Thursday, February 12, 2009

MARAFIKI WANAWEZA KUWA KIKWAZO CHA MAFANIKIO YAKO

KARIBU mpenzi msomaji katika safu hii ya Maisha Yetu inayokujia kila Alhamisi. Madhumuini makubwa ya safu hii ni kukuelimisha, kukukosoa na kukujenga kiuchumi. Leo utaona ni jinsi marafiki wanavyoweza kuwa kikwazo cha mafanikio yako.
Endapo utapata nafasi ya kutulia na kutafakari marafiki ulio nao, utagundua kuwa una nafasi kubwa ya wewe kusimamia mambo yako mwenyewe.
Nimeanza kwa kusema hivyo kwa sababu mara nyingine rafiki yako ndiye anayekuwa kikwazo cha mafanikio yako kwa kukurudisha nyuma fikra zako kimaendeleo.
Rafiki huyo badala ya kukusaidia kimawazo, atakushawishi muende maeneo ya starehe mara nyingine unapotaka kufanya jambo hukukatisha tamaa kwamba hutafanikiwa na kukutolea mifano ya watu walioshindwa katika maisha yao.
Ieleweke wazi kuwa kwenda katika maeneo ya starehe si vibaya, maadamu ujue unakwenda pale kwa malengo. Sasa basi kupitia marafiki zako, utaweza kugundua mambo wanayoyapenda na shughuli wanazopenda kuzifanya zinazofanana na za kwako.
Vile vile ukiwaangalia kwa makini marafiki zako, utagundua kama wanastahili, wana ujasiri, furaha na wenye kupenda mafanikio yako, hapo ndipo utakuwa na uhakika kwamba unachanganyika na watu wa aina gani.
Endapo utagundua rafiki zako mawazo yao hayaendani na mawazo yako, ni vema ukaamua kuachana nao ili wasiweze kukukwamisha katika mipango yako.
Mtaalamu mmoja wa saikolojia, Dk. Freud, anasema kuna aina mbili za watu katika dhana ya mafanikio. Wapo wale wanaojiona kana kwamba wameshindwa kimaisha na wale wanaopenda kuwa na mafanikio kwa kufanya bidii.
Wale wenye mawazo ya kushindwa hujiona wanavuka hatua moja na kwenda hatua nyingine ya kushindwa, wale wanaopenda kufanikiwa hupiga hatua moja kila siku. Hujiambia nafsini mwao kwamba hawawezi kushindwa. Kuna msemo usemao ‘ tajiri atazidi kuongezewa na masikini hata kile kidogo alichonacho atanyang’anywa’.
Hivyo basi, utaona kuwa matajiri hufikiria utajiri, masikini hufikiria umaskini na kila mmoja anapata kile anachokifikiri. Kwa mtu anayependa kuwa na maisha ya mafanikio, ni vema akasimamia maisha yake katika kuyaandaa maisha yake ya baadaye anayoyapenda.
Usifikirie mambo ya zamani kwa kuwa yameshapita. Usipoteze muda na nguvu zako kwa makosa yaliyopita yalioyokufanya ukapoteza bahati yako.
Ni vyema katika maisha ukajua kuwa unasimamia mambo yako ya sasa na ya baadaye kwa kusimamia nia yako, wazo, hisia na imani kuhusu wewe, vitu na watu wengine.
Maisha bora kwako yatatokana na jitihada zako unazozifanya.Yale unayoyafikiria siku ya leo ndiyo yatakayofanyika siku ya kesho. Unajitengenezea mafanikio ya baadaye kwa kukuza fikra zako leo.
Kumbuka kuwa leo si jana. Kuna mabadiliko makubwa. Ni vema kujiuliza mabadiliko hayo ni kwa vipi? Unaweza kupata jawabu kuwa, mabadiliko hayo ni jinsi akili zetu na fikra zetu zinavyofanya kazi. Kwani mara nyingine mabadiliko huweza kuwa maumivu, lakini baadaye huwa ni faraja.
Kumbuka mabadiliko yoyote ni msingi wa mafanikio yako. Ni kweli kwamba watu wengi hawapendi mabadiliko si tu katika maisha yao lakini hata kwa maisha ya wengine. Wamekuwa waking’ang’ania mambo yaliyopita, wanakata mawazo mapya na changamoto mpya.
Mawazo hayo yanaondoa ubunifu ambao umekuwa ukija akilini mwake. Kumbuka wewe si yule uliyekuwa, hivyo, mwezi uliopita au mwaka uliopita. Kila dakika ya kila saa ya kila siku asili ya fikra zako hukua. Unakua kiakili, kiroho na kimaumbile.
Kile unachopanda ndicho unachovuna. Kama unajijengea mawazo ya utajiri, upendo na furaha hisia zako ndizo zitakavyokuwa. Ili uwe imara na maisha yako ni vyema kujiuliza maswali yafuatayo.
Kwa nini nipo hapa nilipo? Wapi ninakwenda na ni mahitaji gani ninayoyataka kubadili maisha ninayotaka kuishi? Ni vyema kuliangalia jibu lako kwa umakini - kutoka hapo ndipo utakapoweza kuchora ramani halisi ya maisha yako unayoyataka.
Tukutane wiki ijayo

