Saturday, February 22, 2014

KWA NINI WATU WANAWAKATISHA TAMAA WENGINE?

FRANK John anasema, amekuwa akipata ujumbe mbalimbali kupitia simu ama barua pepe yake zikieleza kuwa kuna baadhi ya watu wamekuwa wakiwakatisha tamaa wengine wasifikie malengo ama mafanikio waliojiwekea.
 
Anasema sababu aliyoipata wakati anasoma ujumbe hizo ni kwamba baadhi ya wale wanaokatishwa tamaa wanawaamini hao wanaowakatisha tamaa.
 
Si vibaya kuwazungumzia hao wanaokukatisha tamaa, lakini pale unapoanza kujiuliza maswali baada ya kuzungumza nao jua kwamba uko kwenye hatari kubwa.
 
Njia inayoweza kukusaidia ambayo haitakudhuru kutokana na watu wa aina hiyo ni kutaka ujue kwa nini watu wanawavunja moyo ama kuwakatisha tamaa wengine.
 
Zipo sababu zinazowafanya baadhi ya watu kuwakatisha tamaa wengine.
 
Kwanza watu hao hawawezi kufanya mambo unayotaka kuyafanya., mfano “ Kama ninaamini kuwa siwezi kufanikiwa lakini ninafikiri kuwa wengine wana bahati hiyo, ndiyo maana ninapokutana na mtu ninayeamini anamafanikio ninaanza kumvunja moyo ama kumkatisha tamaa kutokana na imani yangu potofu,”.
 
Pili mtu wa aina hiyo anatishiwa na wewe kwa kila unachokifanya hata kama ni cha kawaida ambacho kama angejaribu kukifanya naye angefanikiwa.
 
Baadhi ya watu wanahisi kushindwa kufanya jambo pale wanapomwona mtu anajaribu kufanya kitu fulani. Kama wakati wote mtu fulani anataka kuwa tajiri lakini hajishughulishi kufanya shughuli binafsi, huhisi kutishika pale anapoona wewe unachukua hatua ya kuanza jambo la mafanikio.
 
Kutokana na hali hiyo, mtu wa aina hiyo hujaribu kukukatisha tamaa ili usiweze kuwa bora kumzidi yeye.
 
Sababu nyingine mtu wa aina hiyo anakuwa na wivu. Amini ama usiamini. Rafiki yako wa karibu anaweza kujaribu kukuvunja moyo kutokana na wivu alionao kwako. Kama anajihisi ni mnyonge kwako kwa jambo fulani ama kuna mambo unayoyafanya ambayo yeye hawezi kuyafikia hujaribu kukurudisha nyuma kutokana na wivu alionao.
 
Jambo jingine ni woga. Kuna mtu mmoja alitaka kuchapisha kitabu chake cha kwanza , hivyo alimwendea mshapishaji kwa makubaliano maalum kuwa atammalizia fedha zake atakapokiuza kitabu kile, lakini mshapishaji yule alimvunja moyo kuwa huchapisha vitabu vya siasa tu kwa kuwa ndivyo vina biashara. Lakini baadaye mtu huyo aliweza kuchapisha vitabu hivyo na kwa haraka alifanikiwa kuuza zaidi ya nakala milioni moja.
 
Anasema aligundua kuwa, mchapishaji yule aliogopa kupata hasara kwa sababu alimwona kuwa ni kijana, pia alidhamiria kumuangusha asisonge mbele.
 
Sababu nyingine ni kuchukiwa. Kama mtu anakuchukia hataki kukuona ukiendelea katika jambo lolote na ndio maana atajaribu kukuvunja moyo pale anapopata nafasi. Kuwa makini na maadui wa aina hiyo.
 
Vile vile watu wa aina hiyo hawakupi taarifa sahihi. Watu wengi wanapenda kusema ‘sijui’ wanapoulizwa jambo fulani. Wanakuwa hawana elimu muhimu kuhusu kile unachokipanga kukifanya hivyo kurudisha nyuma kwa kusema hawajui.
 
