Tuesday, October 28, 2014

TCRA KUTOA MWONGOZO KWA WATANGAZAJI KWENYE UCHAGUZI


MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imeandaa rasimu ya mwongozo utakaofuatwa na vituo vya utangazaji katika kipindi cha uchaguzi wa serikali za mitaa, wabunge na raisi lengo likiwa kuweka usawa na uwazi katika kipindi cha uchaguzi, wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi kufanyika.
Mwenyekiti wa Kamati ya Maudhui ya mamlaka hiyo Margaret Munyagi alisema hayo katika mkutano wa kupokea maoni ya wadau juu ya utaratibu wa kuandaa na kurusha vipindi vinavyohusu vyama vya siasa wakati wa uchaguzi.
Alisema kuingia kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa nchini 1993, kulienda sambamba na kuanzishwa kwa vituo binafsi vya utangazaji, hivyo ongezeko la vituo hivyo limekuwa ni kichocheo cha kukuza demokrasia, kuboresha amani, kudumisha umoja na mshikamano wa taifa.
“Kama mnavyojua nchi yetu inategemea kuingia kwenye kipindi cha uchaguzi wa serikali za mitaa, wabunge na rais ifikapo 2015. Uchaguzi ni mchakato muhimu sana katika kukuza na kuimarisha demokrasia ya n chi husika,” alisema.
Munyagi alisema kuwa, vipindi vinavyotangaza masuala ya uchaguzi vinahitaji umakini mkubwa pamoja na uwepo wa mizani katika muda wanaopewa vyama vya siasa, kuwepo kwa uwazi, kufuata sheria na kanuni husika.
Alisisitiza kuwa, kukamilika kwa mwongozo huo kutawasaidia watangazaji na waandaaji wa vipindi kuepuka kufanya makosa ambayo kama yasipodhibitiwa yanaweza kusababisha uchochezi na kuleta mifarakano miongoni mwa jamii.
Alisema, tofauti na mategemeo hayo baadhi ya vyombo vya utangazaji vimekuwa vikikiuka sheria na kanuni kwa kuwa maudhui yanayotangazwa hayazingatii maadili ya kitanzania badala yake vimechangia kuharibu utamaduni wetu.
Pia vingine vimesahau madhumuni ya kuanzishwa kwao na wajibu wao katika jamii, hivyo kujiingiza katika masuala ya uchochezi pamoja na uvunjifu wa amani na utulivu.
Awali Mkurugenzi wa Utangazaji TCRA, Habbi Gunze alisema kuwa mpaka sasa kuna vituo vya redio 95, pamoja na  vya televisheni 28 nchini, hivyo ni bora vikapata mwongozo maalum wa namna ya kuandika habari za uchaguzi.


mwisho

Friday, March 14, 2014

JENGA MAZINGIRA MAZURI KAZINI


 KUNA vitu mbalimbali ambavyo kiongozi au meneja anaweza kuvifanya ili kuweka mazingira ya kazi yako yawe katika hali nzuri na kujenga hali ya umoja, mshikamano na furaha miongoni mwa wafanyakazi.
 
Miongoni mwa vitu hivyo ni kiongozi au meneja huyo kujenga kuaminiwa na wale anaowaongoza. Kujenga uaminifu ni jambo muhimu kwa wale wote wanaomhusu katika eneo la kazi.
 
Kiongozi unatakiwa kuaminiwa kwa kile unachokizungumza kwamba utakifanya. Ni njia ya kuwaonyesha wafanyakazi kuwa kila unachokifanya ni kwa ukamilifu sio ubabaishaji, ni jukumu lako.
 
Pia kuwaonyesha wale unaowaongoza kuwa unatarajia kupata mambo kama hayo unayostahili kuwafanyia kutoka kwao.
 
Endapo maneno yako unayoyazungumza na tabia yako vinakwenda sambamba hapo utaaminiwa sana . Inaweza kuchukua muda fulani kwa wafanyakazi wako kuelewa kuwa, kile unachokizungumza ndicho unachokitenda.
 
Lakini kinyume cha hapo utaonekana kuwa mbabaishaji, kama maneno yako hayataendana na matendo yako hutaaminiwa. Siri ni kwamba, inachukua muda mrefu kujenga kuaminika lakini muda mfupi kuondoa uaminifu huo endapo utaenda tofauti na unayoyazungumza.
 