Friday, February 6, 2009

KUFANIKIWA AU KUTOFANIKIWA NI UCHAGUZI WAKO

KARIBUNI wasomaji katika safu hii, leo tutazungumzia kufanikiwa au kushindwa ni uchaguzi wako mwenyewe.
Kumbuka umebarikiwa kuwa na uhuru wa maamuzi, kama vile kuchagua aina ya maisha unayotaka kuishi.
Kama hivyo sivyo, huwezi kuwa na uwezo wa kutumia vipaji vyako ulivyonavyo.
Fahamu kuwa, akili uliyonayo ni nyenzo muhimu ya kukufanya ufanikiwe, kwa kufikiri na kutumia vipaji ulivyo navyo kisha kuvifanyia kazi.
Kwa kuwa mafanikio yako yanatokana na akili yako uliyonayo. Endapo utatumia akili, hisia na imani yako kwa busara na kufanyia kazi, ni lazima maisha yako yatakuwa na mabadiliko makubwa ya mafanikio.
Una uhuru wa kuchagua namna unavyofikiri, unavyohisi na unavyoamini ili uweze kusonga mbele, kamwe usikubali kuwa na fikra mgando ambazo hazitakusogeza hapo ulipo.
Mafanikio au kushindwa kwako inategemea jinsi unavyofikiri.
Kwani afya isiyo njema, hali ya kutokuwa na furaha na umaskini, hizo ni dalili za kushindwa katika maisha ambazo zimesababishwa na kuwaza mawazo hasi.
Vile vile akili yenye afya bora na mawazo ya matumaini yanakufanya uwe na afya bora na maendeleo mazuri.
Safisha akili yako kwa mawazo mazuri. Siri ya kushinda katika maisha ni kusafisha akili kwa kuondoa tabia zinazokufanya uharibikiwe, kama vile imani potofu, mawazo hasi na badala yake uwe na tabia zenye kukufanya usonge mbele, kuwa na imani na mawazo ya kujenga na si kukubomoa.
Mara zote kuwa na mawazo ya kukujenga kwa mfano iambie nafsi yako kwamba, utafanikiwa katika mambo yote uliyopanga kufanikiwa.
Mara zote jione upo imara katika kufanikisha mipango yako mbalimbali, uwe mtu unayependa kuwajali wengine, uwe mwaminifu katika shughuli zako pamoja na familia yako.
Ukweli, ushindi na ujasiri ni silaha kubwa ya mafanikio katika maisha yako.
Kamwe usiruhusu mawazo ambayo hayana tija ya maendeleo kwako.
Jifunze kuwa jasiri, usikate tamaa, kuwa mtu mwenye msimamo, penda kwenda na wakati, usilewe na usiwachukie washirika wako katika biashara.
Njia yoyote ya kubadili hali yako ya kushindwa katika maisha ni kubadili mawazo hasi unayofikiria, utakapofanya hivyo utabadili tabia ya kufikiri, kuhisi na kuamini. Utakapobadili tabia yako ya ndani, hata tabia yako ya nje itajibadili.
Mawazo yana nguvu. Mawazo ya hofu na wasiwasi ni njia ya kushindwa. Utakaposhinda hali ya kutokuwaza kushindwa, kuwa na hofu au wasiwasi utaweza kukabiliana na hali ya ushindi.
Kuna kanuni moja inayotawala mawazo. Huwezi kufikiri kitu hiki na kuzalisha kingine.
Mara kwa mara, hali ya kushindwa inaweza kukujia ili kukujaribu. Ni wakati wako wa kutumia akili kwa vitendo ili uishinde hali hiyo.
Madhara ya kushindwa katika maisha yanaweza kukuletea hali ya uharibifu, imani potofu na mawazo hasi pamoja na hisia za maisha yako.
Kwa maelezo mengine, hali hiyo inakufanya ukose furaha, uwe mpweke, kukosa adabu, kuwa na uamuzi mbaya, magonjwa ya mara kwa mara yasiyoeleweka, kuchanganyikiwa na hali ya kushindwa.
Hali ya kufanikiwa inakufanya uwe na furaha, maendeleo mazuri, kujiamini, matumaini, amani katika moyo, umoja katika familia, mafanikio kibiashara, busara, ukweli na upendo.
Tukutane wiki ijayo.