Jambo lingine ni kwamba watu wa aina hii hawawezi kuiona picha halisi uliyonayo juu ya mipango yako. Baadhi yao watakukatisha tamaa kwa kuwa tu hawaelewi picha unayoipanga katika maisha yako.
 
Sasa basi ni jinsi gani unaweza kuwazuia watu wasikukatishe tamaa.
Kuna mambo mawili unahitaji kuyafanya ili kuzuia hali hiyo. jambo la kwanza ni kutokuzungumza kuhusu mipango yako isipokuwa kwa mtu yule ambaye unadhani kuwa anakupenda kwa dhati. Kama utafanya kinyume na hapo utakuwa ukivunjwa moyo na watu wa aina hiyo kila mara.
 
Jambo la pili ni kuonyesha kuwa jambo ulilokusudia kulifanya unalishikilia hilo hilo mpaka linafikia mwisho na mafaniko yake unayaona. Kutokana na sababu hiyo wale wanaokurudisha nyuma wataanza kukuamini na kile unachokisimamia ni sahihi.
 
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa mtandao.
 
mwisho

JINSI GANI YA KUFANYA KAZI NA ANAYEKUCHUKIA

JE unawezaje kushughulika na mtu anayekuchukia kazini? Hilo ndilo swali la msingi la kujiuliza. Na jinsi gani unaweza kuzuia usichukiwe na wafanyakazi wengine.
 
Kila mmoja ana hisia ambazo zinaweza kumwongoza afanye jambo Fulani ama asilifanye, kwa ajili ya kuzuia ghadhabu au kutokuelewana kusitokee.
 
Sasa ni kwa jinsi gani unaweza kushughulika na mtu anayekuchukia katika eneo la kazi.
 
Kuchukiwa ni hisia iliyopo kwa mtu ambayo mtu huyo anayemchukia mwingine badala ya kumpiga anamalizia hisia hizo kwa kumchukia.
 
Hii inamaanisha kuwa, kama kuna mtu anakuchukia kazini inaonyesha kuwa,  wewe ni mtu wa muhimu hivyo anatumia mbinu hiyo kukudhoofisha kisaikolojia.
 
Inakuaje akili ya huyo anayekuchukia inajiridhisha kuwa wewe ni adui wake wa kwanza? Na kwa nini anakuchukia hata kama hujafanya jambo baya kwake?
 
Wakati mwingine wewe unayechukiwa inawezekana umefanya jambo ambalo ni baya bila kujitambua. Kwa mfano imefikia mahali ukaonekana una akili kupita kawaida ambapo unaitumia akili hiyo  katika eneo la kazi watu wakuogope. Kutokana na hali hiyo ukachukiwa, hakikisha hauonyeshi hisia zako pindi unapochukiwa.
 
Hivyo, yule au watu wale wanaokuchukia eneo la kazi wataweza kuficha hisia zao hizo kwa kuwa wametambua wewe sio mtu mbaya kwao. Mtu anaweza kukuchukia katika kazi kutokana na wivu, kutokujiamini ama hofu.
 
 
Hali halisi inaonyesha kuwa, mtu ama watu wanaweza kukuchukia bila sababu kwa kuwa unawafanya wawe na hofu kila wanapokuona.
 
Ili kushughulika na watu wa aina hiyo ni lazima kwanza utafute sababu inayowafanya wakuchukie na kuonyesha kuwa hujali.
 
Ni jinsi gani utawazuia watu wasikuchukie katika eneo la kazi.
Kwa mfano umejua kuwa Fulani anakuchukia katika kazi kwa sababu anakuonea wivu, katika hali ya namna hii, unaweza kumsaidia mtu huyo nje na kazi kulainisha hali yake ya kuwa na wivu na kumpunguzia asikuchukie.
 