Pale unapoondoa uaminifu wako kwa wale unaowaongoza, itachukua muda mrefu kujenga kuaminiwa tena, pia kamwe hautaaminiwa kama ilivyokuwa mwanzo.
 
Kwa hiyo, ni muhimu yale unayoyazungumza ukayatendea kazi ili kuendelea kujenga uaminifu wako kwa wafanyakazi.
 
Hata kama uko katika mazingira ambayo siyo mazuri, kama wewe ni mwaminifu itarahisisha mambo katika utendaji wako. Kile unachokizungumza na kile unachokifanya kinakueleza wewe ni nani.
 
 
Hata kama hawatapendezwa na kile unachokisema. Kama utakizungumza kwa uaminifu, ukarimu  na umakini utaheshimika na kuaminiwa.
 
Uaminifu wa wafanyakazi wako utazingatia jinsi unavyojenga hali ya kujiamini na uwazi katika mazungumzo yako.
 
Pia wanataka kujua kama wanazungumza nawe kuhusu mambo muhimu au taarifa zitachukuliwa katika hali ya usiri mkubwa.
 
Siri ni jambo la muhimu katika mazingira ya kazi, haitakiwi kutoa siri ya mtu kw amwingine isipokuwa umeizungumza katika hali chanya.
 
Pia  matatizo mengine yanayowakuta wafanyakazi wako yanatakiwa yahifadhiwe kati yako na mwajiri pamoja na kiongozi wako, kama itawezekana.
 
Kiongozi mzuri hawezi kuzungumza mtazamo mbaya juu ya timu yake anayofanya nayo kazi.
 
Pia kiongozi mzuri anapaswa kuwasiliana kwa upole na uwazi na wafanyakazi wake. Ili kujenga mazingira mazuri kazini kila mfanyakazi anahitaji kuheshimiwa. Hili linafanyika kupitia kuwasikiliza kila mmoja na kumheshimu kwa kile anachozungumza.
 
Kwa kufanya hivyo unaonyesha kuwa unajali na kumheshimu kila mmoja. Jambo moja muhimu ni kuweka uwazi kwa wafanyakazi wako ili wawe huru nawe katika kuzungumza maono na malengo ya kampuni waliyonayo.
 
Baada ya kuwasikiliza wafanyakazi wako yale waliyonayo pia nawe chukua muda wa kuwaeleza maono na mipango uliyonayo. Eleza jinsi unavyoona jinsi ya kufanya kazi kama timu kwa kuwa kila mtu  ni sawa anastahili heshima, kuliko kufanya kazi kwa matabaka.
 
Kila mtu ni sawa kwa kuwa kila kazi ina umuhimu sawa katika kufanikisha maono ya kampuni. Pia zungumza nao kuhusu maadili, miiko ya kazi pamoja na uthamani wake.
 
Kuzungumza kuhusu maadili ya kazi kutaonyesha mfano wa matarajio unayotaka kuyaona katika utendaji wa wafanyakazi wako na tabia zao. Hiyo ni pamoja na kujivunia kazi unayoifanya, kumjali kila mmoja kutokana na utendaji wake, pia kutumia kazi yako kama njia mojawapo ya kuendelea kujifunza.
 
mwisho

Monday, March 3, 2014

WIVU HULETA MAFARAKANO KAZINI

Mafanikio huzaa mafanikio, lakini kwa bahati mbaya huleta wivu.

WAKATI unapokuwa na mafanikio katika kampuni ama eneo la kazi, unaweza kujikuta una marafiki wengi, pamoja na maadui wachache.

Hawa maadui mara nyingi wamekuwa wakijaribu kukuangusha ama kukufanya ushindwe katika kazi zako ama kukupa ushirikiano mdogo.

Wakati mwingine maadui hao huweza kutafuta namna ya kukukwamisha kwa kukufanyia visa mbalimbali ikiwemo wivu, fitina, ukorofi lengo likiwa ni kukukwamisha kimaendeleo na hata katika taaluma yako ama shughuli inayokukupatia kipato, pia wanaweza kukuwekea mitego ili ushindwe.

