Thursday, April 4, 2013

Fanya biashara kuendana na wakati uliopo


WIKI iliyopita tuliona ni kwanini biashara inayoanza inashindwa kuingia kwenye ushindani kibiashara, na nini kifanyike ili kukwamua biashara hiyo.
Leo tutaangalia sababu nyingine inayokwamisha ama kuyumbisha biashara inayoanza.
Ni vema mfanyabiashara yeyote akajua muda wa bidhaa yake aliyonayo imetengenezwa lini na inakwisha lini matumizi yake ili kujua kucheza na soko lake.
Endapo umeanzisha biashara na hujafuatilia jambo hilo, inapofikia muda ambao bidhaa hizo zinakwisha muda wake, kwa vyovyote vile utapata hasara kwa kutojiandaa jinsi ya kukabiliana na hali hiyo.
vile vile inakupasa kuwapa wateja wako kile wanachokihitaji. hapa ninamaanisha kuwa, inapaswa uuze bidhaa iliyopo kwa wakati na inayokubalika. Si busara kuuza bidhaa yoyote ile bila kuangalia mfumo uliopo wa utandawazi.
Kama ni mfanyabiashara wa magari inabidi uuze magari ambayo yanaendana na wakati uliopo, kwa kufanya hivyo utateka soko lako kwa haraka.
Tofauti na hivyo, bidhaa utakazokuwa nazo zitapitwa na wakati kwa kukosa wateja, mwisho wa siku zinaondolewa sokoni, hivyo kusababisha biashara.
Katika miaka ya sasa, teknolojia imeleta mapinduzi ya haraka katika biashara. Hivyo kampuni mbalimbali zimekuwa zikiboresha bidhaa zake kila mara ili tu kuwaridhisha wateja wake.
Hali imefanya bidhaa nyingi kuonekana zipo nyuma ya muda wake kwa kuwa haziendani na wakati uliopo.
Ili kuliteka soko lako, inakubidi uwape wateja wako kile wanachokihitaji ambacho kipo kwa kipindi hicho. Kamwe usiache kuagiza biashara ile inayokubalika kwa kuwa, wateja nao hawataacha kuinunua.
Unachotakiwa kukifanya hapa ni kila mara kuiboresha bidhaa hiyo kutokana na wakati uliopo, ili kuipa thamani bidhaa hiyo.
Chukua mfano wa kampuni ya magari ya Toyota na Ford, ni miongoni mwa kampuni zinazofanya vizuri katika kuboresha bidhaa yake hiyo duniani.
Kampuni hizo hazisubiri mpaka watu wakayachoka magari yao, bali hubuni aina mpya ya magari na kuiweka sokoni. Kwa njia hii, magari ya kampuni hiyo yamekuwa yakipendwa na watu.
Inatakiwa uwe na sababu za kutosha za kuwafanya wateja wanunue bidhaa zako kuwashinda washindani wako.
Kumbuka kuwa wewe ni mtumishi, wateja wako ni mabosi. Biashara yako ipo kwa ajili ya kuwahudumia wateja na si wateja kuihudumia. Kama mtumishi unapaswa kufanya kama vile mabosi ambao ni wateja wako wanavyotaka ili kufanikiwa katika biashara hiyo.
Kosa jingine ambalo linayumbisha biashara ni mpangilio mbaya ama kutokuwa na mpangilio kabisa. Hali hii huifanya biashara ndani ya muda mchache kutokusonga mbele.
Mara nyingi mtu anapotaka kuanzisha biashara anakuwa anajiamini kwa asilimia mia kuwa atafanikiwa bila kufanya utafiti wa kutosha kwa kuangalia vitu vidogo vidogo vinavyoweza kukwamisha biashara hiyo.
Wafanyabiashara wengi badala ya kuiangalia biashara ile kwa karibu na uzalishaji wake unavyokwenda, anang’ang’ania kuangalia mambo ya kiutawala zaidi, kama vile majukumu ya viongozi, masuala ya kisheria na huduma nyingine baada ya mauzo.
Kwa biashara ya kawaida, kutumia muda mwingi kwa ajili ya kutuma nyaraka mbalimbali au kuzijaza, kuboresha ‘website’, kuzungumza na simu, kusikiliza malalamiko ya wateja, kujibu malalamiko hayo na shughuli nyingine, kama hujajiwekea mpango mzuri kwa shughuli zote hizo, utakosa wateja au hutazalisha kwa kuwa muda mwingi utaupoteza katika shughuli za kiutalawa kuliko kuangalia uzalishaji na uuzwaji wa bidhaa.
Jambo unalopaswa kulifanya kabla ya kuanza biashara yako ni kufanya utafiti wa mahitaji yote yanayohitajika. Kuwa na mbinu za kiutawala ili kwamba usipoteze muda mwingi katika eneo hilo na kupoteza wateja.
Hapa inapaswa kuajiri watu wengine ambao watahusika na masuala ya kiutawala na shughuli nyingine. Unaweza kuwapa mafunzo ili waweze kukuwakilisha pamoja na biashara yako.
Pia njia nzuri ya kuepuka kufanya vibaya katika biashara yako ni kuandika mpango mkakati wako. Kwa kufanya hivyo utafikia malengo uliyojiwekea.
Kwa kuweka mpango mzuri utajua ni majukumu gani yanakuhusu na yapi unaweza kuyaachia kwa wengine. usijifunge kwa shughuli unazoweza kuwapa wengine wakazifanya. Fanya vile tu unavyoweza kufanya.
Kama unafanya kazi zako mwenyewe ama una wafanyakazi wachache, weka taratibu nzuri za kiutawala utafanikiwa.


0 Maoni:

Twitter Facebook