Ni muhimu sana kutokujifanya una akili sana mbele ya wale ambao hawatambui hilo , na wale ambao wanaweza kujenga chuki kwa ajili hiyo.
 
Pia epuka kujionyesha kuwa una mafanikio zaidi au mwenye akili, ili usijenge maadui wengine bila kujijua au kuwafanya watu wengi wakuchukie katika eneo la kazi bila kufanya jambo lolote baya.
 
Wakati mwingine unashauriwa kufanya makosa madogo madogo mbele ya watu wa aina hiyo ili tu kuwachanganya kwenye mafanikio uliyo nayo kiuhalisia.
 
Pia usijiweke wazi wakajua mipango yako uliyonayo wala kulinganisha ndoto zako kubwa ulizonazo kwa mawazo yao madogo waliyonayo.
 
Ushauri mwingine ni kutokujali mazingira ya namna hiyo, kikubwa kwako ni kusonga mbele.
 
Pia pale unaposulubiwa kwa jinsi yoyote ile onyesha kuwa hujali, we endelea kufanya kile unachotakiwa kukifanya.
 
Kanuni ya kukumbuka ni kwamba, simamia kile unachokiamini, hivyo tabia ya mtu mwingine isikusumbue, chukua muda kumfahamu vizuri mtu huyo na historia yake, pia kile kinachomfanya awe hivyo.
 
Kamwe unapokumbana na adha katika kazi, usitake kufanya ushindani na yule anayekutendea mabaya ili kujiepusha na migongano.
 
mwisho

Thursday, April 4, 2013

Hizi ndizo njia za kufanikiwa kibiashara


ILI ufanikiwe katika biashara yako inakubidi uwe na jitihada za ziada.
Kadiri mtu anavyoongeza jitihada katika usimamizi wa biashara yake, ndivyo anavyopata mafanikio.
Inapaswa kutumia jitihada za kiakili na kimwili.
Watu wengi huanza biashara baada ya kuchoka kutokana na kufanya kazi aliyoajiriwa kwa muda mrefu au kupata ‘presha’ kutoka kwa bosi wake ofisini.
Hivyo fikra kubwa aliyonayo ni kwamba katika biashara yake anakwenda kupumzika kwa kuwa ana wasaidizi, kazi yake itakuwa ni kusaini hundi tu.
Mwisho anakuja kushtukia hakuna biashara inayoendelea kwa kuwa hakuonesha jitihada tokea mwanzo.
Kumbuka kuwa kufanya biashara si jambo rahisi, linahitaji nidhamu ya hali ya juu katika utendaji kazi.
Uanzishwaji na ukuaji wa biashara unahitaji muda mwingi zaidi ya wengi wanavyodhani.
Hapo inabidi ufanye kazi muda mwingi, na kubakia na fedha kidogo za matumizi ya nyumbani, hadi pale biashara yako itakapoimarika.
Biashara inahitaji nidhamu ya hali ya juu, hata kama hakuna mtu anayekufuatilia au kukuonya pale unapokosea.
Inakupasa kuwa kwenye biashara yako kama ulivyojipangia ratiba yako ya kila siku.
Watu watakuwa wanakutafuta, pale wanapokuhitaji inabidi wajue unapatikana muda gani, unapokosekana unawavunja moyo wateja wako na kukosa fursa ambazo zingekupatia faida.
Pia inakubidi kutumia muda wa ziada na rasilimali zaidi endapo mauzo yako hayaendi vizuri.
Fanya soko au biashara yako ionekane kwa wateja wako.
Pia ni vizuri katika biashara unayoifanya, isihusishwe na familia yako. Hapa inamaanisha hata kama unafanya biashara, endapo mwanafamilia atahitaji kitu itambidi akinunue sio kuchukua bure.
Kuruhusu biashara yako iwe holela kwa familia, kutafanya ifilisike baada ya muda mfupi.
Ni vema kuweka muongozo mzuri kwa familia yako ili jambo hili liendelee.
Ushauri mwingine ni kwamba, ili biashara yako isonge mbele inakubidi uwe mvumilivu.
Ni kawaida biashara yoyote haiwezi kukua kwa siku moja. Inachukua muda kueleweka kwenye soko, kukubalika na wateja na kuweka mtandao safi.
Inabidi uwe imara katika malengo uliyojiwekea katika kipindi kigumu utakachokipitia.
Biashara nzuri ni kama miti mizuri inayochukua muda kukua. Lakini pale inapokuwa inastahimili kimbunga cha aina yoyote.
Na kama unaijenga biashara yako katika eneo lenye misukosuko ya kibiashara inakubidi uandae msingi imara unaohitaji uvumilivu.