Hao wafanyakazi ambao wana wivu nawe au wasiopenda ufanikiwe katika kazi yako, ni rahisi kuwatambua kwa kukushusha thamani ama kukunenea maneno ya kushindwa kwa wengine na kukulinganisha na watu hata ambao hawana uwezo ulionao kuwa wapo juu yako kiutendaji ili mradi tu watimize lengo lao.

Kila utakachofanya kwa watu wa aina hii kwao kitakuwa ni gumzo, ama kukushusha thamani hata kama wakiwa wanaujua ukweli halisi juu yako kuhusu utendaji wako wa kazi.

Maadui wa aina hii hutumia fursa ya kuzungumza maneno mabaya au ya kukuvunja moyo pale utakapofanya kosa ama kushindwa jambo. Hawa ni hatari kwa kuwa wanajihesabia haki ama watenda mema wao wenyewe.

Jinsi ya kushughulika na watu wa aina hii katika eneo lako la kazi, kuna njia mbili. Njia ya kwanza ni kuwa kimya na kupuuzia kila wanalokufanyia na ya pili ni kuzungumzia jitihada zao kama zipo.

Katika mazingira kama hayo, inakubidi uwe jasiri na unayejiamini usimamie kile unachokiamini. Pia uwe mnyenyekevu katika kazi yako, toa kile ulichonacho kwa wengine kwa kuwafundisha mbinu mbalimbali za kuweza kufikia mafanikio.

Jitahidi kujiweka katika hali ya kawaida katika mazingira unayofanyia kazi, kuwa na amani na maadui zako, fanya mabadiliko ya kweli katika moyo wako.

Kutokana na umuhimu wa fani yako, epuka migogoro ama migongano isiyokuwa na lazima katika eneo lako la kazi.

Utakapofanya hivyo utapata heshima kutoka kwa wafanyakazi wengine.

Hata kama kwa upande wako umekosea katika eneo Fulani, ni wakati mzuri sasa wa kujirekebisha kutokana na makosa yaliyopita.

Kwa kufanya hivyo watu wataona mabadiliko yako, pia kuwa mtu wa kukubali kubadilika pale unapokosolewa.

Endapo utatambua kuwa wenzako ama msaidizi wako kazini hana furaha nawe, unaweza kuondoa ama kuzuia wivu wake kwako.

Inabidi kuwa mkimya, mtulivu lakini si kwa kiwango ambacho mchango wako utashindwa kuonekana.

Pia wapongeze wenzako katika mafanikio yao. Jitahidi kutokuwa na wivu, endapo nawe utakuwa na wivu kwa wengine, utakuwa huna tofauti na hao wenye wivu katika ofisi yako.

Kama utakuwa hauko imara kuondoa wivu miongoni mwa wafanyakazi, nawe utalazimika kuwa na tabia hiyo katika eneo lako la kazi.

Wakati wote uwapo katika eneo lako la kazi fanya kazi kwa bidii, simamia kile unachokiamini kamwe usijiingize katika makundi ya masengenyo ambayo yanatokea eneo ulilopo.

Kushughulika na watu wa aina hii mara nyingi inakuwa ni vigumu kwa kuwa, wako kwenye mazingira ambayo unataka kuyaepuka. Ni vizuri kufanya jitihada ili kuwa timu moja na kukatama mazingira ya wivu kwa kuwa hali hiyo ikiachwa italeta tatizo.

Mwisho.

Saturday, February 22, 2014

KWA NINI WATU WANAWAKATISHA TAMAA WENGINE?

FRANK John anasema, amekuwa akipata ujumbe mbalimbali kupitia simu ama barua pepe yake zikieleza kuwa kuna baadhi ya watu wamekuwa wakiwakatisha tamaa wengine wasifikie malengo ama mafanikio waliojiwekea.
 
Anasema sababu aliyoipata wakati anasoma ujumbe hizo ni kwamba baadhi ya wale wanaokatishwa tamaa wanawaamini hao wanaowakatisha tamaa.
 
Si vibaya kuwazungumzia hao wanaokukatisha tamaa, lakini pale unapoanza kujiuliza maswali baada ya kuzungumza nao jua kwamba uko kwenye hatari kubwa.
 
