Saturday, February 22, 2014

KWA NINI WATU WANAWAKATISHA TAMAA WENGINE?

FRANK John anasema, amekuwa akipata ujumbe mbalimbali kupitia simu ama barua pepe yake zikieleza kuwa kuna baadhi ya watu wamekuwa wakiwakatisha tamaa wengine wasifikie malengo ama mafanikio waliojiwekea.
 
Anasema sababu aliyoipata wakati anasoma ujumbe hizo ni kwamba baadhi ya wale wanaokatishwa tamaa wanawaamini hao wanaowakatisha tamaa.
 
Si vibaya kuwazungumzia hao wanaokukatisha tamaa, lakini pale unapoanza kujiuliza maswali baada ya kuzungumza nao jua kwamba uko kwenye hatari kubwa.
 
Njia inayoweza kukusaidia ambayo haitakudhuru kutokana na watu wa aina hiyo ni kutaka ujue kwa nini watu wanawavunja moyo ama kuwakatisha tamaa wengine.
 
Zipo sababu zinazowafanya baadhi ya watu kuwakatisha tamaa wengine.
 
Kwanza watu hao hawawezi kufanya mambo unayotaka kuyafanya., mfano “ Kama ninaamini kuwa siwezi kufanikiwa lakini ninafikiri kuwa wengine wana bahati hiyo, ndiyo maana ninapokutana na mtu ninayeamini anamafanikio ninaanza kumvunja moyo ama kumkatisha tamaa kutokana na imani yangu potofu,”.
 
Pili mtu wa aina hiyo anatishiwa na wewe kwa kila unachokifanya hata kama ni cha kawaida ambacho kama angejaribu kukifanya naye angefanikiwa.
 
Baadhi ya watu wanahisi kushindwa kufanya jambo pale wanapomwona mtu anajaribu kufanya kitu fulani. Kama wakati wote mtu fulani anataka kuwa tajiri lakini hajishughulishi kufanya shughuli binafsi, huhisi kutishika pale anapoona wewe unachukua hatua ya kuanza jambo la mafanikio.
 
Kutokana na hali hiyo, mtu wa aina hiyo hujaribu kukukatisha tamaa ili usiweze kuwa bora kumzidi yeye.
 
Sababu nyingine mtu wa aina hiyo anakuwa na wivu. Amini ama usiamini. Rafiki yako wa karibu anaweza kujaribu kukuvunja moyo kutokana na wivu alionao kwako. Kama anajihisi ni mnyonge kwako kwa jambo fulani ama kuna mambo unayoyafanya ambayo yeye hawezi kuyafikia hujaribu kukurudisha nyuma kutokana na wivu alionao.
 
Jambo jingine ni woga. Kuna mtu mmoja alitaka kuchapisha kitabu chake cha kwanza , hivyo alimwendea mshapishaji kwa makubaliano maalum kuwa atammalizia fedha zake atakapokiuza kitabu kile, lakini mshapishaji yule alimvunja moyo kuwa huchapisha vitabu vya siasa tu kwa kuwa ndivyo vina biashara. Lakini baadaye mtu huyo aliweza kuchapisha vitabu hivyo na kwa haraka alifanikiwa kuuza zaidi ya nakala milioni moja.
 
Anasema aligundua kuwa, mchapishaji yule aliogopa kupata hasara kwa sababu alimwona kuwa ni kijana, pia alidhamiria kumuangusha asisonge mbele.
 
Sababu nyingine ni kuchukiwa. Kama mtu anakuchukia hataki kukuona ukiendelea katika jambo lolote na ndio maana atajaribu kukuvunja moyo pale anapopata nafasi. Kuwa makini na maadui wa aina hiyo.
 
Vile vile watu wa aina hiyo hawakupi taarifa sahihi. Watu wengi wanapenda kusema ‘sijui’ wanapoulizwa jambo fulani. Wanakuwa hawana elimu muhimu kuhusu kile unachokipanga kukifanya hivyo kurudisha nyuma kwa kusema hawajui.
 
Jambo lingine ni kwamba watu wa aina hii hawawezi kuiona picha halisi uliyonayo juu ya mipango yako. Baadhi yao watakukatisha tamaa kwa kuwa tu hawaelewi picha unayoipanga katika maisha yako.
 
Sasa basi ni jinsi gani unaweza kuwazuia watu wasikukatishe tamaa.
Kuna mambo mawili unahitaji kuyafanya ili kuzuia hali hiyo. jambo la kwanza ni kutokuzungumza kuhusu mipango yako isipokuwa kwa mtu yule ambaye unadhani kuwa anakupenda kwa dhati. Kama utafanya kinyume na hapo utakuwa ukivunjwa moyo na watu wa aina hiyo kila mara.
 