Mjasiriamali yeyote anaweza kufanikiwa


WATU wengi wameshindwa kuendelea mbele katika shughuli zao za kijasiriamali kutokana na changamoto wanazokabiliana nazo kibiashara.
Lakini ukweli ni kwamba mjasiriamali yeyote anaweza kufanikiwa katika biashara yake kama atafuata sheria na kanuni za kibiashara, ikiwemo kupata mafunzo ya ujasiriamali.
Kama unafanya biashara ambayo wateja wanapata huduma wanazohitaji kwa urahisi, ama michezo au sehemu ya kusoma barua pepe zao na kufanya shughuli nyingine zinazohusu mtandao, unakuwa kwenye nafasi ya mafanikio.
Lakini kama unapata eneo ambalo silo, utajikuta unafunga haraka biashara hiyo tofauti na matarajio uliyokuwa unayategemea.
Biashara nyingi zinafungwa ama kuwa na mafanikio, kutokana na msingi wa eneo iliyopo.
Kama eneo hilo ni zuri pia linavutia, watu wengi watafika kwa kuwa wanapenda vitu vizuri, huduma nzuri kwa wateja ama ubora wake.
Lakini kama eneo hilo si zuri, inahitajika nguvu ya ziada kwa ajili ya kuwashawishi wateja kufika, ambapo itakubidi bidhaa ziwe za gharama ndogo na kufanya jitihaza zaidi za ushawishi ili watu waweze kufika.
Nini kifanyike? Inabidi uchague eneo zuri kuliangana na aina ya biashara yako. Hakuna eneo zuri au baya, hata kama unafanya shughuli zako nyumbani mbali na wateja wako, patakuwa ni pazuri kwa baadhi ya biashara.
Itengeneze biashara yako kutokana na asili yake na kwa walengwa wako.
Katika hilo ni vema ukazingatia miundombinu, ulinzi na wasambazaji wako.
Wakati mwingine inapendeza kama utaanzisha biashara yako kwenye eneo ambalo biashara kama hiyo ipo. Kwa kuwa tayari eneo hilo litakuwa limeshazoeleka kwa bidhaa ya aina hiyo au huduma hiyo.
Pamoja na ushindani utakaokabiliana nao, utakuwa umepata mafanikio kwa kuwa eneo hilo tayari litakuwa la kibiashara.
Eneo zuri ni gharama, pia ni vigumu kulipata. Lakini pale unapolipata, unapunguza gharama za soko. Sio busara kufanya biashara katika eneo unalolipa gharama ndogo, ambapo matokeo yake unapata wateja ambao kazi yao ni kufanya utalii sio kununua.
Sababu nyingine ambayo inasababisha biashara nyingi kushindwa, zinakuwa hazianzishwi na wajasiriamali bali wataalamu mbalimbali ambao wanafikiri kuwa ni wajasiriamali.
Kinachofikiriwa hapa ni kwamba, kama mtu anajua kutengeneza bidhaa kitaalamu, anadhani kuwa anaweza kufungua na kuiendesha biashara bila kuwa na utaalamu wa kibiashara, lakini hili halina ukweli wowote, matokeo yake biashara inakwama.
Biashara nyingi zinakwama kwa kuwa wajasiriamali wengi hawana ujuzi.
Mjasiriamali yeyote anapaswa kuwa na ujuzi wa kibiashara, uelewa wa bidhaa zake anazozizalisha zinapopatikana pamoja na watu sahihi atakaoweza kuwatumia katika shughuli yake hiyo.
Kwa mfano, uendeshaji wa biashara ya shule ni zaidi ya kuwa mwalimu mzuri wa kufundisha. Kujua jinsi ya kutengeneza nywele haimaanishi kuwa unaweza kuendesha biashara ya saluni. Ama kuwa daktari mzuri haimaanishi kuwa unaweza kumiliki hospitali.
Kuanzisha shule hakumaanishi kunahitaji walimu wa ufundishaji tu, na saluni ni zaidi ya kutengeneza nywele, na hospitali sio tu kwa ajili ya kutibu wagonjwa.
Mauzo na masoko, mahesabu na kuwajali wateja ni zaidi ya shughuli zinazochangia mafanikio ya biashara.
Zaidi ya yote, unaweza kujua jinsi ya kutengeneza nywele lakini unakuwa dhaifu katika eneo la masoko au msimamizi mzuri wa fedha. Matokeo yake huwezi kupata wateja wa kutosha au kusimamia shughuli za kifedha, hivyo biashara kuyumba.
Kama wewe una fani yako halafu unataka kuanzisha biashara inayoendana na fani uliyonayo, usidhani kuwa unajua kila kitu. Pata muda wa kusoma jinsi ya kuendesha biashara, masoko, huduma kwa wateja na shughuli nyingine za kibiashara.
Njia nyingine ni kutafuta mbia ambaye ana uzoefu katika maeneo mbalimbali kama masoko, uhasibu na utawala.
Kama unataka kupata mbia kuwa makini kuepuka sababu nyingine zinazosababisha biashara kushindwa.
Kwa kufanya hivyo, biashara yako itakuwa yenye mafanikio.