KILA MTU ANAWEZA KUFANIKIWA

KARIBUNI wapenzi wasomaji katika siku nyingine ambayo Mwenyezi Mungu ametujalia kuiona. Leo katika safu yetu hii tunaangalia ni jinsi kuweza kufanikiwa.
Kumbuka ni juu yako kuchagua kama unataka kufanikiwa, kwani huwezi kupata mafanikio yoyote kwa kuangalia mambo yaliyopita ambayo hayakukuendea vizuri.
Ni vema ukimtegemea Mungu pamoja na kuongeza bidii kwa akili na ujuzi aliokupa. Usimtegemee mwanadamu yeyote katika kufanikisha mambo yako kwani atakukatisha tamaa.
Kama mwanadamu mwenye akili timamu, una uhuru wa kuchagua jambo unalohitaji. Ni vema ukachagua afya, furaha pamoja na kupata mafanikio. Ili ufanikishe malengo yako ni lazima uwe na mpango na siyo kufanya jambo kwa kubahatisha.
Kwani kila mmoja anao uwezo wa kufanikiwa, endapo atakuwa na mipango kamilifu. Kumbuka kila jambo unalolifanya ni kwa mpango maalumu, hivyo unatakiwa kulifanya katika mpango mzuri uliojiwekea ndipo litakapokuwa la ufanisi.
Ni jinsi gani unaweza kupanga utaratibu wa maisha yako vizuri. Ni pale unapokuwa na utaratibu mzuri uliojiwekea, kwani haiwezekani jua likawaka usiku, au mwezi kuwaka mchana, kila kitu kilicho na mafanikio maishani kinakuwa kimepangwa.
Hakuna kitu kilichokuwa na mafanikio bila kuwepo kwa mpangilio. Vile vile si rahisi kufanikisha malengo yoyote ya maisha kwa wakati unaohitaji pasipo kuwa na mpangilio. Kwa kuwa, wote waliofanikiwa walipangilia maisha yao.
“Mafanikio ya kuondoka kwa ndege yametokana na ubunifu wa mtu wa kuangalia mfano wa ndege wanaoruka angani. Mfano mwingine ni wa kompyuta, haiwezi kufanya kazi katika eneo lenye joto, kwani itashindwa kufanya kazi inavyotakiwa na ndiyo maana ikatengenezewa mpango (programu).
Vile vile hakuna watu wanaooana bila kuwapo kwa mipango, naamini hufanya mipangilio kabla ya kuchukua hatua hiyo. Chagua sasa njia zilizo sahihi za kupanga maisha yako. Acha kuwa kama meli isiyokuwa na usukani katika bahari iliyo na mawimbi.