Njia inayoweza kukusaidia ambayo haitakudhuru kutokana na watu wa aina hiyo ni kutaka ujue kwa nini watu wanawavunja moyo ama kuwakatisha tamaa wengine.
 
Zipo sababu zinazowafanya baadhi ya watu kuwakatisha tamaa wengine.
 
Kwanza watu hao hawawezi kufanya mambo unayotaka kuyafanya., mfano “ Kama ninaamini kuwa siwezi kufanikiwa lakini ninafikiri kuwa wengine wana bahati hiyo, ndiyo maana ninapokutana na mtu ninayeamini anamafanikio ninaanza kumvunja moyo ama kumkatisha tamaa kutokana na imani yangu potofu,”.
 
Pili mtu wa aina hiyo anatishiwa na wewe kwa kila unachokifanya hata kama ni cha kawaida ambacho kama angejaribu kukifanya naye angefanikiwa.
 
Baadhi ya watu wanahisi kushindwa kufanya jambo pale wanapomwona mtu anajaribu kufanya kitu fulani. Kama wakati wote mtu fulani anataka kuwa tajiri lakini hajishughulishi kufanya shughuli binafsi, huhisi kutishika pale anapoona wewe unachukua hatua ya kuanza jambo la mafanikio.
 
Kutokana na hali hiyo, mtu wa aina hiyo hujaribu kukukatisha tamaa ili usiweze kuwa bora kumzidi yeye.
 
Sababu nyingine mtu wa aina hiyo anakuwa na wivu. Amini ama usiamini. Rafiki yako wa karibu anaweza kujaribu kukuvunja moyo kutokana na wivu alionao kwako. Kama anajihisi ni mnyonge kwako kwa jambo fulani ama kuna mambo unayoyafanya ambayo yeye hawezi kuyafikia hujaribu kukurudisha nyuma kutokana na wivu alionao.
 
Jambo jingine ni woga. Kuna mtu mmoja alitaka kuchapisha kitabu chake cha kwanza , hivyo alimwendea mshapishaji kwa makubaliano maalum kuwa atammalizia fedha zake atakapokiuza kitabu kile, lakini mshapishaji yule alimvunja moyo kuwa huchapisha vitabu vya siasa tu kwa kuwa ndivyo vina biashara. Lakini baadaye mtu huyo aliweza kuchapisha vitabu hivyo na kwa haraka alifanikiwa kuuza zaidi ya nakala milioni moja.
 
Anasema aligundua kuwa, mchapishaji yule aliogopa kupata hasara kwa sababu alimwona kuwa ni kijana, pia alidhamiria kumuangusha asisonge mbele.
 
Sababu nyingine ni kuchukiwa. Kama mtu anakuchukia hataki kukuona ukiendelea katika jambo lolote na ndio maana atajaribu kukuvunja moyo pale anapopata nafasi. Kuwa makini na maadui wa aina hiyo.
 
Vile vile watu wa aina hiyo hawakupi taarifa sahihi. Watu wengi wanapenda kusema ‘sijui’ wanapoulizwa jambo fulani. Wanakuwa hawana elimu muhimu kuhusu kile unachokipanga kukifanya hivyo kurudisha nyuma kwa kusema hawajui.
 
Jambo lingine ni kwamba watu wa aina hii hawawezi kuiona picha halisi uliyonayo juu ya mipango yako. Baadhi yao watakukatisha tamaa kwa kuwa tu hawaelewi picha unayoipanga katika maisha yako.
 
Sasa basi ni jinsi gani unaweza kuwazuia watu wasikukatishe tamaa.
Kuna mambo mawili unahitaji kuyafanya ili kuzuia hali hiyo. jambo la kwanza ni kutokuzungumza kuhusu mipango yako isipokuwa kwa mtu yule ambaye unadhani kuwa anakupenda kwa dhati. Kama utafanya kinyume na hapo utakuwa ukivunjwa moyo na watu wa aina hiyo kila mara.
 
Jambo la pili ni kuonyesha kuwa jambo ulilokusudia kulifanya unalishikilia hilo hilo mpaka linafikia mwisho na mafaniko yake unayaona. Kutokana na sababu hiyo wale wanaokurudisha nyuma wataanza kukuamini na kile unachokisimamia ni sahihi.
 