Fanya biashara kuendana na wakati uliopo


WIKI iliyopita tuliona ni kwanini biashara inayoanza inashindwa kuingia kwenye ushindani kibiashara, na nini kifanyike ili kukwamua biashara hiyo.
Leo tutaangalia sababu nyingine inayokwamisha ama kuyumbisha biashara inayoanza.
Ni vema mfanyabiashara yeyote akajua muda wa bidhaa yake aliyonayo imetengenezwa lini na inakwisha lini matumizi yake ili kujua kucheza na soko lake.
Endapo umeanzisha biashara na hujafuatilia jambo hilo, inapofikia muda ambao bidhaa hizo zinakwisha muda wake, kwa vyovyote vile utapata hasara kwa kutojiandaa jinsi ya kukabiliana na hali hiyo.
vile vile inakupasa kuwapa wateja wako kile wanachokihitaji. hapa ninamaanisha kuwa, inapaswa uuze bidhaa iliyopo kwa wakati na inayokubalika. Si busara kuuza bidhaa yoyote ile bila kuangalia mfumo uliopo wa utandawazi.
Kama ni mfanyabiashara wa magari inabidi uuze magari ambayo yanaendana na wakati uliopo, kwa kufanya hivyo utateka soko lako kwa haraka.
Tofauti na hivyo, bidhaa utakazokuwa nazo zitapitwa na wakati kwa kukosa wateja, mwisho wa siku zinaondolewa sokoni, hivyo kusababisha biashara.
Katika miaka ya sasa, teknolojia imeleta mapinduzi ya haraka katika biashara. Hivyo kampuni mbalimbali zimekuwa zikiboresha bidhaa zake kila mara ili tu kuwaridhisha wateja wake.
Hali imefanya bidhaa nyingi kuonekana zipo nyuma ya muda wake kwa kuwa haziendani na wakati uliopo.
Ili kuliteka soko lako, inakubidi uwape wateja wako kile wanachokihitaji ambacho kipo kwa kipindi hicho. Kamwe usiache kuagiza biashara ile inayokubalika kwa kuwa, wateja nao hawataacha kuinunua.
Unachotakiwa kukifanya hapa ni kila mara kuiboresha bidhaa hiyo kutokana na wakati uliopo, ili kuipa thamani bidhaa hiyo.
Chukua mfano wa kampuni ya magari ya Toyota na Ford, ni miongoni mwa kampuni zinazofanya vizuri katika kuboresha bidhaa yake hiyo duniani.
Kampuni hizo hazisubiri mpaka watu wakayachoka magari yao, bali hubuni aina mpya ya magari na kuiweka sokoni. Kwa njia hii, magari ya kampuni hiyo yamekuwa yakipendwa na watu.
Inatakiwa uwe na sababu za kutosha za kuwafanya wateja wanunue bidhaa zako kuwashinda washindani wako.