Maisha ni mchezo unaohitaji ubunifu. Kwa kuwa na mipango ya ndoto zako, na kuwa na hamu ya kupata unachokikusudia , epuka hali ya mazoea, kukata tamaa na kushindwa.
Hatua muhimu za kufanya ufanikiwe
Kwanza ni vema kutunza kumbukumbu za maisha yako ya kila siku. Kwa kuwa ni vigumu kukumbuka kila kitu kinachotokea kwa kila siku. Vile vile, kutunza majina ya watu wote unaokutana nao kwa siku, maeneo uliyopita, vitu ulivyoambiwa au ulivyojifunza.
Hivyo, tabia ya kukusanya ujuzi na kuuhifadhi kwa ajili ya kumbukumbu za siku zijazo ni utajiri mzuri na inalipa. Hatua ya pili kuwa mtu unayependa kunukuu. Kuwa na kitabu cha kuhifadhia kumbukumbu na andika mawazo mbalimbali yanayokuvutia.
Utakuwa unajifunza njia mbalimbali za mafanikio kutoka kwenye mijadala mbalimbali unayohudhuria. Andika kwenye kitabu chako kwa ajili ya siku zijazo.
Nyingine ni kuhifadhi makala za jinsi ya kufanikiwa zinazokuvutia kutoka kwenye magazeti au majarida mbalimbali, hiyo itakusaidia katika kukabiliana na changamoto za mafanikio katika maisha yako.
Kumbuka, vitabu vizuri vinavyokusaidia kuwa na uwezo wa kufikiri. Vinakusaidia kuwa mbunifu wa mawazo na hisia kuhusu wewe, vitu na wengine. Vitabu vizuri vinakuwezesha uweze kufanikiwa. Ni nyenzo nzuri kwa yeyote anayetaka kusonga mbele kimaendeleo. Kupitia vitabu hivyo ni njia rahisi ya kukuelimisha.
Soma kitabu chochote kinachokuwa rahisi kwako kukinunua. Kama bajeti yako inakuzuia kununua vitabu vizuri mbalimbali, ni vema ukaazima. Kuwa na tabia ya kujisomea angalau kwa nusu saa kila siku. Anza kwa kusoma magazeti na majarida. Endelea kwa vitabu vinavyochochea mafanikio, au kukupa uwezo mkubwa wa kuelewa maisha.
Kuwa na maktaba yako binafsi, kwa kuwa ni hazina nzuri. Katika maktaba yako, weka vitabu vizuri vya maendeleo. Kwa kuwa, ni mtaji wako mkubwa wa mafanikio. Jivunie maktaba yako, ongeza vitabu kadiri uwezavyo. Usiviache vikaharibika na kupata vumbi, chukua mawazo yote mazuri na uyafanyie kazi.

