Thursday, April 4, 2013

Mjasiriamali yeyote anaweza kufanikiwa


WATU wengi wameshindwa kuendelea mbele katika shughuli zao za kijasiriamali kutokana na changamoto wanazokabiliana nazo kibiashara.
Lakini ukweli ni kwamba mjasiriamali yeyote anaweza kufanikiwa katika biashara yake kama atafuata sheria na kanuni za kibiashara, ikiwemo kupata mafunzo ya ujasiriamali.
Kama unafanya biashara ambayo wateja wanapata huduma wanazohitaji kwa urahisi, ama michezo au sehemu ya kusoma barua pepe zao na kufanya shughuli nyingine zinazohusu mtandao, unakuwa kwenye nafasi ya mafanikio.
Lakini kama unapata eneo ambalo silo, utajikuta unafunga haraka biashara hiyo tofauti na matarajio uliyokuwa unayategemea.
Biashara nyingi zinafungwa ama kuwa na mafanikio, kutokana na msingi wa eneo iliyopo.
Kama eneo hilo ni zuri pia linavutia, watu wengi watafika kwa kuwa wanapenda vitu vizuri, huduma nzuri kwa wateja ama ubora wake.
Lakini kama eneo hilo si zuri, inahitajika nguvu ya ziada kwa ajili ya kuwashawishi wateja kufika, ambapo itakubidi bidhaa ziwe za gharama ndogo na kufanya jitihaza zaidi za ushawishi ili watu waweze kufika.
Nini kifanyike? Inabidi uchague eneo zuri kuliangana na aina ya biashara yako. Hakuna eneo zuri au baya, hata kama unafanya shughuli zako nyumbani mbali na wateja wako, patakuwa ni pazuri kwa baadhi ya biashara.
Itengeneze biashara yako kutokana na asili yake na kwa walengwa wako.
Katika hilo ni vema ukazingatia miundombinu, ulinzi na wasambazaji wako.
Wakati mwingine inapendeza kama utaanzisha biashara yako kwenye eneo ambalo biashara kama hiyo ipo. Kwa kuwa tayari eneo hilo litakuwa limeshazoeleka kwa bidhaa ya aina hiyo au huduma hiyo.
Pamoja na ushindani utakaokabiliana nao, utakuwa umepata mafanikio kwa kuwa eneo hilo tayari litakuwa la kibiashara.
Eneo zuri ni gharama, pia ni vigumu kulipata. Lakini pale unapolipata, unapunguza gharama za soko. Sio busara kufanya biashara katika eneo unalolipa gharama ndogo, ambapo matokeo yake unapata wateja ambao kazi yao ni kufanya utalii sio kununua.
Sababu nyingine ambayo inasababisha biashara nyingi kushindwa, zinakuwa hazianzishwi na wajasiriamali bali wataalamu mbalimbali ambao wanafikiri kuwa ni wajasiriamali.
Kinachofikiriwa hapa ni kwamba, kama mtu anajua kutengeneza bidhaa kitaalamu, anadhani kuwa anaweza kufungua na kuiendesha biashara bila kuwa na utaalamu wa kibiashara, lakini hili halina ukweli wowote, matokeo yake biashara inakwama.
Biashara nyingi zinakwama kwa kuwa wajasiriamali wengi hawana ujuzi.
Mjasiriamali yeyote anapaswa kuwa na ujuzi wa kibiashara, uelewa wa bidhaa zake anazozizalisha zinapopatikana pamoja na watu sahihi atakaoweza kuwatumia katika shughuli yake hiyo.
Kwa mfano, uendeshaji wa biashara ya shule ni zaidi ya kuwa mwalimu mzuri wa kufundisha. Kujua jinsi ya kutengeneza nywele haimaanishi kuwa unaweza kuendesha biashara ya saluni. Ama kuwa daktari mzuri haimaanishi kuwa unaweza kumiliki hospitali.
Kuanzisha shule hakumaanishi kunahitaji walimu wa ufundishaji tu, na saluni ni zaidi ya kutengeneza nywele, na hospitali sio tu kwa ajili ya kutibu wagonjwa.
Mauzo na masoko, mahesabu na kuwajali wateja ni zaidi ya shughuli zinazochangia mafanikio ya biashara.
Zaidi ya yote, unaweza kujua jinsi ya kutengeneza nywele lakini unakuwa dhaifu katika eneo la masoko au msimamizi mzuri wa fedha. Matokeo yake huwezi kupata wateja wa kutosha au kusimamia shughuli za kifedha, hivyo biashara kuyumba.
Kama wewe una fani yako halafu unataka kuanzisha biashara inayoendana na fani uliyonayo, usidhani kuwa unajua kila kitu. Pata muda wa kusoma jinsi ya kuendesha biashara, masoko, huduma kwa wateja na shughuli nyingine za kibiashara.
Njia nyingine ni kutafuta mbia ambaye ana uzoefu katika maeneo mbalimbali kama masoko, uhasibu na utawala.
Kama unataka kupata mbia kuwa makini kuepuka sababu nyingine zinazosababisha biashara kushindwa.
Kwa kufanya hivyo, biashara yako itakuwa yenye mafanikio.


0 Maoni:

Twitter Facebook