Kumbuka kuwa wewe ni mtumishi, wateja wako ni mabosi. Biashara yako ipo kwa ajili ya kuwahudumia wateja na si wateja kuihudumia. Kama mtumishi unapaswa kufanya kama vile mabosi ambao ni wateja wako wanavyotaka ili kufanikiwa katika biashara hiyo.
Kosa jingine ambalo linayumbisha biashara ni mpangilio mbaya ama kutokuwa na mpangilio kabisa. Hali hii huifanya biashara ndani ya muda mchache kutokusonga mbele.
Mara nyingi mtu anapotaka kuanzisha biashara anakuwa anajiamini kwa asilimia mia kuwa atafanikiwa bila kufanya utafiti wa kutosha kwa kuangalia vitu vidogo vidogo vinavyoweza kukwamisha biashara hiyo.
Wafanyabiashara wengi badala ya kuiangalia biashara ile kwa karibu na uzalishaji wake unavyokwenda, anang’ang’ania kuangalia mambo ya kiutawala zaidi, kama vile majukumu ya viongozi, masuala ya kisheria na huduma nyingine baada ya mauzo.
Kwa biashara ya kawaida, kutumia muda mwingi kwa ajili ya kutuma nyaraka mbalimbali au kuzijaza, kuboresha ‘website’, kuzungumza na simu, kusikiliza malalamiko ya wateja, kujibu malalamiko hayo na shughuli nyingine, kama hujajiwekea mpango mzuri kwa shughuli zote hizo, utakosa wateja au hutazalisha kwa kuwa muda mwingi utaupoteza katika shughuli za kiutalawa kuliko kuangalia uzalishaji na uuzwaji wa bidhaa.
Jambo unalopaswa kulifanya kabla ya kuanza biashara yako ni kufanya utafiti wa mahitaji yote yanayohitajika. Kuwa na mbinu za kiutawala ili kwamba usipoteze muda mwingi katika eneo hilo na kupoteza wateja.
Hapa inapaswa kuajiri watu wengine ambao watahusika na masuala ya kiutawala na shughuli nyingine. Unaweza kuwapa mafunzo ili waweze kukuwakilisha pamoja na biashara yako.
Pia njia nzuri ya kuepuka kufanya vibaya katika biashara yako ni kuandika mpango mkakati wako. Kwa kufanya hivyo utafikia malengo uliyojiwekea.
Kwa kuweka mpango mzuri utajua ni majukumu gani yanakuhusu na yapi unaweza kuyaachia kwa wengine. usijifunge kwa shughuli unazoweza kuwapa wengine wakazifanya. Fanya vile tu unavyoweza kufanya.
Kama unafanya kazi zako mwenyewe ama una wafanyakazi wachache, weka taratibu nzuri za kiutawala utafanikiwa.


Twitter Facebook