Tuesday, January 27, 2009

UKIWEKA NIA UTAFANIKIWA

MIUJIZA inaweza kutokea kwenye maisha yako wakati unapotumia akili katika njia ya kukubali. Na pale unapotambua kwamba kitu pekee kitachokutenganisha kutoka kwenye mafanikio au kushindwa ni vile unavyofikiri, unavyohisi na kuamini.
Kama unavyofikiri na kuamini kila saa ya kila siku, unakuwa tayari umeshapanda mbegu ya mafanikio au kushindwa katika mawazo yako.
Amini kuwa kufikiri na kuhisi kunakuletea mafanikio. Unaweza kuwa na vipaji vingi vya asili vinavyosubiri kuendelezwa, jitahidi kuvivumbua.
Amini kuwa vipaji vyako ni vya thamani na unaweza kuvitimiza kwa kuvifanyia kazi. Amini kushinda mara kwa mara katika vita ya ushindi.
Ni bora kuwa na imani ndogo ya kufanya jambo kuliko kukosa kabisa. Huwezi kuwaza mara moja kuwa unataka kuhamia kwenye nyumba mpya bila kufanya maandalizi.
Lakini unaweza ukapata wazo hilo, ukalipangilia, ukachukua hatua na mwishoni ukapata matokeo mazuri. Unaweza kuwa na mawazo mazuri yaliyojaa utajiri katika maisha yako, afya njema na furaha kubwa kwa kumwamini Mungu.
Maendeleo hutokana na changamoto mbalimbali unazo kabiliana nazo. Unaweza kukua kwa kukutana na changamoto hizo na hapo ndipo utakapopata mafanikio, japo kwenye mafanikio vikwazo mbalimbali hutokea lakini inakubidi usikate tamaa.
Chukua changamoto mbalimbali kama mafanikio. Unapokutana na changamoto katika kupata mafanikio yako kabiliana nazo utashinda.
Mafanikio huja wakati unafanya jambo lenye ubunifu. Hujaumbwa kwa ajili ya hali fulani, bali umeumbwa kama wakala uliye huru wa maamuzi yako ambayo yako ndani ya uwezo wako.
Ukiwa na mawazo, malengo na changamoto za mafanikio ndipo utakapofanikiwa. Unafanya shughuli yoyote kwa ajili yako mwenyewe.
Izoeshe akili yako ikubali ukweli kuwa kila unalolipanga unalitimiza kwa kuchukua hatua zote muhimu kuanzia hapo ndio utakapoona mafanikio yako.
Kushindwa mara moja haimaanishi kwamba utashindwa siku zote, si kwamba mmoja anapofanikiwa atakuwa na mafanikio ya kudumu mpaka pale atakapotumia mafanikio hayo kwa kupiga hatua zaidi.
Maisha ni hatua.
Umezaliwa ushinde na utashinda kama utaamini ukweli huo. Ni asili ya mwanadamu kuwa na hali ya wasiwasi. Wasiwasi juu ya familia yake, majirani zake, kazi yake na maisha yake. Kumbuka wasiwasi unasababisha hofu na ndiyo chanzo kikuu cha kushindwa.
Unapokuwa na hofu juu ya siku ya kesho, haileti maana kwani hujui siku ya kesho itakavyokuwa kwako. Usiishi kwa ajili ya kesho, bali kwa ajili ya siku iliyopo yaani leo.
Kama una wasiwasi juu ya yatakayotokea kesho, mwezi ujao au mwaka ujao, unajiweka katika hali ya kushindwa katika mafanikio yako kwa kuvuruga mawazo mazuri uliyojipangia.
Kamwe usifikiri kuhusu matatizo ya kesho, ishi siku ya leo kwa kufanya mipango mizuri uliyoipanga. Huwezi kufanikiwa kama unakaribisha wasiwasi au hofu katika maisha yako. Kama una wasiwasi wa ratiba yako uliyoipanga kwa siku zijazo, ni kupoteza nguvu zako.
Shughulika na mambo yale ambayo ni ya muhimu. Fanya kitu kimoja kwa wakati, kazi moja kwa wakati usichanganye mambo. Unaporuhusu wasiwasi unakaribisha umaskini katika maisha yako. Kamwe usihofu kuhusu hali ya maisha yako ya siku zijazo.
Ujasiri na jitihada katika maisha ndiyo unaotakiwa. Kubali na kabiliana na changamoto unazokumbana nazo bila kuziogopa. Fikiria matarajio uliyoyapanga na uyape kipaumbele katika akili yako na mboni ya jicho lako. Kuwa jasiri katika kila hatua unayopitia.
Jua kwamba lazima utafanikiwa na simama katika ukweli huo.
Jua kuwa kila siku ni mpya.
Kesho bado haijafika hivyo ukiwa na hofu kwa ajili ya kuhofia matatizo ya siku ya kesho ni sawa na kupoteza nguvu katika akili yako. Ni vema kuzungumzia mafanikio katika kila jambo unalolifanya sasa.
Kama unasubiri mafanikio yakufuate, unakosea. Ni vema kuchangamkia mafanikio. Kila jambo linalokuletea mafanikio liko sasa, amani katika moyo wako unaweza kuwa nayo sasa.
Unaweza kuwa na mafanikio na afya njema uliyokuwa nayo sasa. Kila mara usiwaze yaliyopita au kushawishika kuishi matamanio ya siku zijazo.