Jambo la pili ni kuonyesha kuwa jambo ulilokusudia kulifanya unalishikilia hilo hilo mpaka linafikia mwisho na mafaniko yake unayaona. Kutokana na sababu hiyo wale wanaokurudisha nyuma wataanza kukuamini na kile unachokisimamia ni sahihi.
 
Makala hii imeandaliwa kwa msaada wa mtandao.
 
mwisho

JINSI GANI YA KUFANYA KAZI NA ANAYEKUCHUKIA

JE unawezaje kushughulika na mtu anayekuchukia kazini? Hilo ndilo swali la msingi la kujiuliza. Na jinsi gani unaweza kuzuia usichukiwe na wafanyakazi wengine.
 
Kila mmoja ana hisia ambazo zinaweza kumwongoza afanye jambo Fulani ama asilifanye, kwa ajili ya kuzuia ghadhabu au kutokuelewana kusitokee.
 
Sasa ni kwa jinsi gani unaweza kushughulika na mtu anayekuchukia katika eneo la kazi.
 
Kuchukiwa ni hisia iliyopo kwa mtu ambayo mtu huyo anayemchukia mwingine badala ya kumpiga anamalizia hisia hizo kwa kumchukia.
 
Hii inamaanisha kuwa, kama kuna mtu anakuchukia kazini inaonyesha kuwa,  wewe ni mtu wa muhimu hivyo anatumia mbinu hiyo kukudhoofisha kisaikolojia.
 
Inakuaje akili ya huyo anayekuchukia inajiridhisha kuwa wewe ni adui wake wa kwanza? Na kwa nini anakuchukia hata kama hujafanya jambo baya kwake?
 
Wakati mwingine wewe unayechukiwa inawezekana umefanya jambo ambalo ni baya bila kujitambua. Kwa mfano imefikia mahali ukaonekana una akili kupita kawaida ambapo unaitumia akili hiyo  katika eneo la kazi watu wakuogope. Kutokana na hali hiyo ukachukiwa, hakikisha hauonyeshi hisia zako pindi unapochukiwa.
 
Hivyo, yule au watu wale wanaokuchukia eneo la kazi wataweza kuficha hisia zao hizo kwa kuwa wametambua wewe sio mtu mbaya kwao. Mtu anaweza kukuchukia katika kazi kutokana na wivu, kutokujiamini ama hofu.
 
 
Hali halisi inaonyesha kuwa, mtu ama watu wanaweza kukuchukia bila sababu kwa kuwa unawafanya wawe na hofu kila wanapokuona.
 
Ili kushughulika na watu wa aina hiyo ni lazima kwanza utafute sababu inayowafanya wakuchukie na kuonyesha kuwa hujali.
 
Ni jinsi gani utawazuia watu wasikuchukie katika eneo la kazi.
Kwa mfano umejua kuwa Fulani anakuchukia katika kazi kwa sababu anakuonea wivu, katika hali ya namna hii, unaweza kumsaidia mtu huyo nje na kazi kulainisha hali yake ya kuwa na wivu na kumpunguzia asikuchukie.
 
Ni muhimu sana kutokujifanya una akili sana mbele ya wale ambao hawatambui hilo , na wale ambao wanaweza kujenga chuki kwa ajili hiyo.
 
Pia epuka kujionyesha kuwa una mafanikio zaidi au mwenye akili, ili usijenge maadui wengine bila kujijua au kuwafanya watu wengi wakuchukie katika eneo la kazi bila kufanya jambo lolote baya.
 
Wakati mwingine unashauriwa kufanya makosa madogo madogo mbele ya watu wa aina hiyo ili tu kuwachanganya kwenye mafanikio uliyo nayo kiuhalisia.
 
Pia usijiweke wazi wakajua mipango yako uliyonayo wala kulinganisha ndoto zako kubwa ulizonazo kwa mawazo yao madogo waliyonayo.
 
Ushauri mwingine ni kutokujali mazingira ya namna hiyo, kikubwa kwako ni kusonga mbele.
 
Pia pale unaposulubiwa kwa jinsi yoyote ile onyesha kuwa hujali, we endelea kufanya kile unachotakiwa kukifanya.
 
Kanuni ya kukumbuka ni kwamba, simamia kile unachokiamini, hivyo tabia ya mtu mwingine isikusumbue, chukua muda kumfahamu vizuri mtu huyo na historia yake, pia kile kinachomfanya awe hivyo.
 
Kamwe unapokumbana na adha katika kazi, usitake kufanya ushindani na yule anayekutendea mabaya ili kujiepusha na migongano.
 
mwisho

Twitter Facebook