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa mtandao.
 
mwisho

JINSI GANI YA KUFANYA KAZI NA ANAYEKUCHUKIA

JE unawezaje kushughulika na mtu anayekuchukia kazini? Hilo ndilo swali la msingi la kujiuliza. Na jinsi gani unaweza kuzuia usichukiwe na wafanyakazi wengine.
 
Kila mmoja ana hisia ambazo zinaweza kumwongoza afanye jambo Fulani ama asilifanye, kwa ajili ya kuzuia ghadhabu au kutokuelewana kusitokee.
 
Sasa ni kwa jinsi gani unaweza kushughulika na mtu anayekuchukia katika eneo la kazi.
 
Kuchukiwa ni hisia iliyopo kwa mtu ambayo mtu huyo anayemchukia mwingine badala ya kumpiga anamalizia hisia hizo kwa kumchukia.
 
Hii inamaanisha kuwa, kama kuna mtu anakuchukia kazini inaonyesha kuwa,  wewe ni mtu wa muhimu hivyo anatumia mbinu hiyo kukudhoofisha kisaikolojia.
 
Inakuaje akili ya huyo anayekuchukia inajiridhisha kuwa wewe ni adui wake wa kwanza? Na kwa nini anakuchukia hata kama hujafanya jambo baya kwake?
 
Wakati mwingine wewe unayechukiwa inawezekana umefanya jambo ambalo ni baya bila kujitambua. Kwa mfano imefikia mahali ukaonekana una akili kupita kawaida ambapo unaitumia akili hiyo  katika eneo la kazi watu wakuogope. Kutokana na hali hiyo ukachukiwa, hakikisha hauonyeshi hisia zako pindi unapochukiwa.
 
Hivyo, yule au watu wale wanaokuchukia eneo la kazi wataweza kuficha hisia zao hizo kwa kuwa wametambua wewe sio mtu mbaya kwao. Mtu anaweza kukuchukia katika kazi kutokana na wivu, kutokujiamini ama hofu.
 
 
Hali halisi inaonyesha kuwa, mtu ama watu wanaweza kukuchukia bila sababu kwa kuwa unawafanya wawe na hofu kila wanapokuona.
 
Ili kushughulika na watu wa aina hiyo ni lazima kwanza utafute sababu inayowafanya wakuchukie na kuonyesha kuwa hujali.
 
Ni jinsi gani utawazuia watu wasikuchukie katika eneo la kazi.
Kwa mfano umejua kuwa Fulani anakuchukia katika kazi kwa sababu anakuonea wivu, katika hali ya namna hii, unaweza kumsaidia mtu huyo nje na kazi kulainisha hali yake ya kuwa na wivu na kumpunguzia asikuchukie.
 
Ni muhimu sana kutokujifanya una akili sana mbele ya wale ambao hawatambui hilo , na wale ambao wanaweza kujenga chuki kwa ajili hiyo.
 
Pia epuka kujionyesha kuwa una mafanikio zaidi au mwenye akili, ili usijenge maadui wengine bila kujijua au kuwafanya watu wengi wakuchukie katika eneo la kazi bila kufanya jambo lolote baya.
 
Wakati mwingine unashauriwa kufanya makosa madogo madogo mbele ya watu wa aina hiyo ili tu kuwachanganya kwenye mafanikio uliyo nayo kiuhalisia.
 
Pia usijiweke wazi wakajua mipango yako uliyonayo wala kulinganisha ndoto zako kubwa ulizonazo kwa mawazo yao madogo waliyonayo.
 
Ushauri mwingine ni kutokujali mazingira ya namna hiyo, kikubwa kwako ni kusonga mbele.
 
Pia pale unaposulubiwa kwa jinsi yoyote ile onyesha kuwa hujali, we endelea kufanya kile unachotakiwa kukifanya.
 
Kanuni ya kukumbuka ni kwamba, simamia kile unachokiamini, hivyo tabia ya mtu mwingine isikusumbue, chukua muda kumfahamu vizuri mtu huyo na historia yake, pia kile kinachomfanya awe hivyo.
 
Kamwe unapokumbana na adha katika kazi, usitake kufanya ushindani na yule anayekutendea mabaya ili kujiepusha na migongano.
 
mwisho

Twitter Facebook