JINSI GANI UNAWEZA KUFANIKIWA - 2

KARIBUNI wapenzi wasomaji kwa siku nyingine tena ya leo, ambayo tutaangalia ni jinsi gani tutaweza kufanikiwa katika maisha yetu. Makala hii ni mwendelezo wa Alhamisi iliyopita katika safu hii ya Maisha Yetu.
Kumbuka hukuzaliwa katika dunia hii kuishi au kukabiliana na maisha kwa bahati mbaya. Kila mmoja anajua kuwa maisha ni safari ndefu, mwanzo wa mwanadamu ni kuzaliwa. Na siku yoyote anaweza kufa.
Katika maisha tuliyonayo, mwanadamu ana uhuru wa kufanya kile atakacho na kusimamia maisha yake katika jambo alitakalo, kwa nia ya kula matunda mazuri katika maisha. Hivyo mwanadamu anatakiwa kuwa na utayari katika kuyatengeneza maisha yake, ni lazima ajue yeye ni nani na anaelekea wapi.
Malengo makubwa ya kiroho ya mwanadamu ni kuwa karibu na Mungu, malengo katika akili ya mwanadamu ni kutambua na kutumia vipaji alivyonavyo kwa ajili ya faida yake na familia yake. Kumbuka Mungu amekuumba kuwa mbunifu na anakutaka ufanikiwe na siyo ushindwe.
Wewe ni wa thamani kwa nini usiwaache wengine wakalitambua hilo? Hakuna mwingine katika dunia hii kama wewe, ingawa wengine wana mtazamo kama wako na kukuiga. Lakini hakuna atakayeweza kufanya vitu kama vile uvifanyavyo wewe kwa namna hiyo hiyo. Una mawazo yako tofauti yanayokuongoza kufanya jambo tofauti na wengine.
Watu wote ni muhimu, wana vipaji vya kipekee vinavyosubiri kuonyeshwa kipekee na kwa uthamani wake. Leo, zaidi ya ilivyokuwa, wafanyabiashara, wenye taaluma zao na viongozi wa viwanda, huangalia kwa kipekee yule anayeweza kuonyesha kipaji chake katika njia ya ubunifu. Cha msingi ukumbuke kuwa, hauko kama mwingine katika mawazo yako, vitendo na vipaji.
Jaribu kuwa na wazo, wengine wanaoweza kukusaidia waweze kuona kuwa wewe ni wa tofauti na unaweza kuwa wathamani katika vitu muhimu. Kuwa mbunifu na siyo mwigaji. Ni jambo la busara kuelewa, katika ulimwengu huu hakuna mtu anayefanana na wewe. Uwezo ulionao na jinsi unavyowaeleza hawawezi kujieleza kama ulivyo kwa wengine.
Hivyo huwezi kuwa na mshindani bali waigaji. Watu wanaoiga wenzao mara chache hufikia upeo wa juu. Lakini wale wanaobuni na kuzalisha mawazo yao ndiyo wanaofanikiwa, huwa viongozi. Wewe una akili ya ubunifu ya kuzalisha fikra na mawazo yako binafsi na kuelezea vipaji hivyo katika njia ya kipekee.
Acha kushindana na wengine. Wewe ni wewe. Hauko sawa na wengine kiakili, kiroho na kimuonekano. Jitahidi kubuni kitu chako na siyo kuiga. Kuna alama tano zinazoonyesha vipaji vilivyojificha. Kwani kila mmoja ana tabia zilizojificha. Kazi yako ni kugundua na kuviendeleza. Katika maisha unaweza kushangaa kwamba unakosa nafasi muhimu kwa sababu ya kushindwa kuendeleza vipaji vyako. Ni jinsi gani unavyoweza kugundua tabia zilizojificha? Kwanza, tenga dakika thelathini ukiandika tabia zako nzuri na za kawaida ulizo nazo.
Pili, orodhesha vitu ulivyovifanikisha na uvyotarajia kuvifanikisha. Tatu, andika ukurasa mmoja wa wasifu wa maisha yako mpaka hapo ulipo. Nne, tengeneza orodha ya maneno ya sifa ulizowahi kupokea kutoka kwa familia yako na marafiki zako kama tabasamu zuri, mkono wa pongezi, utanashati, utumiaji wa sauti yako, uwezo wako wa kuelezea jambo na mengine mengi.
Tano, tengeneza orodha ya vitu ambavyo unafanya vizuri kuliko vingine, jambo unalolipenda kuliko lingine, michezo na vipaji. Changanya vyote kwa ujumla na uchague vile vilivyobora zaidi kuliko vingine uvifanyie kazi.
Baada ya hapo utajijua kuwa wewe ni mtu wa aina gani, na unataka uweje. Kwa uangalifu changanua vile ulivyoandika na utaona kuwa unazo sifa ambazo hukuwahi kuwaza kwamba unamiliki sifa fulani.
Endeleza tabia zinazopendeza kwa wengine, hakikisha unawajua hao ni akina nani, uwafanye wakufanyie kazi kwa kiwango kinachoridhisha

Twitter Facebook