo makubwa tunayokuwa nayo mimi na wewe, kwamba tatizo tunalohangaika nalo ni jinsi ya kuchagua mawazo sahihi. Kama tutafanikiwa katika hili, tutakuwa kwenye njia sahihi ya kutatua mawazo yetu yote.
Ni ukweli usiopingika kuwa endapo unafikiria mawazo ya furaha utakuwa na furaha maishani mwako, vile vile endapo unafikiria mawazo ya umaskini, utakuwa hivyo.
Kama unawaza mawazo ya hofu, utaishi kwa hofu. Iwapo mawazo yako ni kuumwa, kuna uwezekano wa kupata maradhi. Kama unafikiria kushindwa, utashindwa kweli kwenye mipango yako.
Kama unatabika na kujionea huruma, kila mmoja atakuepuka na kujitenga nawe. Huko vile unavyofikiri, bali kile unachofikiri, ndivyo kilivyo.
Mtu mmoja alikuwa na maisha mazuri, lakini ghafla alifilisika, ingawa mtu huyo alijikuta na madeni makubwa, alijishughulisha hakuwa na hofu kwa kuwa alijua endapo ataruhusu hali hiyo imvunje moyo, atakosa kuthaminiwa, pamoja na mdai wake.
Hivyo alijipa matumaini kwa kuwaza mambo ya mafanikio, mawazo ya kutia moyo na kukataa kuiruhusu hali ya kushindwa.
Hali hiyo ilimfanya atulize akili yake na kupanga mambo ya mafanikio katika maisha yake. Alijitathmini na kuangalia upungufu uliokuwapo hadi hali ile ikamtokea, alimwomba Mungu, pia alijitahidi kufanya kazi yoyote iliyokuwa mbele yake kwa malengo.
Tuangalie mfano uliotolewa na Mwalimu John uliomhusu mwanafunzi wake ambaye alivunjika moyo kutokana na hofu iliyomwandama.
Kwa maelezo ya Mwalimu John, mwanafunzi huyo alikuwa wazi kwake hivyo alimweleza kuwa hali ya wasiwasi ilikuwa ikimtesa kwa muda mrefu.
Hivyo, alikuwa na wasiwasi wa kila kitu, alikuwa na hofu kutokana na wembamba aliokuwa nao, kwamba alihofia kupata fedha za kuoa, alihofu kumpoteza msichana aliyetaka kufunga naye ndoa.
Alihisi kuwa kamwe hatakaa aishi maisha mazuri, alikuwa na hofu kuwa atapata vidonda vya tumbo. Kutokana na hali hiyo, aliamua kuacha kazi.
Mwanafunzi huyo alisema baada ya kujitathmini alijiona ana kasoro, hivyo alimwomba Mungu ampe nguvu ya kufanya shughuli zake na kuondoa hofu hiyo aliyokuwa nayo.
“Hali hiyo ilikuwa ikinitokea mara kwa mara, hivyo sikuweza kuieleza hata familia yangu,” anasema mwanafunzi huyo. Anasema hakuweza kuidhibiti hali hiyo, kwani alikuwa amejaa hofu.
Kutokana na hali hiyo, alijiepusha na kila mtu. Lakini ufumbuzi ulipatikana baada ya kumwomba Mungu ampe nguvu ya kuikabili hali hiyo na kujishughulisha.
Baada ya kuigundua hali hiyo, ilimbidi abadilike kwa kuondoa mawazo yaliyokuwa yakimsumbua. Alipoamua kukondokana na hali hiyo, alijikuta ameirudia kazi yake aliyokuwa ameiacha, miezi minne baadaye alimwoa binti aliyefikiri kuwa angemkosa kutokana na hofu aliyokuwa nayo, hivyo kujikuta anaishi maisha yenye furaha.
Kumbuka unapokuwa katika hali ya kukata tama, unajikuta huwezi kuendelea wala kuwa na mafanikio yoyote katika maisha yako. Unapoikataa hali hiyo maisha yanakuwa mazuri na kuwa kama ni rafiki yako.
Kumbuka amani tuliyonayo na furaha tunayopata haitegemei wapi tulipo au nini tulichonacho ama sisi ni kina nani, lakini ni kutokana na mawazo tunayoyawaza.
Ni vizuri kuitafuta furaha kwa gharama yoyote ili kuondoa hofu na wasiwasi inayokuandama. Iambie nafsi yako kwa leo utakuwa na furaha. Kumbuka furaha inatoka ndani, si jambo linalotoka nje. Pia uhudumie mwili wako kwa mazoezi na kuupamba, usiudharau.
Pia jifunze kuwa na mawazo yenye nguvu ambayo yatakufanya ujifunze mambo kwa ajili ya manufaa. Usiiruhusu akili yako iwaze masuala yasiyo na nguvu yatakayokufanya ujione huna maana. Jizoeze kusoma vijaridia vya kukuwezesha kuwa na jitihada katika shughuli zako, pamoja na akili.
Anza kuwa na ratiba katika maisha yako ya kila siku, kwa kuandika kwenye kijitabu yale mambo unayotarajia kuyafanya kila saa, si lazima ufuate kama ratiba ilivyo, lakini ni vizuri kuwa na ratiba.
Pia ni vizuri kujipa muda wa kutulia na kupumzika, pamoja na kumwomba Mungu. Iambie nafsi yako kwa siku hiyo hautakuwa na hofu, ila furaha na kufurahia vitu vizuri na kuwapenda wengine.
Tukutane Alhamisi ijayo.
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa mtandaohttp://www.lngowi.blogspot.com/lcyngowi@yahoo.com0713 – 331 455 au0733 – 331 455

2 Maoni:

Nimefurahi kusoma blog yako na asante sana kwani nimejifunza kitu.

ooh nimesahau blog zetu zinafanana kidogo kimajina yangu inaitwa maisha

Twitter Facebook